Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukusanya Vitu Vilivyo Mbinguni na Vitu Vilivyo Duniani

Kukusanya Vitu Vilivyo Mbinguni na Vitu Vilivyo Duniani

Kukusanya Vitu Vilivyo Mbinguni na Vitu Vilivyo Duniani

“Ni kulingana na upendezi wake mwema . . . kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.”—WAEFESO 1:9, 10.

1. Yehova ana ‘upendezi gani mwema’ kwa ajili ya mbingu na dunia?

AMANI KILA MAHALI! Hilo ndilo kusudi tukufu la Yehova, “Mungu wa amani.” (Waebrania 13:20) Alimwongoza mtume Paulo kuandika kwamba “upendezi [Wake] mwema” ni “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:9, 10) Ni nini kinachomaanishwa na kitenzi kinachotafsiriwa kuwa “kukusanya tena pamoja” katika mstari huo? Msomi wa Biblia J. B. Lightfoot anasema hivi: “Maneno hayo yanarejelea upatano wote wa ulimwengu, ambao hautakuwa tena na vitu vigeni vinavyosababisha mgawanyiko, lakini sehemu zake zote zitaunganishwa pamoja katika Kristo. Hakutakuwapo tena na dhambi, kifo, huzuni, kutofanikiwa, na mateso.”

“Vitu Vilivyo Mbinguni”

2. “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo vinahitaji kukusanywa ni akina nani?

2 Mtume Petro alieleza vizuri tumaini bora la Wakristo wa kweli alipoandika hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) “Mbingu mpya” zinazoahidiwa hapa zinamaanisha serikali mpya, yaani, Ufalme wa Kimasihi. “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo Paulo alitaja katika barua yake kwa Waefeso vitakusanywa “katika Kristo.” Vitu hivyo ni wale wanadamu wachache ambao wamechaguliwa kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (1 Petro 1:3, 4) Wakristo hao 144,000 waliotiwa mafuta “wamenunuliwa kutoka duniani,” ‘wamenunuliwa kutoka kati ya wanadamu,’ wawe warithi-washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni.—Ufunuo 5:9, 10; 14:3, 4; 2 Wakorintho 1:21; Waefeso 1:11; 3:6.

3. Ni kwa njia gani watiwa-mafuta ‘wameketishwa katika mahali pa kimbingu’ hata wakiwa bado duniani?

3 Wakristo watiwa-mafuta wanazaliwa tena kwa roho takatifu ili wawe wana wa roho wa Yehova. (Yohana 1:12, 13; 3:5-7) Kwa kuwa Yehova amewafanya kuwa “wana,” wao ni ndugu za Yesu. (Waroma 8:15; Waefeso 1:5) Hivyo, hata wakiwa bado duniani, wanasemwa kuwa ‘wameinuliwa na kuketishwa pamoja katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo Yesu.’ (Waefeso 1:3; 2:6) Wana cheo hicho cha juu cha kiroho kwa sababu ‘wametiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa, ambayo ni rehani ya kimbele ya urithi wao’ ambao wamewekewa akiba mbinguni. (Waefeso 1:13, 14; Wakolosai 1:5) Basi, wao ndio “vitu vilivyo mbinguni,” ambao idadi yao kamili iliyoagizwa kimbele na Yehova ilihitaji kukusanywa.

Kukusanywa Kunaanza

4. Kukusanywa kwa “vitu vilivyo mbinguni” kulianza wakati gani na jinsi gani?

4 Kupatana na “usimamizi” wa Yehova, au njia yake ya kusimamia mambo, kukusanywa kwa “vitu vilivyo mbinguni” kulipaswa kuanze “kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi.” (Waefeso 1:10) Wakati huo ulifika siku ya Pentekoste 33 W.K. Siku hiyo, roho takatifu ilimiminwa juu ya mitume na kikundi cha wanafunzi cha wanaume na wanawake. (Matendo 1:13-15; 2:1-4) Hilo lilithibitisha kwamba agano jipya lilikuwa limeanza, na huo ulikuwa mwanzo wa kutaniko la Kikristo na taifa jipya la Israeli wa kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16; Waebrania 9:15; 12:23, 24.

5. Kwa nini Yehova aliumba “taifa” jipya lichukue mahali pa taifa la Israeli la asili?

5 Agano la Sheria lililofanywa pamoja na taifa la Israeli la asili halikutokeza “ufalme wa makuhani na taifa takatifu” ambalo lingetumika milele mbinguni. (Kutoka 19:5, 6) Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini Wayahudi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mathayo 21:43) Taifa hilo, Israeli wa kiroho, limefanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta walio katika agano jipya. Mtume Petro aliwaandikia hivi Wakristo hao: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu. Kwa kuwa wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu.” (1 Petro 2:9, 10) Waisraeli wa asili hawakuwa tena watu wa Yehova wa agano. (Waebrania 8:7-13) Kama Yesu alivyotabiri, walinyang’anywa pendeleo la kuwa sehemu ya Ufalme wa Kimasihi, na badala yao, washirika 144,000 wa Israeli wa kiroho wakapewa pendeleo hilo.—Ufunuo 7:4-8.

Kuingizwa Katika Agano la Ufalme

6, 7. Ni agano gani la pekee ambalo Yesu alifanya pamoja na ndugu zake waliozaliwa kwa roho, nalo linamaanisha nini kwao?

6 Usiku ambao Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.” (Luka 22:28-30) Katika andiko hilo, Yesu alizungumzia agano la pekee ambalo alifanya pamoja na ndugu zake 144,000 waliozaliwa kwa roho, ambao wangebaki ‘waaminifu hata kufikia kifo’ na kujithibitisha kuwa ‘washindi.’—Ufunuo 2:10; 3:21.

7 Wale wa kikundi hicho kidogo huacha kuwa na matumaini yoyote ya kuishi milele duniani wakiwa wanadamu wenye mwili wa nyama na damu. Watatawala pamoja na Kristo mbinguni huku wakiwa wameketi juu ya viti vya ufalme ili kuwahukumu wanadamu. (Ufunuo 20:4, 6) Acheni sasa tuchunguze maandiko mengine ambayo yanawahusu tu hao watiwa-mafuta na ambayo yanaonyesha kwa nini wale wa “kondoo wengine” hawashiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho.—Yohana 10:16.

8. Watiwa-mafuta huonyesha nini kwa kushiriki kula mkate? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 23.)

8 Watiwa-mafuta wanashiriki mateso ya Kristo na wako tayari kufa kama yeye. Akiwa mmoja wa watiwa-mafuta, Paulo alisema kwamba alikuwa tayari kutoa dhabihu yoyote kusudi aweze “kumpata Kristo . . . ili kumjua yeye na nguvu za ufufuo wake na kushiriki katika mateso yake.” Naam, Paulo alikuwa tayari kupatwa na “kifo kama chake.” (Wafilipi 3:8, 10) Wakristo wengi watiwa-mafuta wamevumilia katika miili yao ya kibinadamu “matendo yenye kuleta kifo ambayo Yesu alitendewa.”—2 Wakorintho 4:10.

9. Ni mwili gani unaowakilishwa na mkate wa Ukumbusho?

9 Alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, Yesu alisema hivi: “Huu unamaanisha mwili wangu.” (Marko 14:22) Alikuwa akizungumza kuhusu mwili wake halisi, ambao ulikuwa karibu kupigwa na kupata madoa ya damu. Mkate usio na chachu ulifananisha vizuri mwili huo. Kwa nini? Kwa sababu katika Biblia, chachu inaweza kufananisha dhambi au uovu. (Mathayo 16:4, 11, 12; 1 Wakorintho 5:6-8) Yesu alikuwa mkamilifu, na mwili wake wa kibinadamu haukuwa na dhambi. Angetoa mwili huo mkamilifu kuwa dhabihu ya upatanisho. (Waebrania 7:26; 1 Yohana 2:2) Kufanya hivyo kungewafaidi Wakristo wote waaminifu, iwe wanatumaini kuishi mbinguni au kupata uzima wa milele katika dunia iliyo paradiso.—Yohana 6:51.

10. Ni kwa njia gani wale wanaoshiriki kunywa divai ya Ukumbusho ‘hushiriki katika damu ya Kristo’?

10 Paulo aliandika hivi kuhusu divai ambayo Wakristo watiwa-mafuta hushiriki kunywa wakati wa Ukumbusho: “Kikombe cha baraka ambacho tunabariki, je, hicho si kushiriki katika damu ya Kristo?” (1 Wakorintho 10:16) Ni kwa njia gani wale wanaoshiriki kunywa divai ‘hushiriki katika damu ya Kristo’? Bila shaka, hawashiriki kutoa dhabihu ya fidia, kwa kuwa wao wenyewe wanahitaji ukombozi. Kupitia imani yao katika nguvu za ukombozi za damu ya Kristo, dhambi zao husamehewa, nao wanatangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima huko mbinguni. (Waroma 5:8, 9; Tito 3:4-7) Ni kupitia damu ya Kristo iliyomwagwa kwamba wale warithi-washirika wa Kristo 144,000 ‘wanatakaswa,’ wanawekwa kando, na kusafishwa kutokana na dhambi ili wawe “watakatifu.” (Waebrania 10:29; Danieli 7:18, 27; Waefeso 2:19) Naam, kupitia damu yake iliyomwagwa, Kristo ‘alimnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa, naye akawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10.

11. Watiwa-mafuta huonyesha nini kwa kunywa divai ya Ukumbusho?

11 Yesu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwapa mitume wake waaminifu kikombe cha divai na kusema: “Kinyweeni, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.” (Mathayo 26:27, 28) Kama vile damu ya ng’ombe-dume na mbuzi ilivyohalalisha agano la Sheria kati ya Mungu na taifa la Israeli, damu ya Yesu ilihalalisha agano jipya ambalo Yehova angefanya pamoja na taifa la Israeli wa kiroho, kuanzia siku ya Pentekoste 33 W.K. (Kutoka 24:5-8; Luka 22:20; Waebrania 9:14, 15) Kwa kunywa divai ambayo inafananisha ‘damu ya agano,’ watiwa-mafuta wanaonyesha kwamba wameingizwa katika agano jipya na kwamba wanapata faida zake.

12. Watiwa-mafuta hubatizwaje katika kifo cha Kristo?

12 Watiwa-mafuta wanakumbushwa jambo lingine. Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake waaminifu: “Kikombe ninachokunywa mtakunywa, na ubatizo ninaobatizwa mtabatizwa.” (Marko 10:38, 39) Baadaye, mtume Paulo alisema kwamba Wakristo ‘wamebatizwa katika kifo cha Kristo.’ (Waroma 6:3) Watiwa-mafuta hudhabihu maisha yao. Kifo chao ni cha kidhabihu kwa sababu wanatupilia mbali tumaini lolote la kupata uzima wa milele duniani. Ubatizo wa Wakristo hao watiwa-mafuta katika kifo cha Kristo unamalizika wakati ambapo, baada ya kufa wakiwa waaminifu, wanafufuliwa wakiwa viumbe wa roho ili ‘watawale wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo mbinguni.—2 Timotheo 2:10-12; Waroma 6:5; 1 Wakorintho 15:42-44, 50.

Kushiriki Kula Mkate na Kunywa Divai

13. Kwa nini wale walio na tumaini la kuishi duniani hawashiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho, lakini kwa nini wanahudhuria Ukumbusho?

13 Kwa kuwa kushiriki kula mkate na kunywa divai inayopitishwa wakati wa Ukumbusho kunahusisha mambo yote hayo, ni wazi kwamba haifai kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani kushiriki kula mkate na kunywa divai. Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanatambua kwamba wao si washiriki waliotiwa mafuta wa mwili wa Kristo, wala hawako katika agano jipya ambalo Yehova alifanya pamoja na wale watakaotawala na Yesu Kristo. Kwa kuwa “kikombe” kinawakilisha agano jipya, ni wale tu walio katika agano jipya wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho. Wale wanaotazamia kupata uzima wa milele wakiwa wanadamu wakamilifu duniani chini ya Ufalme, hawabatizwi katika kifo cha Yesu wala hawapati mwito wa kutawala pamoja naye mbinguni. Ikiwa wangekula mkate na kunywa divai hiyo, basi wangekuwa wanafanya jambo lisilofaa. Kwa hiyo, ingawa wanahudhuria Ukumbusho wakiwa watazamaji wenye heshima, hawashiriki kula mkate na kunywa divai. Wanathamini mambo yote ambayo Yehova amewafanyia kupitia Mwana wake, kutia ndani kuwasamehe kwa msingi wa damu ya Kristo iliyomwagwa.

14. Watiwa-mafuta wanaimarishwaje kiroho kwa kushiriki kula mkate na kunywa divai?

14 Kutiwa muhuri kwa mwisho kwa idadi ndogo ya Wakristo walio na mwito wa kutawala pamoja na Kristo mbinguni kunakaribia kumalizika. Hadi mwisho wa maisha yao hapa duniani ambayo wanayadhabihu, watiwa-mafuta huimarishwa kiroho wanaposhiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho. Wanahisi wameunganishwa pamoja na ndugu na dada zao waliotiwa mafuta, wakiwa washiriki wa mwili wa Kristo. Kushiriki kula mkate na kunywa divai huwakumbusha kwamba wana wajibu wa kuwa waaminifu hadi kifo.—2 Petro 1:10, 11.

Kukusanya “Vitu Vilivyo Duniani”

15. Ni nani ambao wamekusanywa upande wa Wakristo watiwa-mafuta?

15 Tangu katikati ya miaka ya 1930, idadi inayoongezeka ya “kondoo wengine,” ambao si sehemu ya “kundi dogo” na ambao wana tumaini la kupata uzima wa milele duniani, wamewaunga mkono watiwa-mafuta. (Yohana 10:16; Luka 12:32; Zekaria 8:23) Wamekuwa waandamani washikamanifu wa ndugu za Kristo, wakiwasaidia sana kuhubiri “habari njema ya ufalme” ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote. (Mathayo 24:14; 25:40) Hivyo, wana nafasi nzuri ya kuhukumiwa na Kristo kuwa “kondoo” zake na kuwekwa kwenye “mkono wake wa kuume” wa kibali wakati atakapokuja kuyahukumu mataifa. (Mathayo 25:33-36, 46) Kupitia imani yao katika damu ya Kristo, watafanyiza “umati mkubwa” ambao utaokoka “dhiki kuu.”—Ufunuo 7:9-14.

16. “Vitu vilivyo duniani” vitatia ndani akina nani, na ni kwa njia gani wote hao watakuwa na nafasi ya kuwa “watoto wa Mungu”?

16 Kutiwa muhuri kwa mwisho kwa mabaki ya wale 144,000 kutakapomalizika, zile “pepo” za uharibifu zitaachiliwa juu ya mfumo mbovu wa mambo wa Shetani duniani. (Ufunuo 7:1-4) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo pamoja na wafalme na makuhani wenzake, umati mkubwa utaunganishwa na idadi kubwa sana ya watu watakaofufuliwa. (Ufunuo 20:12, 13) Watakuwa na nafasi ya kuwa raia wa kidunia wa Mfalme wa Kimasihi, Kristo Yesu, milele. Mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu, ‘vitu vyote hivyo vilivyo duniani’ vitakabili jaribu la mwisho. Wale watakaokuwa waaminifu watafanywa kuwa “watoto wa Mungu” duniani.—Waefeso 1:10; Waroma 8:21; Ufunuo 20:7, 8.

17. Kusudi la Yehova litatimiaje?

17 Hivyo, kupitia “usimamizi” wake wenye hekima isiyo na kifani au njia yake ya kusimamia mambo, Yehova atakuwa ametimiza kusudi lake la “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” Viumbe wote wenye akili mbinguni na duniani watakuwa wamekusanywa pamoja wakifurahia amani kila mahali, nao watajitiisha kwa shangwe chini ya utawala wenye uadilifu wa yule Mkusudiaji Mkuu, Yehova.

18. Watiwa-mafuta na waandamani wao watafaidikaje kwa kuhudhuria Ukumbusho?

18 Imani ya wale watiwa-mafuta wachache na ya mamilioni ya waandamani wao wa kondoo wengine itaimarishwa sana watakapokutanika Aprili 12, 2006! Wataadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo kupatana na amri hii ya Yesu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Wote wanaohudhuria wanapaswa kukumbuka yale ambayo Yehova amewafanyia kupitia Mwana wake mpendwa, Kristo Yesu.

Kwa Kupitia

• Kusudi la Yehova ni nini kwa ajili ya vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani?

• “Vitu vilivyo mbinguni” ni akina nani, nao wamekusanywaje?

• “Vitu vilivyo duniani” ni akina nani, nao wana tumaini gani?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

“Mwili wa Kristo”

Kwenye 1 Wakorintho 10:16, 17, Paulo alitumia neno “mwili” kwa njia ya pekee alipokuwa akizungumzia maana hususa ya mkate kwa ndugu za Kristo waliotiwa mafuta kwa roho. Alisema hivi: “Ule mkate ambao tunamega, je, huo si kushiriki katika mwili wa Kristo? Kwa sababu kuna mkate mmoja, sisi, ingawa tuko wengi, ni mwili mmoja, kwa maana sisi sote tunakula huo mkate mmoja.” Wakristo watiwa-mafuta wanaposhiriki kula mkate wa Ukumbusho, wanatangaza umoja wao katika kutaniko la watiwa-mafuta ambalo ni kama mwili, huku Kristo akiwa ndiye Kichwa.—Mathayo 23:10; 1 Wakorintho 12:12, 13, 18.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa nini watiwa-mafuta tu ndio wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kupitia usimamizi wa Yehova, viumbe wote mbinguni na duniani wataunganishwa