Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nehemia

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nehemia

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nehemia

MIAKA 12 imepita tangu mambo ya mwisho yaliyoandikwa katika kitabu cha Ezra yatendeke. Sasa wakati umekaribia wa “kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu,” ambao pia ni mwanzo wa yale majuma 70 ya miaka yanayoongoza kwenye kuja kwa Masihi. (Danieli 9:24-27) Kitabu cha Nehemia kinasimulia kuhusu watu wa Mungu na pia kujengwa upya kwa ukuta wa Yerusalemu. Kinasimulia kuhusu kipindi muhimu cha miaka zaidi ya 12, kuanzia mwaka wa 456 K.W.K. hadi wakati fulani baada ya mwaka wa 443 K.W.K.

Kitabu hicho kiliandikwa na Gavana Nehemia, na kinasimulia jinsi ibada ya kweli inavyokwezwa watu wanapochukua hatua thabiti na wanapomtegemea kabisa Yehova Mungu. Kinaonyesha waziwazi jinsi Yehova anavyoongoza mambo ili kutimiza mapenzi yake. Pia, kinasimulia kuhusu kiongozi mwenye nguvu na aliye jasiri. Ujumbe wa kitabu cha Nehemia una mambo muhimu kwa waabudu wote wa kweli leo, “kwa maana neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—Waebrania 4:12.

“MWISHOWE UKUTA UKAKAMILIKA”

(Nehemia 1:1–6:19)

Nehemia yuko katika ngome ya Shushani, akimtumikia Mfalme Artashasta Longimano katika cheo chenye kutegemeka. Nehemia anasumbuka sana moyoni anaposikia kwamba watu wake “wako katika hali mbaya sana na katika aibu; na ukuta wa Yerusalemu umebomoka, na malango yake yameteketezwa kwa moto.” Anasali kwa bidii ili apate mwongozo wa Mungu. (Nehemia 1:3, 4) Muda si muda, mfalme anaona huzuni ya Nehemia, na anampa ruhusa ya kwenda Yerusalemu.

Baada ya kufika Yerusalemu, Nehemia anakagua ukuta usiku, kisha anawaambia Wayahudi mipango yake ya kuujenga upya ukuta huo. Ujenzi unaanza, na wakati huohuo, upinzani dhidi ya kazi hiyo unaanza pia. Hata hivyo, chini ya uongozi wa Nehemia mwenye ujasiri, ‘mwishowe ukuta unakamilika.’—Nehemia 6:15.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:1; 2:1—Je, “mwaka wa 20” unaotajwa katika mistari hii miwili unahesabiwa kuanzia wakati mmoja? Ndiyo, ni mwaka wa 20 wa utawala wa Mfalme Artashasta. Hata hivyo, njia ya kuhesabu inayotumiwa katika mistari hiyo ni tofauti. Historia inaonyesha kwamba Artashasta alianza kutawala mwaka wa 475 K.W.K. Kwa kuwa kwa kawaida waandishi wa Babiloni walihesabu miaka ya utawala ya wafalme wa Uajemi kuanzia mwezi wa Nisani (Machi/Aprili) hadi mwezi wa Nisani, mwaka wa kwanza wa utawala wa Artashasta ulianza Nisani ya mwaka wa 474 K.W.K. Hivyo, mwaka wa 20 wa utawala wake ambao unatajwa kwenye Nehemia 2:1, ulianza katika Nisani ya 455 K.W.K. Basi, inapatana na akili kusema kwamba mwezi wa Kislevu (Novemba/Desemba) unaotajwa kwenye Nehemia 1:1, ulikuwa mwezi wa Kislevu wa mwaka uliotangulia, yaani, mwaka wa 456 K.W.K. Nehemia anataja kwamba mwaka wa 20 wa utawala wa Artashasta unatia ndani mwezi huo. Huenda katika kisa hiki, alikuwa akihesabu miaka hiyo kuanzia tarehe ambayo mfalme alianza kutawala. Inawezekana pia kwamba Nehemia alikuwa akihesabu wakati akitumia mwaka wa kilimwengu kama Wayahudi wanavyouita leo, ambao unaanza katika mwezi wa Tishri, unaolingana na Septemba/Oktoba. Vyovyote vile, lile neno la kujenga upya Yerusalemu lilitolewa mwaka wa 455 K.W.K.

4:17, 18—Mtu angeweza kufanyaje kazi ya kujenga upya kwa mkono mmoja tu? Kwa wale waliochukua mizigo, hilo halingekuwa tatizo. Mizigo ilipowekelewa kichwani au begani mwao, waliisawazisha kwa mkono mmoja, huku “mkono wa pili ukiwa umeshika silaha.” Wajenzi waliohitaji kutumia mikono yao miwili kufanya kazi ‘walijifunga, kila mmoja upanga wake kiunoni mwake, wakijenga.’ Walikuwa tayari kutenda iwapo wangeshambuliwa na adui.

5:7—Ni katika njia gani Nehemia alianza “kuwalaumu watu wenye vyeo na watawala-wasaidizi”? Watu hao walikuwa wakidai riba kutoka kwa Wayahudi wenzao kinyume na Sheria ya Musa. (Mambo ya Walawi 25:36; Kumbukumbu la Torati 23:19) Isitoshe, wakopeshaji walidai faida kubwa. Kama faida ingedaiwa kila mwezi, “sehemu moja kwa mia” ingekuwa sawa na asilimia 12 kila mwaka. (Nehemia 5:11) Ilikuwa ukatili kudai faida hiyo kutoka kwa watu ambao tayari walikuwa wamelemewa na kodi za juu na ambao hawakuwa na chakula cha kutosha. Akitumia Sheria ya Mungu, Nehemia aliwalaumu matajiri, akawakaripia na kuwakemea na hivyo kufichua matendo yao maovu.

6:5—Kwa kuwa kwa kawaida barua za siri zilitiwa ndani ya mfuko uliofungwa, kwa nini Sanbalati alimtumia Nehemia “barua iliyokuwa wazi”? Huenda Sanbalati alikusudia kufunua mashtaka ya uwongo kwa kuyatuma katika barua iliyokuwa wazi. Labda alifikiri kwamba hilo lingemkasirisha Nehemia sana na kumfanya aache kazi ya ujenzi ili aende kujitetea. Au huenda Sanbalati alifikiri kwamba ujumbe wa barua hiyo ungewaogopesha sana Wayahudi na hivyo waache kufanya kazi ya ujenzi. Nehemia hakutishika, naye aliendelea kufanya kwa utulivu kazi aliyopewa na Mungu.

Mambo Tunayojifunza:

1:4; 2:4; 4:4, 5Tunapokabili hali ngumu au tunapofanya maamuzi mazito, tunapaswa ‘kudumu katika sala’ na kutenda kulingana na mwongozo unaopatikana katika Neno la Mungu.—Waroma 12:12.

1:11–2:8; 4:4, 5, 15, 16; 6:16. Yehova hujibu sala za watumishi wake zinazotolewa kwa unyoofu.—Zaburi 86:6, 7.

1:4; 4:19, 20; 6:3, 15. Ingawa Nehemia alikuwa mtu mwenye huruma, aliweka mfano mzuri akiwa mtu mwenye bidii ambaye alitetea uadilifu kwa uthabiti.

1:11–2:3. Shangwe ya Nehemia haikutokana na cheo chake chenye kuheshimika cha kuwa mnyweshaji. Ilitokana na kuendeleza ibada ya kweli. Ibada ya Yehova na mambo yote yanayoiunga mkono ndiyo yanayopaswa kuwa hangaiko letu kuu na chanzo kikuu cha shangwe yetu.

2:4-8. Yehova alimchochea Artashasta amruhusu Nehemia kwenda kujenga upya ukuta wa Yerusalemu. Andiko la Methali 21:1 linasema hivi: “Moyo wa mfalme ni kama vijito vya maji mkononi mwa Yehova. Huugeuza kuelekea popote anapopenda.”

3:5, 27. Hatupaswi kuona kazi ya mkono inayofanywa kwa kusudi la kuendeleza ibada ya kweli kuwa yenye kutushushia heshima, kama walivyofanya “watu wa [Watekoa] walio mashuhuri.” Badala yake, tunaweza kuwaiga Watekoa wa kawaida waliojitolea kwa hiari.

3:10, 23, 28-30. Ingawa wengine wanaweza kuhamia maeneo yenye uhitaji wa wahubiri wa Ufalme, wengi wetu tunaunga mkono ibada safi mahali tunapoishi. Tunaweza kufanya hivyo kwa kushiriki kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme na kusaidia waliokumbwa na misiba, lakini tunafanya hivyo zaidi kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme.

4:14. Tunapokabili upinzani, sisi pia tunaweza kushinda woga kwa kumkumbuka “Yeye ambaye ni mkuu na Mwenye kuogopesha.”

5:14-19. Gavana Nehemia amewawekea waangalizi Wakristo mfano bora wa unyenyekevu, kutokuwa na ubinafsi, na busara. Ingawa alikuwa na bidii katika kutekeleza Sheria ya Mungu, hakuwanyanyasa wengine ili ajifaidi. Badala yake, aliwahangaikia walioteseka na maskini. Nehemia aliwawekea watumishi wote wa Mungu mfano mzuri wa ukarimu.

“UNIKUMBUKE KWA AJILI YA WEMA, EE MUNGU WANGU”

(Nehemia 7:1–13:31)

Mara tu ukuta wa Yerusalemu unapokamilika, Nehemia anaweka malango na kufanya mipango kwa ajili ya usalama wa jiji. Kisha anaandika rekodi ya watu wa ukoo. Umati wote unapokusanyika “katika kiwanja cha watu wote kilichokuwa mbele ya Lango la Maji,” Ezra kuhani anakisoma kitabu cha Sheria ya Musa, na Nehemia na Walawi wanawaeleza watu maana ya Sheria hiyo. (Nehemia 8:1) Kujifunza kuhusu Sherehe ya Vibanda kunawafanya waisherehekee kwa shangwe.

Mkutano mwingine unafuata, ambapo “uzao wa Israeli” unaungama dhambi za taifa lao, Walawi wanawakumbusha jinsi Mungu alivyokuwa ametendea Israeli, na watu wanaapa ‘kutembea katika sheria ya Mungu wa kweli.’ (Nehemia 9:1, 2; 10:29) Kwa kuwa bado kuna watu wachache Yerusalemu, kura inapigwa ili mtu mmoja kati ya watu kumi wanaoishi nje ya jiji wahamie jijini. Kisha ukuta unazinduliwa kwa shangwe nyingi sana hivi kwamba “kushangilia kwa Yerusalemu [kunasikika] mbali sana.” (Nehemia 12:43) Miaka 12 tangu alipowasili, Nehemia anatoka Yerusalemu na kurudia kazi yake aliyopewa na Artashasta. Baada ya muda mfupi, Wayahudi wanajitia unajisi tena. Nehemia anaporudi Yerusalemu, anachukua hatua ya kurekebisha mambo. Anaomba hivi kwa unyenyekevu: “Unikumbuke kwa ajili ya wema, Ee Mungu wangu.”—Nehemia 13:31.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

7:6-67—Kwa nini orodha ya Nehemia ya mabaki waliorudi Yerusalemu pamoja na Zerubabeli inatofautiana na ile ya Ezra kwa upande wa idadi ya watu wa kila nyumba? (Ezra 2:1-65) Huenda sababu ikawa kwamba Ezra na Nehemia walitumia vyanzo tofauti. Kwa mfano, huenda idadi ya watu waliojiandikisha kurudi ikawa tofauti na idadi ya watu waliorudi. Pia, labda tofauti hiyo ilikuwapo kwa sababu baadhi ya Wayahudi hawakujua ukoo wao mwanzoni lakini baadaye walipata kuujua. Hata hivyo, masimulizi yote hayo yanapatana kwa njia moja: Idadi ya waliorudi mwanzoni ilikuwa 42,360, bila kuhesabu watumwa na waimbaji.

10:34Kwa nini watu walipaswa kutoa kuni? Matoleo ya kuni hayakuamuriwa katika Sheria ya Musa. Takwa hilo lilitokana na uhitaji. Kuni nyingi zilihitajiwa ili kuteketeza dhabihu kwenye madhabahu. Yaelekea Wanethini, ambao walikuwa watumwa wa hekaluni wasio Waisraeli, walikuwa wachache. Hivyo, watu walipiga kura ili kuhakikisha kwamba kuni zilikuwapo kwa ukawaida.

13:6—Nehemia hakuwa Yerusalemu kwa muda gani? Biblia inasema tu kwamba “wakati fulani baadaye,” Nehemia alimwomba mfalme ruhusa ya kutokuwapo ili arudi Yerusalemu. Kwa hiyo, ni vigumu kujua muda ambao hakuwapo. Hata hivyo, Nehemia aliporudi Yerusalemu, alipata kwamba makuhani hawakuwa wanaungwa mkono, na watu waliacha kushika sheria ya Sabato. Wengi wao walikuwa wameoa wake wageni, na hata watoto wao hawakuzungumza Kiyahudi. Kwa kuwa mambo yote hayo yalitendeka, yaelekea Nehemia hakuwapo kwa muda mrefu.

13:25, 28—Zaidi ya “kuwalaumu” Wayahudi waliorudi nyuma, Nehemia alichukua hatua gani nyingine ili kurekebisha mambo? Nehemia ‘aliwalaani’ kwa kuwasomea hukumu zilizo katika Sheria ya Mungu. ‘Aliwapiga watu fulani kati yao,’ labda kwa kuamuru wachukuliwe hatua ya hukumu. Ili kuonyesha jinsi alivyochukia ukosefu wao wa maadili ‘aling’oa nywele zao.’ Pia, alimfukuza mjukuu wa Kuhani Mkuu Eliashibu ambaye alikuwa amemwoa binti ya Sanbalati, Mhoroni.

Mambo Tunayojifunza:

8:8. Tukiwa walimu wa Neno la Mungu, ‘tunaeleza maana yake’ kwa kuongea kwa njia inayosikika wazi, kukazia maneno, kufafanua Maandiko kwa usahihi, na kuonyesha matumizi yake vizuri.

8:10. Tunapata “shangwe ya Yehova” kwa kujua na kutosheleza mahitaji yetu ya kiroho na kufuata mwongozo wa kitheokrasi. Tunapaswa kujifunza Biblia kwa bidii, kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi kwa bidii!

11:2. Kuacha urithi na kuhamia Yerusalemu kulitia ndani gharama na matatizo mbalimbali. Wale waliojitolea kuhama walionyesha roho ya kujidhabihu. Sisi pia tunaweza kuonyesha roho hiyohiyo kunapokuwa na uhitaji wa kujitolea kuwasaidia wengine makusanyikoni au katika pindi nyinginezo.

12:31, 38, 40-42. Kuimba ni njia moja ya kumsifu Yehova na kumshukuru. Tunapokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, tunapaswa kuimba kutoka moyoni.

13:4-31. Tunapaswa kuwa macho tusiruhusu upendo wa mali, ufisadi, na uasi-imani utuathiri.

13:22. Nehemia alitambua kwamba alikuwa na wajibu kwa Mungu. Sisi pia tunapaswa kutambua wajibu wetu kwa Yehova.

Ni Muhimu Kuwa na Baraka za Yehova!

Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova mwenyewe asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu.” (Zaburi 127:1) Kitabu cha Nehemia kinaonyesha vizuri sana ukweli wa maneno hayo!

Jambo tunalojifunza liko wazi. Ikiwa tunataka kufanikiwa katika jambo lolote tunalofanya, ni lazima tupate baraka za Yehova. Je, tunaweza kutazamia baraka za Yehova ikiwa hatutangulizi ibada ya kweli maishani mwetu? Basi, kama Nehemia, acheni jambo kuu maishani mwetu liwe kuendeleza ibada ya Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 8]

“Moyo wa mfalme ni kama vijito vya maji mkononi mwa Yehova”

[Picha katika ukurasa wa 9]

Nehemia, mtu mwenye bidii na mwenye hisia nyororo, aja Yerusalemu

[Picha katika ukurasa wa 10, 11]

Je, unajua jinsi ya ‘kueleza maana’ ya Neno la Mungu?