Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Hufikiria Nini Hasa Wakati wa Krismasi?

Watu Hufikiria Nini Hasa Wakati wa Krismasi?

Watu Hufikiria Nini Hasa Wakati wa Krismasi?

KWA mamilioni ya watu, majira ya sikukuu ni wakati wa kuwa pamoja na familia na marafiki, wakati wa kuimarisha upendo kati yao. Wengine wengi huiona pindi hiyo kuwa wakati wa kufikiria kuzaliwa kwa Yesu Kristo na daraka lake la kuwaokoa wanadamu. Huko Urusi, tofauti na nchi nyinginezo, kuna wakati ambapo watu hawakuruhusiwa kusherehekea Krismasi. Ingawa kwa karne nyingi wafuasi wa Kanisa Othodoksi la Urusi walisherehekea Krismasi waziwazi, hawakuruhusiwa kufanya hivyo katika miaka mingi ya karne ya 20. Kwa nini?

Muda mfupi tu baada ya mapinduzi ya Kikomunisti ya Bolshevik, mwaka wa 1917, serikali ya Sovieti ilianzisha sera ya kikatili ya kutoamini kuwapo kwa Mungu. Sikukuu ya Krismasi pamoja na sherehe zake za kidini hazikukubaliwa tena. Serikali ikaanza kueneza propaganda kuhusu sherehe za Krismasi na Mwaka Mpya. Pia, viwakilishi vya majira hayo ya sikukuu katika eneo hilo kama vile mti wa Krismasi na Baba Krismasi, ambaye huko Urusi aliitwa Ded Moroz au Babu Frost, vilipigwa marufuku.

Mwaka wa 1935, Warusi walibadili kabisa njia yao ya kusherehekea majira ya sikukuu. Wasovieti walianza tena kutumia Babu Frost, mti wa majira, na kusherehekea Mwaka Mpya, lakini kwa njia tofauti kabisa. Ilisemekana kwamba Babu Frost angeleta zawadi wakati wa Siku ya Mwaka Mpya bali si wakati wa Krismasi. Vivyo hivyo, mti wa Krismasi haungetumiwa tena. Badala yake, kungekuwa na mti wa Mwaka Mpya! Hivyo, kukawa na badiliko kubwa katika Muungano wa Sovieti. Sherehe ya Mwaka Mpya ikachukua mahali pa Krismasi.

Majira ya Krismasi yakawa majira ya sikukuu yasiyo ya kidini. Mti wa sherehe ya Mwaka Mpya ulipambwa kwa mapambo yasiyo ya kidini yaliyoonyesha maendeleo ya Muungano wa Sovieti. Jarida moja la Urusi (Vokrug Sveta) linasema: “Inawezekana kujua historia ya kuanzishwa kwa Ukomunisti kwa kutazama mapambo yaliyo kwenye mti wa sherehe ya Mwaka Mpya ambayo yanaonyesha miaka mbalimbali ya utawala wa Sovieti. Zaidi ya kupamba mti huo kwa sungura wachanga, tepe zenye madoido, na mikate ya mviringo, mapambo mengine yalitengenezwa kama vile yale yenye umbo la mundu, nyundo, na matrekta. Baadaye, mapambo hayo yaliacha kutumiwa na badala yake michongo mingine ikaanza kutumiwa, kama vile michongo ya wachimba migodi na wanaanga, michongo ya mashini za kutoa mafuta baharini, roketi, na magari yanayotumiwa kwenye mwezi.”

Namna gani Siku ya Krismasi? Bila shaka, haikutambuliwa. Badala yake, serikali ya Sovieti iliifanya kuwa siku ya kawaida ya kazi. Wale waliotaka kusherehekea Krismasi kwa sababu zake za kidini, walifanya hivyo kisiri wakihatarisha uhusiano wao na Serikali na kuhofia adhabu ambayo wangepata. Naam, katika karne ya 20 huko Urusi, mambo ya dini yaliacha kuzingatiwa katika majira ya sikukuu.

Badiliko la Hivi Karibuni

Mnamo 1991, Muungano wa Sovieti ulivunjika na watu wakapata uhuru zaidi. Ile sera ya kutoamini kuwapo kwa Mungu ikatoweka. Majimbo mapya mbalimbali hayakufuata mambo ya dini. Serikali na mambo ya dini yalitenganishwa. Watu wengi wa kidini walihisi kwamba wangeweza kudumisha imani yao. Walihisi kwamba njia moja ya kufanya hivyo ni kusherehekea sikukuu ya kidini ya Krismasi. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, watu hao walikatishwa tamaa sana. Kwa nini?

Kila mwaka, sikukuu hiyo imekuwa ya kibiashara. Naam, kama ilivyo katika nchi za magharibi, siku hizi majira ya Krismasi ni wakati bora kwa watengenezaji wa bidhaa, wauzaji wa bidhaa kwa jumla, na wachuuzi kupata pesa. Mapambo ya Krismasi hutandazwa waziwazi madukani. Sasa muziki na nyimbo za Krismasi za nchi za magharibi ambazo awali hazikujulikana nchini Urusi, huuzwa madukani. Wauzaji wanaobeba mifuko mikubwa yenye zawadi za Krismasi huuza bidhaa zao ndani ya magari ya moshi na magari mengine ya umma. Hivyo ndivyo hali ilivyo leo.

Hata watu ambao hawapingi biashara hiyo yenye pupa huenda wakaudhika wanapoona jambo lingine lenye kuhuzunisha katika majira ya sikukuu, yaani, kutumia kileo kupita kiasi na matokeo ya kufanya hivyo. Daktari fulani anayefanya kazi katika chumba cha dharura cha hospitali moja huko Moscow alisema hivi: “Madaktari hukubali kwamba wakati wa sherehe za Mwaka Mpya watu wengi huwa na majeraha mengi kutia ndani uvimbe, majeraha yanayosababishwa na kudungwa kisu au kupigwa risasi, na mengi husababishwa na jeuri katika familia, ugomvi unaotokana na ulevi, na misiba barabarani.” Mwanasayansi mmoja mwenye uzoefu wa tawi la Taasisi ya Kisayansi ya Urusi alisema hivi: “Idadi ya watu wanaokufa kwa sababu ya ulevi imeongezeka. Hasa iliongezeka zaidi mwaka wa 2000. Pia, idadi ya watu waliojiua na ya wauaji iliongezeka.”

Kuna jambo lingine linalofanya watu wajiendeshe vibaya nchini Urusi katika majira ya sikukuu. Chini ya kichwa “Warusi Washerehekea Krismasi Mara Mbili,” gazeti moja (Izvestiya) liliripoti hivi: “Kwa kila Warusi kumi, mmoja husherehekea Krismasi mara mbili. Kulingana na uchunguzi uliofanywa na Kituo cha Urusi cha Maoni ya Umma na Utafiti wa Ununuzi na Uuzaji wa Bidhaa, asilimia 8 ya waliohojiwa walikubali kwamba wao husherehekea Mkesha wa Krismasi mnamo Desemba 25, kulingana na kalenda ya Krismasi ya Kikatoliki, na mnamo Januari 7 kulingana na Kanisa Othodoksi . . . Wengi hawasherehekei Krismasi kwa sababu ya umuhimu wake wa kidini bali wanaona huo kuwa wakati mzuri wa kufanya karamu.” *

Je, Jinsi Watu Wanavyosherehekea Sikukuu ya Krismasi Leo Humtukuza Kristo?

Ni wazi kwamba wakati wa majira ya sikukuu, watu hutenda mambo mengi yasiyofaa. Ingawa matendo hayo hayapendezi, watu fulani huhisi kwamba wanapaswa kuadhimisha sherehe hizo ili kumheshimu Mungu na Kristo. Wanapongezwa kwa kutaka kumpendeza Mungu. Lakini, je, Mungu na Kristo hupendezwa na majira hayo ya Krismasi? Fikiria chanzo chake.

Kwa mfano, hata mtu awe na maoni gani kuelekea mtazamo wa Sovieti kuhusu Krismasi, ni vigumu kupinga ukweli huu wa kihistoria uliochapishwa katika kitabu kimoja cha Sovieti (Great Soviet Encyclopedia): “Krismasi . . . ilitokana na ibada ya miungu ‘waliokufa na kufufuka’ ya kabla ya Ukristo ambayo ilienea hasa miongoni mwa wakulima ambao kila mwaka wakati jua linapochomoza katika majira ya baridi kali kuanzia Desemba 21-25 walisherehekea ‘kuzaliwa’ kwa Mungu-Mwokozi anayerudisha uhai.”

Huenda ukaona umuhimu wa maneno haya sahihi ambayo kitabu hicho kinasema: “Wakristo wa karne za kwanza hawakusherehekea Krismasi. . . . Kuanzia katikati ya karne ya nne, Wakristo walianza kufuata desturi ya kusherehekea kuchomoza kwa jua katika majira ya baridi kali ambayo ilitokana na ibada ya Mithra na wakaifanya kuwa sherehe ya Krismasi. Waroma waliofuatia dini ndio waliokuwa wa kwanza kusherehekea Krismasi. Katika karne ya kumi, Krismasi ilienea pamoja na Ukristo huko Urusi, ambako ilisherehekewa pamoja na sherehe ya majira ya baridi kali ya Waslavoni wa kale ili kuheshimu roho za wafu.”

Huenda ukauliza: ‘Je, Biblia inasema kwamba Yesu alizaliwa Desemba 25?’ Kwa hakika, Biblia haitaji tarehe hususa ambayo Yesu alizaliwa, na hakuna rekodi inayoonyesha kwamba Yesu aliizungumzia wala kuamuru isherehekewe. Hata hivyo, Biblia inatusaidia kukadiria wakati ambapo Yesu alizaliwa.

Kulingana na Injili ya Mathayo, sura ya 26 na 27, Yesu aliuawa wakati wa Nisani 14, karibu na mwisho wa siku ya Pasaka ya Wayahudi iliyoanza Machi 31, 33 W.K. Tunajifunza katika Injili ya Luka kwamba Yesu alikuwa na umri wa miaka 30 hivi alipobatizwa na kuanza huduma yake. (Luka 3:21-23) Huduma yake ilichukua miaka mitatu na nusu. Hivyo, Yesu alikuwa na umri wa miaka 33 1/2 hivi alipokufa. Angekuwa na umri wa miaka 34 mnamo Oktoba 1, 33 W.K. Luka aliandika kwamba wakati Yesu alipozaliwa, wachungaji walikuwa “wakiishi nje, wakichunga makundi yao usiku.” (Luka 2:8) Wachungaji hawangekuwa nje na makundi yao wakati wa baridi ya mwezi wa Desemba, ambapo huenda hata huwa na theluji huko Bethlehemu. Lakini wangekuwa nje pamoja na makundi yao mnamo Oktoba 1 hivi, wakati ambapo kulingana na uthibitisho Yesu alizaliwa.

Lakini, namna gani sherehe ya Mwaka Mpya? Kama vile tumeona, wakati wa sherehe hiyo watu hutenda isivyofaa. Licha ya jitihada za kufanya sherehe hiyo isiwe ya kidini, asili yake inatiliwa shaka pia.

Kwa kweli, kulingana na yale yanayofanyika wakati wa majira ya sikukuu, mwito kama vile, Majira haya ya sikukuu ni kwa ajili ya Yesu, hauna maana. Ikiwa unachukia mwenendo usiofaa na biashara inayofanywa wakati wa majira ya Krismasi na vilevile asili yake ya kipagani, usivunjike moyo. Kuna njia bora ya kumheshimu Mungu na Kristo, na wakati huohuo kuimarisha uhusiano wa familia.

Njia Bora ya Kumheshimu Mungu na Kristo

Biblia inatuambia kwamba Yesu Kristo alikuja “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Alikubali kuuawa kwa ajili ya dhambi zetu. Huenda watu fulani wangependa kumtukuza Kristo, na wanahisi kwamba wanaweza kufanya hivyo katika majira ya Krismasi. Lakini kama vile tumeona, sherehe za Krismasi na za Mwaka Mpya hazina uhusiano wowote na Kristo na zilitokana na sherehe za kipagani. Pia, majira ya Krismasi, hata yawe yanavutia kadiri gani, yanachochewa na biashara inayofanywa kwa pupa. Ni wazi kwamba sikukuu ya Krismasi huhusisha matendo ya aibu yanayomchukiza Mungu na Kristo.

Mtu anayetaka kumpendeza Mungu anapaswa kufanya nini? Badala ya kushikilia desturi za wanadamu zinazomfanya mtu ajihisi kuwa wa kidini lakini zinazopingana na Maandiko, mtu mnyoofu atatafuta njia ya kweli ya kumheshimu Mungu na Kristo. Njia hiyo ya kweli ni gani, nasi tunapaswa kufanya nini?

Kristo mwenyewe anatuambia hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Naam, mtu mnyoofu hujitahidi kupata ujuzi sahihi kuhusu namna ya kumheshimu Mungu na Kristo. Kisha anatumia ujuzi huo katika maisha yake ya kila siku wala si wakati fulani wa mwaka. Mungu hupendezwa na jitihada za aina hiyo ambazo zinaweza kuongoza kwenye uzima wa milele.

Je, ungependa familia yako iwe miongoni mwa wale wanaomheshimu Mungu na Kristo kulingana na Maandiko? Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni ya familia ulimwenguni pote kupata ujuzi muhimu wa Biblia. Tunakualika kwa uchangamfu uwasiliane na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au uwaandikie ukitumia anwani ifaayo kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kabla ya mapinduzi ya Oktoba 1917, Warusi walikuwa wakitumia kalenda ya kale ya Yulio, lakini nchi nyingi zilikuwa zimeanza kutumia kalenda ya Gregory. Mnamo 1917 kalenda ya Yulio ilikuwa nyuma ya ile ya Gregory kwa siku 13. Baada ya mapinduzi, Wasovieti walianza kutumia kalenda ya Gregory na hivyo Urusi ikaanza kutumia kalenda ileile iliyotumiwa ulimwenguni pote. Hata hivyo, Kanisa Othodoksi liliendelea kutumia kalenda ya Yulio kwa ajili ya sherehe zao, na kuiita kalenda ya “Mtindo wa Kale.” Huenda umesikia kwamba huko Urusi Krismasi husherehekewa Januari 7. Hata hivyo, kumbuka kwamba Januari 7 katika kalenda ya Gregory ni Desemba 25 katika kalenda ya Yulio. Hivyo, Warusi wengi hupanga majira yao ya sikukuu hivi: Desemba 25, Krismasi ya Magharibi; Januari 1, sherehe isiyo ya kidini ya Mwaka Mpya; Januari 7, Krismasi ya Kanisa Othodoksi; Januari 14, sherehe ya Mwaka Mpya inayofuata Mtindo wa Kale.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Asili ya Sherehe ya Mwaka Mpya

Simulizi la Mtawa wa Kiume wa Kanisa Othodoksi la Georgia

“Sikukuu ya Mwaka Mpya ilitokana na sikukuu kadhaa za kipagani za Roma ya kale. Januari 1 ilikuwa sikukuu ya mungu wa kipagani anayeitwa Janus, na mwezi huo unaitwa kwa jina lake. Sanamu za Janus zilikuwa na nyuso mbili zinazoangalia pande tofauti, na hiyo ilimaanisha kwamba angeweza kuona wakati uliopita na wakati ujao. Ilisemwa kwamba yeyote aliyesherehekea Januari 1 kwa furaha, kicheko, na kula na kunywa sana angeishi mwaka mzima akiwa mwenye furaha na mwenye afya njema. Desturi hiyo ya ushirikina hufuatwa na watu wengi wa nchi yetu wakati wa kusherehekea mwaka mpya . . . Wakati wa sikukuu fulani za kipagani, watu walikuwa wakitolea sanamu dhabihu moja kwa moja. Wengine walijihusisha na ukosefu wa adili, uzinzi, na uasherati. Kwenye pindi nyingine, kama vile wakati wa sikukuu ya Janus, watu walikula na kunywa kupindukia, walilewa, na kujihusisha na kila aina ya mwenendo mchafu. Tukikumbuka jinsi tulivyosherehekea Mwaka Mpya zamani, tunapaswa kukubali kwamba sote tumeshiriki katika sherehe hiyo ya kipagani.”—Gazeti la Georgia.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Dini zinazodai kuwa za Kikristo zilichanganya ibada yake na ibada ya Mithra

[Hisani]

Museum Wiesbaden

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wachungaji hawangekuwa nje pamoja na makundi yao wakati wa baridi ya mwezi wa Desemba