Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Neno Linalosemwa Wakati Unaofaa Ni Jema Kama Nini!”

“Neno Linalosemwa Wakati Unaofaa Ni Jema Kama Nini!”

“Neno Linalosemwa Wakati Unaofaa Ni Jema Kama Nini!”

KWENYE kusanyiko moja la Mashahidi wa Yehova lililochukua siku nzima, Kim alijitahidi awezavyo kusikiliza na kuandika huku akihakikisha kwamba binti yake mwenye umri wa miaka miwili na nusu ameketi kwa utulivu. Mwishoni mwa programu, dada mmoja Mkristo aliyekuwa ameketi karibu alimgeukia Kim na kumpongeza kwa unyoofu kwa jinsi ambavyo yeye na mume wake walivyomshughulikia binti yao wakati wa programu. Kim alichochewa sana na pongezi hizo hivi kwamba hata sasa, miaka kadhaa baadaye, anasema hivi: “Ninapohisi nimechoka sana wakati wa mikutano, ninakumbuka maneno ya dada huyo. Maneno yake yenye fadhili yangali yananitia moyo niendelee kumzoeza binti yetu.” Naam, maneno yanayofaa yanaweza kumtia mtu moyo. Biblia inasema: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!”—Methali 15:23.

Hata hivyo, huenda wengine wetu wakaona kwamba ni vigumu kuwapongeza wengine. Nyakati nyingine, kufikiria udhaifu wetu kunaweza kufanya iwe vigumu kutoa pongezi. Mkristo mmoja anasema hivi: “Ninapowapongeza wengine mimi huhisi kwamba nimejishusha sana. Kadiri ninavyowasifu wengine, ndivyo ninavyohisi kuwa sifai.” Mambo kama vile haya, kukosa kujiamini, au kuogopa kueleweka vibaya yanaweza pia kufanya iwe vigumu kutoa pongezi. Isitoshe, ikiwa hatukupongezwa au tulipongezwa mara chache sana tulipokuwa tukikua, huenda tukaona ni vigumu kuwapongeza wengine.

Hata hivyo, tunapojua kwamba pongezi zinaweza kumtia moyo yule anayezitoa na yule anayezipokea, hilo linaweza kutuchochea tujitahidi tuwezavyo kutoa pongezi wakati unaofaa. (Methali 3:27) Basi, ni faida gani zinazotokana na kutoa pongezi? Acheni tuchunguze baadhi ya faida hizo.

Faida za Kutoa Pongezi

Pongezi zinazofaa zinaweza kumfanya yule anayepongezwa ajiamini. Mke Mkristo anayeitwa Elaine anasema: “Watu wanaponipongeza, mimi huhisi kwamba wananiamini.” Naam, kumpongeza mtu asiyejiamini kunaweza kumpa ujasiri wa kukabiliana na matatizo, na hivyo kumfanya apate shangwe. Vijana hasa hufaidika wanapopata pongezi wanazostahili. Msichana mmoja anayekubali kwamba yeye huvunjika moyo kwa sababu ya maoni yake yasiyofaa, anasema: “Nyakati zote mimi hujitahidi niwezavyo kumpendeza Yehova, lakini nyakati nyingine ninahisi kwamba hata nikijitahidi jinsi gani, jitihada zangu hazitoshi. Ninapopongezwa, mimi hujihisi vizuri sana moyoni.” Methali hii ya Biblia ni kweli kabisa: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa.”—Methali 25:11.

Pongezi zinaweza kumchochea mtu na kumtia moyo. Mhudumu mmoja wa wakati wote anasema, “Pongezi hunitia moyo kufanya kazi kwa bidii zaidi na kuboresha huduma yangu.” Mama mmoja mwenye watoto wawili anasema kwamba watoto wake wanapopongezwa na wengine katika kutaniko kwa sababu ya maelezo ambayo wanatoa mikutanoni, wao huchochewa kutoa maelezo zaidi. Naam, pongezi zinaweza kuwachochea vijana kufanya maendeleo katika maisha yao ya Kikristo. Ukweli ni kwamba sote huhitaji kuhakikishiwa kwamba tunathaminiwa. Ulimwengu huu wenye matatizo mengi unaweza kutuchosha na kutuvunja moyo sana. Mzee mmoja Mkristo anasema: “Ninapovunjika moyo nyakati nyingine, mimi huona pongezi kuwa majibu ya sala zangu.” Vivyo hivyo, Elaine anasema, “Nyakati nyingine mimi huhisi kuwa Yehova anaonyesha kwamba ananipenda kupitia maneno ya wengine.”

Kupongezwa kunaweza kumfanya mtu ahisi anapendwa na wengine. Kumpongeza mtu kwa unyoofu huonyesha kwamba tunamjali na huongeza shauku, hali ya kuaminiana, na ya kuthaminiana. Kunaonyesha kwamba tunawapenda kikweli Wakristo wenzetu na kwamba tunawathamini. Josie, ambaye ni mama, anasema: “Zamani, nilishikamana na kweli japo nilikuwa katika familia yenye imani tofauti. Wakati huo, kupongezwa na watu waliokomaa kiroho kuliniimarisha nisikate tamaa.” Kwa kweli, “sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.”—Waefeso 4:25.

Kutaka kuwapongeza wengine hutusaidia kuona mambo mema wanayofanya. Tunaona sifa nzuri za watu wengine badala ya udhaifu wao. Mzee mmoja Mkristo anayeitwa David anasema, “Kuthamini mambo ambayo wengine wanafanya kutatusaidia kuwapongeza mara nyingi zaidi.” Kukumbuka jinsi Yehova na Mwana wake wanavyowasifu mara nyingi wanadamu wasio wakamilifu kutatuchochea kutoa pongezi kwa hiari.—Mathayo 25:21-23; 1 Wakorintho 4:5.

Watu Wanaostahili Pongezi

Kwa kuwa Yehova Mungu ndiye Muumba, yeye ndiye mtu wa kwanza kabisa kati ya wale wanaostahili kusifiwa. (Ufunuo 4:11) Ingawa Yehova hahitaji tumtie moyo au kumchochea, tunapomsifu kwa sababu ya ukuu wake na fadhili zake zenye upendo, yeye hutukaribia, nasi husitawisha uhusiano pamoja naye. Kumsifu Mungu hutufanya pia tuwe na maoni yanayofaa na yenye kiasi kuhusu mafanikio yetu na hutufanya tumsifu Yehova kwa mafanikio hayo. (Yeremia 9:23, 24) Yehova hutoa tumaini la kupata uzima wa milele kwa wanadamu wote wanaostahili, na hilo ni jambo lingine linalotuchochea tumsifu. (Ufunuo 21:3, 4) Mfalme Daudi wa kale alitamani sana ‘kulisifu jina la Mungu’ na ‘kumtukuza kwa kutoa shukrani.’ (Zaburi 69:30) Acheni sisi pia tuwe na tamaa kama hiyo.

Waabudu wenzetu wanastahili kupongezwa inapofaa. Tunapowapongeza, tunatenda kupatana na amri ya Mungu ya ‘kufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.’ (Waebrania 10:24) Mtume Paulo ni mfano bora katika jambo hilo. Aliliandikia hivi kutaniko lililokuwa huko Roma: “Kwanza kabisa, namshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kuhusu ninyi nyote, kwa sababu imani yenu inazungumzwa kotekote ulimwenguni.” (Waroma 1:8) Vivyo hivyo, mtume Yohana alimpongeza Mkristo mwenzake Gayo kwa mfano wake bora wa “kutembea katika kweli.”—3 Yohana 1-4.

Leo, Mkristo mwenzetu anapoweka mfano mzuri katika kuonyesha sifa fulani ya Kikristo, anapotayarisha na kushughulikia vizuri sehemu fulani katika mkutano, au kutoa maelezo kutoka moyoni wakati wa mkutano, tunapata nafasi nzuri ya kuonyesha kwamba tunamthamini. Tunaweza pia kumpongeza mtoto anayejitahidi sana kufungua maandiko wakati wa mikutano ya kutaniko. Elaine, aliyetajwa mwanzoni, anasema: “Tumepewa zawadi mbalimbali. Tunapothamini jitihada za mtu mwingine, tunaonyesha kwamba tunathamini zawadi mbalimbali zilizomo miongoni mwa watu wa Mungu.”

Katika Familia

Namna gani juu ya kuwapongeza watu wa familia yetu? Wakati mwingi, jitihada nyingi, na upendo unahitajiwa ili mume na mke waisaidie familia yao kiroho, kihisia, na kimwili. Bila shaka, wanastahili kusikia wakipongezwa na wenzi wao na watoto wao. (Waefeso 5:33) Kwa mfano, Neno la Mungu linasema hivi kuhusu mke mwenye uwezo: “Wanawe wamesimama na kumtangaza kuwa mwenye furaha, mume wake husimama, naye humsifu.”—Methali 31:10, 28.

Watoto pia wanastahili kupongezwa. Kwa kusikitisha, wazazi fulani hupenda kuwaambia watoto wao mambo wanayopaswa kufanya, lakini hawawapongezi mara nyingi kwa jitihada zao za kutii na kuonyesha heshima. (Luka 3:22) Kwa kawaida, mtoto anapopongezwa tangu anapoanza kukua, yeye huhisi kwamba anahitajiwa, naye hujiamini.

Ni kweli kwamba jitihada zinahitajiwa ili kuwapongeza wengine, lakini tunapata faida nyingi tunapofanya hivyo. Kadiri tunavyojitahidi kuwapongeza wale wanaostahili, ndivyo furaha yetu itakavyoongezeka.—Matendo 20:35.

Kubali na Utoe Pongezi Ukiwa na Nia Nzuri

Hata hivyo, huenda kupongezwa kukasababisha tatizo kwa watu wengine. (Methali 27:21) Kwa mfano, mtu mwenye kiburi anaposifiwa anaweza kuhisi kwamba yeye ni bora kuliko wengine. (Methali 16:18) Basi, tunahitaji kuwa waangalifu. Mtume Paulo alitoa shauri hili linalofaa kabisa: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali kufikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama Mungu alivyomgawia kipimo cha imani.” (Waroma 12:3) Ili kuwasaidia wengine wasijifikirie mno, huenda ikafaa kuepuka kuwapongeza kwa sababu wana akili nyingi au sura yenye kuvutia. Badala yake, tunapaswa kuwapongeza wengine kwa matendo yao mazuri.

Pongezi zinapotolewa na kukubaliwa kwa nia nzuri, tunaweza kufaidika. Tunaweza kuchochewa kutambua kwamba Yehova ndiye ametusaidia kutimiza jambo lolote zuri ambalo tumefanya. Pia, pongezi zinaweza kututia moyo tuendelee kujiendesha kwa njia inayofaa.

Pongezi ni zawadi ambayo sisi sote tunaweza kuwapa wengine kwa unyoofu wanapoistahili. Tunapowapa wengine zawadi hiyo, inaweza kumchochea sana yule anayeipokea hata kuliko tulivyotarajia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

Barua Iliyomgusa Moyo Sana

Mwangalizi mmoja anayesafiri anakumbuka sana siku moja ambayo yeye na mke wake walirudi mahali walipokuwa wakikaa baada ya kuwa katika huduma licha ya baridi kali sana. Anasema: “Mke wangu hakuwa na furaha, naye alikuwa amevunjika moyo. Aliniambia kuwa anahisi kwamba hawezi kuendelea na kazi ya kusafiri. Mke wangu alisema, ‘Ni afadhali tuendelee na huduma ya wakati wote huku tukishirikiana na kutaniko fulani, tukae mahali pamoja, na kuongoza mafunzo yetu ya Biblia.’ Niliepuka kufanya uamuzi wakati huo, nami nikasema kwamba tutaendelea kutumikia hadi mwisho wa juma halafu tutaona jinsi atakavyohisi wakati huo. Nilimweleza kwamba ikiwa atahisi kuwa anataka kuacha kazi ya kusafiri, nitaheshimu maoni yake. Siku hiyohiyo, tulienda posta, nasi tukapata barua kutoka kwenye ofisi ya tawi ambayo ilitumwa kwa mke wangu. Barua hiyo ilimpongeza sana kwa sababu ya jitihada zake katika huduma ya shambani na uvumilivu wake, nayo ikaeleza jinsi ilivyo vigumu kulala katika kitanda tofauti kila juma. Mke wangu aliguswa moyo sana na pongezi hizo hivi kwamba hakuzungumza tena kuhusu kuacha kazi ya kusafiri. Hata alinitia moyo mara kadhaa niendelee na kazi hiyo wakati nilipotaka kuiacha.” Wenzi hao wa ndoa waliendelea na kazi ya kusafiri kwa miaka 40 hivi.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ni nani katika kutaniko lenu anayestahili kupongezwa?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Watoto hujihisi vizuri wanapoonyeshwa upendo na kupongezwa