Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iga Subira ya Yehova

Iga Subira ya Yehova

Iga Subira ya Yehova

“Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, . . . bali yeye ni mwenye subira.”—2 PETRO 3:9.

1. Yehova amewaandalia wanadamu zawadi gani isiyo na kifani?

YEHOVA ametuandalia kitu ambacho hakuna mtu mwingine anaweza kuandaa. Ni kitu kinachovutia sana na chenye thamani kwelikweli, lakini hakiwezi kununuliwa wala kuchumwa. Kile ambacho ameandaa ni zawadi ya uzima wa milele, na kwa wengi wetu hilo linamaanisha kuishi milele katika dunia paradiso. (Yohana 3:16) Maisha hayo yatafurahisha kama nini! Mambo yanayosababisha huzuni nyingi kama vile mizozo, jeuri, umaskini, uhalifu, ugonjwa, na hata kifo, hayatakuwapo tena. Watu wataishi kwa amani na umoja chini ya utawala wenye upendo wa Ufalme wa Mungu. Lo! Jinsi tunavyotamani Paradiso hiyo!—Isaya 9:6, 7; Ufunuo 21:4, 5.

2. Kwa nini Yehova hajakomesha mfumo mbovu wa Shetani?

2 Yehova pia anatazamia wakati ambapo ataanzisha Paradiso duniani. Hiyo ni kwa sababu anapenda uadilifu na haki. (Zaburi 33:5) Hafurahii kuona watu ulimwenguni wakipuuza au kudharau kanuni zake za uadilifu, wala hafurahii kuona watu ulimwenguni wakidharau mamlaka yake na kuwadhulumu watu wake. Lakini, kuna sababu nzuri za yeye kuruhusu mfumo mbovu wa Shetani uendelee kuwapo. Sababu hizo zinahusu masuala ya kiadili yanayohusiana na enzi yake kuu. Kwa kutatua masuala hayo, Yehova huonyesha sifa yenye kuvutia sana ambayo watu wengi leo hawana, yaani, subira.

3. (a) Ni nini maana ya maneno ya Kigiriki na ya Kiebrania yanayotafsiriwa katika Biblia kuwa “subira”? (b) Tutazungumzia maswali gani?

3 Kuna neno la Kigiriki ambalo katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya limetafsiriwa mara tatu kuwa “subira.” Mara nyingi neno hilo hutafsiriwa kuwa “ustahimilivu” na limetafsiriwa mara moja kuwa “kuonyesha subira.” Maneno ya Kigiriki na ya Kiebrania yanayomaanisha “subira” hudokeza wazo la uvumilivu wenye subira na kutokasirika upesi. Tunafaidikaje na subira ya Yehova? Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na subira na uvumilivu wa Yehova na wa watumishi wake waaminifu? Ni nini kinachoonyesha kwamba subira ya Yehova ina mipaka? Acheni tuzungumzie mambo hayo.

Fikiria Subira ya Yehova

4. Mtume Petro aliandika nini kuhusu subira ya Yehova?

4 Mtume Petro aliandika hivi kuhusu subira ya Yehova: “Wapendwa, msikose kujua jambo hili moja, kwamba siku moja kwa Yehova ni kama miaka elfu na miaka elfu ni kama siku moja. Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, kama watu fulani wanavyoona kukawia, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:8, 9) Hebu ona mambo mawili yanayotajwa katika andiko hilo ambayo yanaweza kutusaidia kuelewa subira ya Yehova.

5. Maoni ya Yehova kuhusu wakati huhusianaje na matendo yake?

5 Jambo la kwanza ni kwamba maoni ya Yehova kuhusu wakati ni tofauti na yetu. Kwa Yule anayeishi milele, miaka elfu ni kama siku moja tu. Yehova hazuiwi wala kuharakishwa na wakati, lakini kwa upande mwingine yeye hakawii kutenda. Kwa kuwa ana hekima isiyo na kikomo, Yehova anajua wakati bora wa kutenda kwa faida ya wote wanaohusika, naye hungoja kwa subira wakati huo ufike. Hata hivyo, hatupaswi kukata kauli kwamba Yehova hajali watumishi wake wanapopatwa na matatizo sasa. Yeye ni Mungu mwenye “huruma nyororo,” na mfano bora zaidi wa upendo. (Luka 1:78; 1 Yohana 4:8) Yuko tayari kukomesha kabisa madhara yoyote ambayo yamesababishwa kwa sababu ya kuruhusu matatizo yaendelee kwa muda.—Zaburi 37:10.

6. Hatupaswi kukata kauli gani kumhusu Mungu, na kwa nini?

6 Ni kweli kwamba si rahisi kungojea kitu ambacho mtu anataka sana. (Methali 13:12) Hivyo, watu wanapokosa kutimiza ahadi zao haraka, wengine wanaweza kukata kauli kwamba hawataki kuzitimiza. Tukiwa na maoni hayo kumhusu Mungu, basi tutakuwa tumekosa hekima sana! Tukielewa vibaya subira ya Mungu kwa kuona kwamba amekawia, baada ya muda tunaweza kuanza kuwa na shaka, tuvunjike moyo, na kulegea kiroho. Hata tunaweza kupotoshwa na watu ambao Petro alikuwa amewaonya Wakristo wajihadhari nao, yaani, wadhihaki, wale wasio na imani. Watu hao husema hivi kwa dhihaka: “Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.”—2 Petro 3:4.

7. Subira ya Yehova inahusianaje na tamaa yake ya kwamba watu wafikie toba?

7 Jambo la pili ambalo tunajifunza kutokana na maneno ya Petro ni kwamba Yehova ni mwenye subira kwa sababu anataka wote wafikie toba. Yehova atawaangamiza wale wanaokataa katakata kuacha njia zao mbaya. Hata hivyo, Mungu hafurahii kifo cha mwovu. Badala yake, anafurahia kuona watu wakitubu, wakiacha njia zao mbaya, na kuendelea kuishi. (Ezekieli 33:11) Hivyo, anaonyesha subira na kuruhusu habari njema zihubiriwe duniani pote ili watu wapate nafasi ya kuishi.

8. Tunajifunza nini kuhusu subira ya Mungu tunapochunguza jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli?

8 Tunaweza kufahamu subira ya Mungu tunapochunguza jinsi alivyoshughulika na taifa la kale la Israeli. Kwa karne nyingi, alivumilia hali yao ya kutotii. Kupitia manabii wake, aliwasihi hivi mara nyingi: “Geukeni kutoka katika njia zenu mbaya, mshike amri zangu, sheria zangu, kulingana na sheria yote niliyowaamuru mababu zenu na ambayo nimepeleka kwenu kupitia watumishi wangu manabii.” Matokeo? Inasikitisha kwamba watu hao “hawakusikiliza.”—2 Wafalme 17:13, 14.

9. Yesu alimwigaje Baba yake katika kuonyesha subira?

9 Hatimaye, Yehova alimtuma Mwana wake, ambaye alijitahidi sana kuwasaidia Wayahudi wajipatanishe na Mungu. Yesu aliiga subira ya Baba yake kwa ukamili. Akijua vizuri kwamba atauawa baada ya muda mfupi, Yesu aliomboleza hivi: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na ambaye huwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka.” (Mathayo 23:37) Maneno hayo yenye kugusa moyo si maneno ya mwamuzi mkali anayetamani kumwadhibu mtu, bali ni maneno ya rafiki mwenye upendo ambaye anawatendea watu kwa subira. Kama Baba yake huko mbinguni, Yesu alitaka watu watubu ili waepuke hukumu kali. Wengine waliitikia vizuri maonyo ya Yesu na wakaepuka hukumu kali iliyotekelezwa juu ya Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.—Luka 21:20-22.

10. Tumefaidikaje na subira ya Mungu?

10 Je, hustaajabishwi na subira ya Mungu? Ingawa wanadamu wameasi sana, Yehova amempa kila mmoja wetu nafasi ya kumjua na kuwa na tumaini la kuokoka pamoja na mamilioni ya watu wengine. Petro aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Ioneni subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.” (2 Petro 3:15) Tunafurahi kwamba subira ya Yehova inatuwezesha kupata wokovu. Naam, tunasali kwamba Yehova aendelee kutuonyesha subira tunapomtumikia siku baada ya siku.—Mathayo 6:12.

11. Kuelewa subira ya Yehova kutatuchochea kufanya nini?

11 Kuelewa sababu ya Yehova ya kuonyesha subira hutusaidia kungojea wokovu wake kwa subira bila kukata kauli kwamba anakawia kutimiza ahadi zake. (Maombolezo 3:26) Tunapoendelea kusali Ufalme wa Mungu uje, tunasadiki kwamba Mungu anajua wakati barabara wa kujibu sala hiyo. Isitoshe, tunachochewa kuiga subira ya Yehova tunaposhughulika na ndugu zetu na watu tunaowahubiria. Sisi pia hatutaki yeyote aangamizwe, bali tunataka watu watubu na kupata tumaini la uzima wa milele kama sisi.—1 Timotheo 2:3, 4.

Fikiria Subira ya Manabii

12, 13. Kupatana na Yakobo 5:10, nabii Isaya alionyeshaje subira?

12 Kufikiria subira ya Yehova hutusaidia kuthamini na kusitawisha sifa hiyo. Si rahisi kwa wanadamu wasio wakamilifu kusitawisha subira, lakini inawezekana. Tunajifunza kutokana na watumishi wa kale wa Mungu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Akina ndugu, wachukueni manabii kuwa kielelezo cha kupatwa na uovu na kuonyesha subira, wale waliosema katika jina la Yehova.” (Yakobo 5:10) Inafariji na inatia moyo kujua kwamba wengine wamefaulu kukabili matatizo tunayokabili.

13 Kwa mfano, nabii Isaya alihitaji subira katika mgawo wake. Yehova alionyesha hilo alipomwambia hivi: “Nenda, nawe uwaambie watu hawa, ‘Sikieni tena na tena, lakini msielewe; na mwone tena na tena, lakini msipate ujuzi wowote.’ Fanya moyo wa watu hawa kuwa mgumu, na uyafanye masikio yao kuwa magumu, na ushikanishe macho yao pamoja, ili wasione kwa macho yao na kwa masikio yao wasisikie, na ili moyo wao usielewe na ili kwa kweli wasigeuke na kujiponya.” (Isaya 6:9, 10) Ingawa watu hawakuitikia, kwa subira Isaya aliendelea kutangaza maonyo ya Yehova kwa angalau miaka 46! Vivyo hivyo, subira itatusaidia kuendelea kufanya kazi yetu ya kuhubiri habari njema, hata wengi wasipoitikia.

14, 15. Ni nini kilichomsaidia Yeremia kukabiliana na matatizo na kuvunjika moyo?

14 Katika huduma yao, manabii walikabili watu wasioitikia na waliteswa pia. Yeremia aliwekwa katika mikatale, akafungwa gerezani katika “nyumba ya pingu,” na kutupwa ndani ya tangi la maji. (Yeremia 20:2; 37:15; 38:6) Aliteswa na watu walewale ambao alitaka kuwasaidia. Lakini Yeremia hakuwachukia, wala hakulipiza kisasi. Alivumilia kwa subira kwa makumi ya miaka.

15 Yeremia hakunyamazishwa na dhihaka na mateso, nasi pia leo hatunyamazishwi na mambo hayo. Ni kweli kwamba huenda tukavunjika moyo nyakati nyingine. Hata Yeremia alivunjika moyo. Aliandika hivi: “Neno la Yehova lilikuwa kwangu kisababishi cha shutuma na cha dhihaka mchana kutwa. Nami nilisema: ‘Sitamtaja tena, wala sitasema tena katika jina lake.’” Matokeo yalikuwa nini? Je, Yeremia aliacha kuhubiri? Aliendelea kusema: “Moyoni mwangu [neno la Mungu likawa] kama moto unaowaka ambao umefungiwa ndani ya mifupa yangu; nami nikachoka kujizuia, nami sikuweza kuivumilia.” (Yeremia 20:8, 9) Ona kwamba wakati Yeremia alipokazia fikira dhihaka za watu, alipoteza shangwe yake. Alipokazia fikira uzuri na umuhimu wa ujumbe huo, alipata shangwe tena. Isitoshe, Yehova alikuwa pamoja na Yeremia “kama mwenye nguvu anayetisha,” naye akamwimarisha kutangaza neno la Mungu kwa bidii na kwa ujasiri.—Yeremia 20:11.

16. Tunaweza kudumishaje shangwe katika kazi yetu ya kuhubiri habari njema?

16 Je, nabii Yeremia alipata shangwe katika kazi yake? Bila shaka! Alimwambia hivi Yehova: “Maneno yako yalipatikana, nami nikayala; na neno lako linakuwa kwangu furaha na kushangilia kwa moyo wangu; kwa maana jina lako limeitwa juu yangu, Ee Yehova.” (Yeremia 15:16) Yeremia alishangilia kwa sababu ya pendeleo lake la kumwakilisha Mungu wa kweli na kuhubiri kuhusu neno lake. Sisi pia tunaweza kushangilia. Isitoshe, kama malaika mbinguni, sisi tunashangilia kwamba ulimwenguni pote watu wengi sana wanakubali ujumbe wa Ufalme, wanatubu, na wanaingia kwenye njia ya uzima wa milele.—Luka 15:10.

“Uvumilivu wa Ayubu”

17, 18. Ayubu alionyeshaje uvumilivu, na matokeo yakawaje?

17 Baada ya kuzungumza kuhusu manabii wa kale, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu nanyi mmeona matokeo ambayo Yehova alileta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa kuwa “uvumilivu” katika andiko hilo linafanana na neno ambalo Yakobo alitumia katika mstari unaotangulia ambalo limetafsiriwa kuwa “subira.” Msomi mmoja alieleza tofauti iliyopo kati ya maneno hayo mawili alipoandika hivi: “Neno linalotumiwa katika mstari wa kwanza linamaanisha subira inayoonyeshwa wakati watu wanapotutendea vibaya, nalo neno linalotumiwa katika mstari unaofuata linamaanisha uvumilivu unaoonyeshwa tunapokabili taabu.”

18 Ayubu alipata taabu nyingi. Alipoteza mali na watoto, naye akapatwa na ugonjwa wenye kuumiza. Pia alishutumiwa kwa uwongo kwamba Yehova alikuwa akimwadhibu. Ayubu hakunyamaza alipoteseka, bali aliomboleza kuhusu hali yake na hata akadokeza kwamba alikuwa mwadilifu kuliko Mungu. (Ayubu 35:2) Hata hivyo, hakuacha imani yake, wala hakuacha kuwa mtimilifu. Hakumlaani Mungu kama Shetani alivyodai. (Ayubu 1:11, 21) Matokeo yakawaje? Yehova ‘aliubariki mwisho wa Ayubu baadaye kuliko mwanzo wake.’ (Ayubu 42:12) Yehova alimwezesha Ayubu awe na afya tena, akaongeza mali zake mara mbili, naye akambariki kwa kumpa maisha mazuri ya furaha pamoja na wapendwa wake. Pia, kwa kuwa Ayubu alivumilia kwa uaminifu, aliweza kumjua Yehova kwa ukamili zaidi.

19. Tunajifunza nini kutokana na vile Ayubu alivyovumilia kwa subira?

19 Tunajifunza nini kutokana na vile Ayubu alivyovumilia kwa subira? Kama Ayubu, huenda tukawa wagonjwa au tukapatwa na matatizo mengine. Huenda tusielewe kabisa kwa nini Yehova ameruhusu tupatwe na jaribu fulani. Lakini tunaweza kuwa na uhakika wa jambo hili: Tukibaki waaminifu, tutabarikiwa. Yehova hatakosa kuwapa thawabu wale wanaomtafuta kwa bidii. (Waebrania 11:6) Yesu alisema hivi: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 10:22; 24:13.

“Siku ya Yehova Itakuja”

20. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba siku ya Yehova itakuja?

20 Ingawa Yehova ni mwenye subira, yeye pia ni mwenye haki na hatavumilia uovu milele. Subira yake ina mipaka. Petro aliandika hivi: “[Mungu] hakujizuia kuuadhibu ulimwengu wa kale.” Ingawa Noa na familia yake waliokolewa, ulimwengu huo wa watu wasiomwogopa Mungu uliangamizwa kwa maji. Yehova pia alitekeleza hukumu juu ya majiji ya Sodoma na Gomora na kuyaharibu kabisa. Hukumu hizo ni “kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.” Tunaweza kuwa na uhakika wa jambo hili: “Siku ya Yehova itakuja.”—2 Petro 2:5, 6; 3:10.

21. Tunaweza kuonyeshaje subira na uvumilivu, na tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

21 Basi, acheni tuige subira ya Yehova kwa kuwasaidia wengine wafikie toba ili waokolewe. Acheni pia tuwaige manabii kwa kutangaza habari njema kwa subira hata wale tunaowahubiria wasipoitikia. Isitoshe, tukivumilia majaribu na kudumisha utimilifu kama Ayubu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatubariki sana. Tunapotambua jinsi ambavyo Yehova amebariki sana jitihada za watu wake za kuhubiri habari njema duniani pote, sisi hupata sababu nzuri za kushangilia katika huduma yetu. Tutachunguza jambo hilo katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Yehova huonyesha subira?

• Tunajifunza nini kutokana na subira ya manabii?

• Ayubu alionyeshaje uvumilivu, na matokeo yakawaje?

• Tunajuaje kwamba subira ya Yehova ina mipaka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu aliiga subira ya Baba yake kwa ukamili

[Picha katika ukurasa wa 20]

Yehova alimbarikije Yeremia kwa kuonyesha subira?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yehova alimbarikije Ayubu kwa kuonyesha uvumilivu?