Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Manukuu ya Awali Zaidi ya Biblia Kuwahi Kupatikana”

“Manukuu ya Awali Zaidi ya Biblia Kuwahi Kupatikana”

“Manukuu ya Awali Zaidi ya Biblia Kuwahi Kupatikana”

MIAKA 25 iliyopita, wanaakiolojia wa Israel waligundua jambo la kustaajabisha. Katika pango la kuzikia kwenye miteremko ya Bonde la Hinomu huko Yerusalemu, walipata hati mbili za kukunjwa zilizotengenezwa kwa fedha ambazo zilikuwa na maandiko ya Biblia. Hati hizo zilitengenezwa kabla ya Wababiloni kuharibu Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Hati hizo zilinukuu baadhi ya baraka zinazotajwa kwenye Hesabu 6:24-26. Jina la Mungu, Yehova, lilipatikana mara kadhaa katika hati hizo. Hati hizo zimetajwa kuwa “maandishi ya kale zaidi kuwahi kupatikana ambayo yanarekodi masimulizi ya Biblia ya Kiebrania.”

Hata hivyo, wasomi fulani walitilia shaka tarehe ya hati hizo na wakasema kwamba ziliandikwa katika karne ya pili K.W.K. Sababu moja ni kwamba picha za awali za hati hizo ndogo hazikuwawezesha kuzichunguza vizuri. Ili kutatua ubishi huo kuhusu tarehe za hati hizo, kikundi fulani cha wasomi kilifanya uchunguzi mwingine. Walitumia mashini na kompyuta za kisasa za kutokeza picha ili kupata picha nzuri zaidi za hati hizo. Matokeo ya uchunguzi huo yalichapishwa hivi karibuni. Wasomi hao waligundua nini?

Kwanza, wasomi hao wanasisitiza kwamba habari zilizopatikana mahali hati hizo zilipovumbuliwa zinaonyesha kwamba ziliandikwa kabla ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni huko Babiloni. Uchunguzi wa hati hizo kwa kukagua herufi zilizoandikwa, yaani, umbo lake, mtindo wake, mkao wake, mfuatano wake, na upande ambao herufi hizo zilielekezwa, unaonyesha kwamba ziliandikwa katika kipindi hichohicho, yaani, karibu na mwisho wa karne ya saba K.W.K. Hatimaye, baada ya kuchunguza usahihi wa maneno, wasomi hao walisema: “Uchunguzi wa usahihi wa maneno yaliyo katika [hati] hizo unaonyesha kwamba ziliandikwa wakati uleule ambao umethibitishwa kupitia habari zilizopatikana mahali zilipovumbuliwa na kwa kuchunguza herufi.”

Jarida Bulletin of the American Schools of Oriental Research linakata kauli hii kuhusu uchunguzi huo wa hati hizo za fedha, ambazo pia huitwa maandishi ya Ketef Hinnom: “Hivyo, tunaweza kuunga mkono kauli iliyofikiwa na wasomi wengi kwamba maandishi yaliyo kwenye hati hizo ndiyo manukuu ya awali zaidi ya Biblia kuwahi kupatikana.”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]

Cave: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.; inscriptions: Photograph © Israel Museum, Jerusalem; courtesy of Israel Antiquities Authority