Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mpinge Shetani, Naye Atakimbia!

Mpinge Shetani, Naye Atakimbia!

Mpinge Shetani, Naye Atakimbia!

“Jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—YAKOBO 4:7.

1, 2. (a) Ni sifa gani ya Ibilisi inayoonyeshwa katika tangazo linalopatikana kwenye Isaya sura ya 14? (b) Ni maswali gani tutakayozungumzia?

IBILISI ndiye kiumbe mwenye kiburi zaidi. Maneno yaliyoandikwa na nabii wa Mungu Isaya yanaonyesha wazi kiburi chake. Zaidi ya miaka 100 kabla ya Babiloni kuwa serikali kuu ya ulimwengu, watu wa Yehova waliwakilishwa wakisema maneno yafuatayo dhidi ya “mfalme wa Babiloni”: “Wewe umesema moyoni mwako, ‘Nitaenda juu mbinguni. Nitakiinua kiti changu cha ufalme juu ya nyota za Mungu [wafalme wa ukoo wa Daudi] . . . Mimi nitajifananisha na Aliye Juu Zaidi.’” (Isaya 14:3, 4, 12-15; Hesabu 24:17) Kiburi cha “mfalme wa Babiloni” kilifanana na mwelekeo wa Shetani, “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Lakini, kama vile ukoo wa kifalme huko Babiloni ulivyofikia mwisho wenye aibu, ndivyo na kiburi cha Shetani kitakavyomletea msiba.

2 Hata hivyo, maadamu Ibilisi yupo, huenda tukasumbuliwa na maswali kama haya: Je, inafaa kumwogopa Shetani? Kwa nini anachochea mateso ya Wakristo? Na tunaweza kuepukaje kushindwa na Ibilisi?

Je, Tumwogope Ibilisi?

3, 4. Kwa nini Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao hawamwogopi Ibilisi?

3 Maneno haya ya Yesu Kristo yanawaimarisha sana Wakristo watiwa-mafuta: “Usiogope mateso ambayo yanakaribia kukupata. Tazama! Ibilisi ataendelea kuwatupa gerezani baadhi yenu ili mjaribiwe kwa ukamili, na ili muwe na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.” (Ufunuo 2:10) Watiwa-mafuta na waandamani wao walio na tumaini la kuishi duniani hawamwogopi Ibilisi. Hawakuzaliwa wakiwa na ujasiri. Wana ujasiri huo kwa sababu wanamwogopa na kumheshimu Mungu, nao ‘wanapata kimbilio katika kivuli cha mabawa yake.’—Zaburi 34:9; 36:7.

4 Wanafunzi wa mapema wa Yesu Kristo wasio na woga walibaki waaminifu hadi kifo licha ya mateso waliyokabili. Hawakuogopa yale ambayo Shetani Ibilisi angefanya, kwa sababu walijua kwamba Yehova hawezi kuwaacha wale walio washikaminifu kwake. Vivyo hivyo, wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao waliojiweka wakfu wameazimia kuwa washikamanifu kwa Mungu hata wanapokabili mateso makali sasa. Hata hivyo, mtume Paulo alionyesha kwamba Ibilisi anaweza kusababisha kifo. Je, hilo linapaswa kutuogopesha?

5. Tunajifunza nini kutokana na Waebrania 2:14, 15?

5 Paulo alisema kwamba Yesu ‘alishiriki damu na mwili’ ili “kupitia kifo chake apate kumwangamiza yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi; na ili awaweke huru wale wote ambao kwa kuogopa kifo walikuwa wametiishwa chini ya utumwa katika maisha yao yote.” (Waebrania 2:14, 15) Akiwa “yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo,” Shetani alimdhibiti Yuda Iskariote kisha akawatumia viongozi wa Kiyahudi na Waroma ili kumuua Yesu. (Luka 22:3; Yohana 13:26, 27) Hata hivyo, kupitia kifo chake cha kidhabihu, Yesu anawaweka wanadamu wenye dhambi huru kutokana na uvutano wa Shetani na anatuwezesha kupata uzima wa milele.—Yohana 3:16.

6, 7. Uwezo wa Shetani wa kusababisha kifo ni mwingi kadiri gani?

6 Uwezo wa Ibilisi wa kusababisha kifo ni mwingi kadiri gani? Tangu Shetani aanze matendo yake maovu, uwongo na mwongozo wake umesababisha vifo vya wanadamu. Hiyo ni kwa sababu Adamu alitenda dhambi naye akapitisha dhambi na kifo kwa jamii ya wanadamu. (Waroma 5:12) Isitoshe, watumishi wa Shetani hapa duniani wamewatesa waabudu wa Yehova, na nyakati nyingine hata wamewaua, kama walivyofanya katika kisa cha Yesu Kristo.

7 Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba Ibilisi anaweza kumuua mtu yeyote yule anayetaka. Mungu huwalinda watumishi Wake na hatamruhusu kamwe Shetani awaangamize waabudu wote wa kweli duniani. (Waroma 14:8) Naam, Yehova huruhusu watu wake wote wapatwe na mateso, naye huruhusu wengine wetu wafe kwa sababu ya mashambulizi ya Ibilisi. Hata hivyo, Maandiko yanatoa tumaini zuri la ufufuo kwa wale walio katika “kitabu cha kumbukumbu” cha Mungu, na Ibilisi hawezi kufanya lolote ili kuzuia watu wasifufuliwe!—Malaki 3:16; Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

Kwa Nini Shetani Hututesa?

8. Kwa nini Ibilisi anawatesa watumishi wa Mungu?

8 Ikiwa sisi ni watumishi washikamanifu wa Mungu, kuna sababu ya msingi inayomfanya Ibilisi atutese. Kusudi lake ni kutufanya tuache kuwa na imani. Tuna uhusiano wenye thamani sana pamoja na Baba yetu wa mbinguni, na Shetani anatamani kuuharibu. Jambo hilo halipaswi kutushangaza. Katika Edeni, Yehova alitabiri kwamba kungekuwa na uadui kati ya “mwanamke” wa mfano na “nyoka” na pia kati ya ‘wazao’ wao. (Mwanzo 3:14, 15) Maandiko yanamtambulisha Ibilisi kuwa “yule nyoka wa zamani” na yanaonyesha kwamba sasa wakati wake ni mfupi na kwamba ana hasira kali. (Ufunuo 12:9, 12) Kwa kuwa uadui kati ya ‘wazao’ hao wawili unaendelea, wale wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu wanaweza kutarajia kuteswa. (2 Timotheo 3:12) Je, unajua sababu kuu inayofanya tuteswe na Shetani?

9, 10. Ni suala gani ambalo Ibilisi ametokeza, na linahusianaje na mwenendo wa wanadamu?

9 Ibilisi ametokeza suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Pia, amezusha suala linalohusiana na hilo kwa kutilia shaka utimilifu wa wanadamu kwa Muumba wao. Shetani alimtesa mwanamume mnyoofu Ayubu. Kwa nini? Kusudi lake lilikuwa kuvunja utimilifu wa Ayubu kwa Yehova. Mke wa Ayubu na “wafariji wasumbufu” watatu walitumiwa na Ibilisi kwa kusudi hilo. Kama inavyoonyeshwa katika kitabu cha Ayubu, Ibilisi alimpinga Mungu kwa kudai kwamba hakuna mwanadamu ambaye angeendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu ikiwa Shetani angeruhusiwa kumjaribu. Lakini Ayubu alibaki mtimilifu, hivyo akathibitisha kwamba Shetani ni mwongo. (Ayubu 1:8–2:9; 16:2; 27:5; 31:6) Leo, Ibilisi huwatesa Mashahidi wa Yehova ili kujaribu kuvunja utimilifu wao na hivyo kuthibitisha ukweli wa dai lake.

10 Kujua kwamba Ibilisi anatutesa kwa sababu anataka sana kuvunja utimilifu wetu kwa Mungu kunaweza kutusaidia kuwa wajasiri na wenye nguvu. (Kumbukumbu la Torati 31:6) Mungu wetu ni Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, naye atatusaidia kudumisha utimilifu wetu. Acheni tujitahidi sikuzote kufanya moyo wa Yehova ushangilie kwa kudumisha utimilifu wetu, ili apate kumjibu mdhihaki mkuu, Shetani Ibilisi.—Methali 27:11.

“Utukomboe Kutokana na Yule Mwovu”

11. Ni nini maana ya ombi hili, “Usituingize katika jaribu”?

11 Kuendelea kuwa mtimilifu si jambo rahisi. Ili mtu aendelee kuwa mtimilifu, anahitaji kusali kwa bidii. Maneno yaliyo katika sala ya kielelezo yanasaidia sana. Kwa sehemu, Yesu alisema hivi: “Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) Yehova hatujaribu ili tutende dhambi. (Yakobo 1:13) Hata hivyo, nyakati nyingine Maandiko yanaposema kwamba Mungu hufanya au kusababisha mambo, kwa kweli yeye huwa ameyaruhusu tu. (Ruthu 1:20, 21) Tunaposali kama Yesu alivyoonyesha, tunamwomba Yehova asituache tushindwe na jaribu. Bila shaka yeye hatatuacha, kwa kuwa tuna uhakikisho huu katika Maandiko: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

12. Kwa nini sisi husali hivi: “Utukomboe kutokana na yule mwovu”?

12 Baada ya kuzungumza kuhusu jaribu katika sala ya kielelezo, Yesu alisema hivi kwa kufaa: “Utukomboe kutokana na yule mwovu.” Tafsiri nyingine za Biblia zinasema hivi: “Utukomboe kutokana na uovu” (King James Version; Revised Standard Version) au “Utulinde kutokana na uovu.” (Contemporary English Version) Hata hivyo, katika Maandiko, maneno ‘kukomboa kutokana na’ yanatumiwa hasa kuwahusu watu, na Injili ya Mathayo inaonyesha kuwa Ibilisi ni “Mjaribu,” yaani, ni mtu. (Mathayo 4:3, 11) Hivyo, ni muhimu kusali kwa ajili ya kukombolewa kutokana na “yule mwovu,” Shetani Ibilisi. Anajaribu kutuchochea tutende dhambi dhidi ya Mungu. (1 Wathesalonike 3:5) Tunaposali, “Utukomboe kutokana na yule mwovu,” tunamwomba Baba yetu wa mbinguni atuongoze na kutusaidia ili tusishindwe akili na Ibilisi.

Usishindwe Akili na Ibilisi

13, 14. Kwa nini Wakorintho walihitaji kubadili njia yao ya kumshughulikia mtu ambaye hakuwa na maadili kutanikoni?

13 Paulo aliandika hivi alipowahimiza Wakristo huko Korintho kuwa wenye kusamehe: “Jambo lolote ambalo mnamsamehe yeyote kwa fadhili, mimi vilevile namsamehe. Kwa kweli, kwa habari yangu mimi, lolote lile ambalo nimesamehe kwa fadhili, ikiwa nimesamehe kwa fadhili jambo lolote, imekuwa ni kwa ajili yenu machoni pa Kristo; ili Shetani asitushinde akili, kwa maana sisi hatukosi kuzijua mbinu zake.” (2 Wakorintho 2:10, 11) Ibilisi anaweza kutushinda akili katika njia mbalimbali, lakini kwa nini Paulo alisema maneno yaliyonukuliwa hapa juu?

14 Paulo aliwakaripia Wakorintho kwa sababu walimruhusu mwanamume fulani asiye na maadili aendelee kubaki kutanikoni. Yaelekea jambo hilo lilimfurahisha Shetani, kwa kuwa kutaniko lilipata aibu kwa kuruhusu “uasherati wa namna ambayo hata haimo kati ya mataifa.” Mwishowe, mkosaji huyo alitengwa na ushirika. (1 Wakorintho 5:1-5, 11-13) Baadaye mtu huyo alitubu. Ikiwa Wakorintho wangekataa kumsamehe na kumrudisha mtu huyo, Ibilisi angewashinda akili katika njia nyingine. Katika njia gani? Wangeonekana kuwa wagumu na wasio na rehema, kama Shetani mwenyewe. Ikiwa mtu huyo aliyetubu ‘angemezwa na huzuni yake ya kupita kiasi’ na kuacha kabisa kumwabudu Mungu, wazee hasa ndio wangetoa hesabu mbele za Mungu mwenye rehema, Yehova. (2 Wakorintho 2:7; Yakobo 2:13; 3:1) Bila shaka, hakuna Mkristo wa kweli ambaye angetaka kumwiga Shetani kwa kuwa mkatili, mgumu, na asiye na rehema.

Tunalindwa na Silaha Kutoka kwa Mungu

15. Tunapigana vita gani, na ushindi wetu unategemea nini?

15 Ili tukombolewe kutokana na Ibilisi, tunapaswa kupigana vita vya kiroho dhidi ya majeshi ya roho waovu. Ushindi dhidi ya roho waovu unategemea jinsi tunavyovaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.” (Waefeso 6:11-18) Silaha hizo zinatia ndani “bamba la kifuani la uadilifu.” (Waefeso 6:14) Mfalme Sauli wa Israeli la kale hakumtii Mungu, na hivyo akapoteza roho takatifu. (1 Samweli 15:22, 23) Lakini tukifuatia uadilifu na kuvaa mavazi kamili ya silaha za kiroho, tutapata roho takatifu ya Mungu na ulinzi tunaohitaji dhidi ya Shetani na malaika wake waovu, yaani, roho waovu.—Methali 18:10.

16. Tunaweza kuendeleaje kulindwa dhidi ya majeshi ya roho waovu?

16 Ili kuendelea kulindwa dhidi ya majeshi ya roho waovu, tunapaswa kufanya mambo fulani kama vile kusoma na kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida, huku tukitumia vizuri vichapo vinavyotayarishwa na “msimamizi-nyumba mwaminifu.” (Luka 12:42) Tukifanya hivyo, tutakuwa tukijaza akili zetu mambo mazuri ya kiroho, kama shauri hili la Paulo linavyoonyesha: “Akina ndugu, mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Wafilipi 4:8.

17. Ni nini kitakachotusaidia kuwa wahubiri wa habari njema wenye matokeo?

17 Yehova hutuwezesha kuvaa ‘miguuni mwetu viatu vya habari njema ya amani.’ (Waefeso 6:15) Kutoa maelezo kwa ukawaida katika mikutano ya Kikristo hututayarisha kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Tunapata shangwe iliyoje tunapowasaidia wengine kujifunza kweli kumhusu Mungu na kupata uhuru wa kiroho! (Yohana 8:32) “Upanga wa roho, yaani, neno la Mungu,” ni muhimu katika kujilinda wenyewe dhidi ya mafundisho ya uwongo na “kupindua ngome zenye nguvu.” (Waefeso 6:17; 2 Wakorintho 10:4, 5) Kutumia kwa ustadi Neno la Mungu lililoandikwa, Biblia, hutusaidia kufundisha kweli na pia hutulinda ili tusishindwe na ujanja wa Ibilisi.

18. Tunaweza “kusimamaje imara kupinga hila za Ibilisi”?

18 Paulo alianza mazungumzo yake kuhusu silaha zetu za kiroho kwa kusema hivi: “Endeleeni kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake. Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.” (Waefeso 6:10, 11) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kusimama imara” linahusiana na askari anayesimama mahali pake. Sisi husimama imara katika vita vya kiroho, ingawa Shetani hutumia njia mbalimbali za ujanja ili kujaribu kuvuruga umoja wetu, kupotosha mafundisho yetu, au kuvunja utimilifu wetu kwa Mungu. Hata hivyo, mpaka sasa mashambulizi ya Ibilisi hayajafanikiwa, nayo hayatafanikiwa kamwe! *

Mpinge Ibilisi, Naye Atakimbia

19. Ni njia gani moja ya kuchukua hatua thabiti ya kumpinga Ibilisi?

19 Tunaweza kushinda katika vita vyetu vya kiroho dhidi ya Ibilisi na majeshi ya roho waovu ambayo yanaongozwa naye. Hatuna sababu ya kutetemeka kwa kumwogopa Shetani, kwa kuwa mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Njia moja ya kuchukua hatua thabiti ya kumpinga Shetani na roho waovu wanaoshirikiana naye ni kukataa kujihusisha katika mambo ya uchawi na wale wanaoyafanya. Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba watumishi wa Yehova wanapaswa kukataa kusoma ishara za bahati au kujihusisha katika unajimu, uaguzi, na kuwasiliana na pepo. Tukiwa na nguvu kiroho na mengi ya kufanya katika utendaji mbalimbali wa Kikristo, hatuhitaji kuogopa kwamba mtu fulani ataturoga.—Hesabu 23:23; Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Isaya 47:12-15; Matendo 19:18-20.

20. Tunaweza kumpingaje Ibilisi?

20 ‘Tunampinga Ibilisi’ kwa kushikamana na kweli na kanuni za Biblia, na kusimama imara dhidi yake. Ulimwengu unapatana na Shetani kwa sababu yeye ndiye mungu wa ulimwengu huu. (2 Wakorintho 4:4) Hivyo, sisi hukataa mazoea mabaya ya ulimwengu, kama vile kiburi, ubinafsi, ukosefu wa adili, jeuri, na kupenda vitu vya kimwili. Tunajua kwamba Ibilisi alikimbia wakati Yesu alipoyakabili mashambulizi yake kwa kutumia Maandiko alipojaribiwa nyikani. (Mathayo 4:4, 7, 10, 11) Vivyo hivyo, tukijitiisha kikamili kwa Yehova na kumtegemea katika sala, Shetani ‘atatukimbia’ kwa sababu tumemshinda. (Waefeso 6:18) Kwa msaada wa Yehova Mungu na Mwana wake mpendwa, hakuna anayeweza kutuletea madhara ya kudumu, hata Ibilisi!—Zaburi 91:9-11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kwa habari zaidi kuhusu mavazi ya silaha za kiroho kutoka kwa Mungu, ona Mnara wa Mlinzi wa Mei 15, 1992, ukurasa wa 21-23.

Unajibuje?

• Je, tunapaswa kumwogopa Shetani Ibilisi?

• Kwa nini Shetani anawatesa Wakristo?

• Kwa nini sisi husali tukombolewe kutokana na “yule mwovu”?

• Tunaweza kushindaje vita vya kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wafuasi wa mapema wa Kristo wasio na woga walibaki waaminifu hadi kifo

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ibilisi hawezi kuzuia wale walio katika kumbukumbu ya Yehova wasifufuliwe

[Picha katika ukurasa wa 28]

Je, unasali ili ukombolewe kutokana na “yule mwovu”?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Je, wewe unavaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu”?