Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimeazimia Kuendelea Kumtumikia Muumba Wangu

Nimeazimia Kuendelea Kumtumikia Muumba Wangu

Simulizi la Maisha

Nimeazimia Kuendelea Kumtumikia Muumba Wangu

LIMESIMULIWA NA CONSTANCE BENANTI

Mambo yalitukia haraka! Kwa muda wa siku sita tu, Camille, binti yetu mwenye umri wa miezi 22, alipata homa kali naye akafa. Nilihuzunika sana. Nilitamani kufa pia. Kwa nini Mungu aliruhusu jambo kama hilo? Nilichanganyikiwa.

WAZAZI wangu walikuwa wahamiaji kutoka Castellammare del Golfo, mji ulio huko Sicily, Italia. Walihamia New York City, ambako nilizaliwa mnamo Desemba 8, 1908. Familia yetu ilitia ndani baba yangu, mama yangu, na watoto wao wanane, yaani, wavulana watano na wasichana watatu. *

Mnamo 1927, baba yangu, Santo Catanzaro, alianza kuhudhuria mikutano ya kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Ndugu mmoja Mwitaliano, Giovanni De Cecca, aliyetumikia kwenye makao makuu (yanayoitwa Betheli) huko Brooklyn, New York, aliongoza mikutano mahali tulipoishi, karibu na New Jersey. Baada ya muda, Baba alianza kuhubiri na pia akaanza huduma ya wakati wote. Aliendelea na kazi hiyo hadi kifo chake mnamo 1953.

Mama alipokuwa kijana, alitaka sana kuwa mtawa wa kike, lakini wazazi wake hawakumruhusu kufanya hivyo. Mwanzoni, Mama alinikataza nisijiunge na Baba katika kujifunza Biblia. Hata hivyo, punde si punde niliona kwamba baba alikuwa amefanya mabadiliko. Sasa alikuwa mpole na mtulivu, na tulikuwa na amani nyingi nyumbani. Nilifurahia jambo hilo.

Wakati huohuo, nilikutana na Charles, mwanamume wa umri wangu aliyezaliwa huko Brooklyn. Familia yao, kama vile yetu, ilitoka Sicily. Punde si punde, tulianza kuchumbiana, na Baba aliporudi kutoka kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la mwaka wa 1931 huko Columbus, Ohio, tukafunga ndoa. Baada ya muda wa mwaka mmoja hivi, binti yetu Camille akazaliwa. Alipokufa, nilihuzunika sana. Siku moja, Charles aliniambia hivi huku akilia: “Camille alikuwa binti yangu pia. Kwa nini tusiendelee na maisha na kufarijiana?”

Tunakubali Kweli ya Biblia

Charles alinikumbusha kwamba Baba alizungumza kuhusu ufufuo alipotoa hotuba kwenye mazishi ya Camille. “Je, kweli unaamini katika ufufuo?” nikamwuliza.

Akajibu: “Bila shaka, ninaamini! Kwa nini tusitafute habari zaidi kuhusu yale ambayo Biblia inasema?”

Sikuweza kulala usiku huo. Saa kumi na mbili asubuhi, kabla Baba hajaondoka kwenda kazini, nilienda kumwona na kumwambia kwamba mimi na Charles tunataka kujifunza Biblia. Alifurahi sana naye akanikumbatia. Mama alikuwa bado kitandani akitusikiliza. Akaniuliza ni nini kilichotukia. Nikamjibu, “Hakuna. Mimi na Charles tumeamua tu kujifunza Biblia.”

Kisha akasema hivi: “Sote tunahitaji kujifunza Biblia.” Hivyo, sisi sote tukiwa watu 11, kutia ndani ndugu na dada zangu, tukaanza kujifunza pamoja tukiwa familia.

Kujifunza Biblia kulinifariji, na pole kwa pole niliacha kuchanganyikiwa na kuhuzunika nami nikapata tumaini. Mwaka mmoja baadaye, mnamo 1935, mimi na Charles tukaanza kuwafundisha wengine kweli za Biblia. Mnamo Februari 1937, baada ya kusikiliza hotuba kwenye makao makuu ya Brooklyn iliyofafanua maana ya Kimaandiko ya ubatizo wa maji, tulibatizwa pamoja na wengine wengi katika kidimbwi cha hoteli moja iliyokuwa karibu. Nilichukua hatua hiyo si kwa sababu tu nilitumaini siku fulani kumwona tena binti yangu, lakini pia kwa sababu nilitamani kumtumikia Muumba wangu ambaye nilipata kumjua na kumpenda.

Kuanza Huduma ya Wakati Wote

Lilikuwa jambo lenye kuchochea na kupendeza kuwaeleza wengine yale niliyojifunza, hasa kwa kuwa wakati huo wengi walikubali ujumbe wa Ufalme na kushiriki kuutangaza. (Mathayo 9:37) Mnamo 1941, mimi na Charles tukawa mapainia, kama Mashahidi wa Yehova wanavyowaita wahudumu wao wa wakati wote. Muda mfupi baadaye, tulinunua nyumba ya kukokotwa, kisha Charles akamwachia ndugu yangu Frank kiwanda cha kutengeneza suruali cha familia yetu. Baada ya muda, tulisisimuka kupokea barua iliyotujulisha kwamba tulikuwa tumewekwa rasmi kutumikia kama mapainia wa pekee. Kwanza kabisa, tulitumikia huko New Jersey, na baadaye tukatumwa katika Jimbo la New York.

Mnamo 1946, tulipokuwa tukihudhuria kusanyiko huko Baltimore, Maryland, tuliombwa tuhudhurie mkutano uliosimamiwa na wawakilishi wa pekee wa Mashahidi wa Yehova. Katika mkutano huo, tulikutana na Nathan H. Knorr na Milton G. Henschel. Walizungumza nasi kuhusu kazi ya umishonari, na hasa, kuhusu kazi ya kuhubiri huko Italia. Walituomba tufikirie uwezekano wa kuhudhuria Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead).

Walituambia hivi: “Fikirieni jambo hilo, kisha mtatujibu.” Baada ya kutoka ofisini, mimi na Charles tuliangaliana, tukaenda kando, nasi tukarudi tena moja kwa moja ofisini. Tukawaambia: “Tumefikiria jambo hilo. Tuko tayari kuhudhuria Shule ya Gileadi.” Siku kumi baadaye, tulikuwa tukihudhuria darasa la saba la Gileadi.

Hatukusahau mazoezi ambayo tulipata kwa miezi kadhaa. Jambo lililotupendeza hasa ni subira na upendo wa walimu, ambao walitutayarisha kukabiliana na matatizo katika nchi za kigeni. Baada ya kuhitimu mnamo Julai 1946, tulipewa mgawo wa kuhubiri kwa muda huko New York City, ambako kulikuwa watu wengi kutoka Italia. Kisha, siku yenye kusisimua ikafika! Mnamo Juni 25, 1947, tulienda Italia katika mgawo wetu wa umishonari.

Kuzoea Mgawo Wetu

Tulisafiri kwa meli ambayo ilitumiwa na wanajeshi zamani. Baada ya siku 14 baharini, tulifika kwenye bandari ya Italia ya Genoa. Jiji hilo liliathiriwa vibaya wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu ambavyo vilikuwa vimemalizika miaka miwili mapema. Kwa mfano, kituo cha garimoshi hakikuwa na vioo vya madirisha kwa sababu ya mashambulizi ya mabomu. Kutoka Genoa tulisafiri kwa garimoshi la kubeba mizigo hadi Milan, ambako kulikuwa na ofisi ya tawi na makao ya wamishonari.

Baada ya vita, hali ya maisha huko Italia ilikuwa mbaya sana. Jitihada za kurekebisha hali zilikuwa zikiendelea, lakini umaskini ulikuwa umeenea. Baada ya muda mfupi, nikawa mgonjwa sana. Daktari mmoja alisema kwamba nilikuwa na ugonjwa mbaya sana wa moyo na kwamba ingekuwa vizuri kwangu kurudi Marekani. Nafurahi kwamba alikuwa amekosea. Baada ya miaka 58, bado niko Italia katika mgawo wangu.

Tulikuwa tumetumikia tu kwa miaka michache katika mgawo wetu wakati ndugu zangu huko Marekani walipotaka kutupa gari. Hata hivyo, kwa fadhili, Charles alikataa zawadi hiyo. Nilifurahia uamuzi huo. Tulijua kwamba hakuna Shahidi huko Italia aliyekuwa na gari wakati huo, na Charles alihisi kwamba ilikuwa vizuri tuishi tu kama ndugu zetu Wakristo. Hatukuwa na gari mpaka mwaka wa 1961 tulipopata gari dogo.

Jumba letu la kwanza la Ufalme huko Milan lilikuwa katika chumba cha chini ya ardhi kilichokuwa na sakafu ya udongo. Hakukuwa na choo, na maji yalijaa sakafuni mvua iliponyesha. Pia, kulikuwa na panya wadogo waliokuwa wakikimbia huku na huku. Kulikuwa na taa mbili zilizotumiwa wakati wa mikutano. Licha ya hali hizo, ilitia moyo kuona watu wanyoofu wakihudhuria mikutano yetu na hatimaye kujiunga nasi katika huduma.

Mambo Tuliyojionea Tukiwa Wamishonari

Wakati mmoja tulimwachia mtu fulani kijitabu Peace—Can It Last? Tulipokuwa tukiondoka, mke wake, Santina, alifika akiwa amebeba mboga na matunda. Alikasirika sana, naye akasema kwamba alikuwa na mabinti wanane wanaohitaji kutunzwa na kwamba hakuwa na wakati wa kupoteza. Nilipomtembelea tena Santina, mume wake hakuwa nyumbani, na Santina alikuwa akifuma. Aliniambia hivi: “Sina wakati wa kukusikiliza. Zaidi ya hilo, sijui kusoma.”

Nilisali kwa Yehova kimya-kimya kisha nikamuuliza ikiwa ningemlipa pesa amfumie mume wangu nguo ya kujikinga na baridi. Majuma mawili baadaye, alinipa nguo hiyo, tukaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na Santina tukitumia kitabu “The Truth Shall Make You Free.” Santina alijifunza kusoma, na licha ya upinzani wa mume wake, alifanya maendeleo naye akabatizwa. Watano kati ya binti zake wakawa Mashahidi, na Santina amewasaidia wengine wengi kukubali kweli ya Biblia.

Mnamo Machi 1951, sisi pamoja na wamishonari wengine wawili, Ruth Cannon * na Loyce Callahan, ambaye baadaye aliolewa na Bill Wengert, tulihamishwa hadi Brescia, ambako hakukuwa na Mashahidi. Tulipata nyumba iliyokuwa na fanicha, lakini miezi miwili baadaye, mwenye nyumba alitupa saa 24 tuondoke. Kwa kuwa hakukuwa na Mashahidi wengine katika eneo hilo, tulilazimika kwenda hotelini, ambako tulikaa kwa muda wa miezi miwili hivi.

Hatungeweza kula vyakula vingi. Tulikunywa kahawa, tukala mikate, jibini, na matunda. Licha ya hali hizo, kwa kweli tulibarikiwa. Baada ya muda, tulipata nyumba ndogo, na kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 1952, watu 35 walihudhuria katika chumba kidogo tulichotumia kama Jumba la Ufalme.

Kukabiliana na Matatizo

Wakati huo, makasisi walikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu. Kwa mfano, tulipokuwa tukihubiri huko Brescia, wavulana fulani walichochewa na kasisi watutupie mawe. Hata hivyo, baada ya muda, watu 16 walianza kujifunza Biblia pamoja nasi, na baada ya muda mfupi wakawa Mashahidi. Na ni nani aliyekuwa miongoni mwao? Mmoja wa wale wavulana waliotisha kututupia mawe! Anatumikia sasa akiwa mzee katika mojawapo ya makutaniko ya Brescia. Tulipoondoka Brescia mwaka wa 1955, wahubiri 40 walikuwa wakishiriki katika kazi ya kuhubiri.

Baadaye, tulitumika kwa muda wa miaka mitatu huko Leghorn (Livorno), ambako karibu Mashahidi wote walikuwa wanawake. Hilo lilimaanisha kwamba sisi akina dada ndio tuliopaswa kushughulikia mambo ya kutaniko ambayo kwa kawaida hushughulikiwa na akina ndugu. Baadaye, tulihamia Genoa, ambako tulianzia utumishi wetu wa umishonari miaka 11 mapema. Wakati huo, kulikuwa na kutaniko moja. Jumba la Ufalme lilikuwa kwenye orofa ya kwanza katika jengo tulimokuwa tukiishi.

Punde tu tulipofika Genoa, nilianza kujifunza pamoja na mwanamke mmoja ambaye mume wake alikuwa mpiganaji wa ngumi zamani na msimamizi wa ukumbi wa michezo. Mwanamke huyo alifanya maendeleo ya kiroho na punde si punde akawa dada yetu. Hata hivyo, mume wake alimpinga kwa miaka mingi. Kisha, mwanamume huyo akaanza kuandamana na mke wake mikutanoni. Badala ya kuingia ndani ya jumba, aliketi nje na kusikiliza. Baadaye, tulipoondoka Genoa, tulisikia kwamba ameanza kujifunza Biblia. Baada ya muda, akabatizwa naye akawa mwangalizi Mkristo mwenye upendo. Aliendelea kuwa mwaminifu hadi kifo chake.

Pia, nilijifunza Biblia pamoja na mwanamke mmoja ambaye alikuwa akichumbiwa na polisi mmoja. Mwanzoni, polisi huyo alionyesha kwamba anapendezwa na ukweli kwa kadiri fulani, lakini baada ya arusi, akabadili mtazamo wake. Alimpinga mke wake, na mkewe akaacha kujifunza. Baadaye, alipoanza tena kujifunza Biblia, mume wake alimtisha na kumwambia kwamba atakapotukuta tukijifunza, atatuua. Hata hivyo, mwanamke huyo alifanya maendeleo ya kiroho naye akabatizwa na kuwa Shahidi. Mume wake hakutuua. Miaka mingi baadaye, nilipokuwa nikihudhuria kusanyiko huko Genoa, mtu fulani alikuja nyuma yangu, akanifumba macho kwa mikono yake, naye akaniuliza ikiwa ninaweza kumtambua. Sikuweza kujizuia kulia nilipomwona mume wa mwanamke huyo. Baada ya kunikumbatia, aliniambia kwamba alijiweka wakfu kwa Yehova na kwamba alikuwa amebatizwa siku hiyo!

Tangu mwaka wa 1964 hadi 1972, nilikuwa na pendeleo la kuandamana na Charles alipoyatembelea makutaniko ili kuyaimarisha kiroho. Tulitumikia karibu sehemu yote ya kaskazini ya Italia, yaani, Piedmont, Lombardy, na Liguria. Kisha, tukarudia utumishi wa painia karibu na Florence na baadaye huko Vercelli. Mnamo 1977, kulikuwa na kutaniko moja tu huko Vercelli, lakini tulipoondoka huko mwaka wa 1999, yalikuwa matatu. Mwaka huo, nilifikisha umri wa miaka 91, na tulitiwa moyo kuhamia kwenye nyumba ya wamishonari huko Roma, nyumba ndogo maridadi iliyo katika eneo lenye utulivu.

Jambo Lingine Lenye Kuhuzunisha

Mnamo Machi 2002, Charles ambaye sikuzote alikuwa mwenye afya nzuri, aliugua ghafula. Afya yake ilidhoofika hadi alipokufa mnamo Mei 11, 2002. Kwa muda wa miaka 71, tulilia pamoja nyakati za huzuni na kufurahi pamoja tulipopokea baraka. Kifo chake kilinihuzunisha sana.

Mara nyingi, ninamkumbuka Charles akiwa amevalia suti yake yenye safu mbili za vifungo na kofia yake ya miaka ya 1930. Ninakumbuka tabasamu yake, na ni kana kwamba ninasikia kicheko chake ambacho nilizoea kusikia. Kwa msaada wa Yehova na kupitia upendo wa ndugu na dada wengi wapendwa, nimeweza kuvumilia kipindi hiki chenye huzuni. Ninangojea kwa hamu nyingi wakati nitakapomwona Charles tena.

Naendelea na Utumishi Wangu

Kumtumikia Muumba wangu ndilo jambo muhimu zaidi maishani mwangu. Kwa miaka mingi, ‘nimeonja na kuona kwamba Yehova ni mwema.’ (Zaburi 34:8) Nimehisi upendo wake na kuona jinsi anavyonijali. Hata ingawa mtoto wangu alikufa, Yehova amenipa wana na mabinti wengi wa kiroho kotekote katika Italia ambao huniletea shangwe na kumfanya Yehova ashangilie pia.

Kuzungumza na wengine kuhusu Muumba wangu ndilo jambo ambalo sikuzote nimependa zaidi. Hiyo ndiyo sababu ninaendelea kuhubiri na kuongoza mafunzo ya Biblia. Nyakati nyingine ninasikitika kwamba siwezi kufanya mengi zaidi kwa sababu ya afya yangu. Hata hivyo, ninaelewa kwamba Yehova anajua mipaka yangu, ananipenda, na anathamini yale ninayoweza kufanya. (Marko 12:42) Ninajitahidi kuishi kulingana na maneno haya ya Zaburi 146:2: “Nitamsifu Yehova muda wote wa maisha yangu. Nitampigia Mungu wangu muziki maadamu nipo.” *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Simulizi la maisha la ndugu yangu Angelo Catanzaro lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1975 (Kiingereza), ukurasa 205-207, au Julai 15, 1975 (Kifaransa), ukurasa 429-431.

^ fu. 28 Ona simulizi lake la maisha katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1971 (Kiingereza), ukurasa 277-280 au Desemba 1, 1971 (Kifaransa), ukurasa 724-726.

^ fu. 41 Dada Benanti alikufa mnamo Julai 16, 2005, wakati makala hii ilipokuwa ikitayarishwa. Alikuwa na umri wa miaka 96.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Camille

[Picha katika ukurasa wa 14]

Siku ya arusi yetu, 1931

[Picha katika ukurasa wa 14]

Ingawa mwanzoni Mama hakupendezwa, alikubali kwamba sote tunapaswa kujifunza Biblia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Pamoja na Ndugu Knorr wakati wa kuhitimu Gileadi, 1946

[Picha katika ukurasa wa 17]

Pamoja na Charles muda mfupi kabla ya kifo chake