Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Hubiri Kuachiliwa Huru kwa Mateka’

‘Hubiri Kuachiliwa Huru kwa Mateka’

‘Hubiri Kuachiliwa Huru kwa Mateka’

MWANZONI mwa huduma yake, Yesu alisema kwamba utume wake ungetia ndani “kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka.” (Luka 4:18) Kwa kufuata kielelezo cha Bwana wao, Wakristo wa kweli huhubiri habari njema ya Ufalme kwa “watu wa namna zote,” ili wawe huru kutokana na utumwa wa kiroho na kuboresha maisha yao.—1 Timotheo 2:4.

Leo, kazi hiyo inatia ndani kuwahubiria wafungwa halisi, yaani, watu ambao wamefungwa kwa sababu ya makosa mbalimbali na ambao wangependa kuwa huru kiroho. Furahia kusoma masimulizi haya yenye kutia moyo kuhusu kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri katika magereza ya Ukrainia na kwingineko Ulaya.

Waacha Kutumia Dawa za Kulevya na Kuwa Wakristo

Serhii, * mwenye umri wa miaka 38, amekuwa gerezani kwa miaka 20. Hata alikamilisha masomo yake gerezani. Anasema hivi: “Miaka kadhaa iliyopita, nilifungwa kwa sababu ya kuua na bado nitaendelea kuwa gerezani kwa miaka mingine zaidi. Nilikuwa mkatili gerezani, na wafungwa wengine waliniogopa.” Je, hilo lilifanya awe huru? Hapana. Kwa miaka mingi, Serhii alikuwa mtumwa wa dawa za kulevya, kileo, na tumbaku.

Kisha, mfungwa mwenzake akamweleza kuhusu kweli ya Biblia. Ilikuwa kama mwangaza gizani. Baada ya miezi michache, aliacha mazoea yake, akawa mhubiri wa habari njema, na akabatizwa. Serhii sasa ana shughuli nyingi gerezani akiwa mhudumu wa Yehova wa wakati wote. Amewasaidia wahalifu saba kubadili njia zao na kuwa ndugu zake wa kiroho. Sita kati yao wameachiliwa, lakini Serhii bado yuko gerezani. Hahuzuniki kwa sababu hiyo kwa kuwa anafurahi kwamba anaweza kuwasaidia wengine kupata uhuru wa kiroho.—Matendo 20:35.

Victor ni mmoja wa wanafunzi wa Serhii huko gerezani, ambaye zamani aliuza dawa za kulevya na alizoea kuzitumia. Baada ya kuachiliwa kutoka gerezani, Victor alifanya maendeleo ya kiroho na hatimaye akahitimu katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Ukrainia. Sasa yeye ni painia wa pekee huko Moldova. Victor anasema hivi: “Nilianza kuvuta sigara nikiwa na umri wa miaka 8, nikaanza kutumia kileo nikiwa na umri wa miaka 12, na nikaanza kutumia dawa za kulevya nikiwa na umri wa miaka 14. Nilitaka kubadili maisha yangu lakini jitihada zangu zote hazikufanikiwa. Halafu mwaka wa 1995, wakati mimi na mke wangu tulipokuwa tumepanga kuacha mashirika mabaya, mke wangu aliuawa kwa kudungwa kisu na mtu mwenye ugonjwa wa akili. Maisha yangu yaliharibika. ‘Mke wangu yuko wapi? Inakuwaje mtu anapokufa?’ Nilijiuliza maswali bila kupata majibu. Nilitumia dawa nyingi za kulevya ili kuepuka upweke. Nilikamatwa kwa kuuza dawa za kulevya na nikahukumiwa miaka mitano gerezani. Nikiwa huko, Serhii alinisaidia kupata majibu ya maswali yangu. Nilijaribu kuacha kutumia dawa za kulevya mara nyingi, lakini Biblia tu ndiyo iliyonisaidia kufanikiwa. Neno la Mungu lina nguvu sana!”—Waebrania 4:12.

Wahalifu Sugu Wabadilika

Vasyl hakutumia dawa za kulevya kamwe, lakini alifungwa gerezani. Anasema: “Nilipenda sana mchezo wa kupigana mateke na ngumi. Nilijizoeza kupiga watu ngumi bila kuwaacha na majeraha.” Vasyl alitumia jeuri kuwaibia watu. “Nilikuwa gerezani mara tatu, jambo ambalo lilimfanya mke wangu anitaliki. Wakati wa kifungo changu cha mwisho cha miaka mitano, nilipata vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Vilinichochea kusoma Biblia, lakini bado nilipenda sana kushiriki mchezo wa kupigana mateke na ngumi.

“Hata hivyo, baada ya kusoma Biblia kwa miezi sita, nilihisi badiliko fulani. Kushinda pigano hakukuniridhisha kama ilivyokuwa zamani. Hivyo, nikaanza kuchanganua maisha yangu kwa msingi wa andiko la Isaya 2:4 na nikatambua kwamba ikiwa sitabadili maoni yangu, nitatumia maisha yangu yote gerezani. Basi nikatupa vifaa vyangu vya kupigana na nikaanza kurekebisha utu wangu. Haikuwa rahisi, lakini kutafakari na kusali kulinisaidia hatua kwa hatua kuacha mazoea yangu mabaya. Wakati mwingine nilimlilia Yehova nikimwomba anipe nguvu za kuacha mazoea hayo. Hatimaye nikafaulu.

“Baada ya kutoka gerezani, niliungana na familia yangu. Sasa ninafanya kazi katika mgodi wa makaa ya mawe. Hivyo, ninakuwa na wakati wa kutosha kuhubiri na mke wangu na kutimiza majukumu yangu kutanikoni.”

Mykola na rafiki zake waliiba katika benki kadhaa nchini Ukrainia. Alifungwa gerezani kwa miaka kumi kwa sababu hiyo. Kabla ya kufungwa, alikuwa ameenda kanisani mara moja tu, ili kupanga kuiba katika kanisa hilo. Hakufanikiwa, lakini kwenda huko kulimfanya Mykola aamini kwamba Biblia ina hadithi nyingi zenye kuchosha kuhusu makasisi wa Kanisa Othodoksi, mishumaa, na sikukuu za kidini. Anasema hivi: “Nilianza kusoma Biblia ingawa sikujua kilichonifanya niisome. Nilishangaa kugundua kwamba haikuwa vile nilivyofikiria!” Alianza kujifunza Biblia na akabatizwa mwaka wa 1999. Ukimwona leo, huwezi kuamini kwamba mtumishi huyo wa huduma mnyenyekevu aliwahi kuwa mwizi hatari wa benki anayetumia silaha!

Vladimir alihukumiwa kifo. Akingoja kuuawa, alisali kwa Mungu na kuahidi kumtumikia iwapo hatauawa. Wakati huohuo, sheria ilibadilishwa na hukumu yake ikapunguzwa naye akahukumiwa kifungo cha maisha gerezani. Ili kutimiza ahadi yake, Vladimir alianza kutafuta dini ya kweli. Alijiandikisha ili apate elimu kupitia barua, naye akapata diploma katika kanisa la Waadventisti, lakini hakuridhika.

Hata hivyo, baada ya kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika maktaba ya gereza, Vladimir aliiandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ukrainia akiomba atembelewe. Ndugu wa eneo hilo walipomtembelea, tayari alikuwa anajiona kuwa Shahidi na alikuwa akihubiri gerezani. Alisaidiwa kufanya maendeleo na kuwa mhubiri wa Ufalme. Kufikia wakati makala hii ilipokuwa ikiandikwa, Vladimir na wengine saba katika gereza hilo walikuwa wakingoja kubatizwa. Lakini wana tatizo. Kwa kuwa wafungwa wa dini ileile ambao wamehukumiwa kifungo cha maisha huwekwa katika chumba kimoja cha gereza, Vladimir na wafungwa wenzake wenye imani yake wanaishi katika chumba kimoja. Basi watamhubiria nani? Wao huwahubiria walinzi wa gereza, nao huhubiri pia kupitia barua.

Nazar alihamia Jamhuri ya Cheki kutoka Ukrainia, naye akajiunga na kundi la wezi. Kwa sababu hiyo, alifungwa miaka mitatu na nusu gerezani. Akiwa gerezani, alikubali ujumbe wa Mashahidi wa Yehova waliotoka jiji la Karlovy Vary, akajifunza kweli na kubadilika kabisa. Baada ya kuona mabadiliko hayo, mlinzi mmoja aliwaambia wafungwa wengine hivi: “Kama nyote mngekuwa kama mtu huyo wa Ukrainia, ningebadili kazi.” Mwingine alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova ni wataalamu kweli. Mtu huja gerezani akiwa mhalifu; lakini huondoka akiwa mtu mzuri.” Sasa Nazar amerudi nyumbani. Alijifunza useremala na akaoa. Sasa yeye na mke wake ni watumishi wa wakati wote. Anashukuru sana kwamba Mashahidi walimtembelea gerezani!

Kutambuliwa Rasmi

Si wafungwa tu wanaofurahia kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova. Miroslaw Kowalski, msemaji wa mojawapo ya magereza ya Poland, alisema hivi: “Tunathamini sana ziara zao. Baadhi ya wafungwa wametoka katika mazingira mabaya sana. Huenda hawakuwahi kutendewa kama wanadamu. . . . Tunathamini msaada huo [wa Mashahidi] kwa sababu hatuna wafanyakazi na walimu wa kutosha.”

Msimamizi wa gereza lingine huko Poland aliiandikia ofisi ya tawi, akiwaomba Mashahidi watembelee gereza lao mara nyingi zaidi. Kwa nini? Alieleza hivi: “Ziara zaidi za wawakilishi wa Mnara wa Mlinzi zinaweza kuwasaidia wafungwa kusitawisha sifa nzuri, na kupunguza jeuri miongoni mwao.”

Gazeti moja la Ukrainia liliripoti kuhusu mfungwa mmoja aliyekuwa ameshuka moyo na ambaye alikuwa amejaribu kujiua lakini akasaidiwa na Mashahidi wa Yehova. Ripoti hiyo inasema: “Kwa sasa mtu huyo anaendelea kupata nafuu. Yeye hutii maagizo ya gereza na anawawekea wafungwa wengine kielelezo kizuri.”

Faida Zaendelea Hata Baada ya Kuwekwa Huru

Kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova haiwi na faida gerezani tu. Wafungwa huendelea kufaidika hata baada ya kuwekwa huru. Kwa miaka kadhaa, Wakristo wawili, Brigitte na Renate, wamekuwa wakiwasaidia wafungwa. Gazeti moja la Ujerumani (Main-Echo Aschaffenburg) liliripoti hivi kuwahusu: “Wao huwatunza wafungwa kwa miezi mitatu hadi mitano baada ya kuachiliwa, wakiwatia moyo kutafuta kusudi maishani. . . . Wanatambuliwa rasmi kuwa maofisa waliojitolea kuchunguza tabia za wakosaji. . . . Pia wanashirikiana vizuri na wafanyakazi wa gereza.” Watu wengi wamejiweka wakfu kwa Yehova kwa sababu ya msaada kama huo.

Hata wafanyakazi wa gereza hufaidika kutokana na elimu ya Biblia inayotolewa na Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, Roman alikuwa meja wa jeshi na pia mtaalamu wa akili katika gereza moja huko Ukrainia. Mashahidi walipomtembelea, alikubali kujifunza Biblia. Kisha akatambua kwamba Mashahidi hawakuruhusiwa kuwatembelea wafungwa mahali alipofanya kazi. Basi alimwomba ruhusa msimamizi wa gereza ili atumie Biblia anapofanya kazi na wafungwa. Aliruhusiwa kufanya hivyo, na karibu wafungwa kumi walipendezwa. Roman alishiriki ujuzi wake wa Biblia ulioongezeka pamoja na wafungwa hao, na alifanikiwa sana katika jitihada zake. Baada ya kuachiliwa, baadhi yao walifanya maendeleo, wakawa Wakristo waliobatizwa. Baada ya kuona nguvu ya Neno la Mungu, Roman alichukua funzo lake kwa uzito zaidi. Aliacha jeshi na kuendelea na elimu ya Biblia. Sasa yeye huhubiri pamoja na mwingine aliyekuwa mfungwa.

Mfungwa mmoja aliandika hivi: “Hapa, sisi hutegemezwa na Biblia, vichapo vya Biblia, na kujifunza Biblia.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba baadhi ya magereza yanahitaji sana vichapo vya Biblia. Kutaniko moja huko Ukrainia linaripoti hivi kuhusu kazi ya kufundisha watu Biblia katika gereza moja: “Wasimamizi wanathamini vichapo tunavyowapelekea. Sisi huwapelekea nakala 60 za kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni!” Kutaniko lingine liliandika: “Tunashughulikia gereza lenye maktaba ndogo 20. Tuliweka vitabu vyetu vya msingi katika kila maktaba. Hiyo ilikuwa jumla ya makatoni 20 ya vichapo.” Katika gereza moja, walinzi huhifadhi magazeti yetu katika maktaba ili wafungwa wafaidike na kila toleo.

Mwaka wa 2002, ofisi ya tawi ya Ukrainia ilianzisha Idara ya Kuwashughulikia Wafungwa. Kufikia sasa, idara hiyo imewasiliana na magereza 120 hivi, na makutaniko mbalimbali yamepewa migawo ya kuyashughulikia. Kila mwezi, ofisi hiyo inapokea karibu barua 50 kutoka kwa wafungwa, na wengi wao huomba vichapo au funzo la Biblia. Kabla ya ndugu wa eneo lao kuwatembelea, ofisi ya tawi huwatumia vitabu, magazeti, na broshua.

Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Wakumbukeni wale walio katika vifungo vya gereza.” (Waebrania 13:3) Alikuwa anazungumzia wale waliofungwa kwa sababu ya imani yao. Leo, Mashahidi wa Yehova huwakumbuka wafungwa, hutembelea magereza, na “kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka.”—Luka 4:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ukuta wa gereza la huko L’viv, Ukrainia

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mykola

[Picha katika ukurasa wa 10]

Vasyl akiwa na mke wake, Iryna

[Picha katika ukurasa wa 10]

Victor