Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati

KITABU cha Pili cha Mambo ya Nyakati kinaanza wakati Sulemani anapotawala akiwa mfalme wa Israeli. Kitabu hicho kinamalizika kwa maneno haya ya Mfalme Mwajemi Koreshi kwa Wayahudi walio uhamishoni huko Babilonia: “[Yehova] mwenyewe amenipa utume nimjengee nyumba katika Yerusalemu, huko Yuda. Yeyote aliye katikati yenu ninyi watu wake wote, Yehova Mungu wake na awe pamoja naye. Basi apande na kwenda [Yerusalemu].” (2 Mambo ya Nyakati 36:23) Kitabu hicho kilichokamilishwa na kuhani Ezra mwaka wa 460 K.W.K., kinazungumzia matukio ya miaka 500 tangu mwaka wa 1037 K.W.K. hadi mwaka wa 537 K.W.K.

Amri ya Koreshi inawawezesha Wayahudi kurudi Yerusalemu na kurudisha ibada ya Yehova huko. Hata hivyo, miaka mingi utekwani huko Babiloni imesababisha matokeo mabaya. Wanaorudi kutoka uhamishoni hawajui historia ya taifa lao. Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati kinawapa Waisraeli hao muhtasari wa mambo yaliyotukia wakati wa wafalme wa ukoo wa Daudi. Sisi pia tunapendezwa na masimulizi hayo kwa sababu yanakazia baraka zinazotokana na kumtii Mungu wa kweli na matokeo ya kutomtii.

MFALME AMJENGEA YEH

OVA NYUMBA

(2 Mambo ya Nyakati 1:1–9:31)

Yehova anampa Mfalme Sulemani maombi ya moyo wake, yaani, hekima, ujuzi, pamoja na utajiri na heshima. Mfalme anamjengea Yehova nyumba yenye utukufu huko Yerusalemu, na watu wana ‘shangwe na wanachangamka moyoni.’ (2 Mambo ya Nyakati 7:10) Sulemani anakuwa “mkuu katika utajiri na hekima kuliko wafalme wengine wote wa dunia.”—2 Mambo ya Nyakati 9:22.

Baada ya kutawala Israeli kwa miaka 40, Sulemani ‘analala pamoja na mababu zake, na Rehoboamu mwana wake anaanza kutawala mahali pake.’ (2 Mambo ya Nyakati 9:31) Ezra hazungumzii kukengeuka kwa Sulemani kuhusiana na ibada ya kweli. Makosa anayotaja yanahusu tu jinsi mfalme anavyojipatia farasi wengi kutoka Misri bila kutumia hekima na kuoa binti ya Farao. Hivyo, mwandishi wa kitabu hicho anakazia sifa nzuri tu.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:14—Kwa nini ukoo wa fundi anayetajwa katika andiko hili ni tofauti na ukoo unaotajwa katika 1 Wafalme 7:14? Kitabu cha Kwanza cha Wafalme kinasema kwamba mama ya fundi huyo alikuwa “mwanamke mjane kutoka katika kabila la Naftali” kwa sababu alikuwa ameolewa na mwanamume wa kabila hilo. Hata hivyo, mwanamke huyo alikuwa wa kabila la Dani. Baada ya kifo cha mume wake, mwanamke huyo aliolewa na mwanamume wa Tiro, na fundi huyo akazaliwa kutokana na ndoa hiyo.

2:18; 8:10—Mistari hiyo inaonyesha kwamba idadi ya wasaidizi waliotumikia wakiwa waangalizi na wasimamizi wa kazi ya kulazimishwa ilikuwa 3,600 kuongeza 250, lakini andiko la 1 Wafalme 5:16; 9:23 linaonyesha kwamba idadi yao ilikuwa 3,300 kuongeza 550. Kwa nini idadi hizo zinatofautiana? Inaonekana tofauti hiyo inatokana na jinsi wasaidizi wanavyopangwa katika vikundi. Huenda ikawa kwamba Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati kinatofautisha kati ya wale 3,600 ambao hawakuwa Waisraeli na wale wasaidizi Waisraeli 250, huku Kitabu cha Kwanza cha Wafalme kikitofautisha kati ya wale wasimamizi wa kazi za kulazimishwa 3,300 na wale wasimamizi wakuu wa vyeo vya juu zaidi 550. Kwa vyovyote vile, jumla ya idadi ya wale waliotumikia wakiwa wasaidizi ilikuwa 3,850.

4:2-4—Kwa nini kiwakilishi cha ng’ombe-dume kilitumiwa katika ujenzi wa sehemu ya chini ya bahari ya kuyeyushwa? Katika Maandiko, ng’ombe-dume wanawakilisha nguvu. (Ezekieli 1:10; Ufunuo 4:6, 7) Kuchagua ng’ombe-dume kuwa kiwakilishi kulifaa kwa sababu ng’ombe-dume 12 wa shaba walitegemeza ile “bahari” kubwa, ambayo uzito wake ulikuwa kilogramu 30,000 hivi. Kutumia ng’ombe-dume kwa kusudi hilo hakukuvunja kwa vyovyote amri ya pili, ambayo ilikataza kutengeneza sanamu kwa ajili ya ibada.—Kutoka 20:4, 5.

4:5—Ni kiasi gani cha maji kingeweza kujaa katika bahari ya kuyeyushwa? Ilipojazwa, bahari hiyo ingeweza kutoshea vipimo elfu tatu vya bathi au lita 66,000 hivi. Hata hivyo, kwa kawaida maji yaliyokuwa ndani ya bahari hiyo yalifikia kipimo cha theluthi mbili hivi. Andiko la 1 Wafalme 7:26 linasema hivi: “[Bahari hiyo] ingeweza kuchukua vipimo elfu mbili [lita 44,000] vya bathi.”

5:4, 5, 10—Ni vyombo gani kutoka kwenye maskani ya kwanza vilivyopelekwa kwenye hekalu la Sulemani? Sanduku ndicho chombo kimoja tu kutoka katika hema la awali la mkutano ambacho kilihifadhiwa katika hekalu la Sulemani. Baada ya ujenzi wa hekalu, maskani ilitolewa Gibeoni hadi Yerusalemu na yaelekea iliwekwa huko.—2 Mambo ya Nyakati 1:3, 4.

Mambo Tunayojifunza:

1:11, 12. Ombi la Sulemani lilimthibitishia Yehova kwamba kupata hekima na ujuzi ndilo lililokuwa jambo muhimu kwa mfalme. Kwa kweli, sala zetu kwa Mungu hufunua yaliyo muhimu kwetu. Ni jambo la hekima kuchunguza yale tunayosema katika sala zetu.

6:4. Uthamini wa kutoka moyoni kwa ajili ya fadhili zenye upendo na wema wa Yehova unapaswa kutuchochea kumbariki Yehova, yaani, kumtukuza kwa upendo na shukrani.

6:18-21. Ingawa Mungu hawezi kutoshea katika jengo lolote lile, hekalu lilikuwa kituo cha ibada ya Yehova. Leo, Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova ni vituo vya ibada ya kweli katika jumuiya.

6:19, 22, 32. Yehova angeweza kusikiliza sala za watu wote—za mfalme na hata za watu wadogo zaidi katika taifa—hata mgeni aliyemkaribia kwa moyo mnyoofu. *Zaburi 65:2.

MFUATANO WA WAFALME KATIKA UKOO WA DAUDI

(2 Mambo ya Nyakati 10:1–36:23)

Ufalme ulioungana wa Israeli unagawanyika katika sehemu mbili, yaani, ufalme wa kaskazini wa makabila kumi na ufalme wa kusini wa makabila mawili ya Yuda na Benyamini. Makuhani na Walawi katika Israeli yote wanaonyesha ushikamanifu wao kwa agano la Ufalme badala ya kuonyesha ushikamanifu kwa taifa, nao wanamuunga mkono Rehoboamu mwana wa Sulemani. Miaka 30 hivi baada ya kumaliza ujenzi wa hekalu, hazina ya hekalu inaibwa.

Kati ya wafalme 19 ambao wanatawala baada ya Rehoboamu, 5 ni waaminifu, 3 wanaanza vizuri wakiwa waaminifu lakini baadaye wanakuwa wasio waaminifu, na mmoja anatubu na kuacha njia zake mbaya. Watawala wengine wote wanatenda yaliyo mabaya machoni pa Yehova. * Matendo ya wafalme watano ambao wanamtegemea Yehova yanakaziwa. Masimulizi yanayoeleza jinsi Hezekia alivyoanzisha tena huduma hekaluni na jinsi Yosia alivyofanya matayarisho kwa ajili ya Pasaka kuu yaliwatia moyo Wayahudi waliopendezwa na kurudishwa kwa ibada ya Yehova huko Yerusalemu.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

13:5—Maneno “agano la chumvi” yanamaanisha nini? Kwa sababu ya uwezo wake wa kuhifadhi, chumvi ilitumiwa kuwakilisha hali ya kudumu na ya kutoweza kuharibika. Hivyo, “agano la chumvi,” linamaanisha agano la kudumu.

14:2-5; 15:17—Je, Mfalme Asa aliondoa ‘mahali pote pa juu’? Yaelekea hakufanya hivyo. Huenda ikawa kwamba Asa aliondoa tu mahali pa juu palipohusiana na ibada ya miungu ya uwongo lakini si mahali pa juu ambapo watu walimwabudia Yehova. Huenda pia mahali pa juu palijengwa tena mwishoni mwa utawala wa Asa. Mwana wake Yehoshafati aliondoa mahali hapo. Kwa kweli, mahali pa juu hapakutoweka kabisa, hata wakati wa utawala wa Yehoshafati.—2 Mambo ya Nyakati 17:5, 6; 20:31-33.

15:9; 34:6—Kabila la Simeoni lilikuwa upande gani katika ule mgawanyo wa ufalme wa Israeli? Kwa kuwa lilipata urithi wa sehemu mbalimbali za eneo la Yuda, eneo la kabila la Simeoni lilikuwa katika ufalme wa Yuda na Benyamini. (Yoshua 19:1) Hata hivyo, kidini na kisiasa, kabila hilo liliunga mkono ufalme wa kaskazini. (1 Wafalme 11:30-33; 12:20-24) Hivyo, kabila la Simeoni lilihesabiwa pamoja na ufalme wa makabila kumi.

16:13, 14—Je, Asa aliteketezwa? La. “Mfukizo wa mazishi ulio mkubwa” unahusu, si kuteketekezwa kwa Asa, bali kufukiza manukato.

35:3—Yosia alilitoa wapi Sanduku takatifu ili kulileta katika hekalu? Biblia haisemi ikiwa Sanduku hilo liliondolewa mapema na mmojawapo wa wafalme waovu au ikiwa Yosia alilihamisha mahali pengine ili kulilinda wakati wa marekebisho makubwa ya hekalu. Baada ya siku za Sulemani, Sanduku linatajwa mara moja tu wakati Yosia alipolileta hekaluni.

Mambo Tunayojifunza:

13:13-18; 14:11, 12; 32:9-23. Tunajifunza kuhusu umuhimu wa kumtegemea Yehova.

16:1-5, 7; 18:1-3, 28-32; 21:4-6; 22:10-12; 28:16-22. Ushirikiano pamoja na watu wasiomwabudu Yehova au wasioamini una matokeo mabaya. Ni jambo la hekima kuepuka kujiingiza katika mambo ya ulimwengu.—Yohana 17:14, 16; Yakobo 4:4.

16:7-12; 26:16-21; 32:25, 26. Majivuno yalimfanya Mfalme Asa ajiendeshe vibaya katika miaka ya mwisho ya maisha yake. Roho ya majivuno ilimfanya Uzia aanguke. Hezekia alitenda bila hekima na labda kwa kiburi alipowaonyesha wajumbe kutoka Babiloni hazina yake. (Isaya 39:1-7) Biblia inaonya hivi: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.”—Methali 16:18.

16:9. Yehova huwasaidia wale ambao moyo wao ni kamili kumwelekea, na yuko tayari kutumia nguvu zake kwa faida yao.

18:12, 13, 23, 24, 27. Kama Mikaya, tunapaswa kuwa wenye uhodari na ujasiri kusema kumhusu Yehova na makusudi yake.

19:1-3. Yehova huona mema yaliyo ndani yetu hata tunapomkasirisha.

20:1-28. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataturuhusu tumpate tunapojinyenyekeza kwake ili atuongoze.—Methali 15:29.

20:17. Ili ‘tuone wokovu wa Yehova,’ tunapaswa ‘kusimama mahali petu’ kwa kuunga mkono Ufalme wa Mungu. Badala ya kushughulikia mambo sisi wenyewe, tunapaswa ‘kusimama tuli,’ huku tukimtegemea kabisa Yehova.

24:17-19; 25:14. Ibada ya sanamu ilikuwa mtego kwa Yehoashi na mwana wake Amazia. Leo, ibada hiyo inaweza pia kuwa yenye kushawishi, hasa inapoonyeshwa kupitia pupa au uzalendo.—Wakolosai 3:5; Ufunuo 13:4.

32:6, 7Sisi pia tunapaswa kuwa wenye ujasiri na nguvu kwa ‘kuvaa mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu’ na kuendelea na vita vya kiroho.—Waefeso 6:11-18.

33:2-9, 12, 13, 15, 16. Mtu anaonyesha toba ya kweli kwa kuacha mwenendo wake mbaya na kuazimia kutenda yaliyo sawa. Kupitia toba ya kweli, hata mtu ambaye alitenda maovu kama Mfalme Manase anaweza kupata rehema za Yehova.

34:1-3. Hali zozote mbaya za utotoni hazipaswi kutuzuia tusimjue Mungu na kumtumikia. Huenda uvutano mzuri ambao Yosia alikuwa nao wakati wa miaka yake ya utotoni ulitokana na Manase, babu yake aliyetubu. Uvutano wowote mzuri ambao huenda Yosia alipata ulitokeza matokeo mazuri hatimaye. Inaweza kuwa hivyo kwetu pia.

36:15-17. Yehova ni mwenye huruma na subira. Hata hivyo, subira na huruma zake zina mipaka. Ikiwa watu wanataka kuokolewa wakati Yehova atakapoleta mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo, ni lazima wakubali ujumbe wa Ufalme unaohubiriwa.

36:17, 22, 23. Sikuzote neno la Yehova hutimia.—1 Wafalme 9:7, 8; Yeremia 25:9-11.

Kitabu Kilimchochea Kuchukua Hatua

Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 34:33 linasema hivi: “Yosia akaondoa machukizo yote kutoka katika nchi zote za wana wa Israeli, naye akawafanya wote waliopatikana katika Israeli wachukue utumishi, wamtumikie Yehova Mungu wao.” Ni nini kilichomchochea Yosia kuchukua hatua hiyo? Wakati Shafani mwandishi alipomletea Mfalme Yosia kitabu cha Sheria ya Yehova kilichopatikana, Mfalme Yosia aliamuru kitabu hicho kisomwe kwa sauti kubwa. Yosia aliguswa moyo sana na yale aliyosikia hivi kwamba akaendeleza ibada safi kwa bidii katika maisha yake yote.

Kusoma Neno la Mungu na kutafakari yale tunayosoma kunaweza kutuchochea sana. Je, hukubali kwamba kutafakari masimulizi kuhusu wafalme katika ukoo wa Daudi kunatutia moyo kuiga vielelezo vya wale waliomtegemea Yehova na kuepuka mwenendo wa wale ambao hawakufanya hivyo? Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati kinatuchochea kujitoa kikamili kwa Mungu wa kweli na kubaki waaminifu kwake. Kwa kweli, ujumbe wa kitabu hicho uko hai na una nguvu.—Waebrania 4:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Maswali juu ya kuwekwa wakfu kwa hekalu na yale tunayoweza kujifunza kutokana na sala ya Sulemani katika pindi hiyo yanapatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2005, ukurasa wa 28-31.

^ fu. 24 Ili upate orodha ya mfuatano wa wafalme wa Yuda, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2005, ukurasa wa 12.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unajua ni kwa nini ng’ombe-dume waliokuwa katika sehemu ya chini ya bahari ya kuyeyushwa walikuwa kiwakilishi kinachofaa?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Ingawa Yosia hakupata msaada wa kutosha utotoni, alikua akawa mwaminifu kwa Yehova