Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wewe Humtii Nani—Mungu Au Wanadamu?

Wewe Humtii Nani—Mungu Au Wanadamu?

Wewe Humtii Nani—Mungu Au Wanadamu?

“Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—MATENDO 5:29.

1. (a) Ni nini andiko la msingi la funzo hili? (b) Kwa nini mitume walifungwa gerezani?

HAIKOSI waamuzi wa mahakama kuu ya Kiyahudi walikasirika. Wafungwa walikuwa wametoweka. Wafungwa hao walikuwa mitume wa Yesu Kristo, mtu ambaye mahakama kuu ilimhukumia kifo majuma machache mapema. Sasa mahakama ilikuwa tayari kukabiliana na wafuasi wake wa karibu zaidi. Lakini walinzi walipoenda kuwachukua ili kuwarudisha mahakamani, walitambua kwamba jela lilikuwa tupu, ingawa milango ilikuwa imefungwa. Baada ya muda, walinzi walipata habari kwamba mitume walikuwa hekaluni huko Yerusalemu wakifundisha watu bila woga kumhusu Yesu Kristo. Naam, walikuwa wakifanya kazi ileile ambayo ilisababisha wakamatwe! Walinzi walienda moja kwa moja hekaluni, wakawarudisha mitume gerezani, na kuwaleta mahakamani.—Matendo 5:17-27.

2. Malaika aliwaamuru mitume wafanye nini?

2 Malaika ndiye aliyewafungua mitume kutoka gerezani. Je, aliwaweka huru ili wasiteswe tena? Hapana. Waliwekwa huru ili wakaaji wa Yerusalemu wasikie habari njema kumhusu Yesu Kristo. Malaika aliwaagiza mitume waendelee ‘kusema na watu maneno yote juu ya maisha haya.’ (Matendo 5:19, 20) Hivyo, walinzi wa hekalu walipofika hekaluni, waliwapata mitume wakitekeleza amri hiyo.

3, 4. (a) Walipoamuriwa waache kuhubiri, Petro na Yohana walitendaje? (b) Mitume wengine walitendaje?

3 Wahubiri hao wenye bidii walitia ndani mitume Petro na Yohana, ambao walikuwa wamefikishwa mbele ya mahakama awali, na hakimu mkuu Yosefu Kayafa aliwakumbusha jambo hilo kwa ukali. Alisema hivi: “Hakika tuliwaagiza msiendelee kufundisha juu ya msingi wa [jina la Yesu], na bado, tazameni! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu.” (Matendo 5:28) Kayafa hakupaswa kushangaa kuwaona tena Petro na Yohana mahakamani. Walipoamuriwa mara ya kwanza waache kuhubiri, mitume hao wawili walijibu hivi: “Kama ni jambo la uadilifu mbele za macho ya Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” Kama nabii wa kale Yeremia, Petro na Yohana hawangeacha kutimiza utume wao wa kuhubiri.—Matendo 4:18-20; Yeremia 20:9.

4 Sasa, si Petro na Yohana tu, bali mitume wote—kutia ndani Mathia ambaye alikuwa amewekwa rasmi karibuni—walikuwa na pendeleo la kutangaza hadharani msimamo wao mbele ya mahakama. (Matendo 1:21-26) Walipoamuriwa waache kuhubiri, walijibu hivi kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Kumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu

5, 6. Kwa nini mitume hawakutii amri ya mahakama?

5 Mitume walitii sheria na kwa kawaida hawangeasi agizo la mahakama. Hata hivyo, hakuna mwanadamu, hata awe na nguvu kadiri gani, aliye na mamlaka ya kumwagiza mwingine avunje sheria ya Mungu. Yehova ndiye ‘Aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.’ (Zaburi 83:18) Yeye si “Mwamuzi wa dunia yote” tu, bali pia ni Mpaji-Sheria Mkuu, na Mfalme wa milele. Mungu huona agizo lolote la mahakama linalopinga amri yoyote yake kuwa ubatili.—Mwanzo 18:25; Isaya 33:22.

6 Jambo hilo limekubaliwa na baadhi ya wataalamu bora wa sheria. Kwa mfano, mwanasheria Mwingereza wa karne ya 18 anayejulikana sana William Blackstone, aliandika kwamba hakuna sheria ya mwanadamu inayopaswa kuruhusiwa kuipinga “sheria ya ufunuo” ipatikanayo katika Biblia. Hivyo, Sanhedrini ilivuka mipaka ya mamlaka yake ilipowaamuru mitume waache kuhubiri. Mitume hawangetii agizo hilo.

7. Kwa nini kazi ya kuhubiri iliwakasirisha wakuu wa makuhani?

7 Azimio la mitume la kuendelea kuhubiri liliwakasirisha wakuu wa makuhani. Baadhi ya makuhani, kutia ndani Kayafa mwenyewe, walikuwa Masadukayo, ambao hawakuamini ufufuo. (Matendo 4:1, 2; 5:17) Hata hivyo, mitume waliendelea kusisitiza kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa. Isitoshe, wakuu wengine wa makuhani walikuwa wamejitahidi sana kupata kibali cha watawala wa Roma. Kwenye kesi ya Yesu, Pilato alipowapa nafasi ya kumkubali Yesu kuwa mfalme wao, wakuu wa makuhani walimkataa kwa kupaaza sauti hivi: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” (Yohana 19:15) * Mitume hawakusisitiza tu kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa lakini pia walifundisha kwamba, mbali na jina la Yesu, “hakuna jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Matendo 2:36; 4:12) Makuhani waliogopa kwamba ikiwa watu wangemwona Yesu aliyefufuliwa kuwa Kiongozi wao, huenda Waroma wangekuja na labda viongozi wa Kiyahudi wangepoteza ‘mahali pao na taifa lao pia.’—Yohana 11:48.

8. Ni shauri gani la hekima ambalo Gamalieli aliitolea Sanhedrini?

8 Ilionekana kwamba mitume wa Yesu Kristo hawakuwa na matumaini yoyote. Waamuzi wa Sanhedrini waliazimia kuwaua. (Matendo 5:33) Hata hivyo, mambo yalibadilika ghafula. Gamalieli, mtaalamu wa Sheria, alisimama na kuwaonya wenzake wasiwachukulie mitume hatua haraka. Aliwashauri hivi kwa hekima: “Ikiwa mpango huu au kazi hii imetoka kwa wanadamu, itaangamizwa; lakini ikiwa imetoka kwa Mungu, hamtaweza kuwaangamiza.” Kisha, Gamalieli akasema jambo muhimu sana: “Ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa kwa kweli mnapigana na Mungu.”—Matendo 5:34, 38, 39.

9. Kuna uthibitisho gani kwamba kazi ya mitume ilitoka kwa Mungu?

9 Jambo la kushangaza ni kwamba mahakama ilikubali shauri la Gamalieli. Waamuzi wa Sanhedrini “wakawaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza waache kusema juu ya msingi wa jina la Yesu, kisha wakawaacha waende zao.” Hata hivyo, badala ya kuogopeshwa, mitume waliazimia kutii amri ya malaika ya kuhubiri. Hivyo, baada ya kuachiliwa huru, ‘kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba mitume hao waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ (Matendo 5:40, 42) Yehova alibariki jitihada zao. Kwa kadiri gani? “Neno la Mungu likaendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana katika Yerusalemu.” Hata “umati mkubwa wa makuhani ukaanza kuitii imani.” (Matendo 6:7) Haikosi jambo hilo liliwafadhaisha sana wakuu wa makuhani! Uthibitisho ulikuwa wazi: Hapana shaka kwamba kazi ya mitume ilitoka kwa Mungu!

Wanaopigana na Mungu Hawawezi Kufanikiwa

10. Kwa maoni ya wanadamu, kwa nini huenda Kayafa alijihisi salama kwa sababu ya cheo chake, lakini kwa nini hakupaswa kuwatumaini wanadamu?

10 Katika karne ya kwanza, makuhani wakuu wa Kiyahudi waliwekwa rasmi na watawala wa Roma. Yosefu Kayafa, ambaye alikuwa tajiri, alipewa cheo na Valerio Grato, na alishikilia cheo hicho kwa muda mrefu kuliko wale waliomtangulia. Yaelekea Kayafa aliona kuwa mafanikio hayo yalitokana na ustadi wake wa kufanyiza uhusiano mzuri na watu wengine na pia urafiki wake pamoja na Pilato wala hakuona kuwa yalitokana na Mungu. Lakini hakupaswa kuwatumaini wanadamu. Miaka mitatu tu baada ya mitume kufikishwa mbele ya Sanhedrini, Kayafa alipoteza kibali cha watawala wa Roma naye akaachishwa kuwa kuhani mkuu.

11. Matokeo yalikuwa nini kwa Pontio Pilato na mfumo wa mambo wa Kiyahudi, na unajifunza nini kutokana na hilo?

11 Amri ya kumwachisha Kayafa cheo chake ilitolewa na Lusio Vitelio, gavana wa Siria, aliyekuwa na mamlaka kuliko Pilato, naye Pilato rafiki mkuu wa Kayafa hakuweza kuzuia jambo hilo lisitendeke. Kisha, mwaka mmoja tu baada ya Kayafa kuondolewa katika cheo chake, Pilato mwenyewe aliondolewa mamlakani na akaagizwa arudi Roma ili kujibu mashtaka mazito. Kwa habari ya wale viongozi wa Kiyahudi waliomtumaini Kaisari, Waroma ‘walipaondolea mbali mahali pao na taifa lao.’ Hilo lilitukia mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yalipoliharibu kabisa jiji la Yerusalemu, kutia ndani hekalu na jumba la Sanhedrini. Maneno haya ya mtunga-zaburi yalitimia katika kisa hicho: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote”!—Yohana 11:48; Zaburi 146:3.

12. Kisa cha Yesu kinathibitishaje kwamba kumtii Mungu ndiyo njia ya hekima?

12 Tofauti na hilo, Mungu alimweka rasmi Yesu Kristo aliyefufuliwa kuwa Kuhani Mkuu wa hekalu kubwa la kiroho. Hakuna mwanadamu anayeweza kumwondoa katika cheo hicho. Kwa kweli, Yesu “ana ukuhani wake bila kuwa na waandamizi wowote.” (Waebrania 2:9; 7:17, 24; 9:11) Pia, Mungu alimweka rasmi Yesu kuwa Mwamuzi wa walio hai na wafu. (1 Petro 4:5) Akiwa katika cheo hicho, Yesu ataamua ikiwa Yosefu Kayafa na Pontio Pilato wataishi tena wakati ujao.—Mathayo 23:33; Matendo 24:15.

Wahubiri Wenye Ujasiri wa Siku Zetu

13. Leo, ni kazi gani imethibitika kuwa imetoka kwa wanadamu, na ni gani imethibitika kuwa imetoka kwa Mungu? Unajuaje hilo?

13 Leo, kama katika karne ya kwanza, kumekuwa na watu wengi ‘wanaopigana na Mungu.’ (Matendo 5:39) Kwa mfano, Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani walipokataa kumpigia Adolf Hitler saluti ya kuwa Mtawala wao, Hitler aliapa kwamba angewaangamiza. (Mathayo 23:10) Kikundi chake cha kutekeleza mauaji kilikuwa na uwezo wa kutosha wa kufanya hivyo. Wanazi walifaulu kuwakamata maelfu ya Mashahidi na kuwapeleka kwenye kambi za mateso. Hata walifaulu kuwaua baadhi ya Mashahidi. Hata hivyo, hawakufanikiwa kuvunja azimio la Mashahidi la kumwabudu Mungu pekee, nao walishindwa kuwaangamiza watumishi wa Mungu wakiwa kikundi. Kazi ya Wakristo hao ilitoka kwa Mungu, si kwa mwanadamu, na kazi ya Mungu haiwezi kuangamizwa. Miaka 60 baadaye, waokokaji waaminifu wa kambi za mateso za Hitler bado wanaendelea kumtumikia Yehova ‘kwa moyo wao wote na kwa nafsi na akili yao yote,’ huku Hitler na chama chake cha Nazi wakikumbukwa tu kwa matendo yao maovu.—Mathayo 22:37.

14. (a) Ni jitihada zipi ambazo wapinzani wamefanya ili kuwachongea watumishi wa Mungu, na matokeo yamekuwa nini? (b) Je, jitihada hizo zitasababisha madhara yoyote ya kudumu kwa watu wa Mungu? (Waebrania 13:5, 6)

14 Tangu wakati wa Nazi, wengine wamepigana na Yehova na watu wake bila mafanikio. Katika nchi kadhaa za Ulaya, makundi fulani ya kidini na ya kisiasa yenye hila, yamewaita Mashahidi wa Yehova ‘madhehebu hatari,’ na shtaka hilo ni sawa na lile ambalo lilifanywa dhidi ya Wakristo wa karne ya kwanza. (Matendo 28:22) Ukweli ni kwamba Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu imetambua Mashahidi wa Yehova kuwa dini, na si madhehebu. Wapinzani wanajua vizuri uamuzi huo. Hata hivyo, bado wanaendelea kuwachongea Mashahidi. Kwa sababu hiyo, baadhi ya Wakristo wamepoteza kazi zao. Watoto ambao ni Mashahidi wamenyanyaswa shuleni. Wenye nyumba za kukodisha ambazo Mashahidi wametumia kwa miaka mingi kwa ajili ya mikutano wamevunja mapatano kuhusu nyumba hizo kwa sababu tu ya kuogopa wanadamu. Katika visa vichache, mashirika ya serikali yamewanyima watu uraia eti kwa sababu wao ni Mashahidi wa Yehova! Hata hivyo, Mashahidi hawavunjiki moyo.

15, 16. Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa wametendaje kuhusu upinzani dhidi ya kazi yao ya Kikristo, na kwa nini wanaendelea kuhubiri?

15 Kwa mfano, huko Ufaransa, kwa kawaida watu wana usawaziko na hawana ubaguzi. Hata hivyo, wapinzani wachache wameendeleza sheria zinazokusudiwa kuzuia kazi ya Ufalme. Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa wametendaje? Wameongeza juhudi zao katika kazi ya kuhubiri kuliko hapo awali nao wamepata matokeo yenye kutia moyo. (Yakobo 4:7) Kwa kushangaza, katika kipindi cha miezi sita tu, idadi ya mafunzo ya Biblia ya nyumbani imeongezeka kwa asilimia 33 nchini humo! Ni wazi kwamba ongezeko hilo linamkasirisha sana Ibilisi anapoona watu wanyoofu wakikubali habari njema nchini Ufaransa. (Ufunuo 12:17) Wakristo wenzetu huko Ufaransa wana hakika kwamba maneno haya ya nabii Isaya yatathibitika kuwa kweli kuwahusu: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu.”—Isaya 54:17.

16 Mashahidi wa Yehova hawafurahi wanapoteswa. Hata hivyo, ili kutii amri ambayo Mungu amewapa Wakristo wote, hawataacha kusema kuhusu mambo ambayo wamesikia. Wanajitahidi kuwa raia wazuri. Hata hivyo, sheria ya Mungu inapopingana na ile ya wanadamu, wao humtii Mungu kuwa mtawala.

Msiwaogope

17. (a) Kwa nini hatupaswi kuogopa adui zetu? (b) Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuwaelekea wale wanaotutesa?

17 Adui zetu wako hatarini kabisa. Wanapigana na Mungu. Hivyo, kulingana na amri ya Yesu, badala ya kuwaogopa, tunasali kwa ajili ya wale wanaotutesa. (Mathayo 5:44) Tunasali kwamba ikiwa kuna yeyote anayempinga Mungu bila kujua, kama alivyofanya Sauli wa Tarso, kwa fadhili Yehova atamfungua macho ili akubali ukweli. (2 Wakorintho 4:4) Sauli aligeuka na kuwa mtume Mkristo Paulo, na aliteswa sana na watawala wa siku zake. Hata hivyo, aliendelea kuwakumbusha waamini wenzake kwamba “wajitiishe na kuzitii serikali na mamlaka zikiwa watawala, wawe tayari kwa ajili ya kila kazi njema, wasiseme vibaya juu ya yeyote [hata kuhusu wale wanaowatesa zaidi], wasiwe wataka-vita, wawe wenye usawaziko, wakionyesha upole wote kuelekea watu wote.” (Tito 3:1, 2) Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa na kwingineko hujitahidi kufuata shauri hilo.

18. (a) Huenda Yehova akatumia njia zipi ili kuwakomboa watu wake? (b) Matokeo yatakuwa nini?

18 Mungu alimwambia nabii Yeremia hivi: “Mimi niko pamoja nawe ili kukukomboa.” (Yeremia 1:8) Leo, Yehova anaweza kutukomboaje na mateso? Anaweza kutokeza mwamuzi mwenye usawaziko kama Gamalieli. Au huenda akahakikisha kwamba mtawala mbaya au anayetupinga anaondolewa ghafula na mahali pake kuchukuliwa na mwingine mwenye usawaziko zaidi. Hata hivyo, huenda wakati mwingine Yehova akaruhusu watu wake wateswe. (2 Timotheo 3:12) Ikiwa Mungu anaruhusu tuteswe, ni wazi kwamba sikuzote atatupa nguvu ili tuvumilie mateso hayo. (1 Wakorintho 10:13) Hata iwe Mungu ataruhusu nini, bila shaka tunajua jinsi matokeo yatakavyokuwa: Wale wanaopigana na watu wa Mungu wanapigana na Mungu, na wale wanaopigana na Mungu hawatashinda.

19. Ni nini andiko la mwaka wa 2006, na kwa nini linafaa?

19 Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba wangetarajia dhiki. (Yohana 16:33) Kwa hiyo, maneno haya ya andiko la Matendo 5:29 yanafaa sana wakati huu kuliko wakati mwingine wowote: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” Kwa sababu hiyo, maneno hayo yenye kuchochea yamechaguliwa kuwa andiko la mwaka la Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya mwaka wa 2006. Acheni azimio letu mwaka ujao na katika umilele wote liwe kumtii Mungu kuwa Mtawala vyovyote iwavyo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 “Kaisari” huyo ambaye wakuu wa makuhani walimwunga mkono hadharani katika pindi hiyo alikuwa Maliki Mroma Tiberio aliyedharauliwa na watu na aliyekuwa mnafiki na muuaji. Tiberio alijulikana pia kwa mazoea yake machafu ya ngono.—Danieli 11:15, 21.

Je, Unaweza Kujibu?

• Mitume walituwekea kielelezo gani chenye kutia moyo kuhusiana na jinsi walivyokabiliana na upinzani?

• Kwa nini sikuzote tunapaswa kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu?

• Wapinzani wetu wanapigana na nani hasa?

• Wote wanaovumilia mateso wanaweza kutarajia matokeo gani?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Andiko la mwaka wa 2006 litakuwa: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29

[Picha katika ukurasa wa 19]

“Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu”

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kayafa aliwatumaini wanadamu badala ya kumtumaini Mungu