Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Wema Utakavyoshinda Uovu

Jinsi Wema Utakavyoshinda Uovu

Jinsi Wema Utakavyoshinda Uovu

Mfalme Daudi alikuwa mtu mwema. Alimpenda Mungu sana, alipenda haki, na alimhangaikia kwa upendo mtu wa hali ya chini. Hata hivyo, mfalme huyohuyo mwema alifanya uzinzi na mke wa mmoja wa wanaume wake wenye kutegemeka. Na baada ya Daudi kugundua kwamba mwanamke huyo, Bath-sheba, alikuwa na mimba yake, Daudi alipanga kumuua mume wake. Kisha, akamuoa Bath-sheba ili kujaribu kuficha matendo yake ya uhalifu.—2 Samweli 11:1-27.

NI WAZI kwamba wanadamu wana uwezo wa kutenda mambo mengi mazuri. Lakini, kwa nini basi wanatenda maovu mengi hivyo? Biblia inaonyesha sababu mbalimbali za msingi. Pia, inafunua jinsi Mungu atakavyoondoa uovu milele kupitia Kristo Yesu.

Mwelekeo wa Kutenda Mabaya

Mfalme Daudi mwenyewe alionyesha mojawapo ya sababu za matendo maovu. Baada ya matendo yake mabaya kujulikana, alikubali makosa yake. Aliandika hivi baada ya kutubu: “Tazama! Nilizaliwa kwa maumivu nikiwa na kosa, na mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” (Zaburi 51:5) Mungu hakukusudia kamwe akina mama wazae watoto ambao wangekuwa watenda-dhambi. Hata hivyo, Hawa na Adamu walipochagua kumwasi Mungu, walipoteza uwezo wao wa kuzaa watoto wasio na dhambi. (Waroma 5:12) Jamii ya wanadamu wasio wakamilifu ilipoendelea kuongezeka, sasa ilionekana wazi kwamba “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.”—Mwanzo 8:21.

Mwelekeo huo wa kutenda mabaya usipodhibitiwa, unaweza kuongoza kwenye “uasherati, . . . uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda,” na tabia nyingine zenye kuharibu ambazo Biblia inazitaja kuwa “matendo ya mwili.” (Wagalatia 5:19-21) Kuhusu kisa cha Mfalme Daudi, ni wazi kwamba alishindwa na udhaifu wa mwili naye akafanya uasherati, ambao ulisababisha mizozo. (2 Samweli 12:1-12) Angeweza kushinda mwelekeo wake wa ukosefu wa adili. Badala yake, kwa kuendelea kumtamani Bath-sheba, Daudi alifuata mwelekeo ambao baadaye ulitajwa hivi na mwanafunzi Yakobo: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.”—Yakobo 1:14, 15.

Kuuawa kwa watu wengi, kulala wanawake kinguvu, na uporaji wa mali uliotajwa katika makala iliyotangulia ni mifano ya mambo ambayo hutokea watu wanaporuhusu tamaa mbaya ziongoze matendo yao.

Uovu Huchochewa na Ukosefu wa Ujuzi

Mambo ambayo mtume Paulo alijionea maishani yanakazia sababu ya pili inayofanya watu watende maovu. Hadi kufikia kifo chake, Paulo alijulikana kuwa mtu mpole na mwenye upendo. Alijitoa bila ubinafsi kuwatumikia ndugu na dada zake Wakristo. (1 Wathesalonike 2:7-9) Hata hivyo, mapema kabla ya hapo, alipojulikana kwa jina la Sauli, ‘alitisha na kutaka kuua’ kikundi hichohicho. (Matendo 9:1, 2) Kwa nini Paulo alikubali na kushiriki katika matendo hayo maovu dhidi ya Wakristo wa mapema? Anasema hivi: “Kwa sababu nilikosa ujuzi.” (1 Timotheo 1:13) Naam, kabla ya hapo Paulo alikuwa na “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.”—Waroma 10:2.

Kama Paulo, watu wengi wanyoofu wamejiingiza katika matendo maovu kwa sababu ya kukosa ujuzi sahihi kuhusu mapenzi ya Mungu. Kwa mfano, Yesu aliwaonya wafuasi wake hivi: “Saa inakuja wakati ambapo kila mtu anayewaua ninyi atafikiri amemtolea Mungu utumishi mtakatifu.” (Yohana 16:2) Mashahidi wa Yehova wa leo wanatambua ukweli wa maneno hayo ya Yesu. Katika nchi nyingi, wameteswa na hata kuuawa na watu wanaodai kumtumikia Mungu. Ni wazi kwamba bidii hiyo katika mambo yasiyofaa haimpendezi Mungu wa kweli.—1 Wathesalonike 1:6.

Mwanzilishi wa Uovu

Yesu alionyesha sababu kuu ya kuwapo kwa uovu. Akizungumza na viongozi wa kidini waliotaka kumuua, Yesu alisema hivi: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu. Huyo alikuwa muuaji alipoanza.” (Yohana 8:44) Akichochewa na sababu za ubinafsi, Shetani ndiye aliyewashawishi Adamu na Hawa wamwasi Mungu. Uasi huo ulileta dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa wanadamu wote.

Jinsi Shetani alivyomtendea Ayubu ilionyesha wazi mwelekeo wake wa kuwa muuaji. Yehova alipomruhusu ajaribu utimilifu wa Ayubu, Shetani hakuridhika tu kuharibu mali za Ayubu. Alisababisha hata kifo cha watoto kumi wa Ayubu. (Ayubu 1:9-19) Katika karne iliyopita, wanadamu walishuhudia ongezeko la uovu, kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu na ukosefu wa ujuzi na pia kwa sababu ya Shetani kujihusisha sana katika mambo ya wanadamu. Biblia inasema kwamba Ibilisi ‘alitupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.’ Unabii huohuo ulitabiri kwa usahihi kwamba kutupwa kwa Shetani kungesababisha ‘ole isiyo na kifani duniani.’ Ingawa Shetani hawezi kuwalazimisha watu watende mambo maovu, yeye ni bingwa katika ‘kuipotosha dunia nzima inayokaliwa.’—Ufunuo 12:9, 12.

Kuondolewa kwa Mwelekeo wa Kutenda Mabaya

Ikiwa uovu utakomeshwa katika jamii ya wanadamu, mwelekeo uliorithiwa wa mwanadamu wa kutenda mabaya, ukosefu wa ujuzi sahihi, na uvutano wa Shetani unapaswa kuondolewa. Lakini mwelekeo wa mwanadamu wa kutenda dhambi unaweza kuondolewaje moyoni?

Hakuna jambo lolote ambalo mwanadamu anaweza kufanya ili kuondoa mwelekeo wa kutenda dhambi. Hata hivyo, Yehova Mungu amefanya maandalizi ya kuondoa dhambi iliyorithiwa na kutokamilika kwa wote walio tayari kuyakubali. Mtume Yohana aliandika hivi: “Damu ya Yesu . . . hutusafisha kutoka katika dhambi yote.” (1 Yohana 1:7) Wakati Yesu, mtu mkamilifu, alipotoa uhai wake kwa hiari, “alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tuachane kabisa na dhambi na kuishi kwa uadilifu.” (1 Petro 2:24) Kifo cha dhabihu cha Yesu kingeondoa madhara ya uovu wa Adamu. Paulo anasema kwamba Kristo Yesu alikuwa “fidia inayolingana kwa ajili ya wote.” (1 Timotheo 2:6) Naam, kifo cha Kristo kilifungua njia ili wanadamu wote wapate tena ukamilifu ambao Adamu alipoteza.

Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa kifo cha Yesu kilichotukia miaka 2,000 hivi iliyopita kiliwezesha wanadamu kupata tena ukamilifu, kwa nini bado kuna uovu na kifo?’ Kupata jibu kwa swali hilo kunaweza kusaidia kuondoa sababu ya pili ya uovu, yaani, mwanadamu amekosa ujuzi kuhusu makusudi ya Mungu.

Wema Waimarishwa na Ujuzi Sahihi

Kupata ujuzi sahihi kuhusu yale ambayo Yehova na Yesu wanafanya sasa ili kuondoa uovu huenda kukamzuia mtu mnyoofu asiunge mkono matendo maovu bila kujua, au hata kumzuia ‘asipigane na Mungu.’ (Matendo 5:38, 39) Yehova Mungu yuko tayari kusamehe makosa yaliyofanywa kwa sababu ya kukosa ujuzi. Akizungumza huko Athene, mtume Paulo alisema hivi: “Mungu ameachilia mbali nyakati hizo za kutojua, lakini sasa anawaambia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu. Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.”—Matendo 17:30, 31.

Kutokana na mambo aliyojionea, Paulo alijua kwamba Yesu alifufuliwa kwa kuwa, baada ya kufufuliwa, Yesu mwenyewe alizungumza na Paulo, naye akamzuia asiwatese Wakristo wa mapema. (Matendo 9:3-7) Paulo alipata ujuzi sahihi wa makusudi ya Mungu, akabadilika na kuwa mtu mwema kabisa kwa kumwiga Kristo. (1 Wakorintho 11:1; Wakolosai 3:9, 10) Isitoshe, Paulo alihubiri kwa bidii “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Kwa miaka 2,000 hivi tangu Yesu alipokufa na kufufuka, amechagua kati ya wanadamu wale ambao, kama Paulo, watatawala pamoja naye katika Ufalme wake.—Ufunuo 5:9, 10.

Muda wote wa karne iliyopita hadi leo, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitimiza kwa bidii kazi hii ambayo Yesu aliagiza ifanywe: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Wale wanaokubali ujumbe huo wana tarajio la kuishi milele duniani chini ya serikali ya kimbingu ya Kristo. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Kumsaidia mtu fulani kupata ujuzi huo ndio wema mkuu zaidi tunaoweza kumtendea mtu mwingine.

Wale wanaokubali habari njema ya Ufalme huonyesha sifa kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia,” licha ya uovu wote unaowazunguka. (Wagalatia 5:22, 23) Wanamwiga Yesu kwa ‘kutomlipa yeyote uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Wakiwa mtu mmoja-mmoja, wanajitahidi ‘kuendelea kuushinda uovu kwa wema.’—Waroma 12:21; Mathayo 5:44.

Ushindi Juu ya Uovu

Bila kusaidiwa, wanadamu hawawezi kamwe kumshinda yule mchochezi mkuu wa uovu, Shetani Ibilisi. Hata hivyo, hivi karibuni, Yehova atamtumia Yesu kuponda kichwa cha Shetani. (Mwanzo 3:15; Waroma 16:20) Pia, Yehova atamwagiza Kristo Yesu ‘kuivunja na kuikomesha’ mifumo yote ya kisiasa, ambayo imesababisha uovu mwingi katika historia yote. (Danieli 2:44; Mhubiri 8:9) Wakati wa siku ya hukumu ijayo, wale wote “wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu . . . watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.”—2 Wathesalonike 1:8, 9; Sefania 1:14-18.

Baada ya Shetani na wale wanaomuunga mkono kuondolewa, Yesu akiwa mbinguni atawasaidia waokokaji kuifanya dunia iwe kama ilivyokuwa mwanzoni. Pia, Kristo atawafufua wale wote wanaostahili kuishi katika dunia iliyofanywa kuwa mpya. (Luka 23:32, 39-43; Yohana 5:26-29) Kwa kufanya hivyo, atakomesha madhara ya uovu ambayo yamewapata wanadamu.

Yehova hawalazimishi watu waitii habari njema kumhusu Yesu. Hata hivyo, anawapa watu nafasi ya kupata ujuzi uongozao kwenye uzima. Ni muhimu kwako kutumia nafasi hiyo sasa! (Sefania 2:2, 3) Ukifanya hivyo, utajifunza jinsi ya kukabiliana na uovu wowote unaoathiri maisha yako sasa. Pia, utaona jinsi Kristo atakavyoongoza ushindi wa mwisho juu ya uovu.—Ufunuo 19:11-16; 20:1-3, 10; 21:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Sauli alikubali matendo maovu kwa sababu hakuwa na ujuzi sahihi

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kumsaidia mtu fulani kupata ujuzi sahihi kumhusu Mungu ndio wema mkuu zaidi tunaoweza kumtendea mtu mwingine