Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwanzoni Walifukuzwa, Kisha Wakakaribishwa

Mwanzoni Walifukuzwa, Kisha Wakakaribishwa

Mwanzoni Walifukuzwa, Kisha Wakakaribishwa

MIAKA michache iliyopita, Santiago na mke wake, Lourdes, walihamia mji wenye kuvutia wa Huillcapata nchini Peru, ili kuwaeleza watu wa eneo hilo ujumbe wa Biblia. Hata hivyo, baada ya muda, kasisi mmoja alikuja kutoka Cuzco, naye akafanya mkutano pamoja na wakaaji wa mji wa Huillcapata. Kasisi huyo aliwaonya kwamba kuwapo kwa Mashahidi wa Yehova katika mji wao kutasababisha msiba mbaya na mvua kubwa ya theluji ambayo itaua ng’ombe wao na kuharibu mimea yao.

Watu wengi waliathiriwa na “unabii” huo, na kwa zaidi ya miezi sita, hakuna mtu yeyote katika mji huo aliyekubali kujifunza Biblia pamoja na Santiago na Lourdes. Ofisa mmoja wa mji huo anayeitwa Miguel, ambaye ni gavana msaidizi, aliwafukuza Santiago na Lourdes barabarani huku akiwatupia mawe. Lakini, nyakati zote wenzi hao wa ndoa walitenda kwa amani, kama Wakristo.

Baada ya muda, wakaaji fulani wa mji huo walikubali kujifunza Biblia. Hata Miguel alibadili maoni yake. Alianza kujifunza pamoja na Santiago, akaacha kunywa kileo kupita kiasi, naye akawa mtu mwenye amani. Hatimaye Miguel, mke wake, na binti zake wawili wakakubali ukweli wa Biblia.

Leo, kuna kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika mji huo. Miguel anafurahi kwamba Santiago na Lourdes hawakugongwa na mawe mengi ambayo aliwatupia, naye anawashukuru wenzi hao kwa sababu ya mfano wao mzuri wa kuwa wenye amani.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Miguel (kulia kabisa) alibadili maoni yake kwa sababu Santiago na Lourdes (juu) walikuwa wenye amani