Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matatizo ya Kutafsiri Biblia ya Kiitaliano

Matatizo ya Kutafsiri Biblia ya Kiitaliano

Matatizo ya Kutafsiri Biblia ya Kiitaliano

“BIBLIA ni kati ya vitabu vilivyoenezwa sana katika nchi yetu [Italia], lakini pia ni miongoni mwa vitabu visivyosomwa sana. Wakatoliki hawatiwi moyo kuijua Biblia wala hawapewi msaada wa kuisoma ikiwa Neno la Mungu. Kuna wale wanaotaka kuijua Biblia lakini hakuna mtu wa kuwafundisha.”

Taarifa hiyo iliyosemwa katika Mkutano wa Maaskofu wa Italia mwaka wa 1995, hutokeza maswali kadhaa. Biblia ilisomwa kwa kadiri gani nchini Italia katika karne zilizopita? Kwa nini haikuenezwa sana kama katika nchi nyingine? Kwa nini bado ni miongoni mwa vitabu visivyosomwa sana nchini Italia? Baadhi ya maswali hayo yatajibiwa baada ya kuchunguza historia ya tafsiri za Biblia katika Kiitaliano.

Karne nyingi zilipita kabla ya lugha zilizotokana na Kilatini, kama vile, Kifaransa, Kihispania, Kiitaliano, Kireno, na kadhalika, kusitawi. Katika nchi mbalimbali za Ulaya zilizotumia Kilatini, lugha za kienyeji zilianza kuheshimiwa pole kwa pole na hata kutumiwa katika vitabu. Kusitawi kwa lugha za kienyeji kulikuwa na matokeo katika kutafsiri Biblia. Jinsi gani? Wakati fulani, Kilatini, ambacho kilitumiwa na Kanisa Katoliki, kilitofautiana sana na lugha za kienyeji zenye lahaja na matamshi mbalimbali hivi kwamba hakikueleweka na watu ambao hawakuwa na elimu.

Kufikia mwaka wa 1000, wakaaji wengi wa peninsula ya Italia hawangeweza kusoma Vulgate ya Kilatini hata kama wangekuwa nayo. Kwa karne nyingi, viongozi wa Kanisa Katoliki waliwazuia watu wasipate elimu, kutia ndani kupata masomo kwenye vyuo vikuu vichache vilivyokuwepo. Ni watu wachache tu waliofaidika kutokana na elimu hiyo. Hatimaye, Biblia ikawa “kitabu kisichojulikana.” Hata hivyo, watu wengi walitaka kuwa na Neno la Mungu na kulielewa katika lugha yao wenyewe.

Kwa ujumla, viongozi wa kidini walipinga kutafsiriwa kwa Biblia wakihofia kuenea kwa upinzani. Kulingana na mwanahistoria Massimo Firpo, “kutumia lugha ya kienyeji [kungemaanisha] kuondoa kizuizi cha lugha [Kilatini] ambacho kililinda mambo ya kidini ambayo ni viongozi wa kidini tu walioyajua.” Hivyo, mchanganyiko wa desturi, dini, na mambo ya kijamii ndio unaosababisha ukosefu wa elimu ya Biblia nchini Italia mpaka leo.

Tafsiri za Kwanza Zenye Visehemu vya Biblia

Katika karne ya 13 tafsiri za kwanza za vitabu vya Biblia zilitafsiriwa katika Kiitaliano kutoka katika Kilatini. Baadhi ya tafsiri hizo ziliandikwa kwa mkono na ziligharimu pesa nyingi sana. Kwa kuwa katika karne ya 14 tafsiri ziliongezeka, karibu Biblia nzima ilipatikana katika Kiitaliano ingawa vitabu mbalimbali vilitafsiriwa na watu tofauti, wakati tofauti, na mahali tofauti. Majina ya watafsiri hayakujulikana, na ni matajiri au wasomi tu walioweza kununua tafsiri hizo. Kulingana na mwanahistoria Gigliola Fragnito, ingawa uchapishaji ulipunguza gharama za vitabu, ni “watu wachache tu walioweza kuipata” Biblia.

Kwa karne nyingi, idadi kubwa ya watu hawakuwa na elimu. Hata wakati ambapo Italia iliungana mwaka wa 1861, asilimia 74.7 ya watu hawakuwa na elimu. Wakati serikali mpya ya Italia ilipopanga kufanya elimu kuwa ya lazima na bila malipo kwa wote, Papa Pius wa Tisa alimwandikia mfalme mwaka wa 1870 akimsihi apinge sheria hiyo ambayo papa aliifafanua kuwa “pigo” lililokusudiwa “kuharibu kabisa shule za Katoliki.”

Biblia ya Kwanza ya Kiitaliano

Biblia nzima ya kwanza ya Kiitaliano ilichapishwa huko Venice mwaka wa 1471, miaka 16 baada ya mashini ya uchapaji yenye herufi zilizopangwa kutumiwa kwa mara ya kwanza huko Ulaya. Nicolò Malerbi, mtawa wa kiume wa Camaldoli, alitokeza tafsiri yake kwa muda wa miezi minane. Alitegemea sana tafsiri zilizokuwapo, akazisahihisha kwa kutegemea Vulgate ya Kilatini na kubadilisha maneno kadhaa na kutumia yale yaliyojulikana katika eneo alimoishi, yaani, Venetia. Tafsiri yake ndiyo iliyokuwa chapa ya kwanza ya Biblia kuchapishwa katika Kiitaliano na kuenezwa sana.

Mtu mwingine aliyechapisha tafsiri nyingine ya Biblia huko Venice alikuwa Antonio Brucioli. Alikuwa mwanafunzi wa sanaa ya Ugiriki aliyependelea mambo ya Uprotestanti lakini hakujitenga na Kanisa Katoliki. Mwaka wa 1532, Brucioli alitafsiri Biblia kutoka katika lugha za awali za Kiebrania na Kigiriki. Hiyo ndiyo iliyokuwa Biblia ya kwanza ya Kiitaliano kutafsiriwa kutoka maandishi ya awali. Ingawa tafsiri hiyo haitumii Kiitaliano bora, imeshikamana kabisa na maandishi ya awali, kwa kuwa wakati huo watu hawakujua sana lugha za kale. Brucioli alirudisha jina la Mungu katika mistari fulani na katika tafsiri fulani akitumia jina, “Ieova.” Kwa karne moja hivi, Biblia yake ilipendwa sana na Waprotestanti wa Italia na wapinzani wa kidini.

Tafsiri nyingine za Kiitaliano—ambazo zilitokezwa kwa kurekebisha Biblia ya Brucioli—zilichapishwa, na nyingine zikachapishwa na Wakatoliki. Hazikuenezwa sana. Mnamo 1607, Giovanni Diodati, kasisi wa dini ya Calvin ambaye wazazi wake walikuwa wamehamia Uswisi ili kuepuka kuteswa kwa sababu ya dini, alichapisha tafsiri nyingine ya Kiitaliano kutoka lugha za awali akiwa huko Geneva. Tafsiri yake ilitumiwa sana na Waprotestanti wa Italia kwa karne nyingi. Tafsiri hiyo huonwa kuwa tafsiri bora ya Kiitaliano katika kipindi hicho. Biblia ya Diodati iliwasaidia Waitaliano kuelewa mafundisho ya Biblia. Lakini makasisi walipinga kuenezwa kwa tafsiri hiyo na nyinginezo.

Biblia—“Kitabu Kisichojulikana”

Kitabu kimoja (Enciclopedia Cattolica) kinasema hivi: “Sikuzote Kanisa limefaulu kudhibiti vitabu, lakini kabla ya uchapaji kuvumbuliwa, halikuona uhitaji wa kuwa na orodha ya vitabu vilivyokatazwa kwa sababu vitabu vilivyoonwa kuwa hatari viliteketezwa.” Hata baada ya Mapinduzi ya Kiprotestanti kuanza, makasisi wa nchi mbalimbali za Ulaya walijaribu sana kupunguza uenezaji wa vitabu walivyoviona kuwa vya upinzani. Badiliko kubwa lilitokea baada ya Baraza la Trent la mwaka wa 1546 kukutana na kujadili iwapo Biblia ilipaswa kutafsiriwa katika lugha za kienyeji. Maoni mawili tofauti yalitokezwa. Wale ambao hawakutaka Biblia itafsiriwe katika lugha hizo walidai kwamba kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha za kienyeji ‘kungesababisha upinzani.’ Wale waliokubali itafsiriwe, walisema kwamba “wapinzani” wao, yaani, Waprotestanti wangedai kwamba kanisa halikutaka Biblia itafsiriwe katika lugha za kienyeji ili kuficha “ulaghai na hila” zao.

Baraza hilo halikupatana, kwa hiyo halikufikia uamuzi kuhusu suala hilo, badala yake liliidhinisha tafsiri ya Vulgate kuwa tafsiri kuu ya Kanisa Katoliki. Hata hivyo, Carlo Buzzetti, mwalimu katika Chuo cha Mapapa cha Salesianum, huko Roma, anasema kwamba “kuidhinisha” Vulgate ni “kuunga mkono dai la kwamba hiyo tu ndiyo tafsiri halali ya Biblia.” Mambo yaliyotukia baadaye yalithibitisha jambo hilo.

Mwaka wa 1559, Papa Paul wa Nne, alichapisha orodha ya kwanza ya vitabu vilivyokatazwa, yaani, orodha ya vitabu ambavyo Wakatoliki walikatazwa kusoma, kuuza, kutafsiri, au kuwa navyo. Vitabu hivyo vilionwa kuwa viovu na hatari kwa imani na maadili. Orodha hiyo ilipiga marufuku kusoma Biblia zilizotafsiriwa katika lugha za kienyeji, kutia ndani tafsiri ya Brucioli. Wale waliokiuka sheria hizo walifukuzwa kanisani. Orodha ya mwaka wa 1596 ilikuwa na sheria kali hata zaidi. Ilipiga marufuku kutafsiri au kuchapisha Biblia katika lugha za kienyeji. Biblia hizo zilipaswa kuharibiwa.

Hivyo, Biblia ziliteketezwa kwa wingi katika viwanja vya makanisa mwanzoni mwa karne ya 17. Kwa ujumla, watu waliiona Biblia kuwa kitabu cha wapinzani, na bado kuna watu walio na maoni kama hayo leo. Karibu Biblia zote na vitabu vilivyozungumzia Biblia katika maktaba za umma na za kibinafsi viliharibiwa, na kwa miaka 200 iliyofuata, hakuna Mkatoliki ambaye angeweza kutafsiri Biblia katika Kiitaliano. Biblia zilizotafsiriwa na wasomi Waprotestanti ndizo tu zilizoenezwa kisiri katika peninsula ya Italia, ili zisichukuliwe. Mwanahistoria Mario Cignoni alisema hivi: “Kihalisi kwa karne nyingi hakuna mtu aliyeisoma Biblia isipokuwa makasisi. Biblia ikawa kitabu kisichojulikana, na mamilioni ya Waitaliano hawakusoma hata ukurasa mmoja wa Biblia maishani mwao.”

Marufuku Yalegezwa

Baadaye, Papa Benedict wa 14 alitoa agizo katika orodha ya Juni 13, 1757 ili kurekebisha sheria ya awali na “kuwaruhusu watu kusoma tafsiri za lugha za kienyeji ambazo ziliidhinishwa na papa na kuchapishwa kwa mwongozo wa maaskofu.” Kwa hiyo, Antonio Martini, ambaye baadaye alikuwa askofu mkuu wa Florence, alijitayarisha kutafsiri Vulgate. Sehemu ya kwanza ilichapishwa mwaka wa 1769, na kazi hiyo ikakamilishwa mwaka wa 1781. Kulingana na kichapo kimoja cha Kikatoliki, tafsiri ya Martini ndiyo iliyokuwa “tafsiri ya kwanza bora katika Kiitaliano.” Kabla ya wakati huo, Wakatoliki ambao hawakujua Kilatini hawangeweza kusoma Biblia iliyoidhinishwa na kanisa. Kwa miaka 150 iliyofuata, Wakatoliki wa Italia waliruhusiwa tu kusoma tafsiri ya Martini.

Badiliko kubwa lilitukia wakati wa baraza la makanisa la Vatican ya Pili. Mwaka wa 1965, kwa mara ya kwanza hati fulani (Dei Verbum) ilipendekeza kuwe na “tafsiri sahihi zinazofaa . . . katika lugha mbalimbali, hasa kutokana na maandishi ya awali ya vitabu vitakatifu.” Muda mfupi mapema, mwaka wa 1958, Taasisi ya Kipapa ya Biblia (Pontificio istituto biblico) ilichapisha “tafsiri kamili ya kwanza ya Kikatoliki kutokana na maandishi ya awali.” Tafsiri hiyo ilirudisha jina la Mungu katika sehemu chache ikitumia jina “Jahve.”

Upinzani kuelekea Biblia za lugha za kienyeji umekuwa na matokeo mabaya hadi leo. Kama Gigliola Fragnito alivyosema, upinzani huo “umewafanya waamini watilie shaka uhuru wao wa kufikiri na wa kutegemea dhamiri zao.” Isitoshe, umetokeza desturi za kidini ambazo Wakatoliki wengi wanathamini sana kuliko Biblia. Mambo hayo yamewazuia watu wengi wasiyafahamu Maandiko, hata ingawa wanajua kusoma.

Hata hivyo, kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kueneza Injili, imewafanya wengi wapendezwe na Biblia nchini Italia. Mwaka wa 1963, Mashahidi walichapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiitaliano. Biblia nzima ilichapishwa mwaka wa 1967. Zaidi ya nakala 4,000,000 za tafsiri hiyo zimegawanywa nchini Italia peke yake. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyo na jina la Mungu, Yehova, ni ya pekee sana kwa sababu inashikamana kabisa na maandishi ya awali.

Mashahidi wa Yehova huhubiri nyumba kwa nyumba, wakisoma na kuwaeleza wote watakaosikiliza ujumbe wa Maandiko unaotoa tumaini. (Matendo 20:20) Utakapokutana na Mashahidi wa Yehova, waombe wakuonyeshe kile ambacho Biblia yako inasema kuhusu ahadi nzuri ya Mungu ya kwamba karibuni ataleta “dunia mpya” ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

[Ramani katika ukurasa wa 13]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Venice

ROMA

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tafsiri ya Brucioli ilitumia jina la Mungu Ieova

[Picha katika ukurasa wa 15]

Orodha ya vitabu vilivyokatazwa ilisema kwamba tafsiri za Biblia katika lugha za kienyeji ni hatari

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Bible title page: Biblioteca Nazionale Centrale di Roma

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 15]

Brucioli’s translation: Biblioteca Nazionale Centrale di Roma; Index: Su concessione del Ministero per i Beni e le Attività Culturali