Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangwe na Matatizo ya Kuwalea Watoto Wanane Ili Wafuate Njia za Yehova

Shangwe na Matatizo ya Kuwalea Watoto Wanane Ili Wafuate Njia za Yehova

Simulizi la Maisha

Shangwe na Matatizo ya Kuwalea Watoto Wanane Ili Wafuate Njia za Yehova

LIMESIMULIWA NA JOYCELYN VALENTINE

Mwaka wa 1989, mume wangu alienda kufanya kazi katika nchi nyingine. Aliahidi kunitumia pesa ili niweze kuwatunza watoto wangu wanane. Majuma yalipita bila kupokea habari zozote juu yake. Kisha miezi ikapita bila kuwasiliana na mume wangu. Niliendelea kujifariji kwamba, ‘Punde tu atakapofanikiwa, atarudi nyumbani.’

NILIPATWA na mfadhaiko kwa kuwa sikuwa na pesa za kutunza familia yangu. Mara nyingi nilikosa usingizi usiku huku nikijiuliza hivi kwa mshangao, ‘Anawezaje kuitendea hivi familia yake?’ Hatimaye, ilinibidi nikubali kwamba mume wangu ametuacha. Leo, miaka 16 hivi imepita tangu alipotuacha, na bado hajarudi. Hivyo, niliwalea watoto wangu bila kusaidiwa na mwenzi wa ndoa. Imekuwa vigumu kufanya hivyo, lakini nimepata shangwe nyingi kwa kuwaona watoto wangu wakikubali kufuata njia za Yehova. Hata hivyo, kabla sijasimulia jinsi tulivyofanikiwa tukiwa familia, acheni niwaeleze kuhusu malezi yangu.

Kutafuta Mwongozo wa Biblia

Nilizaliwa mwaka wa 1938 kwenye kisiwa cha Karibea cha Jamaika. Ingawa Baba hakushirikiana na dini yoyote, alijiona kuwa mtu anayemwogopa Mungu. Usiku, aliniomba mara nyingi nimsomee kitabu cha Biblia cha Zaburi. Baada ya muda, niliweza kukariri zaburi nyingi. Mama alishirikiana na kanisa moja lililokuwa karibu, na mara kwa mara alinipeleka kwenye mikutano ya kidini.

Kwenye mikutano hiyo, tuliambiwa kwamba Mungu huwapeleka watu wazuri mbinguni na kuwateketeza wabaya milele katika moto wa mateso. Pia, tuliambiwa kwamba Yesu ni Mungu na kwamba anawapenda watoto. Nilichanganyikiwa na nikamwogopa Mungu. Nilijiuliza hivi, ‘Mungu anayetupenda anawezaje kuwatesa watu motoni?’

Niliogopeshwa sana nilipofikiria moto wa mateso. Baada ya muda, nilianza masomo ya Biblia ambayo yalitolewa na Kanisa la Seventh-Day Adventist kupitia barua. Walifundisha kwamba waovu hawatateswa milele, bali watateketezwa motoni na kuwa majivu. Mafundisho hayo yalionekana kuwa yanapatana na akili, nami nikaanza kuhudhuria mikutano yao ya kidini. Lakini mafundisho yao yalinivuruga akili, na mambo niliyojifunza hayakubadili maoni yangu yasiyofaa kuhusu maadili.

Wakati huo, kwa ujumla watu walikubali kwamba uasherati ni kosa. Lakini, mimi na watu wengine wengi tuliamini kwamba waasherati ni wale tu wanaofanya ngono pamoja na watu wengi. Hivyo, tuliamini kwamba si dhambi kwa watu wawili ambao hawajaoana kufanya ngono pamoja maadamu hawafanyi ngono na mtu mwingine. (1 Wakorintho 6:9, 10; Waebrania 13:4) Kwa sababu ya kuwa na maoni hayo, nilipata watoto sita kabla ya kuolewa.

Kufanya Maendeleo ya Kiroho

Katika mwaka wa 1965, Vaslyn Goodison na Ethel Chambers walikuja kuishi katika kijiji cha karibu cha Bath. Walikuwa mapainia, au wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, na siku moja walizungumza na baba yangu. Baba alikubali kujifunza Biblia pamoja nao. Walizungumza na mimi pia wakati waliponipata nyumbani. Ingawa nilikuwa na shaka sana kuhusu Mashahidi wa Yehova, niliamua kujifunza Biblia pamoja nao ili kuthibitisha kwamba hawafundishi ukweli.

Niliuliza maswali mengi wakati wa funzo, na Mashahidi waliyajibu yote kwa kutumia Biblia. Kwa msaada wao, niligundua kwamba wafu hawajui lolote na hawateseki katika moto wa mateso. (Mhubiri 9:5, 10) Pia, nilijifunza kuhusu tumaini la uzima wa milele katika Paradiso duniani. (Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 21:3, 4) Ingawa baba yangu aliacha kujifunza Biblia, nilianza kuhudhuria mikutano katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la eneo hilo. Kwa kuwa mikutano hiyo iliongozwa kwa njia ya amani na utaratibu, niliweza kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova. Pia, nilihudhuria makusanyiko makubwa ya Mashahidi kama vile makusanyiko ya mzunguko na ya wilaya. Kufahamu Biblia kupitia njia hizo kulinichochea nitamani sana kumwabudu Yehova kwa njia anayoikubali. Hata hivyo, nilikabili kizuizi fulani.

Wakati huo, nilikuwa nikiishi pamoja na baba ya watoto wangu watatu kati ya watoto wangu sita. Hatukuwa tumefunga ndoa. Kupitia Biblia, nilijifunza kwamba Mungu hushutumu ngono nje ya ndoa, na dhamiri yangu ilianza kunisumbua. (Methali 5:15-20; Wagalatia 5:19) Upendo wangu kwa ajili ya ukweli ulipoongezeka, nilitamani kuishi kulingana na sheria ya Mungu. Hatimaye, nikafanya uamuzi. Nilimweleza mwanamume huyo tuliyeishi naye kwamba tusipofunga ndoa basi nitakatiza uhusiano wetu. Ingawa hakukubali mambo niliyoamini, tulifunga ndoa kisheria mnamo Agosti 15, 1970, miaka mitano baada ya Mashahidi kuzungumza pamoja nami kwa mara ya kwanza. Mnamo Desemba 1970, nilionyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji.

Siwezi kusahau siku ya kwanza ambayo nilishiriki katika kazi ya kuhubiri. Nilikuwa na wasiwasi, nami sikujua jinsi ya kuanzisha mazungumzo ya Biblia. Nilifurahi sana wakati mwenye nyumba wa kwanza alipokatiza mazungumzo haraka. Lakini baada ya muda niliacha kuwa na wasiwasi. Mwishoni mwa siku hiyo, nilifurahi sana, kwa sababu nilikuwa nimezungumza kwa ufupi na watu kadhaa kuhusu Biblia na nilikuwa nimewaachia baadhi ya vichapo vyetu vya Biblia.

Kufanya Familia Iendelee Kuwa Imara Kiroho

Kufikia mwaka wa 1977, nilikuwa na watoto wanane. Niliazimia kujitahidi juu chini kuisaidia familia yangu kumtumikia Yehova. (Yoshua 24:15) Hivyo, nilijitahidi sana kuongoza funzo la Biblia kwa ukawaida katika familia. Nyakati nyingine, kwa sababu ya uchovu, nilikuwa nikisinzia wakati mtoto mmoja alipokuwa akisoma fungu kwa sauti, kisha wale watoto wengine waliniamsha. Lakini uchovu haukutuzuia kamwe tusijifunze Biblia katika familia.

Pia, nilisali mara nyingi sana pamoja na watoto wangu. Walipokuwa wakubwa kidogo, niliwafundisha kusali kwa Yehova kibinafsi. Nilihakikisha kwamba kila mmoja wao anasali kabla ya kulala. Nilisali pamoja na kila mmoja wa watoto wangu wachanga ambao hawangeweza kusali peke yao.

Mwanzoni, mume wangu hakutaka niende na watoto kwenye mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, upinzani wake ulipungua alipotambua kwamba angehitaji kuwatunza watoto wakati ambapo ningekuwa mikutanoni. Usiku, alipenda kuwatembelea rafiki zake. Lakini hakupenda wazo hilo alipotambua kwamba atahitaji kuandamana na watoto wanane! Baadaye, hata alianza kunisaidia kuwatayarisha watoto ili waende kwenye Jumba la Ufalme.

Baada ya muda, watoto walizoea kuhudhuria mikutano yote ya kutaniko na kuhubiri. Walipofunga shule wakati wa kiangazi, mara nyingi walienda kuhubiri pamoja na mapainia, au wahudumu wa wakati wote, wa kutaniko letu. Hilo liliwasaidia watoto wangu kupenda sana kutaniko na kazi ya kuhubiri.—Mathayo 24:14.

Nyakati za Majaribu

Ili kuongeza mapato ya familia, mume wangu alianza kusafiri katika nchi nyingine kwa ajili ya kazi. Alikaa kwa muda mrefu mbali na familia lakini alikuwa akirudi kwa ukawaida baada ya kipindi fulani. Hata hivyo, mwaka wa 1989, aliondoka na hakurudi. Kama nilivyotaja mwanzoni, nilifadhaika sana mume wangu alipotuacha. Mara nyingi nililia usiku na kusali kwa Yehova kwa bidii ili anifariji na anisaidie kuvumilia, nami nilihisi akijibu sala zangu. Maandiko kama vile Isaya 54:4 na 1 Wakorintho 7:15 yalinipa amani ya akili na nguvu za kuendelea na maisha. Pia, katika kutaniko la Kikristo watu wa ukoo na marafiki walinitegemeza kihisia na kimwili. Ninamshukuru sana Yehova na watu wake kwa msaada wao.

Tulipatwa na majaribu mengine. Wakati fulani, binti yangu mmoja aliondolewa kutanikoni kwa sababu ya mwenendo usiopatana na maandiko. Ninawapenda sana watoto wangu wote, lakini mimi hutanguliza ushikamanifu wangu kwa Yehova. Kwa hiyo, katika kipindi hicho, mimi na wale watoto wangu wengine tulishikamana na mwongozo wa Biblia kuhusu watu waliotengwa na ushirika. (1 Wakorintho 5:11, 13) Tulishutumiwa sana na watu ambao hawakuelewa msimamo wetu. Hata hivyo, baada ya binti yangu kurudishwa kutanikoni, mume wake aliniambia kwamba alivutiwa na msimamo wetu thabiti kwa ajili ya kanuni za Biblia. Sasa mume wa binti yangu anamtumikia Yehova pamoja na familia yake.

Kukabili Matatizo ya Kiuchumi

Mume wangu alipotuacha, sikuwa na kazi ya kutegemeka, naye aliacha kabisa kuitegemeza familia yetu kifedha. Hali hiyo ilitufundisha kuridhika na maisha rahisi na kuthamini mambo ya kiroho zaidi ya mambo ya kimwili. Watoto wangu walisitawisha uhusiano wa karibu zaidi walipojifunza kupendana na kusaidiana. Wale wakubwa walipoanza kufanya kazi, waliwasaidia kwa hiari wadogo wao. Binti yangu mkubwa Marseree alimsaidia dada yake mdogo kabisa, Nicole, kumaliza masomo ya sekondari. Isitoshe, nilianzisha duka dogo. Pesa chache nilizopata zilinisaidia kushughulikia baadhi ya mahitaji yetu ya kimwili.

Yehova hajatuacha kamwe. Wakati fulani, nilimwambia dada mmoja Mkristo kwamba hatutaweza kuhudhuria kusanyiko la wilaya kwa sababu ya hali za kiuchumi. Dada huyo aliniambia: “Dada Val, utakaposikia kuhusu kusanyiko, anza kujitayarisha kusafiri! Yehova atashughulikia mahitaji yako.” Nilifuata shauri lake. Yehova alishughulikia mahitaji yetu, naye anaendelea kufanya hivyo. Familia yetu haijakosa kamwe kusanyiko kwa sababu ya pesa.

Mwaka wa 1988, Kimbunga kinachoitwa Gilbert kilisababisha uharibifu nchini Jamaika, nasi tuliondoka nyumbani kwetu ili kutafuta makao katika mahali salama zaidi. Dhoruba hiyo ilipopungua, mimi na mwana wangu tuliondoka mahali tulipokimbilia ili kukagua nyumba yetu ambayo sasa ilikuwa imeharibiwa. Tulipokuwa tukikagua vitu vilivyoharibiwa, niliona kitu nilichotaka kuchukua. Kwa ghafula, pepo zikavuma tena, lakini niliendelea kukishika kitu hicho. “Mama, achana na televisheni hiyo. Je, wewe ni mke wa Loti?” (Luka 17:31, 32) Maneno hayo ya mwana wangu yaliamsha fikira zangu. Niliangusha televisheni hiyo iliyokuwa imelowa maji, nasi tukakimbia ili kujiokoa.

Mimi hutetemeka ninapokumbuka jinsi nilivyohatarisha maisha yangu kwa ajili ya televisheni tu. Lakini mimi huchangamka ninapokumbuka maneno hayo ya mwana wangu yaliyoonyesha hali yake thabiti ya kiroho. Kwa sababu ya mazoezi mazuri ya Biblia aliyopata katika kutaniko la Kikristo, alinisaidia kuepuka kuumia kimwili na labda kiroho pia.

Kimbunga hicho kiliharibu nyumba yetu, mali zetu, na kutuvunja moyo sana. Baadaye, ndugu zetu Wakristo waliwasili. Walitutia moyo tukabili hasara hiyo kwa kumtegemea Yehova na kuendelea kushiriki kwa bidii katika huduma, nao wakatusaidia kujenga upya nyumba yetu. Kazi hiyo ya upendo na kujidhabihu, iliyofanywa na Mashahidi waliojitolea kutoka Jamaika na nchi nyingine, ilitutia moyo sana.

Kumtanguliza Yehova

Baada ya kumaliza masomo, mtoto wangu wa pili, Melaine, alitumikia akiwa painia. Halafu akakubali kutumikia akiwa painia katika kutaniko lingine, ingawa ilimbidi aache kazi. Ingawa kazi hiyo ilimwezesha kuisaidia sana familia yetu kifedha, tuliamini kwamba Yehova angetutunza ikiwa kila mmoja wetu angetanguliza mambo ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Baadaye, mwana wangu, Ewan, aliombwa pia atumikie akiwa painia. Ingawa alikuwa akiisaidia familia kifedha, tulimtia moyo akubali mwaliko huo huku tukimhakikishia kwamba Yehova atambariki. Sijawahi kamwe kuwavunja moyo watoto wangu wasisonge mbele katika utumishi wa Ufalme, na sisi tuliobaki nyumbani hatujakosa kamwe mambo ya msingi. Badala yake, shangwe yetu imeongezeka, na nyakati nyingine tumewasaidia wengine wenye uhitaji.

Leo, ninashangilia sana kuwaona watoto wangu ‘wakiendelea kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 4) Kwa sasa, binti yangu mmoja, Melaine, anamuunga mkono mume wake ambaye ni mwangalizi wa mzunguko. Binti yangu Andrea na mume wake ni mapainia wa pekee, naye huandamana pamoja na mume wake anapotembelea makutaniko akiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala. Mwana wangu, Ewan, na mke wake ni mapainia wa pekee, na Ewan ni mzee wa kutaniko. Binti yangu mwingine, Ava-Gay, anafanya kazi pamoja na mume wake kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Jamaika. Jennifer, Genieve, na Nicole wanatumikia kwa bidii katika makutaniko mbalimbali pamoja na waume wao na watoto wao. Mimi huishi na Marseree, nasi tuko katika Kutaniko la Port Morant. Nimepata baraka chungu nzima kwa sababu watoto wangu wote wanane wanaendelea kumwabudu Yehova.

Nimepatwa na magonjwa fulani kadiri umri wangu unavyosonga. Ingawa nina ugonjwa wa baridi yabisi, bado ninafurahia kuwa painia. Wakati fulani uliopita, ilikuwa vigumu sana kwangu kutembea kwenye vilima karibu na mahali nilipoishi. Ilikuwa vigumu kwenda katika huduma. Nilijaribu kuendesha baiskeli, nami nikatambua kwamba kufanya hivyo ni rahisi zaidi kuliko kutembea. Basi nikanunua baiskeli ambayo tayari ilikuwa imetumika. Mwanzoni, watoto wangu hawakufurahia kuona mama yao anayeugua baridi yabisi akiendesha baiskeli. Hata hivyo, walifurahia sana kuona nikiendelea kuhubiri kulingana na tamaa ya moyo wangu.

Ninashangilia sana kuona watu niliojifunza nao wakikubali ukweli wa Biblia. Sikuzote ninasali kwa Yehova awasaidie wote katika familia yangu waendelee kuwa waaminifu kwake katika wakati huu wa mwisho hadi milele. Ninamsifu na kumshukuru Yehova, “Msikiaji [Mkuu] wa Sala,” kwa kunisaidia kufanikiwa kuwalea watoto wangu wanane kufuata njia zake.—Zaburi 65:2.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa na watoto wangu, wenzi wao wa ndoa, na wajukuu wangu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Sasa ninatumia baiskeli ili kutimiza huduma yangu