Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu “Kutoka Katika Lugha Zote” Wanasikia Habari Njema

Watu “Kutoka Katika Lugha Zote” Wanasikia Habari Njema

Watu “Kutoka Katika Lugha Zote” Wanasikia Habari Njema

“Watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa [watasema]: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’”—ZEKARIA 8:23.

1. Yehova alichaguaje wakati unaofaa na mahali panapofaa ili kuanzisha Ukristo na kazi ya kimataifa ya kuwahubiria watu wanaozungumza lugha mbalimbali?

WAKATI na mahali pa tukio hilo palifaa sana. Ilikuwa siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Majuma kadhaa mapema, Wayahudi na wageuzwa-imani kutoka maeneo 15 hivi ya Milki ya Roma na kwingineko walikuwa wamemiminika Yerusalemu ili kusherehekea Pasaka. Siku hiyo, maelfu kati yao walisikia watu wa kawaida ambao walijazwa roho takatifu wakitangaza habari njema katika lugha nyingi zilizozungumzwa katika milki hiyo, nao hawakufanya hivyo kwa sababu ya kuvurugika kama ilivyokuwa kwa watu walioishi katika Babeli ya kale, bali walielewana. (Matendo 2:1-12) Huo ulikuwa mwanzo wa kutaniko la Kikristo na mwanzo wa kazi ya kimataifa ya kuwahubiria watu wanaozungumza lugha mbalimbali ambayo inaendelea hata leo.

2. Wanafunzi wa Yesu ‘waliwashangazaje’ wasikilizaji kutoka maeneo mbalimbali wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?

2 Huenda wanafunzi wa Yesu walizungumza Kigiriki cha kawaida, lugha iliyotumiwa na watu wengi wakati huo. Pia walizungumza Kiebrania, lugha iliyotumiwa hekaluni. Hata hivyo, siku hiyo ya Pentekoste, watu kutoka maeneo mbalimbali “walishangaa” waliposikia wanafunzi wakizungumza lugha za asili za watu hao. Ikawaje? Mioyo ya wasikilizaji hao iliguswa na kweli muhimu walizosikia katika lugha zao za asili. Mwishoni mwa siku hiyo, kikundi kidogo cha wanafunzi kiliongezeka kufikia zaidi ya watu 3,000!—Matendo 2:37-42.

3, 4. Kazi ya kuhubiri iliongezekaje wakati wanafunzi walipohama Yerusalemu, Yudea, na Galilaya?

3 Muda mfupi baada ya tukio hilo la pekee, mateso makubwa yalitokea Yerusalemu na “wale waliokuwa wametawanywa wakapita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Matendo 8:1-4) Kwa mfano, katika Matendo sura ya 8 tunasoma kumhusu Filipo, mweneza-injili ambaye huenda alizungumza Kigiriki. Filipo aliwahubiria Wasamaria. Pia, alimhubiria ofisa Mwethiopia aliyeitikia ujumbe kumhusu Kristo.—Matendo 6:1-5; 8:5-13, 26-40; 21:8, 9.

4 Wakristo walipohama na kutafuta mahali ambapo wangeanza upya maisha yao nje ya maeneo ya Yerusalemu, Yudea, na Galilaya, walikabili vizuizi vingine vya kikabila na vya lugha. Huenda wengine wao waliwahubiria Wayahudi tu. Lakini mwanafunzi Luka anaripoti hivi: “Kulikuwa na wanaume fulani wa Kipro na Kirene waliokuja Antiokia na kuanza kuongea na watu wenye kusema Kigiriki, wakitangaza habari njema ya Bwana Yesu.”—Matendo 11:19-21.

Mungu Asiye na Ubaguzi Ana Ujumbe kwa Ajili ya Wote

5. Kupitia habari njema, tunajuaje kwamba Yehova hana ubaguzi?

5 Maendeleo hayo yanapatana na njia za Mungu; yeye hana ubaguzi. Baada ya mtume Petro kusaidiwa na Yehova kubadili maoni yake kuhusu watu wa mataifa, alisema hivi kwa uthamini: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35; Zaburi 145:9) Mtume Paulo, ambaye zamani aliwatesa Wakristo, alionyesha tena kwamba Mungu hana ubaguzi wakati alipotangaza kwamba “mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Tunatambua kwamba Muumba hana ubaguzi kwa sababu anatoa tumaini la Ufalme kwa watu wa jinsia zote, jamii zote, mataifa yote, na lugha zote.

6, 7. Ni unabii gani mbalimbali wa Biblia uliotabiri jinsi ambavyo habari njema ingehubiriwa kwa watu wa mataifa na lugha mbalimbali?

6 Ongezeko hilo la kimataifa lilitabiriwa karne nyingi mapema. Kulingana na unabii wa Danieli, Yesu ‘alipewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.’ (Danieli 7:14) Tunajua kwamba unabii huo wa Biblia unatimia kwa kuwa gazeti hili linachapishwa katika lugha 151 na kugawanywa ulimwenguni pote ili kukuwezesha usome kuhusu Ufalme wa Yehova.

7 Biblia ilitabiri kuhusu wakati ambapo watu wa lugha mbalimbali wangesikia ujumbe wake unaowawezesha kupata uhai. Zekaria alieleza jinsi ambavyo ibada ya kweli ingewavutia wengi, alipotabiri hivi: “Na itakuwa katika siku hizo kwamba watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi [Mkristo aliyetiwa mafuta kwa roho, ambaye ni sehemu ya “Israeli wa Mungu”], wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23; Wagalatia 6:16) Na mtume Yohana alisema hivi alipozungumzia yale ambayo aliona katika maono: “Tazama! umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:9) Tumeona unabii kama huo ukitimia!

Kuwahubiria Watu wa Namna Zote

8. Ni jambo gani linalotukia leo ambalo linatokeza uhitaji wa kufanya mabadiliko katika kazi yetu ya kuhubiri?

8 Leo, watu wengi zaidi wanahamia maeneo mapya. Jitihada za kusitawisha uchumi ulimwenguni pote zimewawezesha watu kuhamahama kuliko wakati mwingine wowote. Watu wengi kutoka katika maeneo ya vita na yenye matatizo ya kiuchumi wamehamia maeneo yenye hali nzuri za maisha ili wawe na maisha mazuri. Kwa sababu ya ongezeko la wahamiaji na wakimbizi katika nchi nyingi, kuna maeneo yenye watu wanaozungumza lugha za kigeni. Kwa mfano, lugha zaidi ya 120 huzungumzwa nchini Finland, na lugha zaidi ya 200 huzungumzwa huko Australia. Katika jiji la San Diego huko Marekani, lugha zaidi ya 100 huzungumzwa!

9. Tunapaswa kuwaonaje watu wanaozungumza lugha tofauti katika eneo letu?

9 Je, sisi wahudumu Wakristo huwaona watu wanaozungumza lugha tofauti kuwa kizuizi kwa huduma yetu? La hasha! Badala yake, sisi hufurahi kwa kuwa eneo letu la kuhubiri linaongezeka, naam, ‘mashamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.’ (Yohana 4:35) Sisi hujitahidi kuwashughulikia watu wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, licha ya taifa lao au lugha yao. (Mathayo 5:3) Ndiyo sababu kila mwaka watu wengi zaidi wa ‘kila lugha’ wanakuwa wanafunzi wa Kristo. (Ufunuo 14:6) Kwa mfano, kufikia Agosti 2004, kazi ya kuhubiri nchini Ujerumani ilikuwa ikifanywa katika lugha 40 hivi. Kufikia wakati huo pia, habari njema ilikuwa ikihubiriwa katika lugha 30 hivi huko Australia; na hilo ni ongezeko kwa sababu miaka kumi mapema habari njema ilihubiriwa katika lugha 18. Nchini Ugiriki, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiwahubiria watu katika lugha 20 hivi. Ulimwenguni pote, asilimia 80 hivi ya Mashahidi wa Yehova huzungumza lugha nyingine mbali na Kiingereza, ambayo ndiyo lugha kuu ya kimataifa.

10. Kila mhubiri ana daraka gani katika kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa “mataifa yote”?

10 Kwa kweli, amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ inatekelezwa! (Mathayo 28:19) Mashahidi wa Yehova wanatii utume huo kwa bidii katika nchi 235, huku wakigawanya vichapo katika lugha zaidi ya 400. Ingawa tengenezo la Yehova hutayarisha vichapo vinavyohitajiwa ili kuwahubiria watu, kila mhubiri wa Ufalme anahitaji kuchukua hatua ya kutangaza ujumbe wa Biblia kwa “watu wa namna zote” katika lugha ambayo wanaielewa vizuri. (Yohana 1:7) Jitihada zetu kwa ujumla huwawezesha mamilioni ya watu wanaozungumza lugha mbalimbali kufaidika na habari njema. (Waroma 10:14, 15) Naam, kila mmoja wetu hutimiza daraka muhimu!

Kukabili Kazi Ngumu

11, 12. (a) Ni hali gani ngumu ambazo tunahitaji kukabiliana nazo, na roho takatifu hutoa msaada gani? (b) Kwa nini mara nyingi inafaa kuwahubiria watu katika lugha yao ya asili?

11 Leo, wahubiri wengi wa Ufalme wangependa kujifunza lugha nyingine, lakini hawawezi kutegemea wala kutarajia zawadi za kimuujiza za roho ya Mungu. (1 Wakorintho 13:8) Kujifunza lugha mpya ni kazi ngumu. Huenda hata wale ambao tayari wanazungumza lugha nyingine wakahitaji kubadili maoni yao na njia zao za kuhubiri ili kufanya ujumbe wa Biblia uwavutie watu wanaozungumza lugha hiyo ambao wana malezi na utamaduni tofauti. Isitoshe, mara nyingi wahamiaji wapya huwa na haya na woga, hivyo jitihada nyingi zinahitajiwa ili kuelewa njia yao ya kufikiri.

12 Hata hivyo, bado roho takatifu inawaongoza watumishi wa Yehova katika jitihada zao za kuwasaidia watu wanaozungumza lugha tofauti. (Luka 11:13) Badala ya kutufundisha lugha kimuujiza, roho hiyo inaweza kukuza tamaa yetu ya kuwasiliana na watu ambao hawazungumzi lugha yetu. (Zaburi 143:10) Watu wanapohubiriwa au kufundishwa ujumbe wa Biblia katika lugha wasiyoielewa, ujumbe huo unaweza kufika akilini tu. Hata hivyo, ili kufikia mioyo ya watu tunaohubiria, mara nyingi inafaa kutumia lugha yao ya asili, yaani, lugha inayoweza kubadili tamaa zao za ndani, nia zao, na matumaini yao.—Luka 24:32.

13, 14. (a) Ni nini huwachochea wengine kuhubiri katika lugha nyingine? (b) Roho ya kujidhabihu huonyeshwaje?

13 Wahubiri wengi wa Ufalme wameamua kuhubiri katika maeneo yenye watu wanaozungumza lugha za kigeni wanapoona jinsi watu wanavyoitikia vizuri kweli ya Biblia. Wengine huimarishwa wanapokabili hali ngumu au hali zenye kufurahisha katika utumishi wao. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi moja iliyo kusini mwa Ulaya inasema hivi: “Watu wengi wanaohama Ulaya Mashariki wana kiu kwa ajili ya kweli.” Inaridhisha sana kuwasaidia watu kama hao wanaoitikia vizuri!—Isaya 55:1, 2.

14 Hata hivyo, ili kupata matokeo katika kazi hiyo, tunahitaji kuwa na nia na kujidhabihu. (Zaburi 110:3) Kwa mfano, familia kadhaa za Mashahidi huko Japani zimehama nyumba za starehe katika majiji makubwa na kuhamia maeneo ya mbali ili kusaidia vikundi vya wahamiaji Wachina kuelewa Biblia. Kwenye pwani ya magharibi ya Marekani, wahubiri huendesha gari kwa saa moja au mbili ili kuwafikia na kuwafundisha Biblia watu wanaozungumza Kifilipino. Huko Norway, wenzi fulani wa ndoa hujifunza pamoja na familia iliyotoka Afghanistan. Wenzi hao hutumia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? * ya Kiingereza na ya Kinorway. Familia hiyo husoma mafungu katika Kiajemi, ambayo ni lugha inayofanana sana na lugha yao ya asili inayoitwa Kidari. Mazungumzo hufanywa kwa Kiingereza na Kinorway. Roho hiyo ya kujidhabihu na ya kubadilika kulingana na hali hubarikiwa sana wakati wahamiaji wanapokubali habari njema. *

15. Sote tunaweza kufanya nini ili kushiriki katika kazi ya kuhubiri katika lugha nyingi?

15 Je, unaweza kushiriki katika kazi hiyo inayofanywa katika lugha nyingi? Unaweza kuanza kwa kuchunguza lugha za kigeni zinazotumiwa sana katika eneo lenu. Kisha unaweza kubeba trakti au broshua kadhaa katika lugha hizo. Kijitabu Good News for People of All Nations, kilichotolewa katika mwaka wa 2004, tayari kimesaidia sana katika kutangaza tumaini la Ufalme kwa sababu kina ujumbe rahisi na wenye kujenga katika lugha nyingi.—Ona makala yenye kichwa “Good News for People of All Nations,” kwenye ukurasa wa 32.

‘Kumpenda Mkaaji Mgeni’

16. Ndugu wenye madaraka wanaweza kuonyeshaje roho isiyo na ubinafsi wanapowasaidia watu wanaozungumza lugha ya kigeni?

16 Iwe tunajua au hatujui lugha nyingine, sote tunaweza kuwasaidia watu wa nchi za kigeni katika eneo letu wapate elimu ya kiroho. Yehova aliwaagiza watu wake ‘wampende mkaaji mgeni.’ (Kumbukumbu la Torati 10:18, 19) Kwa mfano, katika jiji moja kubwa huko Amerika Kaskazini, makutaniko matano hutumia Jumba moja la Ufalme. Kama inavyokuwa katika majumba mengi, saa za mikutano hubadilika kila mwaka. Jambo hilo lingesababisha mikutano ya Kichina ifanywe baadaye sana Jumapili, na lingewazuia wahamiaji wengi wanaofanya kazi katika mikahawa wasihudhurie. Hivyo, wazee wa makutaniko yale mengine walikubali kwa hiari kufanya marekebisho ili mikutano ya Kichina ianze mapema Jumapili.

17. Tunapaswa kuhisije wengine wanapoamua kuhama ili kusaidia kikundi kinachozungumza lugha nyingine?

17 Waangalizi wenye upendo huwapongeza akina ndugu na dada wanaostahili na wenye ustadi ambao wanataka kuhamia maeneo mengine ili kusaidia vikundi vya lugha nyingine. Ijapokuwa huenda kutaniko likawakosa sana walimu hao wa Biblia wenye uzoefu, waangalizi huwa na maoni kama yale ya wazee wa Listra na Ikoniamu. Ingawa Timotheo alitegemewa sana katika makutaniko yao, wazee hao hawakumzuia asisafiri pamoja na Paulo. (Matendo 16:1-4) Isitoshe, wale ambao wanaongoza kazi ya kuhubiri hawavunjwi moyo na maoni, desturi, au tabia tofauti za watu wa nchi za kigeni. Badala yake, wao hufurahia unamna-namna huo na hujitahidi kusitawisha mahusiano mazuri kwa ajili ya habari njema.—1 Wakorintho 9:22, 23.

18. Ni mlango gani mkubwa wa utendaji uliofunguliwa kwa wote?

18 Kama ilivyotabiriwa, habari njema inahubiriwa katika “lugha zote za mataifa.” Bado kuna uwezekano mkubwa wa kupata ongezeko katika maeneo yenye watu wanaozungumza lugha za kigeni. Maelfu ya wahubiri wenye ubunifu wameingia “mlango [huo] mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.” (1 Wakorintho 16:9) Lakini, kama makala inayofuata inavyoonyesha, mengi zaidi yanahitajiwa ili kuhubiri katika maeneo hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 14 Ili upate mifano mingine, ona makala yenye kichwa “Tumebarikiwa Sana kwa Kujidhabihu Katika Mambo Madogo,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 2004, ukurasa wa 24-28.

Je, Unaweza Kueleza?

• Tunaweza kumwigaje Yehova kwa kutowabagua watu?

• Tunapaswa kuwaonaje watu katika eneo letu ambao hawazungumzi lugha yetu?

• Kwa nini inafaa kuwahubiria watu katika lugha yao ya asili?

• Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali watu wa nchi za kigeni katika eneo letu?

[Maswali ya Funzo]

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Roma

KRETE

ASIA

FRIGIA

PAMFILIA

PONTO

KAPADOKIA

MESOPOTAMIA

EMEDI

PARTHIA

ELAMU

UARABU

LIBYA

MISRI

YUDEA

Yerusalemu

[Bodies of water]

Bahari ya Mediterania

Bahari Nyeusi

Bahari Nyekundu

Ghuba ya Uajemi

[Picha]

Mnamo Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., watu kutoka katika maeneo 15 ya Milki ya Roma na kwingineko walisikia habari njema katika lugha zao za asili

[Picha katika ukurasa wa 24]

Watu wengi kutoka nchi za kigeni hukubali kweli ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ishara ya Jumba la Ufalme katika lugha tano