Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunahitaji Masihi?

Je, Tunahitaji Masihi?

Je, Tunahitaji Masihi?

HUENDA ukajiuliza hivi: “Je, tunahitaji Masihi?” Naam, ni jambo linalopatana na akili kujiuliza ikiwa Masihi anaweza kuwa na uvutano wowote juu yako.

Watu fulani ambao huenda unaheshimu maoni yao wanaweza kukuhakikishia kwamba jibu la swali hilo ni wazi. Bila shaka, unahitaji Masihi kama vile kila mtu anavyomhitaji. Mtaalamu mmoja wa sheria ya Kiyahudi katika karne ya kwanza aliandika hivi kuhusu Masihi: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake.” Hivyo, alikazia jukumu muhimu ambalo Masihi anatimiza katika kusudi la Muumba wetu la kuyabariki mataifa yote ya dunia. (2 Wakorintho 1:20) Jukumu la Masihi ni muhimu sana hivi kwamba kuja kwake na maisha yake yanakaziwa sana katika unabii wa Biblia. Katika kitabu kimoja kilichotumiwa na mamilioni ya watu kwa zaidi ya miaka 70 iliyopita, Henry H. Halley alisisitiza hivi: “Agano la Kale liliandikwa ili kufanya watu watarajie na kutayarisha njia kwa ajili ya Kuja kwa [Masihi].” Lakini je, kuja kwake ni muhimu? Kwa nini unapaswa kuhangaikia jambo hilo?

Neno “Masihi” humaanisha hasa “Mtiwa-Mafuta” nalo linalingana na neno linalojulikana sana, yaani, “Kristo.” Kichapo fulani (Encyclopædia Britannica, chapa ya 1970), kinataja kwamba Kristo ambaye ni “mkombozi mkuu zaidi,” alipaswa kuja kwa sababu ya kutotii kwa wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa. Wanadamu hao waliumbwa wakiwa wakamilifu, nao walikuwa na matarajio mazuri ya kuishi milele katika Paradiso, lakini wakayapoteza. Malaika mwasi ambaye alijulikana baadaye kuwa Shetani Ibilisi, alidokeza kwamba Muumba wao aliwawekea vizuizi vingi na kwamba wangekuwa katika hali nzuri zaidi ikiwa wangejiamulia wenyewe yaliyo mema na yaliyo mabaya.—Mwanzo 3:1-5.

Hawa alidanganywa, naye akaamini uwongo huo. Yaelekea Adamu alipendelea zaidi uhusiano wake pamoja na mke wake kuliko ushikamanifu wake kwa Mungu, hivyo akajiunga na Ibilisi katika uasi huo. (Mwanzo 3:6; 1 Timotheo 2:14) Kwa matendo yao, walifanya mengi zaidi ya kutupilia mbali matarajio yao ya kuishi milele katika mazingira ya kiparadiso. Waliwapitishia watoto wao ambao hawakuwa wamezaliwa dhambi na matokeo yake, yaani, kifo.—Waroma 5:12.

Muumba wetu Yehova aliamua mara moja njia ya kuondoa madhara yaliyosababishwa na uasi huo. Angejipatanisha tena na wanadamu kupitia ile kanuni ya kisheria ya uhai kwa uhai iliyotajwa baadaye katika Sheria ya Musa. (Kumbukumbu la Torati 19:21; 1 Yohana 3:8) Kanuni hiyo ya kisheria ilipaswa kutekelezwa ili wazao wa Adamu na Hawa waishi milele katika dunia paradiso kama Muumba alivyokuwa amekusudia kwa ajili ya wanadamu. Kusudi hilo hutuelekeza kwa Masihi.

Alipokuwa akimhukumu Ibilisi, Yehova Mungu alisema hivi katika unabii wa kwanza wa Biblia: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwanzo 3:15) Msomi mmoja wa Biblia alisema kwamba “katika Maandiko, habari kuhusu ahadi za kimasihi zinaanza kwa maneno [hayo].” Msomi mwingine alisema kwamba Masihi alitumiwa na Mungu “kuondoa matatizo yote yaliyosababishwa na dhambi,” na wakati huohuo kuwaletea wanadamu baraka.—Waebrania 2:14, 15.

Hata hivyo, huenda unajua vizuri kwamba hadi sasa wanadamu hawajabarikiwa. Badala yake, jamii ya wanadamu imekata tamaa kabisa. Kwa hiyo, kichapo kimoja (The World Book Encyclopedia) kinasema kwamba “Wayahudi wengi wangali wanatarajia Masihi aje” na kwamba “atarekebisha mambo na kuwashinda maadui wa watu.” Hata hivyo, Biblia inasema kwamba tayari Masihi amekuja. Je, kuna sababu yoyote ya kuamini yale ambayo Biblia inasema? Makala inayofuata itajibu swali hilo.