Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema Yaenezwa Katika Miji ya Mbali ya Bolivia

Habari Njema Yaenezwa Katika Miji ya Mbali ya Bolivia

Habari Njema Yaenezwa Katika Miji ya Mbali ya Bolivia

TUKIWA watu 20 hivi tunakusanyika kwenye ufuo, tukitarajia kwa hamu kutembelea vijiji vilivyo kwenye chanzo cha mto. Tuko chini ya Milima ya Andes, mahali ambapo Mto Beni unafika kwenye maeneo tambarare ya bonde la Amazoni. Hilo ni eneo maridadi sana.

Hata hivyo, sisi si watalii. Baadhi yetu ni wenyeji wa eneo hilo; na wengi wetu walitoka katika miji ya mbali ili kuishi hapa Rurrenabaque, mji mdogo mzuri wenye miti inayochipuka maua, nyumba zilizoezekwa nyasi, na teksi za pikipiki zinazopita mara kwa mara kwenye barabara tulivu. Kwa nini tunasafiri?

Watu hufunga safari kama hizo pia katika sehemu nyingine nyingi za Bolivia. Mashahidi wa Yehova kutoka katika majiji na nchi nyingine hupeleka habari njema ya Ufalme wa Mungu kwenye miji midogo zaidi.—Mathayo 24:14.

Nchi ya Bolivia iko katikati ya Amerika Kusini. Nchi hiyo ni kubwa mara mbili zaidi ya Ufaransa, na idadi ya raia wake inazidi ile ya Ufaransa kwa asilimia 10 hivi. Wakaaji wengi wa Bolivia huishi katika majiji na miji yenye migodi iliyo kwenye milima au kwenye vituo vikuu vya kilimo kwenye mabonde. Hata hivyo, kwenye maeneo ya chini ya tropiki, miji imetenganishwa na misitu mikubwa.

Katika miaka ya 1950 na miaka ya 1960, wamishonari wajasiri, kama Betty Jackson, Elsie Meynberg, Pamela Mosely, na Charlotte Tomaschafsky, waliongoza kazi ya kuhubiri katika miji mingi ya mbali. Waliwafundisha watu wanyoofu kweli za Biblia na wakaanzisha makutaniko madogo. Katika miaka ya 1980 na miaka ya 1990, kulikuwa na ongezeko la zaidi ya mara sita katika idadi ya Mashahidi wa Yehova hasa katika majiji. Sasa kuna makutaniko katika sehemu mbalimbali za majiji. Makutaniko hayo yako katika wilaya zenye ufanisi ambako watu hufanya kazi katika majengo marefu, huishi katika nyumba kubwa, na hununua vitu kwenye maduka makubwa. Lakini kuna makutaniko pia katika maeneo ya mbali ambako watu huishi katika nyumba za matope, hununua vitu katika masoko, na kuvaa nguo zenye rangi nyingi. Hata hivyo, ni nini kinachohitajiwa ili kuwasaidia watu wengi zaidi katika maeneo ya mbali kumjua Yehova?

Kujinyima Maisha ya Jijini

Kwa muda wa miaka 20 iliyopita, watu wengi wamehama kutoka miji ya migodi ya Bolivia na mashambani na kwenda majijini. Si kawaida watu kuhama kutoka jijini kwenda kijijini. Vijiji vingi vina simu moja tu na vina umeme kwa saa chache tu kila siku. Huenda Mashahidi wanaoishi katika miji hiyo midogo wakaonana na waamini wenzao wakati wa makusanyiko ya kila mwaka tu, na wakati mwingine safari za kwenda kwenye makusanyiko hayo zinakuwa ghali, hatari, na zenye kuchosha. Shule za vijijini huandaa tu elimu ya msingi. Ni nini basi kinachowachochea Mashahidi wa Yehova wengi kutoka katika majiji na kuhamia vijijini?

Hivi karibuni, Luis alisema hivi: “Nilikuwa na nafasi ya kufuatia kazi katika jiji la La Paz. Lakini sikuzote wazazi wangu walisema kwamba kufanya wanafunzi ndiyo kazi bora zaidi. Hivyo, nilisomea mambo ya ujenzi kwa muda mfupi. Wakati wa likizo huko Rurrenabaque, nilitambua kwamba watu walisikiliza kwa hamu habari njema. Nilipoona idadi ndogo ya akina ndugu, niliona kwamba ninapaswa kwenda huko kuwasaidia. Sasa ninaongoza mafunzo 12 ya Biblia. Kwa mfano, ninajifunza na mwanamume mmoja na mke wake ambao wana watoto wanne. Mwanamume huyo alikuwa akinywa pombe kupindukia na kucheza kamari, lakini ameacha mambo yote hayo na ameanza kuwaeleza marafiki wake yale anayojifunza kumhusu Yehova. Sikuzote yeye hutayarisha kwa ajili ya funzo. Kwa sababu hapendi kukosa utendaji wa Kikristo, yeye huhuzunika sana anapoenda kukata miti msituni kwa muda wa siku tatu au nne. Ninapowaona wote kwenye mikutano ya Kikristo, ninahisi kwamba nilifanya jambo zuri kwa kujidhabihu ili kuja hapa.”

Juana ni mzazi asiye na mwenzi. Anasema hivi: “Nilikuwa nikifanya kazi ya nyumba huko La Paz. Mwanangu alipokuwa mchanga, nilianza utumishi wa wakati wote huko jijini. Nilipotembelea eneo la Rurrenabaque, nilitambua kwamba ningetimiza mengi kwa kuhamia hapa. Kwa hiyo, tukaja, nami nikapata kazi ya nyumba. Mwanzoni, ilikuwa vigumu kuvumilia kwa sababu ya joto na wadudu. Lakini tumekuwa hapa kwa miaka saba sasa. Ninaongoza mafunzo mengi ya Biblia kila juma, na wanafunzi wengi wanaonyesha uthamini kwa kuhudhuria mikutano.” Juana na mwana wake ni miongoni mwa wale wanaosafiri mtoni kwa mashua ndogo. Unakaribishwa kwenda pamoja nao.

Kusafiri Mtoni

Injini ya mashua ndogo inanguruma huku tunapoelekea kwenye njia nyembamba katikati ya milima. Kasuku wanapiga kelele wanapotuona. Maji yenye matope kutoka milimani yanazunguka mashua yetu huku mwendeshaji wa mashua akiiongoza kwa ustadi katikati ya mawimbi. Kufikia saa sita tunafika kwenye kijiji fulani. Tunakutana na mwangalizi wa Kutaniko la Rurrenabaque, naye anatuonyesha eneo tutakalohubiri.

Tunakaribishwa kwa shauku na wenyeji wa kijiji, iwe ni chini ya kivuli cha mti au ndani ya nyumba iliyojengwa kwa mianzi na kuezekwa makuti. Punde si punde, tunakutana na mume na mke ambao wanasaga miwa ndani ya shinikizo la kienyeji la mbao. Maji ya miwa yanaingia kwenye bakuli la shaba. Baadaye, watachemsha maji hayo ya miwa hadi yawe asali nyeusi ya miwa ambayo inauzwa mjini. Wanatualika ndani ya nyumba yao, na wanatuuliza maswali mengi kuhusu Biblia.

Tunaendelea kupanda mto, huku tukihubiri kijiji kwa kijiji. Wengi wanafurahia kusikiliza yale ambayo Biblia inasema kuhusu mwisho wa magonjwa na kifo. (Isaya 25:8; 33:24) Inasikitisha kwamba kwa sababu ya ukosefu wa huduma nyingi za tiba katika eneo hilo, watoto wa familia nyingi wamekufa. Maisha ni magumu na yenye mahangaiko kwa wakulima na wavuvi hao wanaojitahidi kuishi kutokana na mazao yao. Hivyo, wengi wanapendezwa sana na ahadi ya Mungu kwenye Zaburi ya 72 kuhusu serikali ambayo itakomesha umaskini. Hata hivyo, je, unafikiri kwamba watu wenye kupendezwa wanaoishi katika sehemu hizo za mbali watajitahidi kuhudhuria mikutano ya Kikristo? Swali hilo liliwasumbua Eric na Vicky, ambao ni wahudumu wa wakati wote huko Santa Rosa, ambalo liko mbali zaidi katika bonde la Amazoni. Inachukua muda wa saa tatu kusafiri kwa gari hadi huko.

Je, Watu Wanaopendezwa Walikuja?

Eric na Vicky walikuja Bolivia kutoka California, Marekani, miaka 12 iliyopita. Mwangalizi mmoja anayesafiri alipendekeza kwamba wahamie Santa Rosa. Vicky anasema hivi: “Kuna simu mbili tu mjini na hakuna kituo cha mawasiliano ya Intaneti. Kuna wanyama-pori wengi. Tunapoenda kwa pikipiki kwenye maeneo ya mbali, mara nyingi tunaona mamba, mbuni, na nyoka wakubwa. Hata hivyo, jambo linalopendeza zaidi kuliko wanyama ni watu. Tunajifunza Biblia na familia ya Vaca, yaani, mume na mke na watoto wadogo wanne. Wanaishi umbali wa kilometa 26 nje ya mji. Zamani mwanamume huyo alikuwa mlevi, lakini sasa amebadilika. Kila juma, analeta familia yake yote na dada yake mdogo kwenye Jumba la Ufalme. Anambeba mke wake na mtoto kwenye baiskeli yake kubwa. Mtoto wake mwenye umri wa miaka tisa humbeba dada yake mdogo kwenye baiskeli nyingine, halafu yule wa miaka minane huendesha baiskeli yake. Safari hiyo huwachukua saa tatu.” Familia hiyo inampenda sana Yehova na inajitahidi sana kushirikiana na kutaniko.

Kwa muda wa miezi 18 tu, watu 3 wamebatizwa, na wengine 25 hivi huja kwenye Jumba jipya la Ufalme huko Santa Rosa. Ingawa watu wengi wanataka kujifunza Biblia, wengi wanahitaji kushinda vizuizi vikubwa ili wamtumikie Yehova.

Matatizo ya Kuhalalisha Ndoa

Marina na Osni ambao ni wamishonari wanaotumika katika mji mmoja wa mbali wa Bolivia ulio karibu na mpaka wa Brazili, wanaeleza kwamba watu wengi huko hawaoni ndoa kuwa kifungo cha kudumu. Wana wenzi wengi. Osni anasema hivi: “Hilo ndilo tatizo linalozuia maendeleo ya kiroho. Watu wanapotaka kuwa Wakristo wa kweli, wao hukabili tatizo gumu linalogharimu pesa nyingi. Inawabidi baadhi yao wavunje uhusiano wao na wenzi wa zamani na kuhalalisha ndoa. Hata hivyo, wanapotambua kwamba kuhalalisha ndoa ni takwa la Kimaandiko, baadhi yao hufanya kazi kwa bidii ili wapate pesa zinazohitajiwa ili kulipia gharama za kuhalalisha ndoa.”—Waroma 13:1, 2; Waebrania 13:4.

Marina anaeleza kisa cha Norberto. “Aliishi na wanawake wengi kabla ya kuanza kuishi na mwanamke mmoja ambaye alikuwa mwokaji wa mikate. Norberto alikuwa amemzidi kwa miaka 35 naye alikuwa na mvulana ambaye Norberto alikubali kumlea. Mvulana huyo alipoendelea kukua, Norberto alitaka kumwekea kielelezo kizuri. Hivyo, Shahidi mmoja alipotembelea mahali hapo pa kuokea mikate na kupendekeza funzo la Biblia la nyumbani bila malipo, Norberto alikubali, hata ingawa hangeweza kusoma na alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 70. Norberto na mwenzi wake walipojifunza kuhusu matakwa ya Yehova, walihalalisha ndoa yao na baadaye wakabatizwa. Yule mvulana amekuwa kijana Mkristo anayechukua mambo kwa uzito, kama tu vile baba yake wa kambo alivyotamani. Norberto alijifunza kusoma, na hata ametoa hotuba kwenye mikutano ya kutaniko. Licha ya kuwa dhaifu kwa sababu ya umri wake, yeye ni mhudumu mwenye bidii wa habari njema.”

Waimarishwa na Roho ya Yehova

Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake wa mapema: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Inatia moyo kama nini kuona roho ya Mungu ikiwachochea wanaume na wanawake Wakristo kuhamia sehemu za mbali! Kwa mfano, mwaka wa 2004, Wakristo 30 hivi wenye bidii huko Bolivia walikubali kwenda kwa muda katika migawo ya mbali wakiwa wahudumu mapainia wa pekee. Wanafurahia kielelezo cha wageni 180 hivi ambao wamehamia Bolivia ili kutumika wakiwa mapainia, waangalizi wa mzunguko, Wanabetheli, au wamishonari. Wahubiri wa Ufalme 17,000 huko Bolivia wanaongoza mafunzo ya Biblia 22,000 hivi katika nyumba za watu wanaopendezwa.

Kutambua kwamba wanaongozwa kwa roho ya Yehova huwaletea ndugu hao shangwe kubwa sana. Kwa mfano, Robert na Kathy walikubali mgawo wa kwenda Camiri kutumika wakiwa wamishonari. Mji wa Camiri uko karibu na mto katikati ya vilima vyenye mimea na uko mbali kutoka kwenye miji mingine. Robert anasema hivi: “Yaelekea tulikuja kwa wakati unaofaa. Kwa miaka miwili, watu 40 hivi wamekuwa wahubiri wa habari njema.”

Mtu Aliyekuwa Mlevi na Mchezaji Kamari Asikiliza

Watu wengi mjini wanashangazwa na mabadiliko ambayo yanafanywa na wale wanaojifunza Biblia. Kwa mfano, miaka minne hivi iliyopita, mwanamume mmoja mlevi aliyeitwa Ariel alikuwa amechoka kitandani baada ya kulewa sana. Ingawa kucheza kamari kulimfanya awe mashuhuri, aliteseka sana kiakili kwa sababu ya madeni yake yaliyoongezeka, matatizo ya ndoa, na kutopata wakati wa kuwatunza binti zake. Mawazo yake yalikatizwa na Shahidi mmoja wa Yehova aliyekuwa akihubiri nyumba kwa nyumba. Ariel alisikiliza kwa makini ndugu huyo alipokuwa akieleza Maandiko. Baadaye, akiwa kitandani, Ariel alisoma kuhusu maisha ya familia yenye furaha, Paradiso, na kumtumikia Mungu. Mwishowe, alikubali kujifunza Biblia.

Kufikia wakati ambapo wamishonari walifika huko Camiri, mke wa Ariel, Arminda, alikuwa pia akijifunza, lakini hakupendezwa sana. Arminda alisema hivi: “Nitajaribu kila niwezalo ili kumzuia asinywe pombe. Lakini sijui ikiwa nitafaulu. Hawezi kubadilika.” Hata hivyo, Arminda alifurahia funzo la Biblia kuliko alivyofikiri. Katika muda wa mwaka mmoja tu, Arminda alikuwa amebatizwa na alikuwa akiwahubiria watu wa familia. Punde si punde, watu wengi wa jamaa yake walijiweka wakfu kwa Yehova.

Kwa upande wa Ariel, haikuwa rahisi kwake kuacha kunywa pombe, kuvuta tumbaku, na kucheza kamari. Ariel alibadili kabisa mtazamo wake alipowaalika marafiki wake kwenye Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Alifanya uamuzi huu: “Wale ambao hawatakuja, nitaacha kabisa kushirikiana nao. Nitajifunza Biblia na wale watakaokuja.” Alianzisha mafunzo matatu ya Biblia kwa njia hiyo. Hata kabla ya kuwa mshiriki wa kutaniko, Ariel alijifunza Biblia pamoja na mtu mmoja wa jamaa yake ambaye alifanya maendeleo na kubatizwa siku ileile Ariel alipobatizwa. Arminda anasema: “Ariel amebadilika kabisa.”

Robert anasema: “Tulipohesabu mara ya mwisho, watu 24 wa familia hiyo walikuwa wakihudhuria mikutano kwa ukawaida. Kumi wamebatizwa, na wengine wanane ni wahubiri ambao hawajabatizwa. Watu walioshuhudia mabadiliko katika mwenendo wao walianza pia kujifunza Biblia na wanahudhuria mikutano ya kutaniko. Hudhurio limeongezeka kutoka 100 hadi 190. Mimi na Kathy tunaongoza mafunzo ya Biblia 30 hivi, na wote wanahudhuria mikutano. Tunafurahi sana kuwa hapa.”

Mambo yanayotukia katika miji ya mbali huko Bolivia ni sehemu ndogo tu ya mavuno ya ulimwenguni pote yaliyotabiriwa katika Ufunuo sura ya 7, ambayo inazungumza kuhusu kukusanywa katika “siku ya Bwana” kwa wale watakaookoka dhiki kuu. (Ufunuo 1:10; 7:9-14) Haijatukia kamwe katika historia ya wanadamu kuona mamilioni ya watu kutoka mataifa yote wakiungana katika ibada ya Mungu wa pekee wa kweli. Ni uthibitisho wenye kuchochea kama nini kwamba utimizo wa ahadi za Mungu unakaribia!

[Picha katika ukurasa wa 9]

Betty Jackson

[Picha katika ukurasa wa 9]

Elsie Meynberg

[Picha katika ukurasa wa 9]

Pamela Moseley

[Picha katika ukurasa wa 9]

Charlotte Tomaschafsky, kulia kabisa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kila juma familia ya Vaca husafiri saa tatu kwa baiskeli hadi kwenye Jumba la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 10]

Eric na Vicky walikuja kutumika katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wanavijiji karibu na Mto Beni wanasikiliza kwa makini habari njema

[Picha katika ukurasa wa 12]

Robert na Kathy ni wamishonari huko Camiri