Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uthibitisho wa Upendo, Imani, na Utii

Uthibitisho wa Upendo, Imani, na Utii

Uthibitisho wa Upendo, Imani, na Utii

ASUBUHI ya Mei 16, 2005, hali ya hewa ilikuwa nzuri na kulikuwa na jua katika eneo la Watchtower Farms huko Wallkill, New York. Mvua ilikuwa imenyesha kabla ya mapambazuko na nyasi zilizokatwa vizuri na bustani za maua zilivutia sana. Bata mmoja na vifaranga wake wanane walikuwa wakiogelea kwa utulivu ndani ya maji karibu na ukingo wa kidimbwi. Wageni walistaajabia mandhari hiyo yenye kuvutia. Wageni hao walizungumza kwa sauti ya chini kana kwamba hawakutaka kuharibu utulivu huo wa asubuhi.

Wageni hao walikuwa Mashahidi wa Yehova waliotoka katika nchi 48. Lakini hawakuwa wamekuja kutazama mandhari hiyo. Walitaka kujua yaliyokuwa yakifanywa ndani ya jengo kubwa lililojengwa kwa matofali mekundu, ambalo ndilo jengo jipya zaidi katika Betheli ya Marekani huko Wallkill. Wakiwa ndani ya jengo hilo, walistaajabu tena kwa sababu ya kazi nyingi inayofanywa humo.

Kutoka kwenye orofa moja, wageni walitazama mashini mbalimbali. Mashini tano kubwa za kuchapishia zilikuwa juu ya sakafu ya saruji ambayo ni kubwa kuliko viwanja sita vikubwa vya mpira. Biblia, vitabu, na magazeti huchapishiwa huko. Makunjo makubwa ya karatasi huzunguka kama magurudumu ya gari kubwa linaloenda kwa kasi sana, na kila kunjo lina uzito wa kilogramu 1,700. Kila kunjo la karatasi lenye urefu wa kilometa 23 hukunjuka na kupita ndani ya mashini ya kuchapishia kwa dakika 25 tu. Wakati huo, mashini ya kuchapishia hutia na kukausha wino kisha hufanya karatasi ipoe ili iweze kukunjwa kama magazeti ambayo hupita juu ya mikanda ili yatiwe ndani ya makatoni na kusafirishwa kwenye makutaniko. Mashini nyingine huchapisha kurasa za vitabu zilizounganishwa pamoja, ambazo hupelekwa haraka kwenye chumba cha kuhifadhia ambako zinahifadhiwa hadi zinapotumwa ili ziunganishwe pamoja kutengeneza vitabu. Kazi hiyo yote huelekezwa kwa usahihi kwa kutumia kompyuta.

Baada ya hapo, wageni walitembelea sehemu ya kutia vitabu majalada. Katika sehemu hiyo, kwa siku moja mashini hutokeza nakala 50,000 za vitabu vyenye jalada gumu na Biblia zenye karatasi iliyopambwa kwa dhahabu. Mafungu ya kurasa hukusanywa kwa mpangilio mzuri, huunganishwa, kisha kingo zake hukatwa. Halafu, majalada huunganishwa. Vitabu huingizwa ndani ya makatoni. Kwa kutumia mashini, makatoni hayo hufungwa, hutiwa kibandiko, kisha hupangwa juu ya mbao za kusafirishia mizigo. Isitoshe, mashini ya kutokeza vitabu vyenye jalada nyepesi hukusanya na kupakia vitabu 100,000 hivi kwa siku. Mashini hiyo ina sehemu nyingi kama vile mota nyingi, mikanda, gia, na magurudumu na zote husonga kwa kasi sana ili kutokeza vichapo vya Biblia.

Mashini za kiwanda hicho cha uchapishaji ni za kisasa na za hali ya juu, nazo hufanya kazi kwa usahihi kabisa. Kama tutakavyoona, huo pia ni uthibitisho wa upendo, imani, na utii wa watu wa Mungu. Hata hivyo, kwa nini kazi ya uchapishaji ilihamishwa kutoka Brooklyn, New York, hadi Wallkill?

Sababu kuu ilikuwa kurahisisha kazi ya uchapishaji na usafirishaji wa vichapo kwa kuifanya mahali pamoja. Kwa miaka mingi, vitabu vilichapishiwa Brooklyn na kusafirishwa kutoka huko, na magazeti yalichapishiwa Wallkill na kusafirishwa kutoka huko. Kufanya kazi hizo mahali pamoja kungepunguza idadi ya wafanyakazi, na michango iliyotengwa kwa ajili ya kazi ya Mungu ingetumiwa vizuri zaidi. Isitoshe, kwa kuwa mashini za kuchapishia huko Brooklyn zilianza kuchakaa, mashini mpya mbili za kuchapishia (aina ya MAN Roland Lithoman) ziliagizwa kutoka Ujerumani. Mashini hizo zilikuwa kubwa sana na hazingeweza kutoshea katika kiwanda cha uchapishaji huko Brooklyn.

Yehova Ategemeza Kazi

Sikuzote, kusudi la kuchapisha vichapo limekuwa kuendeleza habari njema za Ufalme wa Mungu. Kuna uthibitisho kwamba Yehova amebariki kazi hiyo ya kuchapisha tangu ilipoanza. Tangu mwaka wa 1879 hadi 1922, vitabu vilichapishwa na mashirika ya kibiashara. Katika mwaka wa 1922, jengo lenye orofa sita lilikodishwa kwenye barabara ya 18 Concord Street huko Brooklyn na vifaa vya kuchapishia vitabu vikanunuliwa. Wakati huo, watu fulani walitilia shaka iwapo ndugu wangefaulu kufanya kazi hiyo.

Mmoja wa wale waliotilia shaka jambo hilo alikuwa msimamizi wa kampuni iliyokuwa ikichapisha vitabu vyetu. Alipotembea huko Concord Street, alisema hivi: “Mna kiwanda cha uchapishaji chenye mashini za hali ya juu, na hamna mtu anayejua jinsi ya kuzitumia. Baada ya miezi sita mashini zote hizi zitakuwa zimeharibika; na mtatambua kwamba watu ambao wamekuwa wakiwafanyia uchapishaji ndio tu wanaostahili kuifanya kazi hii kwa sababu wana ujuzi huo.”

Mwangalizi wa kiwanda cha uchapishaji wakati huo, Robert J. Martin, alisema hivi: “Maneno hayo yalionekana kuwa ya kweli, lakini aliyeyasema alimpuuza Bwana; na sikuzote Bwana amekuwa pamoja nasi. . . . Muda mfupi baadaye, tulianza kutengeneza vitabu.” Kwa miaka 80 iliyofuata, Mashahidi wa Yehova walichapisha mabilioni ya vichapo kwa kutumia mashini zao wenyewe.

Kisha mnamo Oktoba 5, 2002, katika mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, ilitangazwa kwamba Baraza Linaloongoza limekubali kuhamisha kazi ya uchapishaji ya ofisi ya tawi ya Marekani hadi Wallkill. Mashini mbili mpya zilikuwa zimeagizwa, nazo zilitazamiwa mnamo Februari 2004. Akina ndugu wangehitaji kuchora ramani ya ujenzi na kupanua kiwanda cha uchapishaji ili kiwe tayari baada ya miezi 15 kabla ya mashini hizo kufika. Kisha, kazi ya kutia vitabu majalada na kusafirisha ilihitaji kupangwa kwa muda wa miezi tisa iliyofuata. Huenda wengine walitilia shaka waliposikia kuhusu ratiba hiyo—kazi hiyo ilionekana kuwa nyingi sana na isiyowezekana. Hata hivyo, akina ndugu walijua kwamba ingewezekana kwa baraka za Yehova.

“Watu Walishirikiana kwa Furaha”

Wakijua kwamba watu wa Yehova wangejitoa kwa hiari, akina ndugu walianza mradi huo. (Zaburi 110:3) Kazi hiyo kubwa ilihitaji wafanyakazi wengi kuliko wale wa idara ya Betheli ya ujenzi. Akina ndugu na dada zaidi ya 1,000 walio na ustadi katika kazi ya ujenzi kutoka Marekani na Kanada walijitolea kutumika kati ya juma moja hadi miezi mitatu wakiwa wajitoleaji wa muda. Wengine ambao ni watumishi wa kimataifa na wajitoleaji walialikwa kushiriki katika mradi huo. Pia, Halmashauri za Ujenzi za Mikoa zilisaidia sana.

Wengi waliojitolea ili kufanya kazi katika mradi huo huko Wallkill walitumia pesa nyingi kusafiri na wakati mwingi ambao wangetumia katika kazi zao za kimwili. Hata hivyo, walifurahia kujidhabihu. Wanabetheli walipata nafasi ya kuunga mkono kazi hiyo kwa kuwapa makao na kuwalisha wajitoleaji hao wengi. Zaidi ya Wanabetheli 535 kutoka Brooklyn, Patterson, na Wallkill, walijitolea kufanya kazi kwenye mradi huo Jumamosi, licha ya kufanya kazi zao za kawaida katikati ya juma. Kazi ambayo watu wa Mungu walifanya kwa kuunga mkono mradi huo wa pekee ilifaulu tu kwa sababu Yehova aliitegemeza.

Wengine walitoa michango ya pesa. Kwa mfano, akina ndugu walipokea barua kutoka kwa msichana mwenye umri wa miaka tisa anayeitwa Abby. Aliandika hivi: “Nathamini sana kazi yote mnayofanya ya kutengeneza vitabu vizuri. Huenda nitawatembelea hivi karibuni. Baba yangu alisema tutakuja mwaka ujao! Nitavaa beji ili mnitambue. Ninatoa hizi dola 20 kuchangia mashini hizo mpya za kuchapishia! Ni pesa zangu za matumizi, lakini nataka kuwapa ninyi akina ndugu.”

Dada mmoja aliandika hivi: “Tafadhali pokeeni zawadi hii ya kofia nilizofuma kwa mikono yangu mwenyewe. Ningependa wafanyakazi wa mradi wa Wallkill wapewe kofia hizo. Kitabu fulani kinachozungumza kuhusu hali ya hewa kilisema kwamba kutakuwa na baridi kali sana. Sijui ikiwa habari hizo ni sahihi au si sahihi. Lakini ninajua kwamba kazi nyingi huko Wallkill zitafanywa nje, na ninataka kuhakikisha kwamba ndugu na dada zangu wamejikinga vichwa dhidi ya baridi. Sina ustadi wowote ambao unahitajiwa kwa ajili ya kazi hiyo, lakini ninaweza kufuma, hivyo, niliamua kutumia ustadi huo kufanya yale ambayo ningeweza.” Dada huyo alituma kofia 106!

Kiwanda cha uchapishaji kilikamilika kwa wakati. John Larson, mwangalizi wa kiwanda cha uchapishaji alisema hivi: “Watu walishirikiana kwa furaha. Hapana shaka kwamba Yehova alibariki kazi hiyo. Kazi ilifanywa haraka. Nakumbuka nikisimama kwenye matope mnamo Mei 2003 huku nikiwatazama akina ndugu wakiweka msingi wa jengo hilo. Mwaka mmoja hivi baadaye, nilisimama mahali palepale kutazama mashini ya kuchapishia ikifanya kazi.”

Programu ya Kuweka Wakfu

Programu ya kuweka wakfu kiwanda hicho kipya cha uchapishaji, pamoja na majengo matatu ya makao, ilifanywa huko Wallkill mnamo Jumatatu, Mei 16, 2005. Majengo ya Betheli ya Patterson na Brooklyn, pamoja na Betheli ya Kanada, yalipokea programu hiyo kupitia video. Kwa ujumla, watu 6,049 walifurahia programu hiyo. Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikuwa mwenyekiti naye alitoa historia fupi kuhusu kazi ya uchapishaji. Kupitia mahojiano na video, John Larson na John Kikot, ambao ni washiriki wa Halmashauri ya Tawi, walizungumzia historia ya kazi ya ujenzi na ya uchapishaji nchini Marekani. John Barr, ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya mwisho, na kuweka wakfu kwa Yehova Mungu kiwanda hicho kipya cha uchapishaji na majengo matatu ya makao.

Juma lililofuata, Wanabetheli kutoka Patterson na Brooklyn walipewa pendeleo la kutembelea majengo hayo mapya. Kwa ujumla, Wanabetheli 5,920 walitembea huko wakati huo.

Tunakionaje Kiwanda Hicho cha Uchapishaji?

Katika hotuba ya wakfu, Ndugu Barr aliwakumbusha wasikilizaji kwamba si mashini zinazofanya kiwanda hicho kiwe muhimu. Watu ndio muhimu. Vichapo tunavyochapisha hubadili sana maisha ya watu.

Kila moja ya mashini hizo mpya inaweza kuchapisha trakti milioni moja kwa saa moja hivi! Hata hivyo, trakti moja tu inaweza kubadili sana maisha ya mtu. Kwa mfano, mwaka wa 1921, kikundi cha mafundi wa reli huko Afrika Kusini, walikuwa wakifanya kazi kwenye reli moja. Mmoja wao, anayeitwa Christiaan, aliona kipande cha karatasi chini ya reli. Kumbe ilikuwa trakti yetu. Christiaan aliisoma kwa makini sana. Akaenda upesi kumwona mwana-mkwe wake na kumwambia hivi kwa furaha: “Leo nimepata kweli!” Punde baadaye, waliandika barua ili kupata habari zaidi. Ofisi ya tawi ya Afrika Kusini ilituma vichapo zaidi vya Biblia. Watu hao wawili walijifunza, wakabatizwa, nao wakawaeleza wengine kweli za Biblia. Kwa sababu hiyo, watu wengi walikubali kweli. Kufikia miaka ya mapema ya 1990, zaidi ya watu mia moja wa ukoo wao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Yote hayo yaliwezekana kwa sababu mtu mmoja alipata trakti moja kwenye reli!

Ndugu Barr alisema kwamba vichapo tunavyochapisha, huleta watu katika kweli, huwasaidia wadumu katika kweli, huwachochea waongeze bidii, na kuunganisha akina ndugu. Na zaidi ya yote, vichapo ambavyo sisi hugawanya, humtukuza Mungu wetu Yehova!

Yehova Anakionaje Kiwanda Hicho?

Pia, Ndugu Barr aliwaomba wasikilizaji wafikirie jinsi ambavyo Yehova anaona kiwanda hicho. Bila shaka, yeye hategemei kiwanda hicho. Anaweza kufanya mawe yahubiri habari njema! (Luka 19:40) Isitoshe, hashangazwi na utata, ukubwa, na uwezo wa mashini au muda ambao zinatumia kufanya kazi. Hiyo ni kwa sababu yeye ndiye aliyeumba ulimwengu! (Zaburi 147:10, 11) Yehova anajua njia bora zaidi za kuchapisha vichapo ambazo hazijawahi kubuniwa wala hata kuwaziwa na wanadamu. Hivyo, Yehova huona nini ambacho anakithamini sana? Kwa kweli, kupitia kiwanda hiki, Yehova anaona sifa nzuri za watu wake, upendo, imani, na utii wao.

Ndugu Barr alitoa mfano unaofuata kuonyesha jinsi upendo unavyohusika. Hebu wazia msichana akioka keki kwa ajili ya wazazi wake. Yaelekea wazazi wake watafurahia jambo hilo. Hata keki hiyo iweje, kile kinachowavutia wazazi ni upendo wa mtoto wao ambao umeonyeshwa kupitia ukarimu wake. Vivyo hivyo, Yehova anapotazama kiwanda hiki kipya, haoni tu majengo na mashini. Kwanza kabisa, anakiona kuwa uthibitisho wa upendo kwa ajili ya jina lake.—Waebrania 6:10.

Isitoshe, kama vile Yehova alivyoiona safina kuwa uthibitisho wa imani ya Noa, ndivyo anavyokiona kiwanda hiki kuwa uthibitisho wa imani yetu. Imani katika nini? Noa alikuwa na imani kwamba yale ambayo Yehova alitabiri, yangetimia. Tuna imani kwamba tunaishi katika siku za mwisho, kwamba habari njema ndiyo ujumbe muhimu zaidi unaotangazwa duniani, na ni muhimu watu wausikie. Tunajua kwamba ujumbe wa Biblia unaweza kuokoa maisha.—Waroma 10:13, 14.

Bila shaka, kupitia kiwanda hiki, Yehova anaona pia uthibitisho wa utii wetu. Kama tunavyojua, anataka habari njema ihubiriwe ulimwenguni pote kabla ya mwisho kuja. (Mathayo 24:14) Mashini zilizo katika kiwanda hiki pamoja na nyingine zilizopo katika maeneo mengine ulimwenguni, zitachangia kutimiza kazi hiyo.

Naam, upendo, imani, na utii unaoonyeshwa kupitia michango, ujenzi wa kiwanda hiki, na uendeshaji wa mashini hizo, unaonyeshwa pia na bidii ya watu wa Yehova kotekote wanapoendelea kutangaza kweli kwa watu wote wanaotaka kusikia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

MAENDELEO YA KAZI YA UCHAPISHAJI HUKO MAREKANI

1920: Magazeti yaanza kuchapishwa kwa mashini ya kwanza ya uchapishaji yenye mtambo unaozunguka huko 35 Myrtle Avenue, Brooklyn.

1922: Kiwanda cha uchapishaji kilihamishwa kwenye jengo lenye orofa sita huko 18 Concord Street. Vitabu vikaanza kuchapishwa.

1927: Kiwanda cha uchapishaji kilihamishwa kwenye jengo jipya huko 117 Adams Street.

1949: Orofa tisa nyingine zilijengwa na kufanya kiwanda cha uchapishaji kipanuke maradufu.

1956: Kiwanda cha uchapishaji huko Adams Street kilipanuliwa tena maradufu wakati jengo jipya lilipojengwa huko 77 Sands Street.

1967: Jengo la orofa kumi lilijengwa na kutokeza kiwanda cha uchapishaji kilichounganishwa ambacho kilikuwa kikubwa mara kumi zaidi ya jengo la awali.

1973: Kiwanda cha uchapishaji cha kazi ya ziada kilijengwa Wallkill, hasa kwa ajili ya kuchapisha magazeti.

2004: Kazi yote ya kuchapisha, kutia vitabu majalada, na ya kusafirisha huko Marekani, ilianza kufanywa huko Wallkill.