Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ushahidi Kwa Mataifa Yote”

“Ushahidi Kwa Mataifa Yote”

“Ushahidi Kwa Mataifa Yote”

“Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—MATENDO 1:8.

1. Ni wakati gani na mahali gani ambapo wanafunzi walisikia kwa mara ya kwanza unabii ulio kwenye Mathayo 24:14?

MANENO ya Yesu kwenye Mathayo 24:14 yanajulikana sana hivi kwamba wengi wetu tunaweza kuyasema bila kuyasoma. Huo ni unabii wenye kuvutia kama nini! Hebu wazia mambo ambayo wanafunzi walifikiria walipousikia kwa mara ya kwanza! Ilikuwa katika mwaka wa 33 W.K. Wanafunzi walikuwa wamekaa pamoja na Yesu kwa miaka mitatu, na sasa walikuwa wamekuja naye Yerusalemu. Walikuwa wameona miujiza yake na kusikiliza mafundisho yake. Ingawa walifurahia kweli zenye thamani ambazo Yesu aliwafundisha, walijua wazi kwamba si watu wote waliozifurahia. Yesu alikuwa na maadui wenye mamlaka na wenye uvutano.

2. Wanafunzi wangekabili hatari na matatizo gani?

2 Kwenye Mlima wa Mizeituni, wanafunzi wanne waliketi pamoja na Yesu, na kusikiliza kwa makini alipozungumza kuhusu hatari na matatizo ambayo wangekabili. Mapema, Yesu alikuwa amewaambia kwamba atauawa. (Mathayo 16:21) Sasa, alitaja wazi kwamba wao pia watateswa vikali. Alisema hivi: ‘Watu watawatia ninyi katika dhiki na kuwaua ninyi, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ Lakini mambo mengine pia yangetukia. Manabii wa uwongo wangewapotosha wengi. Wengine wangekwazika na kusalitiana na kuchukiana. Isitoshe, wengine, naam, “walio wengi zaidi” wangeruhusu upendo wao kwa Mungu na kwa Neno lake upoe.—Mathayo 24:9-12.

3. Kwa nini maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:14 yanashangaza sana?

3 Baada ya Yesu kuzungumzia mambo hayo yenye kuhuzunisha, alisema maneno ambayo haikosi yaliwastaajabisha sana wanafunzi wake. Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Naam, kazi ambayo Yesu alianzisha huko Israeli, yaani ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli,’ ingeendelea na kuongezeka kotekote duniani. (Yohana 18:37) Huo ni unabii wenye kushangaza kama nini! Ingekuwa vigumu sana kueneza kazi hiyo kwa “mataifa yote”; na kufanya kazi hiyo licha ya ‘kuchukiwa na mataifa yote’ kungekuwa kama muujiza. Kutimizwa kwa kazi hiyo kubwa kungetukuza ukuu na nguvu za Yehova na vilevile upendo, rehema, na subira yake. Isitoshe, kungewapa watumishi wake nafasi ya kuonyesha imani na ujitoaji wao.

4. Ni nani waliopewa kazi ya kutoa ushahidi, na Yesu aliwafariji jinsi gani?

4 Yesu aliwaeleza wazi wanafunzi wake kwamba wana kazi kubwa sana. Kabla ya kupaa kwenda mbinguni, Yesu aliwatokea na kusema hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Bila shaka, baada ya muda mfupi wengine wangeungana nao. Lakini bado wanafunzi walikuwa wachache. Haikosi wanafunzi walifarijika sana walipojua kwamba roho takatifu ya Mungu yenye nguvu ingewatia nguvu ili kutimiza kazi hiyo iliyotoka kwa Mungu!

5. Wanafunzi hawakujua nini kuhusu kazi ya kutoa ushahidi?

5 Wanafunzi walijua kwamba waliamuriwa kuhubiri habari njema na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19, 20) Lakini hawakujua kazi ya kuhubiri ingefanywa kwa ukamili jinsi gani wala hawakujua mwisho ungekuja wakati gani. Sisi pia hatujui. Yehova peke yake ndiye anayeamua mambo hayo. (Mathayo 24:36) Yehova atakapotosheka na ushahidi ambao umetolewa, atakomesha mfumo huu mbovu wa mambo. Hapo ndipo Wakristo watakapotambua kwamba kazi ya kuhubiri imefanywa kwa kadiri ambayo Yehova alikusudia. Wanafunzi wa mapema hawangewazia kwamba ushahidi ungetolewa kwa kiwango ambacho kimefikiwa katika wakati huu wa mwisho.

Kutoa Ushahidi Katika Karne ya Kwanza

6. Ni nini kilichotukia siku ya Pentekoste 33 W.K. na punde baadaye?

6 Katika karne ya kwanza, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi ilikuwa na matokeo makubwa ajabu. Siku ya Pentekoste 33 W.K., wanafunzi 120 hivi walikuwa katika chumba fulani cha juu huko Yerusalemu. Roho takatifu ya Mungu ilimwagwa juu yao, mtume Petro alitoa hotuba yenye kuchochea na kueleza maana ya muujiza huo, na watu wapatao 3,000 wakawa waamini na kubatizwa. Huo ulikuwa mwanzo tu. Licha ya jitihada nyingi za viongozi wa kidini za kukomesha kuhubiriwa kwa habari njema, ‘Yehova aliendelea kuongeza [kwa wanafunzi] kila siku wale waliokuwa wakiokolewa.’ Punde baadaye, “hesabu ya wanaume ikawa karibu elfu tano.” Kisha, “waliomwamini Bwana wakaendelea kuongezeka, umati wa wanaume na pia wa wanawake.”—Matendo 2:1-4, 8, 14, 41, 47; 4:4; 5:14.

7. Kwa nini kugeuza imani kwa Kornelio kulikuwa tukio muhimu?

7 Tukio lingine muhimu lilitokea mwaka wa 36 W.K. Kornelio, ambaye hakuwa Myahudi, aligeuza imani na kubatizwa. Alipomwelekeza mtume Petro kwa mtu huyo aliyemwogopa Mungu, Yehova alionyesha kwamba amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote’ haikuhusu tu Wayahudi katika nchi mbalimbali. (Matendo 10:44, 45) Wale walioongoza waliitikiaje? Mitume na wanaume wazee katika Yudea walimtukuza Mungu walipotambua kwamba habari njema ingehubiriwa pia kwa watu wa mataifa, yaani, kwa wasio Wayahudi. (Matendo 11:1, 18) Wakati huohuo, kazi ya kuhubiri iliendelea kuwa na matokeo miongoni mwa Wayahudi. Miaka kadhaa baadaye, yapata mwaka wa 58 W.K., kulikuwa na wasio Wayahudi walioamini na hata “maelfu mengi ya waamini [Wayahudi].”—Matendo 21:20.

8. Habari njema huwasaidiaje watu?

8 Ingawa ongezeko la idadi ya Wakristo wa karne ya kwanza linapendeza, inafaa pia tufikirie watu wenyewe walioongezeka. Ujumbe wa Biblia ambao watu hao walisikia ulikuwa wenye nguvu. (Waebrania 4:12) Ujumbe huo ulibadilisha sana maisha ya wale waliousikia. Watu waliacha mazoea mabaya, wakavaa utu mpya, nao wakapatanishwa na Mungu. (Waefeso 4:22, 23) Ndivyo ilivyo hata leo. Isitoshe, wote wanaokubali habari njema wana tazamio zuri la kuishi milele.—Yohana 3:16.

Wafanyakazi Wenzi Pamoja na Mungu

9. Wakristo wa mapema walitambua kwamba wana pendeleo na daraka gani?

9 Wakristo wa mapema hawakujisifia matokeo ya kazi yao. Walitambua kwamba kazi yao wakiwa wahudumu ilitegemezwa kwa “nguvu za roho takatifu.” (Waroma 15:13, 19) Yehova ndiye aliyesababisha ukuzi wa kiroho. Lakini pia Wakristo hao walitambua kwamba walikuwa na pendeleo na daraka la kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Wakorintho 3:6-9) Hivyo, kupatana na himizo la Yesu, walijitahidi sana kufanya kazi waliyopewa.—Luka 13:24.

10. Wakristo fulani wa mapema walifanya jitihada gani ili kutoa ushahidi kwa mataifa yote?

10 Akiwa “mtume kwa mataifa,” Paulo alisafiri maelfu ya kilometa katika bahari na nchi kavu, akianzisha makutaniko mengi katika mkoa wa Asia wa Roma na katika Ugiriki. (Waroma 11:13) Pia, alisafiri hadi Roma na huenda hata hadi Hispania. Wakati huohuo, mtume Petro, ambaye alikabidhiwa utume wa kutangaza “habari njema kwa . . . wale waliotahiriwa,” alisafiri upande tofauti ili atumikie Babiloni, ambalo lilikuwa kituo muhimu cha Dini ya Kiyahudi wakati huo. (Wagalatia 2:7-9; 1 Petro 5:13) Wengine wengi waliofanya kazi ya Bwana walikuwa wanawake kama Trifaina na Trifosa. Mwanamke mwingine aliyeitwa Persisi anatajwa kuwa “alifanya kazi nyingi katika Bwana.”—Waroma 16:12.

11. Yehova alibarikije jitihada za wanafunzi?

11 Yehova alibariki sana jitihada za wafanyakazi hao na za wengine wenye bidii. Yapata miaka 30 baada ya Yesu kutabiri kwamba ushahidi ungetolewa kwa mataifa yote, Paulo aliandika kwamba “habari njema” ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23) Je, mwisho ulikuja baada ya hapo? Ndiyo, mwisho ulikuja kwa njia fulani. Ulikuja mfumo wa Wayahudi ulipokomeshwa mwaka wa 70 W.K., wakati majeshi ya Roma yalipoharibu Yerusalemu na hekalu. Hata hivyo, Yehova alikuwa ameamua kwamba ushahidi mkubwa zaidi ungetolewa kabla ya kukomesha mfumo wote mbovu wa Shetani.

Ushahidi Unaotolewa Leo

12. Wanafunzi wa Biblia wa mapema walielewaje amri ya kuhubiri?

12 Wakati wa sehemu ya mwisho ya karne ya 19, baada ya kipindi kirefu cha uasi-imani wa kidini, ibada safi ilirudishwa. Wanafunzi wa Biblia, jina ambalo Mashahidi wa Yehova walitumia wakati huo, walielewa vizuri amri ya kufanya wanafunzi katika dunia yote. (Mathayo 28:19, 20) Kufikia mwaka wa 1914, watu 5,100 hivi walihubiri kwa ukawaida, na habari njema ilikuwa imehubiriwa katika nchi 68. Hata hivyo, Wanafunzi hao wa Biblia wa mapema hawakutambua maana kamili ya Mathayo 24:14. Kufikia mwishoni mwa karne ya 19, Biblia, ambayo ina habari njema, au injili, ilikuwa imetafsiriwa katika lugha nyingi na kuchapishwa na sosaiti za Biblia na kugawanywa ulimwenguni. Hivyo, kwa makumi kadhaa ya miaka, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba ushahidi ulikuwa umekwisha kutolewa kwa mataifa.

13, 14. Ni uelewaji gani zaidi wa mapenzi na kusudi la Mungu ambao ulifunuliwa katika gazeti moja la Mnara wa Mlinzi la 1928?

13 Pole kwa pole, Yehova aliwapa watu wake uelewaji zaidi kuhusu mapenzi yake na kusudi lake. (Methali 4:18) Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1928, lilisema hivi: “Je, tunaweza kusema kwamba kugawanywa kwa Biblia kulitimiza unabii wa kuhubiriwa kwa injili ya ufalme? La hasha! Licha ya kugawanywa kwa Biblia, bado ni muhimu kwa kikundi kidogo cha mashahidi wa Mungu walio duniani kichapishe vichapo vinavyoeleza kuhusu [kusudi] la Mungu na kwenda kwenye nyumba ambako Biblia hizo zimegawanywa. La sivyo, watu hawatajua kuhusu kuanzishwa kwa serikali ya Kimasihi katika siku zetu.”

14 Toleo hilohilo la Mnara wa Mlinzi liliendelea kusema: “Katika mwaka wa 1920, . . . Wanafunzi wa Biblia walipata kuelewa kwa usahihi unabii wa Bwana wetu kwenye Mathayo 24:14. Kisha wakatambua kwamba ‘injili hii’ ambayo ilipaswa kuhubiriwa katika ulimwengu wote ili kuwa ushuhuda kwa wasio Wayahudi au kwa mataifa yote, haikuwa injili kuhusu ufalme utakaokuja bali injili inayoonyesha kwamba Mfalme wa Kimasihi ameanza kutawala dunia.”

15. Kazi ya kutoa ushahidi imepanukaje tangu miaka ya 1920?

15 ‘Kikundi hicho kidogo cha mashahidi’ katika miaka ya 1920 kiliongezeka. Katika makumi ya miaka iliyofuata, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ulitambulishwa na kuanza kukusanywa. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Leo, kuna wahubiri 6,613,829 wa habari njema katika nchi 235. Lo! Huo ni utimizo wenye kustaajabisha sana wa unabii! Hakuna wakati mwingine wowote ambapo “habari njema ya ufalme” imehubiriwa kwa kadiri kubwa hivyo. Hakuna wakati mwingine wowote ambapo kumekuwa na watumishi wengi waaminifu wa Yehova duniani kama leo.

16. Ni nini kilichotimizwa katika mwaka wa utumishi uliopita? (Ona chati kwenye ukurasa wa 27-30.)

16 Kwa pamoja, umati huo mkubwa wa Mashahidi umefanya kazi kubwa katika mwaka wa utumishi wa 2005. Zaidi ya saa bilioni moja zilitumiwa ili kuhubiri habari njema katika nchi 235. Mamilioni ya ziara za kurudia zilifanywa, na mamilioni ya mafunzo ya Biblia yaliongozwa. Kazi hiyo ilifanywa na Mashahidi wa Yehova, ambao walitumia kwa hiari wakati wao na mali zao ili kuwaeleza wengine kuhusu Neno la Mungu. (Mathayo 10:8) Kupitia roho yake takatifu yenye nguvu, Yehova huendelea kuwapa nguvu watumishi wake wafanye mapenzi yake.—Zekaria 4:6.

Kufanya Kazi kwa Bidii Ili Kutoa Ushahidi

17. Watu wa Yehova wanaitikiaje maneno ya Yesu kuhusu kuhubiri habari njema?

17 Ingawa miaka 2,000 hivi imepita tangu Yesu aliposema kwamba habari njema itahubiriwa, bidii ya watu wa Mungu ya kufanya kazi hiyo haijapungua. Tunajua kwamba tunapovumilia katika kufanya yaliyo mema, tunaonyesha sifa za Yehova za upendo, rehema, na subira. Kama yeye, hatutaki yeyote aangamizwe bali tunataka watu watubu na kupatanishwa na Yehova. (2 Wakorintho 5:18-20; 2 Petro 3:9) Wakiwa wamewaka roho ya Mungu, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuhubiri kwa bidii habari njema hadi miisho ya dunia. (Waroma 12:11) Ndiyo sababu watu kila mahali wanakubali kweli na kufuata mwongozo ambao Yehova anatoa kwa upendo. Hebu ona mifano kadhaa.

18, 19. Ni mambo gani unayoweza kusimulia kuhusu baadhi ya watu ambao wameitikia vizuri habari njema?

18 Charles alikuwa mkulima magharibi mwa Kenya. Katika mwaka wa 1998, aliuza kilo 8,000 za tumbaku, naye akapewa cheti cha Mkulima Bora wa Tumbaku. Wakati huo, alianza kujifunza Biblia. Baada ya muda, alitambua kwamba mtu anayehusika katika kuzalisha tumbaku anavunja amri ya Yesu ya kupenda jirani. (Mathayo 22:39) Alipotambua kwamba kuwa ‘mkulima bora wa tumbaku’ ni sawa na kuwa ‘muuaji bora,’ Charles aliharibu mimea yake ya tumbaku kwa kuipulizia sumu. Alifanya maendeleo, akajiweka wakfu na kubatizwa, na sasa yeye ni painia wa kawaida na mtumishi wa huduma.

19 Hakuna shaka kwamba Yehova anatikisa mataifa kupitia ushahidi unaotolewa duniani pote, na vitu vyenye kutamanika, yaani, watu, wanaingia. (Hagai 2:7) Pedro, anayeishi Ureno, aliingia chuo cha kuwazoeza makasisi alipokuwa na umri wa miaka 13. Alitaka kuwa mmishonari na kufundisha Biblia. Hata hivyo, baada ya muda mfupi aliondoka chuoni kwa sababu Biblia haikuzungumziwa sana wakati wa masomo. Miaka sita baadaye, alisomea saikolojia kwenye chuo kikuu huko Lisbon. Aliishi pamoja na shangazi yake, ambaye ni Shahidi wa Yehova, naye alimtia moyo ajifunze Biblia. Wakati huo, Pedro hakuwa na uhakika kwamba kuna Mungu, na alisitasita kufanya uamuzi kuhusu kujifunza Biblia. Alizungumza na profesa aliyemfundisha saikolojia kuhusu hali hiyo ya kusitasita. Profesa huyo akasema kwamba kulingana na saikolojia, watu wanaositasita kufanya maamuzi hujiumiza wenyewe. Pedro aliposikia hivyo, akaamua kujifunza Biblia. Alibatizwa hivi majuzi na sasa yeye pia anaongoza mafunzo ya Biblia.

20. Kwa nini tunaweza kushangilia kwamba ushahidi unatolewa kwa mataifa yote kwa kiwango kikubwa sana?

20 Hatujui ni kwa kadiri gani ushahidi utatolewa kwa mataifa, wala hatujui siku wala saa ambayo mwisho utakuja. Tunachojua ni kwamba mwisho uko karibu. Tunashangilia kujua kwamba kuhubiriwa kwa habari njema kwa kiwango kikubwa sana ni jambo moja tu linaloonyesha kuwa karibuni Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali za wanadamu. (Danieli 2:44) Kila mwaka, mamilioni ya watu wanapewa nafasi ya kukubali habari njema, na hilo humtukuza Mungu wetu, Yehova. Basi, acheni tuazimie kubaki waaminifu na kuendelea kwa bidii kufanya kazi ya kutoa ushahidi kwa mataifa yote pamoja na ndugu zetu ulimwenguni pote. Tukifanya hivyo, tutajiokoa wenyewe na wale wanaotusikiliza pia.—1 Timotheo 4:16.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Mathayo 24:14 ni unabii unaostaajabisha sana?

• Ni jitihada gani ambazo Wakristo wa mapema walifanya katika kuhubiri, na matokeo yakawaje?

• Wanafunzi wa Biblia walipataje kuelewa uhitaji wa kutoa ushahidi kwa mataifa yote?

• Ni nini kinachokupendeza kuhusu utendaji wa mwaka uliopita wa watu wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 27-30]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2005 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona buku lililojalidiwa)

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 25]

Paulo alisafiri maelfu ya kilometa juu ya nchi kavu na baharini ili kuhubiri habari njema

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yehova alimwelekeza Petro atoe ushahidi kwa Kornelio na familia yake