Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Majira ya Sikukuu Yatapatana na Matarajio Yako?

Je, Majira ya Sikukuu Yatapatana na Matarajio Yako?

Je, Majira ya Sikukuu Yatapatana na Matarajio Yako?

“Peter [Mkuu] aliamuru ibada ya pekee ya Mwaka Mpya ifanywe katika makanisa yote mnamo Januari 1. Isitoshe, aliagiza kwamba matawi ya kijani kibichi yatumiwe kupamba miimo ya milango ya ndani ya nyumba, na akaamuru kwamba raia wote wa Moscow wanapaswa ‘kuonyesha furaha yao kwa kupongezana kwa sauti’ wakati wa Mwaka Mpya.”—Peter the Great—His Life and World.

UNATARAJIA nini wakati wa kile kipindi ambacho watu wengi hukiita majira ya sikukuu? Ulimwenguni pote watu husema kwamba jambo kuu wakati wa majira hayo ni Krismasi, ambayo kwa kawaida huonwa kuwa siku ya kuzaliwa kwa Kristo, lakini majira hayo yanatia ndani pia sikukuu ya Mwaka Mpya. Hivyo, ni kipindi kirefu cha sikukuu. Huenda wazazi na watoto wakawa likizoni wakati huo, hivyo, huo unaweza kuwa wakati mzuri kwa familia kuwa pamoja. Hata hivyo, wengine huyaita majira hayo “majira ya Krismasi,” kwa sababu wanatamani kumtukuza Kristo wakati huo wa mwaka. Huenda wewe pia ukaona hilo kuwa jambo muhimu zaidi wakati wa majira hayo.

Iwe ni kumtukuza Kristo, au kufurahia kuwa pamoja na familia, mamilioni ya waume, wake, na watoto ulimwenguni pote hutazamia majira hayo kwa hamu nyingi. Namna gani mwaka huu? Je, majira hayo yatakuwa wakati wa pekee kwa familia, na je, ni majira ya pekee kwa Mungu? Ikiwa mtakuwa na karamu ya familia, je, itapatana na matarajio yako, au utakatishwa tamaa?

Wengi wanaotarajia majira ya Krismasi na Mwaka Mpya kwa sababu za kidini, hutambua kwamba mara nyingi watu hawaonyeshi mtazamo wa Kristo katika sherehe hizo. Badala yake, majira hayo huwa pindi za kupokea zawadi tu, kufanya karamu ambazo huenda zikahusisha mienendo isiyomtukuza Kristo, au kuwa tu pamoja na familia. Mara nyingi, wakati wa karamu kama hizo watu wanaweza kula na kunywa kupindukia na kuchochea ugomvi ambao mara nyingi husababisha jeuri katika familia. Huenda umeona hivyo au hata umewahi kuwa katika hali hiyo.

Ikiwa ndivyo, huenda basi ukaona kwamba mambo hayajabadilika sana tangu wakati wa mtawala wa Urusi, Peter Mkuu, aliyetangulia kutajwa. Watu wengi ambao hawapendi jinsi mambo yanavyofanywa leo hutamani majira ya sikukuu yawe wakati wa kutafakari kwa uzito kuhusu mambo ya dini na kushirikiana pamoja na familia kwa njia inayofaa. Baadhi yao hata hupigania mabadiliko wakitumia mwito kama huu, Majira haya ya sikukuu ni kwa ajili ya Yesu. Lakini je, kunaweza kuwa na badiliko? Na je, hilo kwa kweli litamletea Kristo heshima? Je, kuna sababu za kuwa na maoni tofauti kuhusu majira hayo ya sikukuu?

Ili kupata majibu yenye kuridhisha, acheni tuzungumzie hali hiyo tukifikiria maoni ya watu wa taifa moja ambao wana sababu za pekee za kuthamini majira hayo.