Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Pembetatu ya Zambarau Inamaanisha Nini?”

“Pembetatu ya Zambarau Inamaanisha Nini?”

“Pembetatu ya Zambarau Inamaanisha Nini?”

“SIKU chache zilizopita, nilipokea nakala ya Mnara wa Mlinzi kutoka kwa Shahidi wa Yehova,” akaandika mfanyakazi mmoja wa serikali anayefanya kazi na wizara ya haki huko Seoul katika Jamhuri ya Korea. Aliongeza hivi: “Nilipolisoma nilijifunza mambo fulani kuhusu jinsi Mashahidi wa Yehova walivyoteswa na serikali ya Nazi na serikali za Kikomunisti. Lakini nina swali. Picha kwenye jalada inaonyesha Mashahidi wa Yehova wakiwa na pembetatu ya zambarau iliyopinduliwa kwenye upande wa kushoto wa mavazi yao. Hiyo pembetatu ya zambarau inamaanisha nini?”

Nchini Ujerumani, chini ya utawala wa Nazi, Mashahidi wa Yehova walikataa kumpigia Hitler saluti, na hawakujihusisha na masuala ya kisiasa na ya kijeshi. Kwa hiyo, askari wa Nazi waliwatesa kikatili, wakawakamata Mashahidi wapatao 12,000 na kuwafunga vifungo vyenye urefu mbalimbali gerezani na katika kambi za mateso. Karibu 2,000 kati yao walikufa, na wengi kati yao waliuawa.

Pembetatu ya zambarau kwenye mavazi yao ya gereza ilimaanisha nini? “Vikundi mbalimbali vya wafungwa katika kambi [za Nazi] vilikuwa na alama za pekee zilizowatambulisha,” kinasema kitabu kimoja (Anatomy of the SS State). “Mfumo wa kutia alama kwenye nguo za wafungwa ulioanzishwa kabla ya vita ulihusisha kushona kitambaa chenye umbo la pembetatu kwenye nguo ya kila mfungwa, na rangi ya kitambaa hicho ilionyesha kikundi chake: rangi nyekundu ilikuwa ya wafungwa wa kisiasa, zambarau ilikuwa ya Mashahidi wa Yehova, nyeusi ilikuwa ya watu wanaopinga jamii, kijani ilikuwa ya wahalifu, waridi ilikuwa ya wanaume wanaofanya ngono na wanaume, bluu ilikuwa ya wahamiaji. Zaidi ya kuvaa pembetatu yenye rangi, wafungwa Wayahudi walivaa nguo zenye pembe tatu ya manjano ambayo ilishonelewa juu ya pembetatu ya kawaida yenye rangi ili kufanyiza Nyota ya Daudi yenye pembe sita.”

Profesa John K. Roth aliandika hivi katika kitabu chake (Holocaust Politics): “Ikiwa umuhimu wake wa kimaadili utakumbukwa wakati ujao, bado pembetatu ya zambarau itakuwa ulinzi dhidi ya msiba, na pembe zake tatu zitatukumbusha na kutufanya tuwe na wajibu wa kuwa na mwenendo mzuri ambao unastahili sana kuheshimiwa na watu.” Mashahidi wa Yehova wametokeza video iliyoshinda tuzo yenye kichwa Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault. Kwa nini usimuulize Shahidi wa Yehova akufanyie mpango uitazame video hiyo?