Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa Wahudumu Wenye Ubunifu, Wanaobadilika Kulingana na Hali

Kuwa Wahudumu Wenye Ubunifu, Wanaobadilika Kulingana na Hali

Kuwa Wahudumu Wenye Ubunifu, Wanaobadilika Kulingana na Hali

“Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine.”—1 WAKORINTHO 9:22.

1, 2. (a) Ni kwa njia gani mtume Paulo alikuwa mhudumu mwenye matokeo? (b) Paulo alielezaje maoni yake kuhusu utume wake?

ALIKUWA mtulivu alipozungumza na watu wa hali ya juu wenye akili na watengeneza-mahema wa hali ya chini. Alitumia ushawishi alipoongea na wenye mamlaka wa Roma na wakulima wa Frigia. Maandishi yake yaliwachochea Wagiriki waliokubali maoni mapya na vilevile Wayahudi ambao hawakukubali mambo mapya. Alitoa hoja zisizoweza kupingwa, naye akagusa sana hisia za watu. Alipozungumza na mtu yeyote yule alijitahidi kutambua jambo ambalo anaweza kukubaliana nalo ili aweze kuwasaidia watu kadhaa wamwamini Kristo.—Matendo 20:21.

2 Huyo si mwingine ila mtume Paulo, ambaye alikuwa mhudumu mwenye matokeo na mwenye ubunifu. (1 Timotheo 1:12) Yesu alimpa utume wa “kupeleka jina [la Kristo] kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.” (Matendo 9:15) Alionaje utume wake? Alisema hivi: “Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine. Lakini ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.” (1 Wakorintho 9:19-23) Tunaweza kujifunza jambo gani kutokana na mfano wa Paulo ambalo linaweza kutusaidia tuwe wenye matokeo zaidi tunapohubiri na kufundisha?

Mtu Aliyebadilika Afaulu Kutimiza Kazi Ngumu

3. Kabla ya kuwa Mkristo, Paulo aliwaonaje Wakristo?

3 Je, Paulo alizaliwa akiwa mtu mstahimilivu na anayejali, ambaye alistahili kupata utume aliopewa? La hasha! Kwa sababu ya kushikilia dini kupindukia, Sauli (jina la Paulo la zamani) aliwatesa vikali wafuasi wa Kristo. Akiwa kijana, alikubali mauaji ya Stefano. Baadaye, Paulo aliwawinda Wakristo bila huruma. (Matendo 7:58; 8:1, 3; 1 Timotheo 1:13) Aliendelea ‘kuwatisha wanafunzi wa Bwana akitaka kuwaua.’ Kwa kuwa hakuridhika kuwafuata waamini huko Yerusalemu peke yake, aliendeleza jitihada zake za chuki kufikia kaskazini huko Damasko.—Matendo 9:1, 2.

4. Paulo alihitaji kufanya mabadiliko gani ili atimize utume wake?

4 Huenda Paulo alichukia vikali Ukristo kwa sababu ya kusadiki kwamba imani hiyo mpya ingepotosha Dini ya Kiyahudi kwa mafundisho mapya yasiyofaa. Isitoshe, hapo zamani Paulo alikuwa “Farisayo,” jina linalomaanisha “aliyewekwa kando.” (Matendo 23:6) Hebu wazia jinsi Paulo alivyoshangaa alipoambiwa kwamba Mungu amemchagua kuwahubiria watu wasio Wayahudi juu ya Kristo! (Matendo 22:14, 15; 26:16-18) Mafarisayo walikataa hata kula pamoja na watu ambao walikuwa watenda-dhambi kwa maoni ya Mafarisayo! (Luka 7:36-39) Hapana shaka kwamba alihitaji kujitahidi sana kubadili maoni yake na kuyapatanisha na mapenzi ya Mungu kwamba watu wa namna zote wanapaswa kuokolewa.—Wagalatia 1:13-17.

5. Tunaweza kumwigaje Paulo katika huduma yetu?

5 Huenda sisi pia tukahitaji kufanya vivyo hivyo. Tunapokutana na watu tofauti-tofauti katika eneo letu lenye watu kutoka nchi nyingine wanaozungumza lugha mbalimbali, tunahitaji kujitahidi sana kuchunguza maoni yetu na kuondoa ubaguzi wowote tulio nao. (Waefeso 4:22-24) Kwa kawaida sisi hutenda kulingana na malezi na elimu tuliyopata. Jambo hilo linaweza kutufanya tuwe na maoni na mtazamo wa upendeleo na wa ubaguzi, na kutuzuia tusibadilike kulingana na hali. Ni lazima tuondoe akilini maoni hayo ili tufanikiwe kuwapata na kuwasaidia wale walio kama kondoo. (Waroma 15:7) Hivyo ndivyo Paulo alivyofanya. Alijitahidi kuongeza huduma yake. Alichochewa na upendo kusitawisha ustadi wa kufundisha ambao unastahili kuigwa. Naam, uchunguzi wa huduma ya Paulo, ambaye alikuwa “mtume kwa mataifa,” unaonyesha kwamba alikaza uangalifu, alibadilika kulingana na hali, na alitumia ubunifu alipohubiri na kufundisha. *Waroma 11:13.

Jinsi Alivyokuwa Mhudumu Mwenye Ubunifu

6. Paulo alikaziaje uangalifu malezi ya wasikilizaji wake, naye alipata matokeo gani?

6 Paulo alikazia uangalifu imani na malezi ya wasikilizaji wake. Alipokuwa akizungumza na Mfalme Agripa wa Pili, Paulo alikubali kwamba mfalme huyo alikuwa na “ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi.” Kisha, Paulo akatumia kwa ustadi yale aliyojua kuhusu imani ya Agripa na kuzungumza naye kuhusu mambo ambayo mfalme huyo aliyajua vizuri sana. Paulo alieleza hoja zake waziwazi na kwa usadikisho hivi kwamba Agripa akasema: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.”—Matendo 26:2, 3, 27, 28.

7. Paulo alibadilikaje kulingana na hali alipokuwa akihubiria umati huko Listra?

7 Pia, Paulo alibadilika kulingana na hali. Ona jinsi alivyotumia njia tofauti alipojaribu kuusihi umati wa watu katika jiji la Listra wasimwabudu yeye na Barnaba. Inasemekana kwamba watu hao, waliozungumza Kilikaonia, walikuwa kati ya wale ambao hawakuwa na elimu nyingi na walioamini zaidi ushirikina. Kulingana na Matendo 14:14-18, Paulo alizungumzia uumbaji na vitu vingi vya asili ili kuonyesha ukuu wa Mungu wa kweli. Hoja hiyo ilieleweka kwa urahisi, na inaonekana ‘ilizuia umati wasiwatolee dhabihu’ Paulo na Barnaba.

8. Paulo alibadilikaje kulingana na hali licha ya kuwa na hisia kali nyakati nyingine?

8 Ni kweli kwamba Paulo hakuwa mkamilifu na nyakati nyingine alionyesha hisia zake kali kuhusu mambo fulani. Kwa mfano, wakati mmoja aliposhambuliwa isivyo haki na kushushiwa heshima, alimfokea Myahudi aliyeitwa Anania. Lakini Paulo alipoambiwa kwamba alikuwa amemtukana kuhani mkuu bila kujua, aliomba msamaha mara moja. (Matendo 23:1-5) Huko Athene, mwanzoni ‘aliudhika alipoona kwamba jiji hilo lilikuwa limejaa sanamu.’ Hata hivyo, alipokuwa akizungumza kwenye Kilima cha Mars, Paulo hakuonyesha kwamba ameudhika. Badala yake, aliwahutubia Waathene mahali walipokuwa wakikutanika, naye akazungumzia mambo waliyopendezwa nayo kwa kutaja madhabahu yao “Kwa Mungu Asiyejulikana” na kumnukuu mmoja wa washairi wao.—Matendo 17:16-28.

9. Paulo alionyeshaje ubunifu aliposhughulika na watu mbalimbali?

9 Paulo alionyesha ubunifu wa hali ya juu aliposhughulika na watu mbalimbali. Alifikiria utamaduni na malezi yaliyoongoza njia ya kufikiri ya watu waliomsikiliza. Alipowaandikia Wakristo huko Roma, alijua kwamba wanaishi katika jiji kuu la serikali kuu zaidi ya wakati huo. Jambo moja kuu katika barua ya Paulo kwa Wakristo huko Roma ni kwamba nguvu za kuharibu za dhambi ya Adamu hushindwa na nguvu za Kristo za kukomboa. Paulo alizungumza na Wakristo Waroma na wale walioishi karibu nao kwa maneno ambayo yangegusa mioyo yao.—Waroma 1:4; 5:14, 15.

10, 11. Paulo alibadilishaje mifano yake iwafae wasikilizaji? (Ona pia maelezo ya chini.)

10 Paulo alifanya nini alipotaka kuwaeleza wasikilizaji wake kweli nzito za Biblia? Mtume huyo alikuwa na ustadi wa kutumia mifano ya kawaida iliyo rahisi kueleweka ili kueleza mambo magumu ya kiroho. Kwa mfano, Paulo alijua kwamba watu huko Roma walijua sana mfumo wa utumwa uliokuwepo kotekote katika Milki ya Roma. Isitoshe, watu wengi kati ya wale ambao Paulo aliwaandikia walikuwa watumwa. Hivyo, Paulo alitumia mfano wa utumwa kutetea hoja yake nzito, iliyoonyesha kwamba mtu anaweza kuchagua kuwa mtumwa wa dhambi au wa uadilifu.—Waroma 6:16-20.

11 Kitabu kimoja kinasema hivi: “Miongoni mwa Waroma, bwana mkubwa angeweza kumweka huru mtumwa wake bila masharti, au mtumwa angeweza kununua uhuru wake kwa kumlipa bwana wake. Pia, mtu angeweza kuwekwa huru ikiwa angefanywa kuwa mtumwa wa mungu fulani.” Mtumwa aliyewekwa huru angeweza kuendelea kumfanyia kazi bwana wake kwa malipo. Inaonekana Paulo alikuwa akirejelea zoea hilo alipoandika kwamba mtu anaweza kuchagua ni bwana yupi ambaye atatii—dhambi au uadilifu. Wakristo huko Roma walikuwa wamewekwa huru kutokana na dhambi na kuwa mali ya Mungu. Walikuwa huru kumtumikia Mungu, lakini ikiwa wangependa bado wangeweza kuchagua kutumikia dhambi, bwana wao wa zamani. Mfano huo rahisi na wenye kueleweka ungewachochea Wakristo huko Roma kujiuliza, ‘Ninamtumikia bwana yupi?’ *

Kujifunza Kutokana na Mfano wa Paulo

12, 13. (a) Ni jitihada gani inayohitajiwa leo ili kufikia mioyo ya watu mbalimbali tunaowahubiria? (b) Ni nini ambacho kimekuwezesha kupata matokeo unapowahubiria watu wenye utamaduni mbalimbali?

12 Kama Paulo, tunapaswa kukaza uangalifu, kubadilika kulingana na hali, na kutumia ubunifu ili tufikie mioyo ya watu mbalimbali tunaowahubiria. Ili kuwasaidia wale tunaowahubiria waelewe habari njema, tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kuwatembelea kidesturi tu, kuwaeleza ujumbe tuliotayarisha, au kuwaachia vichapo fulani vya Biblia. Tunajitahidi kujua mahitaji yao na mahangaiko yao, mambo wanayopenda na yale wasiyopenda, na mambo wanayoogopa na kuchukia. Ijapokuwa hilo linahitaji mhubiri afikiri na kujitahidi sana, wahubiri wa Ufalme ulimwenguni pote wanafanya hivyo kwa hiari. Kwa mfano, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Hungaria inaripoti hivi: “Akina ndugu huheshimu desturi na njia ya maisha ya watu wa mataifa mengine, nao hawatarajii watu hao wabadilike kulingana na desturi za hapa.” Mashahidi hujitahidi kufanya hivyo katika sehemu nyingine pia.

13 Katika nchi moja iliyo Mashariki ya Asia, watu wengi huhangaikia afya, kulea watoto, na elimu. Wahubiri wa Ufalme katika sehemu hiyo hujitahidi kukazia mambo hayo badala ya kuzungumzia hali mbaya za ulimwengu au matatizo makubwa ya kijamii. Vivyo hivyo, wahubiri katika jiji moja kubwa la Marekani waligundua kwamba watu katika sehemu fulani ya eneo lao wanahangaikia ufisadi, msongamano wa magari, na uhalifu. Mashahidi hufaulu kuanzisha mazungumzo ya Biblia kwa kuzungumzia mambo hayo. Walimu wa Biblia wenye matokeo wanapochagua kuzungumzia jambo lolote, wao hujitahidi kuwa wachangamfu na wenye kujenga, huku wakionyesha waziwazi faida za kutumia kanuni za Biblia sasa na matarajio mazuri ya wakati ujao ambayo Mungu ameahidi.—Isaya 48:17, 18; 52:7.

14. Eleza mambo tunayoweza kufanya ili kubadilika kulingana na mahitaji na hali mbalimbali za watu.

14 Ni muhimu pia tubadilishe njia yetu ya kuhubiri, kwa kuwa watu wana utamaduni mbalimbali, dini tofauti, na viwango tofauti vya elimu. Njia yetu ya kuwahubiria watu wanaoamini kwamba kuna Muumba ingawa hawaiamini Biblia itakuwa tofauti na ile tunayotumia kuzungumza na wale wasioamini kwamba Mungu yuko. Tunapozungumza na mtu anayeamini kwamba vitabu vyote vya kidini hueneza propaganda, tutatumia njia tofauti na ile tunayotumia tunapozungumza na mtu anayekubali mafundisho ya Biblia. Tunahitaji pia kubadilika kulingana na hali kwa kuwa tunakutana na watu wenye viwango tofauti vya elimu. Walimu stadi hutumia hoja na mifano inayofaana na hali.—1 Yohana 5:20.

Kuwasaidia Wahudumu Wapya

15, 16. Kwa nini kuna uhitaji wa kuwazoeza wahudumu wapya?

15 Paulo hakuhangaikia tu kuboresha njia zake za kufundisha. Aliona pia uhitaji wa kuwazoeza na kuwatayarisha vijana, kama vile Timotheo na Tito, ili wawe wahudumu wenye matokeo. (2 Timotheo 2:2; 3:10, 14; Tito 1:4) Vivyo hivyo, leo kuna uhitaji mkubwa wa kuwazoeza wengine na wa kuzoezwa pia.

16 Katika mwaka wa 1914, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme 5,000 hivi ulimwenguni pote; leo, wapya 5,000 hivi hubatizwa kila juma! (Isaya 54:2, 3; Matendo 11:21) Wapya wanapoanza kushirikiana na kutaniko la Kikristo na kutaka kushiriki katika huduma, wanahitaji kuzoezwa na kuongozwa. (Wagalatia 6:6) Ni muhimu tutumie njia za Bwana Mkubwa, Yesu, tunapofundisha na kuwazoeza wanafunzi. *

17, 18. Tunaweza kuwasaidiaje wapya wawe na uhakika katika huduma?

17 Yesu hakutafuta umati wa watu na kuwaambia mitume wake waanze kuhubiri. Kwanza alikazia kwa nini kazi ya kuhubiri inahitajiwa kisha akawatia moyo waendelee kusali kuhusu huduma yao. Halafu akawapa mambo matatu muhimu: mwenzi wa kuhubiri naye, eneo, na ujumbe. (Mathayo 9:35-38; 10:5-7; Marko 6:7; Luka 9:2, 6) Tunaweza kufanya hivyo pia. Iwe tunamsaidia mtoto wetu, mwanafunzi mpya, au mtu fulani ambaye hajashiriki katika kazi ya kuhubiri kwa muda fulani, inafaa tujitahidi kuwazoeza kwa kutumia njia hiyo.

18 Wapya wanahitaji kusaidiwa sana ili wawe na uhakika wanapohubiri ujumbe wa Ufalme. Je, unaweza kuwasaidia kutayarisha mahubiri rahisi na yenye kuvutia kisha uwasaidie kufanya mazoezi? Mnapokuwa shambani, acha wajifunze kupitia mfano wako unapohubiri nyumba chache za kwanza. Unaweza kuiga mfano wa Gideoni, ambaye aliwaambia hivi wapiganaji wenzake: “Jifunzeni kwa kunitazama, nanyi fanyeni vivyo hivyo.” (Waamuzi 7:17) Kisha mruhusu mpya ashiriki. Wapongeze wapya kwa uchangamfu kwa jitihada zao, na inapofaa, waeleze kwa ufupi jinsi wanavyoweza kufanya maendeleo.

19. Umeazimia kufanya nini unapojitahidi ‘kutimiza kwa ukamili huduma yako’?

19 Ili ‘tutimize kwa ukamili huduma yetu,’ acheni tuazimie kubadili njia zetu za kuhubiri kupatana na hali mbalimbali za watu na kuwazoeza wahudumu wapya wafanye hivyo pia. Tunapofikiria umuhimu wa kusudi letu, yaani, kujulisha ujuzi juu ya Mungu ambao unawasaidia watu wapate wokovu, tunasadiki kwamba kuna faida kubwa kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote [tuwaokoe] wengine.”—2 Timotheo 4:5; 1 Wakorintho 9:22.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ili uone jinsi Paulo alivyoonyesha sifa hizo katika huduma yake, soma Matendo 13:9, 16-42; 17:2-4; 18:1-4; 19:11-20; 20:34; Waroma 10:11-15; 2 Wakorintho 6:11-13.

^ fu. 11 Vivyo hivyo, ili kueleza uhusiano mpya kati ya Mungu na “wana” wake waliotiwa mafuta kwa roho, Paulo alitumia wazo la kisheria lililojulikana sana na wasomaji wake katika Milki ya Roma. (Waroma 8:14-17) Kulingana na kitabu kimoja (St. Paul at Rome), “Waroma walikuwa na desturi ya kuwachukua watu wazima au watoto wa watu wengine na kuwafanya kuwa wana wao, nayo ilipatana sana na maoni yao kuhusu familia.”

^ fu. 16 Kwa sasa, kuna programu ya Mapainia Wasaidia Wengine katika makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova. Katika programu hiyo, wahudumu wa wakati wote wenye uzoefu huwazoeza na kuwasaidia wahubiri wasio na uzoefu mwingi.

Je, Unakumbuka?

• Tunaweza kumwiga Paulo katika huduma kwa njia gani?

• Ni maoni gani ambayo huenda tukahitaji kuyaondoa akilini?

• Tunaweza kufanyaje ujumbe wetu uwe wenye kujenga?

• Wahudumu wapya wanahitaji nini ili wawe na uhakika?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Mtume Paulo alikaza uangalifu, alibadilika kulingana na hali, na alitumia ubunifu alipohubiri na kufundisha

[Blabu katika ukurasa wa 31]

Yesu aliwapa wanafunzi wake mambo matatu muhimu: mwenzi wa kuhubiri naye, eneo, na ujumbe

[Picha katika ukurasa wa 28]

Paulo alifaulu kuwahubiria watu mbalimbali kwa kubadilika kulingana na hali

[Picha katika ukurasa wa 30]

Wahudumu wenye matokeo hufikiria utamaduni wa watu ambao wanahubiria

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wahudumu wenye ubunifu huwasaidia wapya wajitayarishe kwa ajili ya huduma