Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tumempata Masihi”

“Tumempata Masihi”

“Tumempata Masihi”

“TUMEMPATA Masihi.” “Tumempata yule ambaye Musa, katika Sheria, na Manabii, aliandika juu yake.” Maneno hayo yenye kushangaza yalisemwa na Wayahudi wawili wa karne ya kwanza waliojitoa kwa Mungu. Hatimaye, Masihi aliyetarajiwa alikuwa amefika. Wayahudi hao walisadiki hilo!—Yohana 1:35-45.

Unapofikiria hali ya kilimwengu na ya kidini ya wakati huo, usadikisho wao ni muhimu sana. Watu wengi waliodai kuwa wakombozi walitokea kwa vishindo na kutoa ahadi nyingi, lakini matumaini ya watu yalididimia watu hao waliposhindwa kuwakomboa Wayahudi kutokana na ukandamizaji wa Waroma.—Matendo 5:34-37.

Hata hivyo, Wayahudi hao wawili, Andrea na Filipo, hawakuwa na shaka kamwe kwamba walikuwa wamempata Masihi wa kweli. Badala yake, katika miaka iliyofuata, uhakika wao uliongezeka waliposhuhudia wenyewe kazi zenye nguvu ambazo mwanamume huyo alifanya katika utimizo wa mambo yaliyotabiriwa kuhusu Masihi.

Kwa nini watu hao wawili na wengine wengi walimwamini na kusadiki kwamba hakuwa Masihi mwingine wa uwongo? Ni mambo gani yaliyothibitisha kwamba alikuwa Masihi wa kweli?

Kulingana na masimulizi ya kihistoria, Andrea na Filipo walimtambua Yesu wa Nazareti, aliyekuwa seremala, kuwa Masihi aliyeahidiwa na kutarajiwa kwa muda mrefu. (Yohana 1:45) Luka, mwanahistoria aliyekuwa makini wa wakati huo, anasema kwamba kuja huko kwa Masihi kulitukia “katika mwaka wa kumi na tano wa kumiliki kwa Kaisari Tiberio.” (Luka 3:1-3) Mwaka huo wa 15 wa kumiliki kwa Tiberio ulianza mnamo Septemba mwaka wa 28 W.K., na ukamalizika mnamo Septemba mwaka wa 29 W.K. Zaidi ya hayo, Luka anasema kwamba wakati huo Wayahudi walikuwa “wakitarajia” kufika kwa Masihi. (Luka 3:15) Kwa nini walikuwa wakimtarajia hasa wakati huo? Tutaona.

Mambo Yaliyomtambulisha Masihi

Kwa kuwa Masihi anatimiza jukumu muhimu, ni jambo linalopatana na akili kutarajia kwamba Muumba, Yehova, angetoa uthibitisho ulio wazi ambao ungewasaidia watu waliokuwa makini na waaminifu kumtambua Masihi aliyeahidiwa. Kwa nini? Kwa kuwa katika njia hiyo, watu waliokuwa makini hawangeweza kudanganywa na walaghai, kama ilivyotukia kwa wengi.

Balozi fulani anapojitambulisha kwa serikali ya nchi nyingine, anatarajiwa kuonyesha vitambulisho vinavyothibitisha kwamba amewekwa rasmi na serikali yake kuwa balozi. Vivyo hivyo, tangu zamani Yehova alionyesha wazi matakwa ambayo Masihi angepaswa kutimiza. Hivyo, wakati ambapo “Wakili Mkuu” angetokea, ingekuwa kana kwamba alikuja na vitambulisho ambavyo vingemthibitisha kuwa Masihi.—Waebrania 12:2.

Matakwa ambayo Masihi halisi angepaswa kutimiza yalionyeshwa katika unabii mwingi wa Biblia ambao uliandikwa karne nyingi mapema. Unabii huo ulionyesha waziwazi jinsi ambavyo Masihi angekuja, huduma yake, jinsi ambavyo angeteswa, na aina ya kifo ambacho kingempata. Huenda ukapendezwa kujua kwamba unabii huo wenye kutegemeka ulitabiri pia ufufuo wake, kuinuliwa kwake kwenye mkono wa kuume wa Mungu, na hatimaye baraka ambazo Ufalme wake wa wakati ujao ungeleta. Katika njia hiyo, unabii wa Biblia ulionyesha mambo ya pekee sana ambayo yanaweza kulinganishwa na alama za vidole zinazomtambulisha mtu mmoja tu.

Bila shaka, Yesu alipotokea mwaka wa 29 W.K., hakutimiza wakati huo unabii wote uliohusiana na Masihi. Kwa mfano, alikuwa bado hajauawa na kufufuliwa. Hata hivyo, Andrea, Filipo, na wengine wengi walimwamini Yesu kwa sababu ya mambo aliyofundisha na kufanya. Waliona uthibitisho mwingi ulioonyesha kwamba, kwa kweli, alikuwa Masihi. Ikiwa ungekuwapo wakati huo na kujionea waziwazi uthibitisho huo ukiwa na maoni yanayofaa, huenda wewe pia ungesadikishwa kwamba Yesu alikuwa Masihi.

Uthibitisho Wenye Sehemu Nyingi

Ni nini ambacho kingekusaidia kufikia mkataa huo? Kwa karne nyingi, manabii wa Biblia walionyesha matakwa hususa ambayo Masihi angepaswa kutimiza, na hivyo kumtambulisha bila kukosea. Manabii walipotangaza mambo hayo kadiri miaka ilivyopita, hatua kwa hatua watu walipata kuyajua. Henry H. Halley alisema hivi: “Tuseme watu kadhaa wa Nchi Mbalimbali ambao hawajawahi kuonana kamwe wala kuwasiliana wanaingia ndani ya chumba, na kila mmoja wao anatoa kipande cha Mchongo wa Marumaru, na vipande hivyo Vinapounganishwa Pamoja vinafanyiza mchongo Kamili—je, kutakuwa na shaka yoyote kwamba Mtu Fulani alichonga Sehemu Mbalimbali za Mchongo Huo na kumpa kila mmoja wa watu hao sehemu moja ya umbo hilo?” Kisha anauliza: “Basi, inawezekanaje kwamba Mambo Mbalimbali Kuhusu Maisha na Kazi ya Yesu, yaliyoandikwa na Waandishi Mbalimbali wa Karne Tofauti-Tofauti, Miaka Mingi Kabla ya Yesu Kuzaliwa, yalipatana ikiwa hayakuandikwa kwa mwongozo wa MTU FULANI MWENYE UWEZO KUPITA WA MWANADAMU?” Halley anamalizia kwa kusema “Huo Ni Muujiza Wenye Kustaajabisha!”

“Muujiza” huo ulianza katika kitabu cha kwanza cha Biblia. Zaidi ya kuandika unabii wa kwanza wa Biblia ambao ulionyesha jukumu la Masihi, mwandikaji wa kitabu cha Mwanzo pia aliandika kwamba Masihi angekuja kupitia ukoo wa Abrahamu. (Mwanzo 3:15; 22:15-18) Utambulisho mwingine ulionyesha kwamba Masihi angetokea katika kabila la Yuda. (Mwanzo 49:10) Mungu aliwaeleza Waisraeli kupitia Musa kwamba Masihi angekuwa mnenaji na mkombozi mkuu zaidi kuliko hata Musa.—Kumbukumbu la Torati 18:18.

Wakati wa Mfalme Daudi, unabii ulionyesha kwamba Masihi angekuwa mrithi wa kiti cha ufalme cha Daudi na kwamba ufalme Wake ‘ungefanywa imara mpaka wakati usio na kipimo.’ (2 Samweli 7:13-16) Kitabu cha Mika kilionyesha kwamba Masihi angezaliwa katika mji wa Daudi, yaani, Bethlehemu. (Mika 5:2) Isaya alitabiri kwamba Angezaliwa na bikira. (Isaya 7:14) Nabii Malaki alitabiri kwamba kuja Kwake kungetangazwa na mtu fulani anayefanana na Eliya.—Malaki 4:5, 6.

Maelezo zaidi kuhusu kutokea kwa Masihi yalitolewa katika kitabu cha Danieli. Unabii huo unaonyesha mwaka hususa wa kutokea kwa Masihi, unaposema hivi: “Ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62. Atarudi na kujengwa hakika, pamoja na kiwanja cha watu wote na handaki, lakini katika dhiki ya nyakati.”—Danieli 9:25.

Mfalme Mwajemi Artashasta alitoa “neno” la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu katika mwaka wa 20 wa utawala wake. Kwa kuwa utawala wake ulianza mwaka wa 474 K.W.K., mwaka wake wa 20 ungekuwa mwaka wa 455 K.W.K. (Nehemia 2:1-8) Kwa hiyo, kipindi cha majuma 69 (7 kuongeza 62) ya unabii kingekuwapo kati ya kutolewa kwa amri ya kurudisha na kujenga upya Yerusalemu na kutokea kwa Masihi. Bila shaka, majuma halisi 69 ni siku 483 tu, au chini ya miaka miwili. Lakini kanuni ya kinabii ya “siku moja kwa mwaka mmoja” inapotumiwa, inaonyesha kwamba Masihi angetokea baada ya miaka 483, yaani, mwaka wa 29 W.K.—Ezekieli 4:6. *

Ingawa watu wengine waliodai kuwa Masihi walitokea nyakati mbalimbali, Yesu wa Nazareti tu ndiye aliyetokea ulimwenguni mwaka wa 29 W.K. (Luka 3:1, 2) Katika mwaka huohuo, Yesu alimwendea Yohana Mbatizaji, na akabatizwa katika maji. Kisha, Yesu akatiwa mafuta kwa roho takatifu kuwa Masihi. Baadaye, Yohana, mtangulizi aliyetabiriwa ambaye alifananishwa na Eliya, alimtambulisha Yesu kwa Andrea na mwanafunzi mwingine, kwa kumwita “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.”—Yohana 1:29; Luka 1:13-17; 3:21-23.

Ukoo na Utambulisho wa Masihi

Unabii ulioongozwa kwa roho ya Mungu ulimhusianisha Masihi na familia hususa za Kiyahudi. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kwamba Muumba anayejua mambo yote angehakikisha kwamba Masihi ametokea wakati ambapo rekodi za ukoo zingepatikana ili kuthibitisha ukoo wake.

Kitabu kimoja (Cyclopedia cha McClintock na Strong) kinasema: “Hakuna shaka kwamba rekodi za ukoo za makabila ya Wayahudi na familia zao zilipotea wakati wa uharibifu wa Yerusalemu [mwaka wa 70 W.K.], na si kabla ya hapo.” Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba Mathayo na Luka waliandika vitabu vyao vya Injili kabla ya mwaka wa 70 W.K. Hivyo, wangeweza kuchunguza rekodi hizo ili kuandika masimulizi yao kuhusu ukoo wa Yesu. (Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38) Bila shaka, kwa sababu ya umuhimu wa habari hiyo, watu wengi wa wakati wao wangetaka kujichunguzia habari za ukoo wa Yesu.

Je, Unabii Ulitimia Katika Yesu Bila Kukusudiwa?

Hata hivyo, je, inawezekana kwamba Yesu alitimiza unabii uliohusu Masihi bila kukusudiwa? Msomi mmoja aliyehojiwa alijibu hivi: “Haiwezekani. Uwezekano wa kwamba unabii ulitimia katika Yesu bila kukusudiwa ni mdogo sana. Mtu fulani alifanya hesabu na kugundua kwamba uwezekano wa unabii nane mbalimbali kutimizwa bila kukusudiwa ni sehemu moja ya bilioni milioni mia moja.” Akijaribu kutoa mfano kueleza idadi hiyo alisema hivi: “Ikiwa ungekuwa na sarafu za dola bilioni milioni mia moja, zingetoshea katika jimbo lote la Texas [kilometa 690,000 za mraba] kufikia kimo cha sentimeta 60. Ikiwa ungetia alama sarafu moja kati ya hizo na umwombe mtu aliyefunikwa macho atembee katika jimbo hilo akitafuta sarafu hiyo, kuna uwezekano gani kwamba angechagua ile iliyotiwa alama?” Kisha, akasema kwamba huo ndio “uwezekano wa mtu yeyote katika historia kutimiza unabii nane mbalimbali [wa Kimasihi].”

Hata hivyo, wakati wa miaka mitatu na nusu ya huduma yake, Yesu hakutimiza tu unabii nane, bali alitimiza unabii mwingi wa Biblia. Kwa sababu ya uthibitisho huo mwingi, msomi huyo alimalizia kwa kusema hivi: “Ni Yesu tu katika historia yote ambaye alifaulu kutimiza unabii mwingi wa Biblia.”

“Kuja” kwa Masihi

Ni wazi kwamba Yesu wa Nazareti ndiye Masihi aliyekuja mwaka wa 29 W.K. Alikuja akiwa mnyenyekevu, Mkombozi aliyeteseka. Hakuja akiwa Mfalme mwenye ushindi ili kuvunja nira ya uonevu ya Waroma, kama Wayahudi wengi, na huenda hata wafuasi wake, walivyotarajia. (Isaya, sura ya 53; Zekaria 9:9; Matendo 1:6-8) Hata hivyo, ilitabiriwa kwamba wakati ujao atakuja katika mamlaka na uwezo mwingi.—Danieli 2:44; 7:13, 14.

Kujifunza kwa makini unabii mbalimbali wa Biblia kumewasadikisha watu wengi ulimwenguni pote kwamba Masihi alikuja katika karne ya kwanza, na kwamba alipaswa kurudi tena. Uthibitisho unaonyesha kwamba kurudi kwake kulikotabiriwa, yaani, mwanzo wa “kuwapo” kwake, kulitukia mwaka wa 1914. * (Mathayo 24:3-14) Katika mwaka huo, Yesu alitawazwa huko mbinguni kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu bila kuonekana na wanadamu. Hivi karibuni, atakomesha matokeo ya uasi wa Edeni duniani. Utawala wake wa Miaka Elfu utakaofuata utawabariki wote wanaomwamini akiwa Uzao ulioahidiwa, Masihi, ‘anayeondolea mbali dhambi ya ulimwengu.’—Yohana 1:29; Ufunuo 21:3, 4.

Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumza nawe kuhusu uthibitisho huo na watakuonyesha katika Biblia kile ambacho utawala wa Masihi unaweza kumaanisha kwako na kwa wapendwa wako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kwa habari zaidi kuhusu andiko la Danieli 9:25, ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 899-904, (au Étude Perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa 995-999), kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 27 Kwa maelezo zaidi, ona sura ya 10 na 11 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 6, 7]

455 K.W.K., “lile neno la kurudisha upya . . . Yerusalemu”

29 W.K., Masihi anawasili

Miaka 483 (69 majuma ya kinabii 69)​—Danieli 9:25

Mwaka wa 1914, Masihi anatawazwa mbinguni

Hivi karibuni Masihi atakomesha uovu na kuifanya dunia kuwa paradiso