Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walifurahisha Mioyo ya Wazazi Wao

Walifurahisha Mioyo ya Wazazi Wao

Walifurahisha Mioyo ya Wazazi Wao

“MWANANGU, ikiwa moyo wako umekuwa na hekima, moyo wangu utashangilia, naam, moyo wangu.” (Methali 23:15) Bila shaka, wazazi Wakristo hufurahi watoto wao wanapopata hekima kutoka kwa Mungu. Mnamo Jumamosi, Septemba 10, 2005, watu 6,859 kutoka mataifa mbalimbali walihudhuria kuhitimu kwa darasa la 119 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Wote walishangilia, lakini hasa wazazi wa wale 56 waliohitimu.

David Walker, ambaye amekuwa katika Betheli ya Marekani kwa muda mrefu, alifungua programu kwa sala ya kutoka moyoni. Kisha, mwenyekiti, David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, akaanzisha programu hiyo kwa kuwaambia wazazi wa wale waliokuwa wakihitimu hivi: “Mnastahili kupongezwa sana. Sifa ambazo mmewasaidia wana na binti zenu kusitawisha zimewachochea kuwa wamishonari.” Huenda wazazi hao walikuwa na wasiwasi kwa sababu karibuni wana na binti zao wangepewa migawo katika nchi za mbali. Hata hivyo, Ndugu Splane aliwahakikishia hivi: “Msiwe na wasiwasi kuhusu watoto wenu. Yehova anaweza kuwatunza vizuri zaidi kuliko mnavyoweza.” Kisha akasema: “Fikirieni mambo mazuri ambayo wana na binti zenu watafanya. Watu wanaoteseka watapata faraja kwa mara ya kwanza maishani mwao.”

Jinsi ya Kuendelea Kuwafanya Wengine Washangilie

Mwenyekiti aliwakaribisha wasemaji wanne. Kwanza, Ralph Walls wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani alizungumzia kichwa hiki, “Fungueni Macho Yenu.” Alikazia kwamba upofu wa kiroho ni mbaya zaidi kuliko upofu halisi. Kutaniko la karne ya kwanza la Laodikia lilikuwa na upofu wa kiroho. Wakristo wa kutaniko hilo waliokuwa vipofu kiroho walisaidiwa, lakini ni afadhali kuzuia upofu huo kwa kufungua macho yetu ya kiroho. (Ufunuo 3:14-18) Msemaji huyo alisema hivi: “Fungueni macho yenu, na mwaone wanaume wenye madaraka kama Yehova anavyowaona.” Wahitimu hawapaswi kuhangaika sana kunapokuwa na matatizo kutanikoni. Bwana Yesu Kristo anajua mambo hayo yote. Atahakikisha kwamba yanashughulikiwa kwa wakati unaofaa.

Kisha, Samuel Herd wa Baraza Linaloongoza akajibu swali hili “Je, Mko Tayari?” Kama vile msafiri anavyobeba mavazi anayohitaji, sikuzote wahitimu wanapaswa kujivika sifa za utu mpya. Wanahitaji kuwa wenye huruma kama Yesu. Mtu mwenye ukoma alipomwambia hivi: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu alimwambia: “Ninataka. Takasika.” (Marko 1:40-42) Kisha msemaji akasema: “Ikiwa kwa kweli mnataka kuwasaidia watu, mtatafuta njia ya kufanya hivyo.” Andiko la Wafilipi 2:3 linawaambia Wakristo wawaone wengine ‘kuwa bora.’ Ndugu Herd alisema hivi: “Kuwa mnyenyekevu ni muhimu kuliko kuwa na ujuzi. Watu mnaowahubiria na pia ndugu na dada zenu kutanikoni watafaidika na ujuzi wenu ikiwa tu ninyi ni wanyenyekevu.” Alimalizia kwa kusema kwamba ikiwa wahitimu wanaendelea kujivika upendo wa Kikristo, basi wako tayari kwenda kwenye migawo yao, wakiwa na uhakika kwamba watafanikiwa.—Wakolosai 3:14.

Kichwa cha hotuba ya Mark Noumair, mmoja wa walimu wa Gileadi, kiliwatia hamu wasikilizaji. Kilikuwa, “Je, Mtaidumisha?” Kile kinachohitaji kudumishwa ni uthamini wetu kwa ajili ya wema wa Yehova. Andiko la Zaburi 103:2 linasema: “Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu, wala usiyasahau matendo yake yote.” Waisraeli walikosa kuithamini mana ambayo iliwategemeza, nao wakaiita “mkate wa kudharaulika.” (Hesabu 21:5) Kadiri wakati ulivyopita, thamani ya mana haikubadilika, lakini uthamini wao ulikwisha. Mwalimu huyo alisema: “Mkisahau matendo ya Yehova na kuona utumishi wenu katika nchi nyingine kuwa jambo la kawaida tu, hilo litaathiri jinsi mnavyoona kazi ambayo Yehova amewapa.” Andiko la Zaburi 103:4 linasema kwamba Yehova ‘anawavika taji la fadhili zenye upendo.’ Wahitimu wataona fadhili zenye upendo za Mungu katika makutaniko yao mapya.

Mwalimu mwingine wa Gileadi, Lawrence Bowen, alizungumzia kichwa hiki “Je, Utapata Baraka?” Alisema kwamba wahitimu wa darasa la 119 la Gileadi wamefanya mazoezi mengi ili wawe wamishonari wenye mafanikio. Lakini sasa, wanapaswa kushikamana na Yehova na kazi ambayo amewapa. Kwenye Ufunuo 14:1-4, wale 144,000 wanasemwa kuwa “wale wanaoendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda.” Wote katika kikundi hicho hushikamana kwa uaminifu pamoja na Yehova na Mwana wake licha ya majaribu yao, nao hufikia mradi wao. Msemaji huyo akasema: “Katika hali yoyote ile, sisi pia hushikamana kwa uaminifu na Yehova na kazi ambayo ametugawia.” Kwa kufanya hivyo, wahitimu wataona kwamba baraka za Yehova ‘zinawafikia.’—Kumbukumbu la Torati 28:2.

Kupata Matokeo Katika Utumishi Wao

Wakati wa masomo yao, wanafunzi walihubiri kila mwishoni mwa juma. Msajili wa shule hiyo, Wallace Liverance, alipowahoji, ilikuwa wazi kwamba walifanikiwa. Walihubiri habari njema katika lugha kumi hivi na kuanzisha mafunzo ya Biblia. Wenzi fulani wa ndoa katika darasa hilo walianza kujifunza Biblia na mwanamume Mchina. Baada ya kumtembelea mara mbili, walimuuliza jinsi alivyohisi kuhusu kujifunza juu ya Yehova. Alifungua Biblia yake na kuwaomba wasome Yohana 17:3. Aliona kwamba yuko kwenye barabara ya uzima.

Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza aliwahoji ndugu watatu wanaotumika katika Halmashauri ya Tawi ya Côte d’Ivoire, Jamhuri ya Dominika, na Ekwado. Ndugu hao waliwahakikishia wahitimu kwamba Halmashauri za Tawi zinawatazamia na zitawasaidia kuzoea migawo yao.

Kisha, Leonard Pearson wa Betheli ya Marekani aliwahoji washiriki watatu wa Halmashauri ya Tawi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Papua New Guinea, na Uganda. Ndugu hao waliwatia moyo wahitimu wahubiri kwa bidii. Wenzi fulani wamishonari ambao wametumika nchini Kongo kwa zaidi ya miaka 21 wamewasaidia watu 60 kufikia wakfu na ubatizo. Sasa wenzi hao huongoza mafunzo 30 ya Biblia, na 22 kati yao wanahudhuria mikutano ya kutaniko. Kukiwa na mavuno hayo mengi ya kiroho, huu ndio wakati mzuri wa kuwa mmishonari.

Kutoa Ushahidi kwa Kutambua Kwamba Wakati Ni Mfupi

Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya mwisho. Kichwa cha hotuba yake kilikuwa “Kusema Juu ya Mungu na Kutoa Ushahidi Kumhusu Yesu Katika Siku ya Bwana.” Maneno “ushahidi,” “mashahidi,” na “kutoa ushahidi” yanapatikana mara 19 katika kitabu cha Ufunuo. Hivyo, Yehova anaeleza wazi kazi ambayo amewapa watu wake. Tunapaswa kutoa ushahidi huo wakati gani? Ni katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:9, 10) Siku hiyo ilianza mwaka wa 1914, inaendelea wakati huu, na itaendelea wakati ujao. Kulingana na Ufunuo 14:6, 7, kazi ya kusema kumhusu Mungu inaungwa mkono na malaika. Andiko la Ufunuo 22:17 linaonyesha kwamba jukumu la kuongoza kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu limekabidhiwa mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta. Lakini sote tunapaswa kutumia pendeleo hilo sasa. Katika mstari wa 20, Yesu ananukuliwa akisema: “Ninakuja upesi.” Ndugu Lösch aliwahimiza hivi wote waliohudhuria: “Waambieni watu, ‘Njooni, mchukue maji ya uzima bure.’ Yesu anakuja upesi. Je, tuko tayari?”

Fred Rusk, ambaye alikuwa mwalimu wa Shule ya Gileadi kwa miaka 11, alimalizia programu kwa sala ya shukrani kwa Yehova ambayo iligusa mioyo ya watu waliohudhuria. Ilikuwa njia bora ya kumalizia siku iliyoleta shangwe kubwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 10

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 25

Idadi ya wanafunzi: 56

Wastani wa umri: 32.5

Wastani wa miaka katika kweli: 16.4

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12.1

[Picha katika ukurasa wa 15]

Darasa la 119 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Helgesen, S.; Daugaard, H.; Pierluissi, A.; Joseph, I.; Racanelli, C. (2) Byrge, T.; Butler, D.; Freedlun, J.; Nuñez, K.; Pavageau, C.; Doumen, T. (3) Camacho, O.; Lindqvist, L.; Broomer, A.; Wessels, E.; Burton, J.; Woodhouse, O.; Doumen, A. (4) Tirion, A.; Connally, L.; Fournier, C.; Gil, A.; Johnsson, K.; Hamilton, L. (5) Byrd, D.; Scribner, I.; Camacho, B.; Laschinski, H.; Hallahan, M.; Libuda, O. (6) Joseph, A.; Lindqvist, M.; Helgesen, C.; Nuñez, D.; Scribner, S.; Fournier, J. (7) Pierluissi, F.; Pavageau, T.; Broomer, C.; Racanelli, P.; Butler, T.; Woodhouse, M.; Libuda, J. (8) Laschinski, M.; Freedlun, S.; Burton, I.; Tirion, M.; Byrd, M.; Byrge, J. (9) Wessels, T.; Hallahan, D.; Connally, S.; Gil, D.; Daugaard, P.; Hamilton, S.; Johnsson, T.