Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutembea Katika Njia ya Nuru Inayoongezeka

Kutembea Katika Njia ya Nuru Inayoongezeka

Kutembea Katika Njia ya Nuru Inayoongezeka

“Njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.”—METHALI 4:18.

1, 2. Watu wa Mungu wamefaidikaje kutokana na nuru ya kiroho inayoongezeka kutoka kwa Yehova?

NI NANI awezaye kueleza vizuri zaidi jinsi ambavyo jua linalochomoza huondolea mbali giza la usiku isipokuwa Yehova Mungu, Chanzo cha nuru? (Zaburi 36:9) Mungu anasema hivi: ‘Asubuhi inaposhika miisho ya dunia, dunia hujigeuza kama udongo chini ya muhuri, na vitu husimama mahali pake kama katika mavazi.’ (Ayubu 38:12-14) Nuru ya jua inapoongezeka, umbo la dunia huonekana wazi zaidi kama vile umbo la udongo laini linavyobadilika linapopata alama ya muhuri.

2 Yehova pia ndiye Chanzo cha nuru ya kiroho. (Zaburi 43:3) Ulimwengu unapoendelea kuwa katika giza zito, Mungu wa kweli anaendelea kuwaangazia nuru watu wake. Matokeo? Biblia inajibu hivi: “Njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” (Methali 4:18) Nuru ya Yehova inayoongezeka huendelea kuangazia njia ya watu wake. Nuru hiyo inawaongoza kufanya mabadiliko ya kitengenezo, kimafundisho, na kiadili.

Nuru Inayoongezeka Yaleta Mabadiliko ya Kitengenezo

3. Andiko la Isaya 60:17 linatoa ahadi gani?

3 Kupitia nabii Isaya, Yehova alitabiri hivi: “Badala ya shaba nitaingiza dhahabu, na badala ya chuma nitaingiza fedha, na badala ya miti, shaba, na badala ya mawe, chuma.” (Isaya 60:17) Kuweka kitu cha hali ya chini mahali pa kitu cha hali ya juu kunaonyesha mabadiliko. Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova wamekuwa na mabadiliko katika mipango yao ya kitengenezo wakati huu wa “umalizio wa mfumo wa mambo” au “siku za mwisho.”—Mathayo 24:3; 2 Timotheo 3:1.

4. Ni mpango gani ulioanzishwa mwaka wa 1919, na ulikuwa na faida gani?

4 Mwanzoni mwa siku za mwisho, makutaniko ya Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, yaliwachagua wazee na mashemasi kwa kupiga kura. Hata hivyo, wazee fulani hawakupenda kuhubiri. Mbali na kutotaka kuhubiri, baadhi yao hata waliwavunja wengine moyo wasihubiri. Hivyo, mwaka wa 1919, mpango mwingine ulianzishwa katika kila kutaniko, yaani, mpango wa kuwa na mkurugenzi wa utumishi. Mkurugenzi wa utumishi hakuchaguliwa kwa kupigiwa kura na kutaniko, bali aliwekwa rasmi na ofisi ya tawi ya watu wa Mungu kwa mwongozo wa roho takatifu. Kazi ya mkurugenzi huyo ilitia ndani kupanga kazi ya kuhubiri, kugawa maeneo, na kuwatia moyo wengine washiriki katika kazi ya kuhubiri. Katika miaka iliyofuata, watu wengi walichochewa kuhubiri Ufalme.

5. Ni mabadiliko gani yaliyofanywa katika miaka ya 1920?

5 Katika kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia lililofanywa mwaka wa 1922 huko Cedar Point, Ohio, Marekani, wote kutanikoni walichochewa zaidi na himizo hili: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Kufikia mwaka wa 1927, kazi ya kuhubiri ilikuwa imepangwa vizuri hivi kwamba Jumapili ikaonwa kuwa siku bora ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa nini Jumapili? Kwa sababu hiyo ndiyo siku ambayo watu wengi hawakwenda kazini. Leo, Mashahidi wa Yehova huonyesha mtazamo kama huo kwa kuwahubiria watu wakati wanapopatikana nyumbani, kama vile mwishoni mwa juma au jioni.

6. Kulikuwa na azimio gani mwaka wa 1931, nalo lilikuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri Ufalme?

6 Alasiri ya Jumapili Julai 26, 1931, watu wa Mungu walichochewa sana kuhubiri Ufalme wakati azimio lilipopitishwa kwanza kwenye kusanyiko huko Columbus, Ohio, Marekani, na baadaye likapitishwa ulimwenguni pote. Kwa sehemu azimio hilo lilisema hivi: “Sisi tu watumishi wa Yehova Mungu walioagizwa kufanya kazi kwa jina lake, na kwa kutii amri yake, tutoe ushuhuda wa Yesu Kristo, na kujulisha watu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na Mweza Yote; kwa hiyo kwa furaha tunalikubali na kulichukua jina ambalo kinywa cha Bwana Mungu kimelitaja, nasi twataka tujulikane na kuitwa kwa jina hili, yaani, mashahidi wa Yehova.” (Isaya 43:10) Jina hilo linaonyesha wazi kazi kuu inayofanywa na wote wanaoitwa Mashahidi wa Yehova! Naam, Yehova alikuwa na kazi kwa ajili ya watumishi wake wote. Kwa ujumla, itikio lilikuwa lenye kupendeza kwelikweli!

7. Kulikuwa na badiliko gani mwaka wa 1932, na kwa nini?

7 Wazee wengi walijitolea kwa unyenyekevu kufanya kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, katika sehemu nyingine, wazee waliochaguliwa kwa kura walipinga wazo la kwamba kila mtu kutanikoni alipaswa kushiriki huduma ya hadharani. Lakini, mabadiliko zaidi yangetokea karibuni. Katika mwaka wa 1932, kupitia gazeti la Mnara wa Mlinzi, makutaniko yaliagizwa yaache kuwachagua wazee na mashemasi kwa kupiga kura. Badala yake, walihitaji kupiga kura ili kuchagua halmashauri ya utumishi yenye wanaume wa kiroho ambao walishiriki katika kazi ya kuhubiri hadharani. Hivyo, usimamizi ulikabidhiwa wale walioshiriki huduma kwa bidii, na kazi ikaendelea kusonga mbele.

Nuru Inayoongezeka Yaleta Mabadiliko Zaidi

8. Kulikuwa na badiliko gani mwaka wa 1938?

8 Nuru ‘ilizidi kuongezeka.’ Katika mwaka wa 1938, kupiga kura kuliondolewa kabisa. Watumishi wote wa kutaniko waliwekwa rasmi kupatana na matakwa ya Maandiko chini ya usimamizi wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Karibu makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova yalikubali badiliko hilo, na kazi ya kuhubiri ikaendelea kuwa na matokeo.

9. Ni mpango gani ulioanzishwa mwaka wa 1972, na kwa nini hiyo ilikuwa hatua muhimu?

9 Kuanzia Oktoba 1, 1972, kulikuwa na badiliko lingine kuhusiana na usimamizi kutanikoni. Badala ya kusimamiwa na mtumishi mmoja wa kutaniko au mwangalizi wa kutaniko, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote yalianza kusimamiwa na mabaraza ya wazee. Mpango huo mpya umewachochea ndugu wengi waliokomaa wafanye maendeleo ili kustahili kuwa waangalizi kutanikoni. (1 Timotheo 3:1-7) Hilo limewawezesha ndugu wengi kupata ujuzi wa kutimiza wajibu mbalimbali kutanikoni. Ndugu hao wamesaidia sana kuwachunga wapya wengi ambao wamekubali kweli ya Biblia!

10. Ni mpango gani ulioanzishwa mwaka wa 1976?

10 Washiriki wa Baraza Linaloongoza walipangwa katika halmashauri sita, na kuanzia Januari 1, 1976, utendaji wote wa tengenezo na wa makutaniko yote duniani ukawa unasimamiwa na halmashauri hizo. Ni baraka iliyoje kwamba sehemu zote za kazi ya Ufalme zinaongozwa na “wingi wa washauri”!—Methali 15:22; 24:6.

11. Ni badiliko gani lililotokea mwaka wa 1992, na kwa nini?

11 Mwaka wa 1992, kulikuwa na badiliko lingine ambalo linaweza kufananishwa na jambo lililotokea baada ya Waisraeli na wengine kurudi kutoka uhamishoni Babiloni. Wakati huo, hakukuwa na Walawi wa kutosha kufanya kazi hekaluni. Hivyo, Wanethini wasio Wayahudi walipewa madaraka zaidi ya kuwasaidia Walawi. Vivyo hivyo, ili kusaidia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara kushughulikia madaraka yake yaliyokuwa yakiongezeka katika kazi inayofanywa duniani, katika mwaka wa 1992 baadhi ya “kondoo wengine” walipata madaraka zaidi ya utumishi. Waliwekwa kuwa wasaidizi wa halmashauri za Baraza Linaloongoza.—Yohana 10:16.

12. Yehova amewekaje amani kuwa waangalizi wetu?

12 Matokeo yamekuwa nini? Yehova anasema hivi: “Nitaweka amani kuwa waangalizi wako na uadilifu kuwa wagawa-kazi wako.” (Isaya 60:17) Kuna “amani” miongoni mwa watumishi wa Yehova leo, na upendo wa “uadilifu” kumekuwa ‘mgawa-kazi’ wao, yaani, nguvu inayowachochea kumtumikia Mungu. Wamepangwa vizuri ili kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Yehova Aendelea Kuangaza Nuru Juu ya Mafundisho

13. Yehova aliwasaidiaje watu wake kuelewa vizuri zaidi mafundisho fulani katika miaka ya 1920?

13 Hatua kwa hatua Yehova anaangazia njia ya watu wake kimafundisho. Andiko la Ufunuo 12:1-9 linatoa mfano. Masimulizi hayo yanarejelea mifano mitatu: “mwanamke” aliye na mimba ambaye anajifungua, “joka,” na “mwana, mwanamume.” Je, unajua kinachowakilishwa na kila mmoja wao? Walitambulishwa katika makala yenye kichwa, “Kuzaliwa kwa Taifa,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1925. Makala hiyo iliwasaidia watu wa Mungu kuelewa vizuri unabii kuhusu kuzaliwa kwa Ufalme, na ikawasaidia kuelewa wazi kwamba kuna matengenezo mawili yaliyo tofauti kabisa, yaani, tengenezo la Yehova na tengenezo la Shetani. Kisha, mwaka wa 1927/1928, watu wa Mungu wakatambua kwamba sherehe za Krismasi na siku za kuzaliwa hazipatani na maandiko, na hivyo wakaacha kuzisherehekea.

14. Ni mafundisho gani yaliyofafanuliwa katika miaka ya 1930?

14 Katika miaka ya 1930, kulikuwa na nuru zaidi kuhusiana na mafundisho matatu. Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba kundi kubwa au “umati mkubwa” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9-17 unatofautiana na wale 144,000, watakaotawala na Kristo wakiwa wafalme na makuhani. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1-5) Hata hivyo, umati huo mkubwa haukueleweka vizuri. Kama vile nuru ya asubuhi inayoongezeka inavyofanya umbo na rangi ya vitu visivyoonekana gizani ionekane wazi zaidi, katika mwaka wa 1935, umati huo mkubwa ulitambulishwa kuwa wale watakaookoka “dhiki kuu” wakiwa na tumaini la kuishi milele duniani. Baadaye mwaka huo, jambo lingine lilifafanuliwa lililowahusu watoto wa Mashahidi wa Yehova katika nchi mbalimbali waliokuwa na umri wa kwenda shule. Uzalendo ulipokuwa ukipamba moto ulimwenguni pote, Mashahidi walitambua kwamba kusalimu bendera hakukuwa jambo dogo tu. Mwaka uliofuata, kweli nyingine ilifafanuliwa wazi. Ilifafanuliwa kwamba Kristo alikufa juu ya mti wala si msalaba.—Matendo 10:39.

15. Utakatifu wa damu ulikaziwa wakati gani na jinsi gani?

15 Kulikuwa na nuru zaidi kuhusu utakatifu wa damu baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu wakati ambapo ilikuwa kawaida kuwatibu wanajeshi waliojeruhiwa kwa kuwatia damu mishipani. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1945 liliwatia moyo “waabudu wote wa Yehova ambao wanataka kuishi milele katika ulimwengu wake mpya wenye uadilifu waheshimu utakatifu wa damu na kujipatanisha na maoni ya uadilifu ya Mungu kuhusiana na suala hilo muhimu.”

16. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa lini, na ina mambo gani mawili ya pekee?

16 Katika mwaka wa 1946, ilionekana kwamba inafaa kutokeza tafsiri mpya ya Biblia ambayo ingetegemea ujuzi wa kisasa na ambayo haingechafuliwa na mafundisho yanayotegemea mapokeo ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kazi ya kutafsiri Biblia hiyo ilianza Desemba 1947. Mnamo 1950, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kiingereza. Maandiko ya Kiebrania katika Kiingereza yalichapishwa hatua kwa hatua kuanzia mwaka wa 1953 yakiwa katika mabuku matano. Buku la mwisho lilitolewa mwaka wa 1960, miaka 12 hivi baada ya kazi ya kutafsiri kuanza. Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa mwaka wa 1961. Tafsiri hiyo inayopatikana sasa katika lugha nyingi, ina mambo kadhaa ya pekee. Inatumia jina la Mungu, yaani, Yehova. Isitoshe, tafsiri yake ya neno kwa neno ya maandishi ya awali imewezesha uelewaji wa kweli ya Neno la Mungu uongezeke.

17. Ni ufafanuzi gani zaidi uliotolewa mwaka wa 1962?

17 Katika mwaka wa 1962, ufafanuzi zaidi ulitolewa kuhusu “mamlaka zilizo kubwa” zinazotajwa kwenye Waroma 13:1 na pia kuhusu ujitiisho ambao Mkristo anapaswa kuonyesha kwa mamlaka hizo. Uchunguzi mwingi kuhusu sura ya 13 ya kitabu cha Waroma na Maandiko mengine kama vile Tito 3:1, 2, na 1 Petro 2:13, 17, ulionyesha wazi kwamba usemi “mamlaka zilizo kubwa” haumrejelei Yehova Mungu wala Yesu Kristo bali unarejelea mamlaka za serikali za wanadamu.

18. Ni baadhi ya kweli gani zilizofafanuliwa katika miaka ya 1980?

18 Miaka iliyofuata, njia ya waadilifu ilizidi kung’aa. Mnamo 1985 ufafanuzi ulitolewa kuhusu maana ya kutangazwa kuwa mwadilifu “kwa ajili ya uzima” na kutangazwa kuwa mwadilifu ili kuwa rafiki ya Mungu. (Waroma 5:18; Yakobo 2:23) Maana ya Yubile ya Kikristo ilielezwa kindani mwaka wa 1987.

19. Yehova amewaangaziaje watu wake nuru zaidi ya kiroho katika miaka ya karibuni?

19 Mwaka wa 1995 kutenganishwa kwa “kondoo” na “mbuzi” kulifafanuliwa wazi zaidi. Ufafanuzi wa maono ya Ezekieli kuhusu hekalu ulitolewa mwaka wa 1998 na unabii huo unaendelea kutimizwa leo. Mnamo 1999, kukawa na ufafanuzi zaidi kuhusu ni wakati gani na jinsi gani ‘lile chukizo lingesimama katika mahali patakatifu.’ (Mathayo 24:15, 16; 25:32) Mwaka wa 2002 kukawa na uelewaji zaidi kuhusu maana ya kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.”—Yohana 4:24.

20. Watu wa Mungu wamekuwa na mabadiliko katika mambo gani mengine?

20 Mbali na mabadiliko ya kitengenezo na ya kimafundisho, kumekuwa na mabadiliko kuhusu mwenendo wa Kikristo. Kwa mfano, katika mwaka wa 1973 ilieleweka kwamba kutumia tumbaku ni “unajisi wa mwili” na jambo hilo lilipaswa kuonwa kuwa kosa zito. (2 Wakorintho 7:1) Miaka kumi baadaye, toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 1983, lilieleza vizuri zaidi msimamo wetu kuhusu matumizi ya bunduki. Hiyo ni baadhi tu ya mifano inayoonyesha jinsi ambavyo nuru imeongezeka katika wakati wetu.

Endelea Kutembea Katika Njia ya Nuru Inayoongezeka

21. Ni mtazamo gani utakaotusaidia kuendelea kutembea katika njia ya nuru inayoongezeka?

21 Mzee mmoja ambaye ametumikia kwa miaka mingi anasema: “Si rahisi kukubali badiliko na kulitumia linapotolewa.” Ni nini ambacho kimemsaidia kukubali mabadiliko mengi ambayo ameona kwa muda wa miaka 48 ambayo amekuwa mhubiri wa Ufalme? Anajibu hivi: “Siri ni kuwa na mtazamo mzuri. Kukataa mabadiliko kunamaanisha kuachwa nyuma tengenezo linaposonga mbele. Ninapohisi kwamba ni vigumu kukubali mabadiliko, ninakumbuka jinsi Petro alivyomwambia Yesu: ‘Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.’ Kisha ninajiuliza, ‘Nitaenda wapi—je, nitaenda nje kwenye giza la ulimwengu?’ Hilo hunisaidia kushikamana kabisa na tengenezo la Mungu.”—Yohana 6:68.

22. Tunafaidikaje kwa kutembea katika nuru?

22 Bila shaka, ulimwengu unaotuzunguka uko gizani. Yehova anapoendelea kuangazia watu wake nuru, tofauti iliyopo kati yao na watu wa ulimwengu inaendelea kuongezeka. Tunafaidikaje na nuru hiyo? Kama vile taa inayomulika shimo lililo kwenye barabara yenye giza isivyoweza kuondoa shimo hilo, ndivyo nuru iliyo katika Neno la Mungu isivyoweza kuondoa vishawishi. Hata hivyo, nuru ya Neno la Mungu hutusaidia kuepuka vishawishi ili tuendelee kutembea katika njia ya nuru inayoongezeka. Basi, acheni tuendelee kukazia uangalifu neno la Yehova la kinabii “kama vile taa inayoangaza mahali penye giza.”—2 Petro 1:19.

Je, Unakumbuka?

• Yehova amewaletea watu wake mabadiliko gani ya kitengenezo?

• Nuru inayoongezeka imeleta mabadiliko gani ya kimafundisho?

• Wewe mwenyewe umejionea mabadiliko gani, na ni nini ambacho kimekusaidia kuyakubali?

• Kwa nini unataka kuendelea kutembea katika njia ya nuru inayoongezeka?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kusanyiko la 1922 huko Cedar Point, Ohio, liliwachochea Wanafunzi wa Biblia kufanya kazi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 29]

“Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo” yatolewa mnamo 1950 na N. H. Knorr

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

© 2003 BiblePlaces.com