Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Wachina Huko Mexico

Kuwasaidia Wachina Huko Mexico

Kuwasaidia Wachina Huko Mexico

“WATU kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23) Leo, unabii huo wenye kupendeza unatimizwa ulimwenguni pote. Watu “kutoka katika lugha zote za mataifa” wanashikamana na Waisraeli wa kiroho ili kumwabudu Yehova Mungu. Mashahidi wa Yehova wanapendezwa sana kuona unabii huo ukitimia. Wengi wao wanajifunza lugha nyingine ili wafanye kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.

Mashahidi wa Yehova nchini Mexico wanafanya hivyo pia. Watu wapatao 30,000 wanaozungumza Kichina wanaishi nchini Mexico. Mnamo mwaka wa 2003, 15 kati yao walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo uliofanyiwa Mexico City. Hivyo, Mashahidi huko Mexico walitambua kwamba kuna uwezekano wa ukuzi wa kiroho katika eneo la watu wanaozungumza Kichina. Ili wahubiri wengi zaidi waweze kuwasaidia watu hao wanaozungumza Kichina, masomo ya miezi mitatu yalianzishwa ili kuwafundisha Mashahidi huko Mexico jinsi ya kuhubiri kwa njia rahisi katika Kichina cha Mandarin. Mashahidi 25 walipata masomo hayo. Masomo hayo yalipomalizika, ofisa mmoja wa jamii ya watu wanaozungumza Kichina cha Mandarin huko Mexico City alihudhuria sherehe ya kuhitimu, na hilo lilionyesha jinsi watu wanaozungumza Kichina walivyochochewa na masomo hayo. Taasisi moja ya Kichina katika eneo hilo iliwafadhili wanafunzi watatu ili waende katika nchi nyingine kupata masomo yatakayowawezesha kujua Kichina vizuri zaidi.

Masomo hayo ya lugha yalitia ndani mazoezi. Baada ya kujifunza sentensi chache za msingi, wanafunzi walianza kuhubiri kwa Kichina katika eneo la biashara la Mexico City. Wanafunzi hao wenye bidii walianzisha mafunzo ya Biblia 21. Broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? katika Kichina iliyo na maandishi yenye herufi za Kiroma, zinazoitwa Pinyin, ilisaidia sana.

Mashahidi waliokuwa wameanza tu kujifunza Kichina walifanikiwaje kuongoza mafunzo ya Biblia? Mwanzoni, walisema tu, “Qing Du [Tafadhali soma]” na kuonyesha fungu, kisha swali. Mtu aliposoma fungu na kujibu katika Kichina, walisema, “Shei shei [Asante]” na, “Hen Hao [Vema sana].”

Funzo la Biblia lilianzishwa kwa njia hiyo pamoja na mwanamke aliyedai kuwa Mkristo. Baada ya kujifunza pamoja naye mara ya tatu, Shahidi huyo alikuwa na shaka ikiwa mwanamke huyo anaelewa kabisa habari hizo. Hivyo, Shahidi huyo aliandamana pamoja na ndugu mwenye asili ya Kichina. Shahidi huyo alipomuuliza mwanamke huyo ikiwa ana maswali yoyote, mwanamke huyo aliuliza: “Ili nibatizwe, je, ninahitaji kujua kuogelea?”

Muda mfupi baadaye, Funzo la Kitabu la Kutaniko lilianzishwa, na kwa wastani watu 9 wanaozungumza Kichina na Mashahidi 23 ambao ni wenyeji wa Mexico walihudhuria. Mmoja wa wale waliohudhuria ni daktari Mchina, ambaye alipokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika Kihispania kutoka kwa mgonjwa wake mmoja. Kwa kuwa hakujua kusoma Kihispania, alimwomba mtu fulani amtafsirie sentensi chache. Alipotambua kwamba magazeti hayo yanazungumzia Biblia, alimuuliza mgonjwa huyo ikiwa anaweza kupata magazeti hayo katika Kichina. Mgonjwa huyo alipata magazeti hayo, na kupitia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico, mipango ilifanywa ili Shahidi anayezungumza Kichina amtembelee. Mama yake huko China alikuwa na Biblia, na daktari huyo alikuwa amefurahia kuisoma. Alipoamua kwenda Mexico, mama yake alimwambia asiache kusoma Biblia. Hivyo, alikuwa akisali apate mtu wa kumsaidia kujifunza zaidi kuhusu Mungu wa Biblia. Alisema hivi: “Mungu amesikiliza sala yangu!”

Wengine waliohudhuria funzo hilo la kitabu ni familia moja ya Kichina iliyokodisha nyumba ya mwanamke mmoja wa Mexico ambaye alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ingawa watu wa familia hiyo ya Kichina hawakujua sana Kihispania, walikuwa wakisikiliza mazungumzo hayo ya Biblia. Baada ya muda, familia hiyo ilimuuliza Shahidi aliyeongoza funzo hilo ikiwa ana vichapo vyovyote vya Kichina. Punde si punde wakaanza kujifunza Biblia katika Kichina. Baada ya muda, familia hiyo ilisema kwamba ingependa kuwahubiria wenzao na kujiweka wakfu kwa Yehova.

Ni kweli kwamba ni vigumu kujifunza Kichina. Hata hivyo, kama masimulizi hayo yanavyoonyesha, kwa msaada wa Yehova watu wanaozungumza lugha mbalimbali, kutia ndani Kichina, wanajifunza mapenzi ya Mungu huko Mexico, na vilevile katika sehemu nyingine za dunia.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Darasa la Kichina huko Mexico City

[Picha katika ukurasa wa 18]

Shahidi Mmexico anaongoza funzo la Biblia katika Kichina

[Picha katika ukurasa wa 18]

Huduma ya nyumba kwa nyumba ikifanywa katika Kichina, huko Mexico City