Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Yosefu, mtumishi mwaminifu wa Yehova, alitumia kikombe cha pekee cha fedha kusoma ishara za bahati, kama ambavyo huenda ikadokezwa na andiko la Mwanzo 44:5?

Kwa kweli, hakuna sababu ya kuamini kwamba Yosefu alitumia aina yoyote ya uaguzi.

Biblia inaonyesha maoni ya Yosefu kuhusu kufanya uchawi ili kujua mambo ya wakati ujao. Mapema, alipoombwa atafsiri ndoto za Farao, Yosefu alisisitiza tena na tena kwamba Mungu tu ndiye anayeweza ‘kutangaza’ matukio ya wakati ujao. Kwa sababu hiyo, Farao mwenyewe aliamini kwamba Mungu ambaye Yosefu anaabudu—Mungu wa kweli, na si nguvu za uchawi—alimwezesha Yosefu kujua mambo ya wakati ujao. (Mwanzo 41:16, 25, 28, 32, 39) Katika Sheria ambayo Musa alipewa baadaye, Yehova alikataza uchawi au uaguzi, hivyo akahakikisha kwamba ni Yeye tu anayetabiri matukio ya wakati ujao.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Kwa nini basi Yosefu alionyesha kupitia mtumishi wake kwamba alitumia kikombe cha fedha “kusoma ishara za bahati kwa ustadi”? * (Mwanzo 44:5) Tunahitaji kufikiria ni katika hali gani maneno hayo yalisemwa.

Kwa sababu ya njaa kali, ndugu za Yosefu walisafiri kwenda Misri ili kutafuta chakula. Miaka kadhaa mapema, ndugu haohao walimwuza Yosefu utumwani. Sasa, kwa kuwa hawakumtambua, waliomba msaada kwa ndugu yao ambaye alikuwa sasa msimamizi wa chakula nchini Misri. Yosefu hakujitambulisha kwao. Badala yake, aliamua kuwajaribu. Yosefu alitaka kujua ikiwa walikuwa wametubu kwelikweli. Pia, alitaka kujua ni kwa kadiri gani walimpenda ndugu yao Benyamini na baba yao, Yakobo, ambaye alimpenda sana Benyamini. Hivyo, Yosefu alitumia ujanja.—Mwanzo 41:55–44:3.

Yosefu alimwamuru mmoja wa watumishi wake kujaza mifuko ya ndugu zake kwa chakula, na kumrudishia kila mmoja pesa zake katika kinywa cha mfuko wake, kisha atie kikombe cha fedha cha Yosefu katika kinywa cha mfuko wa Benyamini. Wakati wote huo, Yosefu alijitambulisha kuwa msimamizi wa nchi ya kipagani. Alijifanya, kwa matendo yake, na kwa lugha yake kuwa msimamizi huyo mpagani ili ndugu zake wasimtambue.

Yosefu alipowakabili ndugu zake, aliendelea kutumia mbinu yake kwa kuwauliza hivi: “Je, hamkujua kwamba mimi naweza kusoma ishara za bahati kwa ustadi?” (Mwanzo 44:15) Hivyo, inaonekana kikombe hicho kilitumiwa kama mbinu tu. Yosefu hakutumia kikombe hicho kusoma ishara za bahati, na pia Benyamini hakukiiba.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kikizungumza kuhusu zoea hilo la nyakati za kale, kichapo The Holy Bible, With an Explanatory and Critical Commentary, kilichohaririwa na F. C. Cook, kinaeleza hivi: “Uaguzi ulifanywa kwa kutumbukiza dhahabu, fedha, au mawe ya thamani, ndani ya maji, kisha sura yake ikachunguzwa; au ulifanywa kwa kutazama maji kama kioo.” Mchanganuzi wa Biblia Christopher Wordsworth, anasema hivi: “Nyakati nyingine kikombe kilijazwa maji, na jibu likatolewa kupitia picha iliyotokezwa na mwangaza wa jua juu ya maji yaliyokuwa ndani ya kikombe.”