Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu

Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu

Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu

AKIFAFANUA maono aliyoona kuhusiana na malaika wa Mungu, nabii Danieli aliandika hivi: “Kulikuwa na maelfu elfu [ya malaika] walioendelea kumtumikia [Mungu], na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Danieli 7:10) Mstari huo unaonyesha kusudi la Mungu la kuwaumba malaika. Waliumbwa ili wamtumikie, nao wako tayari kutimiza maagizo yake.

Wakati mwingine Mungu huwatumia malaika kufanya mambo fulani yanayowahusu wanadamu. Tutazungumzia jinsi anavyowatumia kuwaimarisha na kuwalinda watu wake, kupeleka ujumbe kwa wanadamu, na kutekeleza hukumu yake juu ya waovu.

Malaika Huimarisha na Kulinda

Tangu viumbe wa roho waliposhuhudia kuumbwa kwa dunia na kwa wanadamu wa kwanza, wameonyesha kwamba wanapendezwa sana na wanadamu. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu Kristo anayefananishwa na hekima, alisema hivi: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.” (Methali 8:31) Biblia inatuambia kwamba “malaika wanatamani kuchungulia” mambo yanayomhusu Kristo na mambo ya wakati ujao ambayo yamefunuliwa kwa manabii wa Mungu.—1 Petro 1:11, 12.

Kadiri muda unavyopita, malaika wameona kwamba wanadamu wengi hawamtumikii Muumba wao mwenye upendo. Hilo limewahuzunisha sana malaika waaminifu! Kwa upande mwingine, mtenda-dhambi mmoja anapotubu na kugeuka kumwelekea Yehova, “shangwe hutokea kati ya malaika.” (Luka 15:10) Malaika wanawahangaikia sana wale wanaomtumikia Mungu, na Yehova amewatumia tena na tena kuwaimarisha na kuwalinda watumishi wake waaminifu hapa duniani. (Waebrania 1:14) Fikiria mifano kadhaa.

Malaika wawili walimsaidia Loti na binti zake kuokoka uharibifu kwa kuwatoa nje ya Sodoma na Gomora, yale majiji maovu. * (Mwanzo 19:1, 15-26) Karne nyingi baadaye, ingawa nabii Danieli alitupwa ndani ya shimo la simba, hakuumizwa. Kwa nini? Alisema hivi: “Mungu wangu mwenyewe alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:22) Malaika walimsaidia Yesu mwanzoni mwa huduma yake duniani. (Marko 1:13) Muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu, malaika alimtokea na “akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Msaada wa malaika ulimtia Yesu moyo sana hasa wakati huo muhimu maishani mwake! Pia, malaika alimfungua mtume Petro kutoka gerezani.—Matendo 12:6-11.

Je, malaika hutulinda leo? Tukimwabudu Yehova kulingana na Neno lake, tunaweza kuwa na uhakika kwamba malaika wake wenye nguvu wasioonekana watatulinda. Biblia inaahidi hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.”—Zaburi 34:7.

Hata hivyo, ni lazima tukumbuke kwamba malaika wanamtumikia Mungu wala si wanadamu. (Zaburi 103:20, 21) Wanafuata mwongozo wa Mungu bali si maagizo au maombi ya wanadamu. Hivyo, Yehova Mungu ndiye tunayepaswa kuomba msaada, si malaika. (Mathayo 26:53) Bila shaka, kwa kuwa hatuwaoni malaika, hatuwezi kujua ni kwa kadiri gani Mungu huwatumia kuwasaidia watu katika hali mbalimbali. Lakini tunajua kwamba Yehova ‘huonyesha nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9; Zaburi 91:11) Tuna uhakika kwamba “hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye [Mungu] hutusikia.”—1 Yohana 5:14.

Pia, Maandiko yanatuambia kwamba sala zetu na ibada yetu inapaswa kuelekezwa kwa Mungu peke yake. (Kutoka 20:3-5; Zaburi 5:1, 2; Mathayo 6:9) Malaika waaminifu hututia moyo tufanye hivyo. Kwa mfano, wakati mtume Yohana alipotaka kumwabudu malaika fulani, kiumbe huyo wa roho alimkaripia na kumwambia hivi: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Mwabudu Mungu.”—Ufunuo 19:10.

Malaika Hupeleka Ujumbe wa Mungu

Neno “malaika” humaanisha “mjumbe.” Kwa hiyo, malaika humtumikia Mungu pia wakiwa wajumbe wake kwa wanadamu. Kwa mfano, “malaika Gabrieli alitumwa kutoka kwa Mungu mpaka jiji moja la Galilaya linaloitwa Nazareti.” Kwa nini? Ili kumjulisha Maria, ambaye alikuwa bikira kwamba angechukua mimba katika tumbo lake la uzazi na kuzaa mwana ambaye angeitwa Yesu. (Luka 1:26-31) Pia, malaika alitumwa kwa wachungaji kondeni kuwaambia kwamba “Kristo Bwana” alikuwa amezaliwa. (Luka 2:8-11) Vivyo hivyo, malaika walipeleka ujumbe wa Mungu kwa Abrahamu, Musa, Yesu, na wengineo wanaozungumziwa katika Biblia.—Mwanzo 18:1-5, 10; Kutoka 3:1, 2; Luka 22:39-43.

Malaika hutumikaje kama wajumbe wa Mungu leo? Fikiria kazi ambayo Yesu alitabiri wafuasi wake wangefanya kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo. Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:3, 14) Mashahidi wa Yehova hutumia zaidi ya saa bilioni moja kila mwaka kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Lakini je, ulijua kwamba malaika pia wanahusika katika kazi hiyo? Mtume Yohana alisema hivi akirejelea maono aliyoona: “Nikamwona malaika mwingine . . . , naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6, 7) Andiko hilo linaonyesha kazi muhimu zaidi ambayo malaika wanafanya kwa ajili ya wanadamu leo.

Mashahidi wa Yehova wanapohubiri nyumba kwa nyumba, wao hutambua kwamba wanaelekezwa na malaika. Mara nyingi wao hukuta watu ambao wametoka tu kuomba wapate mtu awasaidie kuelewa makusudi ya Mungu. Kwa sababu ya mwongozo wa malaika na jitihada za Mashahidi, kila mwaka mamia ya maelfu ya watu hupata kumjua Yehova. Unaweza kufaidika kutokana na kazi hii ya kuokoa uhai inayofanywa chini ya mwongozo wa malaika.

Malaika Hutekeleza Hukumu ya Mungu

Ingawa malaika hawakupewa mamlaka ya kuwahukumu wanadamu, wao si watazamaji tu. (Yohana 5:22; Waebrania 12:22, 23) Walitekeleza hukumu za Mungu wakati uliopita. Kwa mfano, Mungu aliwatumia malaika kuwapiga Wamisri wa kale waliowafanya Waisraeli kuwa watumwa. (Zaburi 78:49) Katika usiku mmoja “malaika wa Yehova” aliwaua askari 185,000 katika kambi ya adui za watu wa Mungu.—2 Wafalme 19:35.

Pia, wakati ujao malaika watatekeleza hukumu kali ya Mungu. Yesu atakuja “pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.” (2 Wathesalonike 1:7, 8) Hata hivyo, uharibifu huo utaletwa juu ya wale tu wasioitikia ujumbe ambao unahubiriwa duniani pote kwa msaada wa malaika. Wale wanaomtafuta Mungu na kutii mafundisho ya Maandiko hawatapata madhara.—Sefania 2:3.

Tunawathamini sana malaika hao waaminifu ambao sikuzote hutekeleza maagizo ya Mungu! Yehova huwatumia kuwasaidia na kuwalinda watumishi wake washikamanifu walio duniani. Hilo linatufariji hasa kwa sababu kuna viumbe wa roho hatari ambao wanaitwa roho waovu wanaotaka kutudhuru.

Roho Waovu Wao Ni Akina Nani?

Kwa karne 15 tangu Shetani alipomdanganya Hawa katika bustani ya Edeni, familia ya Mungu ya malaika ilishuhudia kwamba Shetani Ibilisi alifaulu kuwageuza wanadamu wote kumwacha Mungu isipokuwa watu wachache waaminifu, kama vile Abeli, Enoko, na Noa. (Mwanzo 3:1-7; Waebrania 11:4, 5, 7) Pia, baadhi ya malaika walimfuata Shetani. Biblia inawataja kuwa roho ambao hawakutii “katika siku za Noa.” (1 Petro 3:19, 20) Kutotii kwao kulionekanaje?

Katika siku za Noa, malaika fulani waliacha mahali pao katika familia ya Mungu ya mbinguni, wakaja duniani na kujivika miili ya wanadamu. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa wamekuza tamaa ya kufanya ngono na wanawake. Hivyo, wakawa na watoto walioitwa Wanefili, ambao walikuwa majitu yenye jeuri. Isitoshe, “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.” Hata hivyo, Yehova Mungu hakuruhusu uovu huo uendelee. Alileta Gharika juu ya dunia na kuwaangamiza wanadamu wote waovu pamoja na Wanefili. Watumishi waaminifu wa Mungu ndio wanadamu pekee waliobaki.—Mwanzo 6:1-7, 17; 7:23.

Malaika waasi waliponyoka uharibifu wakati wa Gharika. Walibadili miili yao na kurudi katika makao ya roho wakiwa viumbe wa roho. Tangu wakati huo, wanaitwa roho waovu. Wanamuunga mkono Shetani Ibilisi ambaye ni “mtawala wa roho waovu.” (Mathayo 12:24-27) Kama mtawala wao, roho waovu hutamani kuabudiwa na wanadamu.

Roho waovu ni hatari, lakini hatuhitaji kuwaogopa. Nguvu zao zina mipaka. Malaika wasiotii waliporudi mbinguni, hawakuruhusiwa kujiunga na familia ya malaika waaminifu wa Mungu. Hawangeweza kupata ujuzi wowote wa kiroho kutoka kwa Mungu, na hawakuwa na tumaini la wakati ujao. Kwa kweli, waliwekwa katika Tartaro, yaani, giza la kiroho. (2 Petro 2:4) Yehova aliwaweka chini ya “vifungo vya milele,” nao wamo katika giza la kiroho. Isitoshe, sasa hawawezi kujibadili kuwa wanadamu.—Yuda 6.

Unapaswa Kufanya Nini?

Je, bado roho waovu wana uvutano juu ya wanadamu? Ndiyo, wao hutumia “hila,” au matendo ya ujanja, kama yale yanayotumiwa na mtawala wao, Shetani Ibilisi. (Waefeso 6:11, 12) Hata hivyo, tukifuata shauri la Neno la Mungu, tunaweza kusimama imara dhidi ya roho waovu. Isitoshe, wale wanaompenda Mungu hulindwa na malaika wenye nguvu.

Ni muhimu ujifunze matakwa ya Mungu yaliyo katika Maandiko na kutenda kulingana na mambo unayojifunza! Unaweza kujifunza mengi kuhusu mafundisho ya Biblia ukiwasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au ukiwaandikia barua wachapishaji wa gazeti hili. Mashahidi wa Yehova watafurahi kujifunza Biblia pamoja nawe bila malipo na kwa wakati unaokufaa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Katika Biblia, malaika huonyeshwa wakiwa wanaume. Sikuzote waliwatokea wanadamu katika umbo la wanaume.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

JINSI MALAIKA WALIVYOPANGWA

Yehova ana familia kubwa ya malaika iliyopangwa kama ifuatavyo:

Malaika mwenye nguvu na mwenye mamlaka zaidi ni Mikaeli au Yesu Kristo, yule malaika mkuu. (1 Wathesalonike 4:16; Yuda 9) Maserafi, makerubi, na malaika wengine wako chini yake.

Maserafi wana cheo cha juu sana katika mpango wa Mungu. Wanahudumu kwenye kiti cha enzi cha Mungu. Kazi yao inatia ndani kutangaza utakatifu wa Mungu na kudumisha usafi wa kiroho wa watu wake.—Isaya 6:1-3, 6, 7.

Makerubi wanahusianishwa na kiti cha enzi cha Mungu nao huunga mkono ukuu wa Yehova.—Zaburi 80:1; 99:1; Ezekieli 10:1, 2.

Malaika wengine ni wawakilishi wa Yehova, nao hufanya mapenzi yake.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Malaika waliwasaidia Loti na binti zake kuondoka eneo hatari

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wakati mtume Yohana alipojaribu kumwabudu malaika, aliambiwa hivi: “Usifanye hivyo!”

[Picha katika ukurasa wa 6]

Malaika hutekeleza hukumu ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, unafaidika kutokana na kazi ya kuhubiri inayofanywa kwa mwongozo wa malaika?