Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika Mathayo 5:22 Yesu alitoa onyo kuhusu mambo gani matatu?

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Ninawaambia ninyi kwamba kila mtu anayeendelea kuwa na ghadhabu na ndugu yake atatoa hesabu mahakamani; lakini yeyote yule anayemwambia ndugu yake neno la dharau lisilosemeka atatoa hesabu katika Mahakama Kuu Zaidi; na yeyote yule anayesema, ‘Wewe mpumbavu wa kudharauliwa!’ atastahili Gehena ya moto.”—Mathayo 5:22.

Yesu alitumia maneno ambayo Wayahudi waliyajua—mahakama, Mahakama Kuu Zaidi, na Gehena ya moto—kuonyesha kwamba adhabu inayotolewa huongezeka kulingana na uzito wa dhambi.

Kwanza, Yesu alisema kwamba kila mtu anayeendelea kuwa na ghadhabu na ndugu yake atatoa hesabu “mahakamani.” Kulingana na desturi, mahakama hizo zilikuwa katika majiji yenye wanaume 120 au zaidi. (Mathayo 10:17; Marko 13:9) Mahakimu katika mahakama hizo walikuwa na mamlaka ya kutoa hukumu, hata kuhusiana na visa vya mauaji. (Kumbukumbu la Torati 16:18; 19:12; 21:1, 2) Hivyo, Yesu alikuwa akionyesha kwamba mtu anayeendelea kumchukia ndugu yake anafanya dhambi nzito.

Kisha, Yesu alisema kwamba mtu “anayemwambia ndugu yake neno la dharau lisilosemeka atatoa hesabu katika Mahakama Kuu Zaidi.” Neno la Kigiriki rha·kaʹ linalotafsiriwa “neno la dharau lisilosemeka” humaanisha “tupu” au “kichwa maji.” Kulingana na kitabu kimoja (The New Thayer’s Greek-English Lexicon of the New Testament), huo ulikuwa “usemi wa shutuma uliotumiwa na Wayahudi wakati wa Kristo.” Hivyo, Yesu alikuwa akieleza uzito wa kuonyesha chuki dhidi ya mtu mwingine kwa kutumia neno la dharau. Kwa hiyo, ni kama Yesu alikuwa akisema kwamba mtu anayetumia usemi kama huo angehukumiwa si mahakamani tu bali katika Mahakama Kuu Zaidi, Sanhedrini nzima, yaani, baraza la hukumu huko Yerusalemu iliyokuwa na makuhani wakuu, wazee na waandishi 70.—Marko 15:1.

Hatimaye, Yesu alieleza kwamba ikiwa mtu angemwita mwenzake “Wewe mpumbavu wa kudharauliwa!” angestahili Gehena ya moto. Neno “Gehena” linatokana na neno la Kiebrania geh hin·nomʹ, “bonde la Hinomu” lililokuwa upande wa magharibi na kusini mwa Yerusalemu la kale. Katika siku za Yesu, bonde hilo lilikuwa mahali pa kuteketeza takataka kutia ndani miili ya wahalifu sugu ambao walionwa kuwa hawastahili kuzikwa. Hivyo, neno “Gehena” lilikuwa mfano unaofaa wa uharibifu wa milele.

Basi, usemi “mpumbavu wa kudharauliwa” ulimaanisha nini? Neno lililotumiwa hapa linatamkwa kama neno la Kiebrania linalomaanisha “mwasi,” au “mhalifu.” Usemi huo unamaanisha mtu asiye na maadili, mwasi-imani, au mtu anayemwasi Mungu. Kwa hiyo, mtu anapomwita mwenzake “mpumbavu wa kudharauliwa,” ni kana kwamba anasema mtu huyo anapaswa kupata adhabu inayowapata wale ambao wamemwasi Mungu, yaani, uharibifu wa milele. Kwa maoni ya Mungu, yule anayemshutumu mtu mwingine hivyo anaweza kustahili kupata adhabu hiyohiyo kali, yaani, uharibifu wa milele.—Kumbukumbu la Torati 19:17-19.

Kwa hiyo, Yesu alikuwa akiwawekea wafuasi wake kiwango cha juu zaidi kuliko kile kilichokuwa katika kanuni za Sheria ya Musa. Ingawa watu waliamini kwamba muuaji ‘angetoa hesabu mahakamani,’ Yesu alionyesha kuwa mengi zaidi yalihusika. Alifundisha kwamba wafuasi wake hawapaswi kuwachukia ndugu zao.—Mathayo 5:21, 22.