Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutafuta Uadilifu Kutatulinda

Kuutafuta Uadilifu Kutatulinda

Kuutafuta Uadilifu Kutatulinda

“Endeleeni kuutafuta kwanza . . . uadilifu [wa Mungu].”—MATHAYO 6:33.

1, 2. Msichana mmoja Mkristo alifanya uamuzi gani, na kwa nini alifanya uamuzi huo?

MSICHANA mmoja Mkristo huko Asia alikuwa karani katika ofisi moja ya serikali. Alikuwa akifika mapema kazini na alikuwa mwenye bidii. Hata hivyo, kwa sababu hakuwa ameajiriwa rasmi, kazi yake ilikaguliwa. Msimamizi wa idara alimwambia msichana huyo kwamba atamwajiri rasmi na hata kumpa cheo cha juu ikiwa atakubali kufanya ngono naye. Msichana huyo alikataa katakata, licha ya kwamba angepoteza kazi.

2 Je, msichana huyo alitenda bila kufikiri? La, alifuata kwa makini maneno haya ya Yesu: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza . . . uadilifu [wa Mungu].” (Mathayo 6:33) Kwake, kufuata kanuni za uadilifu kulikuwa muhimu sana kuliko kupata faida kwa kujihusisha katika ukosefu wa adili katika ngono.—1 Wakorintho 6:18.

Umuhimu wa Uadilifu

3. Uadilifu ni nini?

3 “Uadilifu” humaanisha kufuata kanuni za maadili. Katika Biblia, maneno ya Kigiriki na ya Kiebrania yanayotumiwa yanamaanisha “uaminifu” au “unyoofu.” Uadilifu si kujiona kuwa mwadilifu kulingana na viwango vyako mwenyewe. (Luka 16:15) Ni unyoofu kulingana na viwango vya Yehova. Ni uadilifu wa Mungu.—Waroma 1:17; 3:21.

4. Kwa nini uadilifu ni muhimu kwa Mkristo?

4 Kwa nini uadilifu ni muhimu? Kwa sababu Yehova, ambaye ni ‘Mungu mwadilifu,’ huwaonyesha kibali watu wake wakati wanapotenda uadilifu. (Zaburi 4:1; Methali 2:20-22; Habakuki 1:13) Mtu yeyote asiye mwadilifu hawezi kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Methali 15:8) Ndiyo sababu mtume Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Zikimbie tamaa zinazotukia ujanani, lakini fuatilia uadilifu,” pamoja na sifa nyingine muhimu. (2 Timotheo 2:22) Ndiyo sababu pia, Paulo alitia ndani “bamba la kifuani la uadilifu” alipoorodhesha sehemu mbalimbali za mavazi yetu ya silaha ya kiroho.—Waefeso 6:14.

5. Viumbe wasio wakamilifu wanaweza kuutafutaje uadilifu?

5 Bila shaka, hakuna mwanadamu aliye mwadilifu kikamili. Wote wamerithi kutokamilika kutoka kwa Adamu, na wote ni wenye dhambi, wasio waadilifu tangu kuzaliwa. Lakini, Yesu alisema tuutafute uadilifu. Inawezekanaje? Inawezekana kwa sababu Yesu alitoa uhai wake mkamilifu kuwa fidia kwa ajili yetu, na tukiwa na imani katika dhabihu hiyo, Yehova yuko tayari kutusamehe dhambi zetu. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; Waroma 5:8, 9, 12, 18) Kwa msingi huo, tunapoendelea kujifunza kanuni za uadilifu za Yehova na kufanya yote tuwezayo kuzifuata, huku tukimwomba msaada ili kushinda udhaifu wetu, Yehova hukubali ibada yetu. (Zaburi 1:6; Waroma 7:19-25; Ufunuo 7:9, 14) Inafariji kama nini!

Kuwa Mwadilifu Katika Ulimwengu Usio na Uadilifu

6. Kwa nini ulimwengu ulikuwa mahali hatari kwa Wakristo wa mapema?

6 Wanafunzi wa Yesu walipopewa utume wa kuwa mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia,” walikabili hali ngumu. (Matendo 1:8) Eneo lote walilopewa ‘lilikuwa likikaa katika nguvu za yule mwovu,’ Shetani. (1 Yohana 5:19) Ulimwengu ulikuwa na roho mbovu ambayo yeye anaendeleza, na Wakristo wangekabili uvutano wenye kuchafua wa roho hiyo. (Waefeso 2:2) Ulimwengu ulikuwa mahali hatari kwao. Wangeweza tu kuvumilia na kudumisha utimilifu wao kwa kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu. Wengi wao walivumilia, lakini wachache walikengeushwa kutoka katika “mapito ya uadilifu.”—Methali 12:28; 2 Timotheo 4:10.

7. Mkristo anapaswa kupinga uvutano wenye kuchafua kwa sababu ya majukumu gani?

7 Je, Wakristo wako salama ulimwenguni leo? La hasha! Ulimwengu ni mbaya hata zaidi kuliko ulivyokuwa katika karne ya kwanza. Isitoshe, Shetani ametupwa duniani na anapigana vita vikali dhidi ya Wakristo watiwa-mafuta, “wale waliobaki wa uzao [wa mwanamke], wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:12, 17) Pia, Shetani anamshambulia yeyote anayeunga mkono “uzao” huo. Hata hivyo, Wakristo hawawezi kuutoroka ulimwengu. Ingawa wao si sehemu yake, ni lazima waishi ndani yake. (Yohana 17:15, 16) Ni lazima wahubiri ndani yake ili kuwatafuta watu walio na mwelekeo unaofaa na kuwafundisha wawe wanafunzi wa Kristo. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kwa hiyo, kwa kuwa Wakristo hawawezi kuepuka kabisa mambo yenye kuchafua ya ulimwengu huu, wanapaswa kuyapinga. Acheni tuzungumzie mambo manne kati ya hayo.

Mtego wa Ukosefu wa Adili

8. Kwa nini Waisraeli walianza kuabudu miungu ya Wamoabu?

8 Walipokaribia kumaliza safari yao ya miaka 40 jangwani, Waisraeli wengi waligeuka na kuacha mapito ya uadilifu. Walikuwa wameshuhudia ukombozi wa Yehova katika njia mbalimbali, na karibuni wangeingia Nchi ya Ahadi. Lakini wakati huo muhimu, walianza kutumikia miungu ya Wamoabu. Kwa nini? Waliangukia “tamaa ya mwili.” (1 Yohana 2:16) Masimulizi yanasema hivi: “Watu wakaanza kufanya uasherati na binti za Moabu.”—Hesabu 25:1.

9, 10. Ni hali gani zilizopo leo zinazofanya iwe muhimu sikuzote kukumbuka uvutano wa tamaa mbaya za mwili?

9 Tukio hilo linaonyesha jinsi tamaa mbaya za mwili zinavyoweza kuwachafua wasio na ujuzi. Tunapaswa kujifunza kutokana na tukio hilo hasa kwa sababu watu wengi wanaona ukosefu wa adili kuwa jambo la kawaida. (1 Wakorintho 10:6, 8) Ripoti moja kutoka Marekani inasema: “Kufikia mwaka wa 1970 hivi, zoea la wanaume na wanawake kuishi pamoja bila kufunga ndoa lilikuwa kinyume cha sheria katika majimbo yote ya Marekani. Leo, hilo ni jambo la kawaida. Zaidi ya nusu ya watu wanaofunga ndoa kwa mara ya kwanza walikuwa wanaishi pamoja kabla ya ndoa.” Zoea hilo na matendo mengine machafu hufanyika katika nchi mbalimbali. Hivyo ndivyo ilivyo ulimwenguni pote, na inasikitisha kwamba Wakristo wengine wamefuata mwenendo huo, na hata wamepoteza msimamo wao katika kutaniko la Kikristo.—1 Wakorintho 5:11.

10 Isitoshe, ukosefu wa adili unapendekezwa kila mahali. Sinema na vipindi vya televisheni huonyesha kwamba ni sawa na inakubalika kwa vijana kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa. Mahusiano ya ngono kati ya watu wa jinsia moja yanaonwa kuwa sawa. Sinema nyingi huonyesha ngono waziwazi. Pia, picha zinazoonyesha ngono waziwazi zinapatikana kwa urahisi kwenye Intaneti. Kwa mfano, mwandishi mmoja wa gazeti aliripoti kwamba mwana wake wa miaka saba alirudi nyumbani kutoka shuleni na kumwambia kwa furaha kwamba rafiki yake shuleni alipata kituo cha Intaneti kinachoonyesha wanawake wakiwa uchi na wakifanya ngono. Baba yake alishtuka. Lakini ni watoto wangapi hutazama vituo kama hivyo kwenye Intaneti bila kuwaambia wazazi wao? Isitoshe, ni wazazi wangapi wanaojua mambo yaliyo katika michezo ya video ambayo watoto wao hucheza? Michezo mingi inayopendwa huonyesha ukosefu wa adili, matendo ya kuwasiliana na roho waovu, na jeuri.

11. Familia inaweza kulindwaje kutokana na ukosefu wa adili katika ulimwengu?

11 Familia inaweza kuepukaje “burudani” chafu kama hiyo? Kwa kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu, na kukataa kujihusisha na mambo yoyote machafu. (2 Wakorintho 6:14; Waefeso 5:3) Wazazi wanaosimamia watoto wao kwa njia inayofaa na kukazia mioyoni mwa watoto wao kumpenda Yehova na kuzipenda amri zake za uadilifu huwalinda dhidi ya picha chafu, michezo ya video yenye picha chafu, sinema zinazoonyesha ukosefu wa adili, na vishawishi vingine.—Kumbukumbu la Torati 6:4-9. *

Hatari ya Uvutano Katika Jamii

12. Kulitokea tatizo gani katika karne ya kwanza?

12 Paulo alipokuwa Listra huko Asia Ndogo, alimponya mwanamume fulani kimuujiza. Masimulizi yanasema hivi: “Umati, walipoona jambo ambalo Paulo alikuwa amefanya, wakapaaza sauti, wakisema katika lugha ya Kilikaonia: ‘Miungu imekuwa kama binadamu nayo imeshuka kwetu!’ Naye Barnaba wakamwita Zeu, lakini Paulo wakamwita Herme, kwa kuwa ndiye aliyekuwa akiongoza katika kusema.” (Matendo 14:11, 12) Baadaye, umati huohuo ulitaka kuwaua Paulo na Barnaba. (Matendo 14:19) Ni wazi kwamba watu hao waliathiriwa sana na uvutano wa jamii. Yaelekea baadhi yao walipokuwa Wakristo, hawakuacha ushirikina. Katika barua yake kwa Wakristo huko Kolosai, Paulo alionya dhidi ya “ibada ya malaika.”—Wakolosai 2:18.

13. Ni zipi baadhi ya desturi ambazo Mkristo anapaswa kuepuka, na anaweza kupataje nguvu za kuziepuka?

13 Leo pia, Wakristo wa kweli wanapaswa kuepuka desturi zinazokubaliwa na wengi ambazo zinatokana na mafundisho ya uwongo ya kidini ambayo huvunja kanuni za Kikristo. Kwa mfano, katika nchi fulani, sherehe za kidesturi ambazo hufanywa wakati wa kuzaliwa au kufa zinatokana na uwongo wa kwamba tuna roho inayoendelea kuishi tunapokufa. (Mhubiri 9:5, 10) Katika nchi nyingine ni kawaida wasichana kutahiriwa. Hilo ni zoea la kikatili lisilo na maana ambalo halipatani na upendo ambao wazazi Wakristo wanapaswa kuwaonyesha watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Waefeso 6:4) Wakristo wanaweza kupingaje mikazo ya kijamii na kuacha mazoea kama hayo? Kwa kumtegemea Yehova kabisa. (Zaburi 31:6) Mungu mwadilifu atawaimarisha na kuwatunza wale wanaomwambia hivi kutoka moyoni: “Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.”—Zaburi 91:2; Methali 29:25.

Usimsahau Yehova

14. Yehova aliwapa Waisraeli onyo gani muda mfupi kabla ya kuingia Nchi ya Ahadi?

14 Muda mfupi kabla ya Waisraeli kuingia Nchi ya Ahadi, Yehova aliwaonya wasimsahau. Alisema hivi: “Jiangalie usije ukamsahau Yehova Mungu wako kwa kutozishika amri zake na maamuzi yake ya hukumu na sheria zake ambazo ninakuamuru leo; usije ukala na kushiba kwelikweli, ukajenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake, na mifugo yako na kundi lako likaongezeka, na fedha na dhahabu zikakuongezekea, na vyote vilivyo vyako vikaongezeka; nao moyo wako uinuke juu, na umsahau Yehova Mungu wako.”—Kumbukumbu la Torati 8:11-14.

15. Ni kwa njia gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba hatumsahau Yehova?

15 Je, jambo kama hilo linawezekana leo? Ndiyo, ikiwa tunatanguliza mambo yasiyofaa. Hata hivyo, tukiutafuta kwanza uadilifu wa Mungu, ibada safi itakuwa jambo la maana zaidi maishani mwetu. Kama Paulo alivyotutia moyo, ‘tutajinunulia wakati unaofaa’ na kufanya huduma yetu tukitambua kwamba muda uliobaki ni mfupi. (Wakolosai 4:5; 2 Timotheo 4:2) Hata hivyo, ikiwa tunaona starehe au njia nyingine za kupata raha kuwa muhimu sana kuliko kuhudhuria mikutano na kuhubiri, tunaweza kumsahau Yehova kwa kumpa nafasi ya pili maishani mwetu. Paulo alisema kwamba katika hizi siku za mwisho watu ‘wangependa raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Timotheo 3:4) Wakristo wanyoofu hujichunguza kwa ukawaida ili kuhakikisha kwamba hawaathiriwi na kufikiri kwa aina hiyo.—2 Wakorintho 13:5.

Jihadhari na Roho ya Kujitegemea

16. Hawa na watu wengine katika siku za Paulo walikuwa na roho gani isiyofaa?

16 Katika bustani ya Edeni, Shetani alifaulu kumnasa Hawa kwa kutumia tamaa yake ya ubinafsi ya kutaka kujitegemea. Hawa alitaka kujiamulia mema na mabaya. (Mwanzo 3:1-6) Katika karne ya kwanza, wengine katika kutaniko la Korintho walikuwa na roho kama hiyo ya kujitegemea. Walifikiri walikuwa na ujuzi kuliko Paulo, na kwa dhihaka aliwaita mitume walio bora sana.—2 Wakorintho 11:3-5; 1 Timotheo 6:3-5.

17. Tunaweza kuepukaje kusitawisha roho ya kujitegemea?

17 Katika ulimwengu leo, watu wengi ni “wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi,” na Wakristo wengine wameathiriwa na kufikiri kwa namna hiyo. Baadhi yao hata wanaipinga ile kweli. (2 Timotheo 3:4; Wafilipi 3:18) Kuhusiana na ibada safi, tunapaswa kumwomba Yehova mwongozo na tushirikiane na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na wazee wa kutaniko. Hiyo ni njia ya kuutafuta uadilifu, nayo itatulinda tusisitawishe roho ya kujitegemea. (Mathayo 24:45-47; Zaburi 25:9, 10; Isaya 30:21) Kutaniko la watiwa-mafuta ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” Yehova hulitumia kutulinda na kutuongoza. (1 Timotheo 3:15) Kutambua jukumu lake muhimu kutatusaidia tusifanye ‘jambo lolote kwa kujisifu’ tunapojitiisha kwa unyenyekevu chini ya mapenzi ya uadilifu ya Yehova.—Wafilipi 2:2-4; Methali 3:4-6.

Iweni Waigaji wa Yesu

18. Tunatiwa moyo kumwiga Yesu katika njia zipi?

18 Biblia inasema hivi kinabii kumhusu Yesu: “Umependa uadilifu nawe unachukia uovu.” (Zaburi 45:7; Waebrania 1:9) Huo ni mtazamo mzuri sana wa kuiga! (1 Wakorintho 11:1) Mbali na kujua viwango vinyoofu vya Yehova, Yesu alivipenda. Hivyo, Shetani alipomjaribu huko jangwani, Yesu hakusitasita bali alikataa katakata kuiacha “njia ya uadilifu.”—Methali 8:20; Mathayo 4:3-11.

19, 20. Kuna matokeo gani mazuri ya kuutafuta uadilifu?

19 Ni kweli kwamba tamaa mbaya za mwili zinaweza kuwa zenye nguvu. (Waroma 7:19, 20) Lakini, ikiwa uadilifu ni wenye thamani kwetu, utatuimarisha tushinde uovu. (Zaburi 119:165) Tukiupenda uadilifu sana, utatulinda tunapokabili mabaya. (Methali 4:4-6) Kumbuka kwamba kila mara tunaponaswa na kishawishi tunampa Shetani ushindi. Inafaa kama nini tumpinge na kumpa Yehova ushindi!—Methali 27:11; Yakobo 4:7, 8.

20 Kwa sababu wanatafuta uadilifu, Wakristo wa kweli ‘wamejazwa matunda ya uadilifu, ambayo ni kupitia Yesu Kristo, kwa utukufu na sifa kwa Mungu.’ (Wafilipi 1:10, 11) Wanavaa “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Waefeso 4:24) Wao ni mali ya Yehova na wanaishi ili wamtumikie, wala si kujipendeza. (Waroma 14:8; 1 Petro 4:2) Hilo ndilo huongoza fikira na matendo yao. Wao hufanya moyo wa Baba yao wa mbinguni ushangilie!—Methali 23:24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Madokezo muhimu kuhusu jinsi wazazi wanavyoweza kulinda familia yao dhidi ya uvutano wa ukosefu wa adili yanaweza kupatikana katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini ni muhimu kuutafuta uadilifu?

• Mkristo asiye mkamilifu anaweza kuutafutaje uadilifu?

• Ni mambo gani ya ulimwengu ambayo Mkristo anapaswa kuepuka?

• Kuutafuta uadilifu kunatulindaje?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa wafuasi wa Yesu, ulimwengu ulikuwa mahali hatari

[Picha katika ukurasa wa 27]

Watoto wanaofundishwa kumpenda Yehova watalindwa dhidi ya ukosefu wa adili

[Picha katika ukurasa wa 28]

Baadhi ya Waisraeli walimsahau Yehova baada ya kufanikiwa katika Nchi ya Ahadi

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kama Yesu, Wakristo wanachukia ukosefu wa uadilifu