Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sasa Ndio Wakati wa Kuchukua Hatua

Sasa Ndio Wakati wa Kuchukua Hatua

Sasa Ndio Wakati wa Kuchukua Hatua

“Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani?”—1 WAFALME 18:21.

1. Ni nini hufanya wakati wetu uwe tofauti sana na wakati uliopita?

JE, UNAAMINI kwamba Yehova ndiye Mungu pekee wa kweli? Je, unaamini pia kwamba unabii mbalimbali wa Biblia unaonyesha kuwa tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa Shetani? (2 Timotheo 3:1) Ikiwa ndivyo, utakubali kwamba kuna uhitaji wa kuchukua hatua sasa kuliko wakati mwingine wowote. Leo, maisha ya watu wengi yako hatarini kuliko wakati mwingine wowote.

2. Kulitukia nini katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi wakati wa utawala wa Mfalme Ahabu?

2 Katika karne ya kumi K.W.K., taifa la Israeli lilihitaji kufanya uamuzi mzito. Wangemtumikia nani? Mfalme Ahabu, akishawishiwa na mke wake mpagani, Yezebeli, aliendeleza ibada ya Baali katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Baali alikuwa mungu wa uzazi aliyedhaniwa kuwa aliandaa mvua na kutokeza mazao mengi. Huenda waabudu wengi wa Baali waliibusu sanamu ya mungu wao au kuiinamia. Ili kumsihi Baali abariki mazao na mifugo yao, waabudu wake walifanya ngono potovu na makahaba wa hekaluni. Walikuwa pia na desturi ya kujikatakata mpaka damu ilipotiririka.—1 Wafalme 18:28.

3. Ibada ya Baali ilikuwa na uvutano gani juu ya watu wa Mungu?

3 Mabaki ya Waisraeli 7,000 hivi walikataa kushiriki katika ibada hiyo ya sanamu, yenye ukosefu wa adili na yenye jeuri. (1 Wafalme 19:18) Walikuwa washikamanifu kwa agano lao pamoja na Yehova Mungu, nao wakateswa kwa sababu hiyo. Kwa mfano, Malkia Yezebeli aliwaua manabii wengi wa Yehova. (1 Wafalme 18:4, 13) Kwa sababu ya hali hizo ngumu, Waisraeli wengi walichanganya imani, huku wakijaribu kumpendeza Yehova na Baali. Lakini ulikuwa uasi-imani kwa Mwisraeli kumwacha Yehova na kuabudu mungu wa uwongo. Yehova aliahidi kuwabariki Waisraeli ikiwa wangempenda na kutii amri zake. Hata hivyo, aliwaonya kwamba ikiwa ‘hawangejitoa kwake kikamili,’ wangeangamizwa.—Kumbukumbu la Torati 5:6-10; 28:15, 63.

4. Ni jambo gani ambalo Yesu na mitume wake walitabiri lingetukia miongoni mwa Wakristo, nalo limetimiaje?

4 Hivyo ndivyo hali ilivyo leo katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Wafuasi wa dini hizo hudai kuwa Wakristo, lakini sikukuu zao, mwenendo wao, na imani zao zinapingana na mafundisho ya Biblia. Kama Yezebeli, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wako mstari wa mbele katika kuwatesa Mashahidi wa Yehova. Pia, makasisi hao wana historia ndefu ya kuunga mkono vita, na katika njia hiyo wanaunga mkono mauaji ya mamilioni ya wafuasi wa kanisa. Biblia inasema kwamba zoea hilo la dini kuunga mkono serikali za kilimwengu ni uasherati wa kiroho. (Ufunuo 18:2, 3) Isitoshe, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimeendelea kuruhusu uasherati halisi hata miongoni mwa makasisi wake. Yesu Kristo na mitume wake walitabiri uasi-imani huo mkubwa. (Mathayo 13:36-43; Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1, 2) Matokeo yatakuwa nini kwa wafuasi zaidi ya bilioni moja wa dini hizo? Waabudu wa kweli wa Yehova wana jukumu gani kuelekea watu hao na wengine ambao wamedanganywa na dini za uwongo? Tunapata jibu lililo wazi kwa kuchunguza matukio muhimu yaliyosababisha ‘kuangamizwa kwa Baali katika Israeli.’—2 Wafalme 10:28.

Upendo wa Mungu kwa Watu Wake Waliopotoka

5. Yehova alionyeshaje kwamba aliwahangaikia kwa upendo watu wake waliopotoka?

5 Yehova Mungu hafurahii kuwaadhibu wale wanaoacha kuwa waaminifu kwake. Akiwa Baba mwenye upendo, anatamani kwamba waovu watubu na kumrudia. (Ezekieli 18:32; 2 Petro 3:9) Kwa mfano, katika siku za Ahabu na Yezebeli, Yehova alitumia manabii wengi ili kuwaonya watu Wake kuhusu matokeo mabaya ya ibada ya Baali. Eliya alikuwa mmoja wa manabii hao. Baada ya ukame uliotabiriwa mapema ambao ulisababisha uharibifu, Eliya alimwambia Mfalme Ahabu awakusanye Waisraeli na manabii wa Baali kwenye Mlima Karmeli.—1 Wafalme 18:1, 19.

6, 7. (a) Eliya alionyeshaje chanzo cha uasi wa Waisraeli? (b) Manabii wa Baali walifanya nini? (c) Eliya alifanya nini?

6 Mkutano huo ulifanyika mahali palipokuwa na madhabahu ya Yehova “iliyokuwa imebomoka,” labda ili kumpendeza Yezebeli. (1 Wafalme 18:30) Kwa kusikitisha, Waisraeli waliohudhuria mkutano huo hawakuwa na uhakika kuhusu ni nani kati ya Yehova na Baali aliyekuwa na uwezo wa kuleta mvua iliyohitajiwa sana. Baali aliwakilishwa na manabii 450, lakini Eliya tu ndiye nabii aliyemwakilisha Yehova. Akitaja moja kwa moja sababu ya tatizo lao, Eliya aliwauliza watu hao hivi: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani?” Kisha, kwa maneno rahisi, akawapa nafasi ya kuchagua: “Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mfuateni yeye.” Ili kuwachochea Waisraeli hao wenye kusitasita wajitoe kikamili kwa Yehova, Eliya alipendekeza jaribu ambalo lingeonyesha ni nani aliye Mungu wa kweli. Ng’ombe-dume wawili wangechinjwa kuwa dhabihu, ng’ombe mmoja kwa ajili ya Yehova na mwingine kwa ajili ya Baali. Mungu wa kweli angeteketeza dhabihu yake kwa moto. Manabii wa Baali walitayarisha dhabihu yao, na kwa muda wa saa nyingi waliendelea kuita: “Ee Baali, tupe jibu!” Eliya alipoanza kuwadhihaki, wakaanza kujikatakata mpaka damu ilipotiririka, huku wakiita kwa sauti yao yote. Lakini hakuna yeyote aliyewajibu.—1 Wafalme 18:21, 26-29.

7 Sasa wakati wa Eliya ukafika. Kwanza, alirekebisha madhabahu ya Yehova na akaweka juu yake vipande vya ng’ombe-dume huyo. Kisha, akaamuru kwamba mitungi minne mikubwa ya maji imwagwe juu ya dhabihu hiyo. Walimwaga maji hayo mara tatu mpaka mtaro uliokuwa kando ya madhabahu hiyo ulipojaa maji. Halafu Eliya akasali hivi: “Ee Yehova Mungu wa Abrahamu, Isaka na Israeli, leo na ijulikane kwamba wewe ni Mungu katika Israeli na mimi ni mtumishi wako na ni kwa neno lako nimefanya mambo haya yote. Unijibu, Ee Yehova, unijibu, ili watu hawa wajue kwamba wewe, Yehova, ndiye Mungu wa kweli na wewe mwenyewe umeugeuza moyo wao urudi.”—1 Wafalme 18:30-37.

8. Mungu aliitikiaje sala ya Eliya, na nabii huyo alichukua hatua gani?

8 Mungu wa kweli alijibu kwa kuteketeza dhabihu na madhabahu kwa kutumia moto uliotoka mbinguni. Moto huo uliteketeza hata maji yaliyokuwa katika mtaro kando ya madhabahu! Fikiria jinsi Waisraeli walivyochochewa! “Wakaanguka kifudifudi mara moja, na kusema: ‘Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!’” Sasa Eliya akachukua hatua zaidi kwa kuwaamuru Waisraeli hivi: “Wakamateni manabii wa Baali! Msiache hata mmoja wao aponyoke!” Kisha manabii wote 450 wa Baali wakauawa chini ya Mlima Karmeli.—1 Wafalme 18:38-40.

9. Waabudu wa kweli walijaribiwaje tena?

9 Siku hiyohiyo isiyoweza kusahaulika, Yehova alisababisha mvua inyeshe kwa mara ya kwanza baada ya miaka mitatu na nusu! (Yakobo 5:17, 18) Unaweza kuwazia yale ambayo Waisraeli walizungumzia walipokuwa wakirudi nyumbani; Yehova alikuwa ametetea Uungu wake. Hata hivyo, waabudu wa Baali, hawakukata tamaa. Yezebeli aliendelea na kampeni yake ya kuwatesa watumishi wa Yehova. (1 Wafalme 19:1, 2; 21:11-16) Hivyo, utimilifu wa watu wa Mungu ukajaribiwa tena. Je, wangekutwa wakijitoa kikamili kwa Yehova wakati ambapo siku ya hukumu ingefika dhidi ya waabudu wa Baali?

Chukua Hatua Sasa

10. (a) Leo, Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa wakifanya nini? (b) Inamaanisha nini kutii amri iliyo kwenye Ufunuo 18:4?

10 Leo, Wakristo watiwa-mafuta wamefanya kazi kama ile ya Eliya. Kwa maneno na kwa vichapo, wamewaonya watu wa mataifa yote kuhusu hatari za dini za uwongo, hata iwe wako au hawako katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kwa sababu hiyo, mamilioni ya watu wamechukua hatua ya kujitenga na dini za uwongo. Watu hao wamejiweka wakfu kwa Yehova na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo waliobatizwa. Naam, wametii onyo hili la Mungu kuhusiana na dini za uwongo: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake.”—Ufunuo 18:4.

11. Ni nini kinachohitajiwa ili kupata kibali cha Yehova?

11 Watu wengine wengi ambao wanavutiwa na ujumbe unaotegemea Biblia ambao unatangazwa na Mashahidi wa Yehova, bado hawana uhakika kuhusu yale wanayopaswa kufanya. Baadhi yao wanahudhuria mara kwa mara mikutano ya Kikristo, kama vile maadhimisho ya Mlo wa Jioni wa Bwana, au wanasikiliza hotuba fulani kwenye kusanyiko la wilaya. Tunawahimiza watu hao wote wachunguze kwa makini maneno haya ya Eliya: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani?” (1 Wafalme 18:21) Badala ya kukawia-kawia, wanahitaji kuchukua hatua sasa na kufanya bidii kufikia mradi wao wa kuwa waabudu wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa. Matarajio yao ya kuishi milele yamo hatarini!—2 Wathesalonike 1:6-9.

12. Baadhi ya Wakristo waliobatizwa wamejiingiza katika hali gani hatari, nao wanapaswa kufanya nini?

12 Kwa kusikitisha, Wakristo fulani waliobatizwa hawahubiri kwa ukawaida au si watendaji katika ibada yao. (Waebrania 10:23-25; 13:15, 16) Wengine wamepoteza bidii yao kwa sababu ya kuogopa kuteswa, mahangaiko ya kupata riziki, jitihada za kuwa matajiri, au kufuatia raha za ubinafsi. Yesu alionya kwamba vitu hivyo hasa vingewakwaza, kuwasonga, na kuwa mtego kwa baadhi ya wafuasi wake. (Mathayo 10:28-33; 13:20-22; Luka 12:22-31; 21:34-36) Badala ya ‘kuyumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti,’ watu hao wanapaswa kuwa ‘wenye bidii na kutubu’ kwa kuchukua hatua ya kuishi kupatana na wakfu wao kwa Mungu.—Ufunuo 3:15-19.

Dini za Uwongo Zakomeshwa Ghafula

13. Eleza jinsi hali ilivyokuwa huko Israeli wakati Yehu alipotiwa mafuta awe mfalme.

13 Sababu inayofanya iwe muhimu kwa wanadamu kuchukua hatua ya haraka sasa inahusiana na yale yaliyotukia huko Israeli miaka 18 hivi baada ya suala la ni nani aliye Mungu wa kweli kutatuliwa kwenye Mlima Karmeli. Siku ya hukumu ya Yehova dhidi ya ibada ya Baali ilikuja ghafula bila kutarajiwa wakati wa huduma ya Elisha, ambaye alichukua nafasi ya Eliya. Yehoramu, mwana wa Mfalme Ahabu, alikuwa akitawala katika Israeli, na Yezebeli alikuwa bado hai akiwa mama malkia. Elisha alimtuma kimya-kimya mtumishi wake kumtia mafuta Yehu, mkuu wa jeshi la Israeli, ili awe mfalme mpya. Wakati huo, Yehu alikuwa upande wa mashariki wa Yordani huko Ramothi-gileadi, akiongoza vita dhidi ya adui za Israeli. Mfalme Yehoramu alikuwa huko Yezreeli katika bonde tambarare karibu na Megido, akipata nafuu kutokana na majeraha ya vita.—2 Wafalme 8:29–9:4.

14, 15. Yehu alipewa kazi gani, naye aliitimizaje?

14 Yehova alimwamuru Yehu hivi: “Uipige nyumba ya Ahabu bwana wako, nami lazima nilipize kisasi damu ya watumishi wangu manabii na damu ya watumishi wote wa Yehova mkononi mwa Yezebeli. Na nyumba yote ya Ahabu lazima iangamie; . . . Mbwa watamla Yezebeli katika sehemu ya shamba kule Yezreeli, wala hakuna atakayemzika.”—2 Wafalme 9:7-10.

15 Yehu alikuwa mtu ambaye hakusita kuchukua hatua. Bila kukawia alipanda gari lake na kuelekea haraka Yezreeli. Mlinzi mmoja huko Yezreeli alitambua namna ya Yehu ya kuendesha gari naye akamjulisha Mfalme Yehoramu, hivyo Yehoramu akapanda gari lake ili kwenda kukutana na mkuu wake wa jeshi. Walipokutana, Yehoramu alimuuliza: “Je, kuna amani, Yehu?” Yehu akamjibu: “Kunaweza kuwa na amani gani wakati kungali na uasherati wa Yezebeli mama yako na ulozi wake mwingi?” Kisha, kabla ya Mfalme Yehoramu kukimbia, Yehu alivuta upinde wake na kumpiga Yehoramu kwa mshale moyoni na kumuua.—2 Wafalme 9:20-24.

16. (a) Ni hali gani ambayo maofisa wa makao ya Yezebeli walikabili ghafula? (b) Neno la Yehova kuhusu Yezebeli lilitimiaje?

16 Bila kukawia, Yehu alipanda gari lake kwenda jijini. Akitazama chini kutoka dirishani, Yezebeli aliyekuwa amejipodoa sana alimsalimu Yehu kwa vitisho. Yehu alimpuuza Yezebeli, naye akaomba msaada: “Ni nani aliye pamoja nami? Ni nani?” Sasa watumishi wa Yezebeli walihitaji kuchukua hatua. Maofisa wawili au watatu wa makao ya kifalme wakaangalia chini toka dirishani. Kisha ushikamanifu wao ukajaribiwa. Yehu aliwaamuru hivi: “Mwangusheni!” Maofisa hao wakamwangusha Yezebeli chini barabarani, ambapo alikanyagwa na gari na farasi wa Yehu. Hivyo, mwanzilishi wa ibada ya Baali katika Israeli akauawa. Na kabla hata azikwe, mbwa walikuwa tayari wamemla, kama tu ilivyotabiriwa.—2 Wafalme 9:30-37.

17. Hukumu ya Mungu juu ya Yezebeli inapaswa kuimarisha imani yetu katika tukio gani la wakati ujao?

17 Mwisho kama huo wenye kushtua sana utampata kahaba wa mfano anayeitwa “Babiloni Mkubwa.” Kahaba huyo anawakilisha dini za uwongo za ulimwengu wa Shetani, ambazo zimetokana na jiji la kale la Babiloni. Baada ya mwisho wa dini za uwongo, Yehova Mungu ataelekeza fikira zake juu ya wanadamu wote ambao ni sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Wao pia wataharibiwa, na hilo litatayarisha njia kwa ajili ya ulimwengu mpya wenye uadilifu.—Ufunuo 17:3-6; 19:19-21; 21:1-4.

18. Ni nini kilichowapata waabudu wa Baali katika Israeli baada ya kifo cha Yezebeli?

18 Baada ya kifo cha Yezebeli, Mfalme Yehu aliwaangamiza bila kukawia wazao wote wa Ahabu na wale waliowaunga mkono. (2 Wafalme 10:11) Hata hivyo, bado kulikuwa na Waisraeli wengi nchini waliomwabudu Baali. Ili kuonyesha kwamba ‘hakuvumilia ushindani wowote kumwelekea Yehova,’ Yehu aliwachukulia hatua. (2 Wafalme 10:16) Akidai kuwa mwabudu wa Baali, Yehu alipanga sherehe kubwa kwenye hekalu la Baali ambalo Ahabu alijenga huko Samaria. Waabudu wa Baali katika Israeli walifika kwenye sherehe hiyo. Wakiwa wamenaswa ndani ya hekalu, wanaume wa Yehu waliwaua wote. Biblia inamalizia simulizi hilo kwa maneno haya: “Kwa hiyo Yehu akaangamiza Baali kutoka katika Israeli.”—2 Wafalme 10:18-28.

19. “Umati mkubwa” wa waabudu washikamanifu wa Yehova una tarajio gani zuri?

19 Ibada ya Baali ilikomeshwa katika Israeli. Vivyo hivyo, dini za uwongo za ulimwengu huu zitafikia ghafula mwisho wenye kushtua sana. Utakuwa upande gani katika siku hiyo kuu ya hukumu? Chukua hatua sasa, na huenda ukawa na pendeleo la kuwa kati ya “umati mkubwa” wa wanadamu watakaookoka “dhiki kuu.” Ndipo utakapoweza kukumbuka kwa shangwe wakati uliopita na kumtukuza Mungu kwa kumhukumu “yule kahaba mkubwa aliyeiharibu dunia kwa uasherati wake.” Kwa umoja pamoja na waabudu wengine wa kweli, utakubaliana na maneno haya yenye kuchochea yanayoimbwa na sauti za kimbingu: “Msifuni Yah, kwa sababu Yehova Mungu wetu, Mweza-Yote, ameanza kutawala akiwa mfalme.”—Ufunuo 7:9, 10, 14; 19:1, 2, 6.

Maswali ya Kutafakari

• Waisraeli wa kale walijihusishaje na ibada ya Baali?

• Biblia ilitabiri uasi-imani gani mkubwa, na unabii huo umetimiaje?

• Yehu aliondoaje ibada ya Baali?

• Tunapaswa kufanya nini ili kuokoka siku ya Mungu ya hukumu?

[Maswali ya Funzo]

[Ramani katika ukurasa wa 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Sokoh

Afeki

Helkathi

Yokneamu

Megido

Taanaki

Dothani

SAMARIA

En-dori

Shunemu

Ofra

Yezreeli

Ibleamu (Gath-rimoni)

Tirsa

Beth-shemeshi

Beth-sheani (Beth-shani)

Yabesh-gileadi?

Abel-mehola

Nyumba ya Arbeli

Ramothi-gileadi

Mountain Peaks

Ml. Karmeli

Ml. Tabori

More

Ml. Gilboa

[Bodies of water]

Bahari ya Mediterania

Bahari ya Galilaya

[River]

Mto Yordani

[Spring and well]

Kisima cha Harodi

[Hisani]

Based on maps copyrighted by Pictorial Archive (Near Eastern History) Est. and Survey of Israel

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri Ufalme ni mambo muhimu ya ibada ya kweli

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Kama Yehu, wote wanaotaka kuokoka siku ya Yehova wanapaswa kuchukua hatua