Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Alinisaidia Nimpate

Yehova Alinisaidia Nimpate

Simulizi la Maisha

Yehova Alinisaidia Nimpate

LIMESIMULIWA NA FLORENCE CLARK

Niliushika mkono wa mume wangu aliyekuwa mgonjwa sana. Nikiwa Mwanglikana, nilisali kwa Mungu ili mume wangu apate nafuu, na nikaahidi kwamba ikiwa angepona, ningemtafuta Mungu hadi nimpate kisha niwe mali yake.

NILIITWA Florence Chulung nilipozaliwa mnamo Septemba 18, 1937, katika Jumuiya ya Waaborijini ya Oombulgurri kwenye Uwanda wa Juu wa Kimberley magharibi mwa Australia.

Mimi hufurahi ninapokumbuka siku zangu za utotoni, wakati mambo yalipokuwa shwari. Kanisani, nilijifunza mambo machache ya msingi kuhusu Mungu na Biblia, lakini mama yangu ndiye aliyenifundisha kanuni za Kikristo. Alinisomea Biblia kwa ukawaida, na tangu utotoni, nilisitawisha upendo kuhusu mambo ya kiroho. Pia, nilivutiwa na mmoja wa shangazi zangu aliyekuwa mmishonari katika kanisa lao. Nilitaka sana kufuata kielelezo chake.

Jumuiya yetu ambayo zamani iliitwa Forrest River Mission, iliandaa masomo ya darasa la kwanza hadi la tano. Nilienda shule kwa muda wa saa mbili tu kila asubuhi. Hiyo ilimaanisha kwamba singepata elimu ya kutosha, na hilo lilimfanya baba yangu awe na wasiwasi. Alitaka watoto wake wapate elimu bora, hivyo akaamua kuondoka Oombulgurri na kuhamisha familia yake katika mji wa Wyndham. Nilihuzunika sana tulipoondoka, lakini huko Wyndham, niliweza kwenda shule siku nzima kwa miaka minne iliyofuata, tangu mwaka wa 1949 hadi 1952. Ninamshukuru sana baba yangu kwa kuniwezesha kupata elimu hiyo.

Mama alimfanyia kazi daktari wa eneo letu, na nilipoacha shule nikiwa na umri wa miaka 15, daktari huyo alinipa kazi ya uuguzi katika hospitali ya Wyndham. Niliikubali, kwa kuwa wakati huo ilikuwa vigumu kupata kazi.

Miaka kadhaa baadaye, nilikutana na Alec, aliyekuwa mfugaji wa ng’ombe. Tulifunga ndoa mwaka wa 1964 katika mji wa Derby, ambapo kwa kawaida nilihudhuria Kanisa la Anglikana. Siku moja Mashahidi wa Yehova walinitembelea. Niliwaambia kwamba sikupendezwa kabisa na mambo yao na nikawaambia wasirudi tena. Hata hivyo, walisema jambo fulani lililonivutia, kwamba Mungu ana jina, yaani, Yehova.

“Je, Huwezi Kujiombea?”

Katika mwaka wa 1965 maisha yalianza kuwa magumu sana. Mume wangu alipata misiba mitatu mibaya, aliumia mara mbili kutokana na farasi na mara moja kutokana na gari. Lakini alipata nafuu kutokana na majeraha hayo naye akarudi kazini. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, aliumia tena kutokana na farasi. Mara hii, aliumia vibaya sana kichwani. Nilipofika hospitali, daktari aliniambia kwamba mume wangu angekufa. Nilifadhaika sana. Muuguzi mmoja alimweleza kasisi anitembelee, lakini padri huyo akasema: “Siji leo. Nitakuja kesho!”

Nilimwambia mtawa wa kike kwamba nilitaka kasisi huyo awe karibu nami ili tuombe pamoja. Mtawa huyo akasema: “Una tatizo gani? Je, huwezi kujiombea?” Hivyo, nikaanza kuomba mbele ya sanamu za kanisa ili kupata msaada, lakini sikufanikiwa. Ilionekana kwamba mume wangu angekufa. Nilianza kufikiri, ‘Nitakabilianaje na hali mume wangu akifa?’ Pia, nilikuwa na wasiwasi kuhusu watoto wangu watatu, Christine, Nanette, na Geoffrey. Wangeishije bila baba? Lakini siku tatu baadaye mume wangu alipata nafuu, na akaondoka hospitali mnamo Desemba 6, 1966.

Ingawa alipata nafuu, ubongo wa mume wangu ulikuwa umeathiriwa. Hangeweza kukumbuka mambo, akawa mjeuri, na hisia zake zilibadilika-badilika. Ilikuwa vigumu kwake kushughulika na watoto, naye akawa mkali sana ikiwa hawangefanya mambo kama watu wazima. Ilikuwa vigumu kumshughulikia. Nilimfanyia karibu kila kitu. Hata nilimfundisha tena kusoma na kuandika. Mkazo niliopata nilipokuwa nikimtunza huku nikishughulikia madaraka mengine ya familia, ulinifanya nichanganyikiwe kiakili. Miaka saba baada ya mume wangu kupata msiba, tulikubaliana tutengane kwa muda ili nipate nafuu.

Nilichukua watoto na tukahamia kusini katika jiji la Perth. Kabla ya kuhama, dada yangu mdogo alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova huko Kununurra, mji mdogo ulio magharibi mwa Australia. Alinionyesha picha katika kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, * inayoonyesha ahadi ya Biblia kuhusu paradiso duniani. Pia, kutokana na kitabu hicho, alinionyesha kwamba Mungu ana jina, Yehova, na hilo likanivutia. Kwa kuwa nilikuwa sijaambiwa kamwe mambo hayo kanisani, niliamua kwamba mara tu nitakapofika Perth nitawapigia simu Mashahidi wa Yehova.

Hata hivyo, nilisita kidogo kuwasiliana nao. Kisha jioni moja, mlango ulibishwa. Mwanangu akaenda kufungua mlango naye akarudi haraka na kuniambia, “Mama, wale watu ambao ulisema utawapigia simu wapo hapa.” Nilishangaa kidogo na kusema, “Waambie sipo!” Lakini mwanangu akajibu, “Mama, unajua kwamba sipaswi kusema uwongo.” Baada ya kukosolewa na mwanangu, nilifungua mlango. Nilipowasalimu, niliona wameshangaa sana. Walikuja kumwona mtu mwingine ambaye alikuwa amehama. Niliwakaribisha ndani na kuwauliza maswali mengi, nami nikapewa majibu yenye kuridhisha kutoka katika Biblia.

Juma lililofuata, nilianza kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na Mashahidi kwa kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Funzo hilo lilichochea upendezi wangu kuhusu mambo ya kiroho. Majuma mawili baadaye, nilihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo Yesu. Nilianza kuhudhuria mikutano kila Jumapili, na baadaye nikaanza pia kuhudhuria mikutano ya katikati ya juma. Pia, nilianza kuzungumza na wengine kuhusu mambo niliyojifunza. Nilitambua kwamba kuwasaidia wengine kujifunza kweli za Biblia kulinisaidia kiakili na kihisia. Miezi sita baadaye, nilibatizwa kwenye kusanyiko la wilaya huko Perth.

Kadiri nilivyofanya maendeleo ya kiroho, ndivyo nilivyothamini maoni ya Yehova kuhusu utakatifu wa ndoa, kutia ndani kanuni ya Biblia kwenye 1 Wakorintho 7:13, inayosema: “Mwanamke aliye na mume asiyeamini, na bado mume huyo anakubali kukaa pamoja naye, basi asimwache mume wake.” Andiko hilo lilinichochea kumrudia Alec.

Kurudi Derby

Nilifika huko Derby mnamo Juni 21, 1979, baada ya kuachana na mume wangu kwa zaidi ya miaka mitano. Bila shaka, sikuwa na uhakika kuhusu jinsi ambavyo angeitikia nikirudi. Nilishangaa kwamba alifurahi kuona nimerudi, ingawa alionyesha kwa kadiri fulani kukatishwa tamaa kwa sababu nilikuwa sasa Shahidi wa Yehova. Mara moja akapendekeza niwe nikienda katika kanisa analoshirikiana nalo, lile nililokuwa nikihudhuria kabla ya kwenda Perth. Nilimweleza kwamba singeweza kufanya hivyo. Nikiwa mke Mkristo, nilijitahidi sana kuheshimu ukichwa wake. Nilijaribu kuzungumza naye kuhusu Yehova na ahadi Zake nzuri za wakati ujao, lakini hakupendezwa.

Baada ya muda, Alec alikubali njia yangu mpya ya maisha na pia akaanza kunisaidia kifedha ili niweze kuhudhuria makusanyiko, na pia mikutano ya kila juma. Nilishukuru sana aliponunua gari ili nilitumie kwa ajili ya huduma ya Kikristo, nalo lilinisaidia sana katika sehemu hiyo ya mbali ya Australia. Mara nyingi, ndugu na dada, kutia ndani mwangalizi wa mzunguko, walilala nyumbani kwetu. Hilo lilimwezesha Alec kujuana na Mashahidi wengi, na alionekana kuwa alifurahia ushirika wao.

Nilihisi Kama Ezekieli

Ingawa nilipendezwa na ziara za akina ndugu na dada, nilikabili tatizo fulani. Ni mimi tu niliyekuwa Shahidi katika mji wa Derby. Kutaniko la karibu zaidi lilikuwa katika mji wa Broome, ulio umbali wa kilometa 220. Hivyo, niliamua kujitahidi niwezavyo kutangaza habari njema. Kwa msaada wa Yehova, nilijipanga, na nikaanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Niliona kazi hiyo kuwa ngumu, lakini niliendelea kujikumbusha maneno haya ya mtume Paulo: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.

Makasisi wa eneo hilo hawakufurahia utendaji wangu, hasa nilipowahubiria Waaborijini wenzangu. Walijaribu kunitisha na kunizuia kuhubiri. Upinzani wao ulizidi tu kunichochea kuendelea kuhubiri, na nilisali kwa ukawaida kwa Yehova ili anisaidie. Mara nyingi nilikumbuka maneno yenye kutia moyo ambayo Ezekieli aliambiwa: “Tazama! Nimeufanya uso wako uwe mgumu kama nyuso zao na paji la uso wako liwe gumu kama mapaji ya nyuso zao. Nimelifanya paji la uso wako kuwa kama almasi, gumu kuliko jiwe gumu. Usiwaogope, wala usiingiwe na hofu kwa sababu ya nyuso zao.”—Ezekieli 3:8, 9.

Mara nyingi, wanaume wawili wa kikundi cha muungano wa makanisa walikuja mahali nilipokuwa nikinunua vitu dukani. Walinidhihaki hadharani na kwa kelele, huku wakijaribu kuvutia uangalifu wa wanunuzi wengine. Niliwapuuza. Wakati mwingine, nilipokuwa nikifanya ziara ya kurudia kwa mtu aliyependezwa, mhudumu kutoka kanisa la eneo hilo alikuja na kuanza kunishutumu kwamba simwamini Yesu. Alininyang’anya Biblia yangu, akaitikisa mbele ya uso wangu, na kuirudisha mkononi mwangu kwa nguvu. Nilimkazia macho na kunukuu kwa upole lakini kwa uthabiti andiko la Yohana 3:16 na kumhakikishia kwamba ninamwamini Yesu. Alishangaa jinsi nilivyomjibu nikiwa na uhakika, naye akaondoka bila kusema neno lingine.

Nilifurahia sana kuwahubiria Waaborijini katika eneo la Derby. Kasisi mmoja alijaribu kunizuia kuwahubiria watu wa eneo fulani, lakini baadaye alihamishwa. Hivyo, niliweza kuwapelekea ujumbe wa Biblia. Sikuzote nilitamani kuwa mmishonari kama shangazi yangu, na sasa nilikuwa nikifanya kazi ya umishonari na kuwasaidia wengine kujifunza Neno la Mungu. Waaborijini wengi waliitikia vizuri mahubiri yangu, na nikaanzisha mafunzo mengi ya Biblia.

Kutambua Uhitaji Wangu wa Kiroho

Kwa miaka mitano, ni mimi tu niliyekuwa Shahidi wa Yehova huko Derby. Ilikuwa vigumu kwangu kuendelea kuwa na nguvu kiroho bila kukusanyika kwa ukawaida pamoja na waabudu wenzangu ili kutiwa moyo. Pindi moja, kwa kuwa nilikuwa nimevunjika moyo sana niliamua kuendesha gari ili kujituliza. Niliporudi nyumbani alasiri hiyo, nilikuta dada mmoja na watoto wake saba wakiningoja. Waliniletea vichapo kutoka kutaniko la Broome, lililo umbali wa kilometa nyingi. Tangu siku hiyo na kuendelea, dada huyo, Betty Butterfield, alikuja Derby mara moja kwa mwezi na kukaa pamoja nami kwa juma zima. Tulienda kuhubiri pamoja na kisha tukajifunza Mnara wa Mlinzi nyumbani kwangu. Mimi pia nilisafiri kwenda Broome mara moja kwa mwezi.

Ndugu huko Broome walinisaidia sana na mara kwa mara walifunga safari ndefu kuja Derby ili kunisaidia kuhubiri. Waliwahimiza akina ndugu au dada kutoka miji mingine wapitie Derby ili kunitembelea na kuhubiri pamoja nami. Pia, ndugu na dada hao waliniletea kaseti za hotuba za watu wote. Wengine walijiunga nami katika funzo la Mnara wa Mlinzi. Ziara hizo fupi zilikuwa zenye kutia moyo sana.

Napata Msaada Zaidi

Kwa miaka kadhaa, nilipata kichocheo zaidi wakati Arthur na Mary Willis, wenzi wa ndoa waliostaafu kutoka sehemu ya kusini ya Australia Magharibi, walipokuja kunisaidia kwa miezi mitatu katika majira ya baridi. Ndugu Willis aliongoza karibu mikutano yote na alituongoza katika mahubiri. Tulisafiri pamoja katika sehemu za mbali za Uwanda wa Kimberley ili kutembelea mashamba yenye mifugo katika maeneo hayo ya mbali. Kila mara Ndugu na Dada Willis waliporudi kwao, nilihisi huzuni nyingi.

Hatimaye, kuelekea mwishoni mwa mwaka wa 1983, nilipokea habari njema kwamba familia moja, yaani, Danny na Denise Sturgeon na wana wao wanne, walikuwa wanahamia Derby. Baada ya wao kufika, tulifanya mikutano ya kila juma kwa ukawaida na kuhubiri pamoja. Kutaniko lilianzishwa mwaka wa 2001. Leo, mji wa Derby una kutaniko la wahubiri wa Ufalme wenye bidii 24, wakiwemo wazee wawili na mtumishi wa huduma mmoja, ambao wanashughulikia mahitaji yetu ya kiroho. Nyakati nyingine, kwenye mikutano yetu tunafikia hudhurio la watu 30.

Ninapokumbuka miaka mingi iliyopita, ninatiwa moyo kuona jinsi Yehova alivyonisaidia ili nimtumikie. Hata ingawa mume wangu hajajiunga nami katika imani, bado anaendelea kunitegemeza katika njia nyingine. Watu watano wa familia yetu wamebatizwa na kuwa Mashahidi, yaani, binti zangu wawili, wajukuu wangu wawili, na mpwa wangu. Isitoshe, watu wengine wa jamaa yetu wanajifunza Biblia na watu wa Yehova.

Ninashukuru sana kwamba Yehova alinisaidia nimpate. Nimeazimia kuwa mali yake milele.—Zaburi 65:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, lakini sasa hakichapishwi tena.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AUSTRALIA

Wyndham

Uwanda wa Kimberley

Derby

Broome

Perth

[Credit Lines]

Kangaroo and lyrebird: Lydekker; koala: Meyers

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nikiwa muuguzi katika hospitali ya Wyndham, mwaka wa 1953

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kutaniko la Derby, mwaka wa 2005