Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usimamizi wa Kutimiza Kusudi la Mungu

Usimamizi wa Kutimiza Kusudi la Mungu

Usimamizi wa Kutimiza Kusudi la Mungu

‘Mungu anatenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.’—WAEFESO 1:11.

1. Kwa nini makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova yatakutanika Aprili 12, 2006?

SIKU ya Jumatano, Aprili 12, 2006, watu milioni 16 hivi watakusanyika kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Kwenye sehemu zote ambako watakutanikia, kutakuwa na meza yenye mkate usiotiwa chachu ambao unawakilisha mwili wa Kristo, na divai nyekundu inayowakilisha damu yake iliyomwagwa. Mwishoni mwa hotuba inayozungumzia umuhimu wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu, mifano hiyo itapitishwa kwa wale watakaohudhuria. Mkate utapitishwa kwanza, kisha divai. Katika makutaniko machache ya Mashahidi wa Yehova, mtu mmoja au zaidi kati ya wale watakaohudhuria atashiriki kula mkate huo na kunywa divai hiyo. Hata hivyo, katika makutaniko mengi hakuna atakayeshiriki kula mkate na kunywa divai. Kwa nini ni Wakristo wachache tu, wale walio na tumaini la kuishi mbinguni, ndio wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai huku wengi, walio na tumaini la kuishi milele duniani, hawashiriki?

2, 3. (a) Yehova alifanyaje kazi ya uumbaji kupatana na kusudi lake? (b) Yehova aliumba dunia na wanadamu kwa kusudi gani?

2 Yehova ni Mungu mwenye kusudi. Katika kutimiza kusudi lake, yeye ‘hutenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.’ (Waefeso 1:11) Kwanza, alimuumba Mwana wake mzaliwa-pekee. (Yohana 1:1, 14; Ufunuo 3:14) Halafu, kupitia Mwana huyo Yehova aliumba familia ya wana wa roho, kisha akaumba ulimwengu unaoonekana kutia ndani dunia na wanadamu.—Ayubu 38:4, 7; Zaburi 103:19-21; Yohana 1:2, 3; Wakolosai 1:15, 16.

3 Yehova hakuiumba dunia iwe mahali pa kuwajaribu wanadamu ili kuona ikiwa wanastahili kuwa wana wa roho huko mbinguni kama vile dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo zinavyofundisha. Aliiumba dunia akiwa na kusudi hususa, kwamba “ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mungu aliiumba dunia kwa ajili ya mwanadamu na alimuumba mwanadamu kwa ajili ya dunia. (Zaburi 115:16) Dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa wanadamu waadilifu ambao wangeilima na kuitunza. Wanadamu wawili wa kwanza hawakuwa kamwe na tumaini la kwenda mbinguni.—Mwanzo 1:26-28; 2:7, 8, 15.

Kusudi la Yehova Latiliwa Shaka

4. Njia ya Yehova ya kutawala ilitiliwaje shaka mwanzoni mwa historia ya wanadamu?

4 Mmoja wa wana wa roho wa Mungu aliasi na akaazimia kuharibu kusudi la Yehova huku akitumia vibaya zawadi aliyopewa na Mungu ya uhuru wa kuchagua. Aliharibu amani ya wale wote wanaojitiisha kwa upendo chini ya utawala wa Yehova. Shetani aliwaongoza wanadamu wa kwanza waanze kujitegemea badala ya kumtegemea Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Hakutilia shaka nguvu za Yehova, bali alitilia shaka njia ya Yehova ya kutawala, yaani, haki ya Yehova ya kutawala. Hivyo, suala kuu kuhusu haki ya Yehova ya kutawala lilizushwa hapa duniani, mwanzoni mwa historia ya wanadamu.

5. Ni suala gani la pili lililozushwa, nalo lilihusisha nani?

5 Katika siku za Ayubu, Shetani alizusha suala lingine linalohusiana sana na suala hilo kuu la haki ya Yehova ya kutawala. Shetani alitilia shaka nia ya viumbe wa Yehova ya kujitiisha kwa Yehova na kumtumikia. Shetani alidokeza kwamba walikuwa wanafanya hivyo kwa sababu za ubinafsi na kwamba ikiwa wangejaribiwa, wangemwasi Mungu. (Ayubu 1:7-11; 2:4, 5) Ingawa dai hilo lilizushwa dhidi ya mtumishi wa Yehova aliye mwanadamu, lilihusisha pia wana wa roho wa Mungu, hata Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova.

6. Yehova alikuwaje mwaminifu kwa kusudi lake na kwa jina lake?

6 Kwa kuwa yeye ni mwaminifu kwa kusudi lake na kwa maana ya jina lake, Yehova alijifanya kuwa Nabii na Mwokozi. * Alimwambia Shetani hivi: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwanzo 3:15) Kupitia Uzao wa “mwanamke” wake, au sehemu ya mbinguni ya tengenezo lake, Yehova angejibu dai la Shetani na kuwapa wazao wa Adamu tumaini la kupata ukombozi na uzima.—Waroma 5:21; Wagalatia 4:26, 31.

“Siri Takatifu ya Mapenzi Yake”

7. Yehova alifunua kusudi gani kupitia mtume Paulo?

7 Katika barua aliyowaandikia Wakristo huko Efeso, mtume Paulo alieleza vizuri sana jinsi Yehova anavyosimamia mambo ili kutimiza kusudi lake. Paulo aliandika hivi: “Alitujulisha siri takatifu ya mapenzi yake. Ni kulingana na upendezi wake mwema alioukusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi, yaani, kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:9, 10) Kusudi tukufu la Yehova ni kufanyiza ulimwengu wenye umoja ulio na viumbe wanaojitiisha kwa upendo chini ya utawala wake. (Ufunuo 4:11) Kwa kufanya hivyo, jina lake litatakaswa, Shetani atathibitishwa kuwa mwongo, na mapenzi ya Mungu yatatendeka “duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10.

8. Ni nini maana ya neno linalotafsiriwa kuwa “usimamizi”?

8 ‘Upendezi mwema’ wa Yehova, au kusudi lake, litatimizwa kupitia “usimamizi” fulani. Paulo alitumia neno ambalo, linapotafsiriwa moja kwa moja humaanisha “usimamizi wa nyumba.” Halirejelei serikali, kama vile Ufalme wa Kimasihi, bali linarejelea njia ya kusimamia mambo. * Njia bora ambayo Yehova angetumia kusimamia mambo ili kutimiza kusudi lake ilihusisha “siri takatifu” ambayo ingefunuliwa hatua kwa hatua kadiri wakati ulivyopita.—Waefeso 1:10; 3:9, maelezo ya chini katika Reference Bible.

9. Yehova alifunuaje hatua kwa hatua siri takatifu ya mapenzi yake?

9 Kupitia maagano mbalimbali yaliyofuatana, Yehova alifunua hatua kwa hatua jinsi ambavyo kusudi lake kuhusiana na Uzao ulioahidiwa huko Edeni lingetimizwa. Agano lake na Abrahamu lilifunua kwamba Uzao ulioahidiwa ungekuja duniani katika ukoo wa Abrahamu, na kupitia Uzao huo “mataifa yote ya dunia” yangejibariki. Agano hilo pia lilidokeza kwamba wengine wangeshirikiana na sehemu ya msingi ya uzao huo. (Mwanzo 22:17, 18) Agano la Sheria lililofanywa pamoja na taifa la Israeli la asili lilifunua kusudi la Yehova la kuwa na “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:5, 6) Agano lililofanywa pamoja na Daudi lilionyesha kwamba Uzao huo ungekuwa Kichwa cha Ufalme mpaka wakati usio na kipimo. (2 Samweli 7:12, 13; Zaburi 89:3, 4) Baada ya agano la Sheria kuwaongoza Wayahudi kwa Masihi, Yehova alifunua mambo mengine kuhusu utimizo wa kusudi lake. (Wagalatia 3:19, 24) Wanadamu ambao wangeshirikiana na sehemu ya msingi ya uzao ndio wangefanyiza “ufalme wa makuhani” uliotabiriwa, nao wangeingizwa katika “agano jipya” wakiwa “Israeli” jipya, taifa la kiroho.—Yeremia 31:31-34; Waebrania 8:7-9. *

10, 11. (a) Yehova alifunuaje Uzao uliotabiriwa? (b) Kwa nini Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuja duniani?

10 Kupatana na usimamizi wa kusudi la Mungu, wakati ulifika ili Uzao uliotabiriwa utokee duniani. Yehova alimtuma malaika Gabrieli amwambie Maria kwamba angemzaa mwana ambaye angeitwa Yesu. Malaika huyo alimwambia Maria hivi: “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Hivyo, Uzao ulioahidiwa ulitambulishwa waziwazi.—Wagalatia 3:16; 4:4.

11 Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova angekuja duniani na kujaribiwa hadi kifo. Maisha ya Yesu ndiyo yangetoa jibu kamili kwa dai la Shetani. Je, angebaki mwaminifu kwa Baba yake? Jambo hilo lilihusisha siri takatifu. Baadaye, mtume Paulo alieleza daraka la Yesu alipoandika hivi: “Ni jambo lenye kukubalika kwamba siri takatifu ya huu ujitoaji-kimungu ni kubwa: ‘Yeye alifunuliwa katika mwili, alitangazwa kuwa mwadilifu katika roho, alionekana kwa malaika, alihubiriwa kati ya mataifa, aliaminiwa katika ulimwengu, alipokewa juu katika utukufu.’” (1 Timotheo 3:16) Naam, kupitia utimilifu wake hadi kifo, Yesu alitoa jibu kamili kwa dai la Shetani. Lakini mambo mengine kuhusu siri takatifu yangefunuliwa baadaye.

“Siri Takatifu ya Ufalme wa Mungu”

12, 13. (a) Ni nini sehemu moja ya “siri takatifu ya ufalme wa Mungu”? (b) Ni nini kilichohusika Yehova alipochagua idadi ndogo ya wanadamu waende mbinguni?

12 Katika mojawapo ya ziara zake za kuhubiri huko Galilaya, Yesu alionyesha kwamba siri takatifu ilihusiana sana na serikali yake ya Ufalme wa Kimasihi. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu za ufalme wa mbinguni [“ufalme wa Mungu,” Marko 4:11].” (Mathayo 13:11) Sehemu moja ya siri hiyo inahusiana na jinsi ambavyo Yehova angechagua “kundi dogo” la wanadamu 144,000 ili washirikiane na Mwana wake wakiwa sehemu ya ule uzao na kutawala pamoja naye mbinguni.—Luka 12:32; Ufunuo 14:1, 4.

13 Kwa kuwa wanadamu waliumbwa waishi duniani, ilibidi Yehova atokeze “kiumbe kipya” ili wanadamu fulani waende mbinguni. (2 Wakorintho 5:17) Akiwa mmoja wa wale waliochaguliwa kupata tumaini hilo la pekee la kwenda mbinguni, mtume Petro aliandika hivi: “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenye urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu.”—1 Petro 1:3, 4.

14. (a) Wasio Wayahudi walihusikaje katika “siri takatifu ya ufalme wa Mungu”? (b) Kwa nini tunaweza kuelewa haya “mambo mazito ya Mungu”?

14 Sehemu nyingine ya siri takatifu inayohusiana na serikali ya wakati ujao ya Ufalme ni mapenzi ya Mungu ya kuwatia ndani wasio Wayahudi katika idadi ndogo ya wanadamu ambao wangepata mwito wa kutawala na Kristo mbinguni. Paulo alieleza jambo hilo kuhusu “usimamizi” wa Yehova au njia ya kusimamia utimizo wa kusudi lake alipoandika hivi: “Katika vizazi vingine siri hii haikujulishwa kwa wana wa binadamu kama vile ambavyo imefunuliwa sasa kwa mitume wake watakatifu na manabii kupitia roho, yaani, kwamba watu wa mataifa wawe warithi wa pamoja na viungo vyenzi vya mwili na washiriki pamoja nasi wa ahadi katika muungano na Kristo Yesu kupitia habari njema.” (Waefeso 3:5, 6) ‘Mitume watakatifu’ walifunuliwa sehemu hiyo ya siri takatifu. Vivyo hivyo leo, hatungeweza kuelewa haya “mambo mazito ya Mungu” bila msaada wa roho takatifu.—1 Wakorintho 2:10; 4:1; Wakolosai 1:26, 27.

15, 16. Kwa nini Yehova alichagua wale watakaoshiriki kutawala pamoja na Kristo kutoka kati ya wanadamu?

15 “Wale 144,000” ambao wanaonekana wakisimama pamoja na “Mwana-Kondoo” juu ya Mlima Sayuni wa mbinguni wanasemwa kuwa “wamenunuliwa kutoka duniani,” naam, “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo,” Kristo Yesu. (Ufunuo 14:1-4) Yehova alichagua mwana wa kwanza kati ya wana wake wa mbinguni kuwa sehemu ya msingi ya uzao ulioahidiwa huko Edeni, lakini kwa nini alichagua washirika wa Kristo kutoka kati ya wanadamu? Mtume Paulo anaeleza kwamba idadi hiyo ndogo ‘iliitwa kulingana na kusudi lake Yehova,’ “kulingana na upendezi mwema wa mapenzi yake.”—Waroma 8:17, 28-30; Waefeso 1:5, 11; 2 Timotheo 1:9.

16 Kusudi la Yehova ni kutakasa jina lake kuu lililo takatifu na kutetea enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima. Kupitia “usimamizi” wake, au njia yake ya kusimamia mambo inayoonyesha hekima yake isiyo na kifani, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza duniani, ambapo alijaribiwa hadi kifo. Isitoshe, Yehova aliamua kwamba serikali ya Ufalme wa Kimasihi ya Mwana wake ingetia ndani wanadamu ambao pia walikuwa wameunga mkono enzi kuu Yake hadi kifo.—Waefeso 1:8-12; Ufunuo 2:10, 11.

17. Kwa nini tunaweza kufurahi kwamba Kristo na wale watakaotawala pamoja naye walikuwa wanadamu wakati fulani?

17 Yehova alionyesha kwamba anawapenda sana wazao wa Adamu kwa kumtuma Mwana wake duniani na kuchagua kutoka kati ya wanadamu wale watakaokuwa warithi-washirika pamoja na Mwana wake katika serikali ya Ufalme. Jambo hilo linaweza kuwafaidije wengine ambao wamekuwa waaminifu kwa Yehova, kuanzia Abeli na kuendelea? Kwa kuwa wamezaliwa wakiwa watumwa wa dhambi na kifo, wanadamu wasio wakamilifu wanahitaji kuponywa kiroho na kimwili na kufanywa wawe wakamilifu, kupatana na kusudi la awali la Yehova kwa ajili ya wanadamu. (Waroma 5:12) Inafariji kama nini kwa wale wote wanaotazamia uzima wa milele duniani kujua kwamba Mfalme wao atawatendea kwa upendo na kwa fadhili kama vile alivyowatendea wanafunzi wake wakati wa huduma yake duniani! (Mathayo 11:28, 29; Waebrania 2:17, 18; 4:15; 7:25, 26) Isitoshe, wanafarijika kama nini wanapotambua kwamba wale watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni wakati mmoja walikuwa wanaume na wanawake wenye imani ambao walikabili udhaifu mbalimbali na matatizo ya maisha, kama sisi!—Waroma 7:21-25.

Kusudi la Yehova Lisiloweza Kushindwa

18, 19. Kwa nini tunaelewa wazi zaidi maneno ya Paulo kwenye Waefeso 1:8-11, na tutachunguza nini katika makala inayofuata?

18 Sasa tunaweza kuelewa vizuri maana ya maneno ya Paulo kwa Wakristo watiwa-mafuta yanayopatikana katika Waefeso 1:8-11. Paulo alisema kwamba Yehova alikuwa amewajulisha “siri takatifu ya mapenzi yake,” kwamba walikuwa ‘wamehesabiwa kuwa warithi’ pamoja na Kristo, na kwamba walikuwa ‘wameagizwa kimbele kulingana na kusudi lake yeye anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.’ Tunatambua kwamba jambo hilo linapatana kabisa na “usimamizi” bora wa Yehova wa kutimiza kusudi lake. Pia, hilo linatusaidia kuelewa kwa nini ni Wakristo wachache tu kati ya wale wanaohudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana ndio wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai.

19 Katika makala inayofuata, tutaona umuhimu wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo kwa Wakristo walio na tumaini la kwenda mbinguni. Pia, tutajifunza ni kwa nini mamilioni ya watu walio na tumaini la kuishi milele duniani wanapaswa kupendezwa sana na maana ya Ukumbusho.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Jina la Mungu linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Yehova anaweza kuwa chochote kinachohitajiwa ili kutimiza kusudi lake.—Kutoka 3:14, maelezo ya chini katika Reference Bible.

^ fu. 8 Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba “usimamizi” huo ulikuwepo katika siku zake, hali Maandiko yanaonyesha kwamba Ufalme wa Kimasihi ulisimamishwa mwaka wa 1914.

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kuhusu maagano hayo yaliyohusika katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu, ona Mnara wa Mlinzi wa Februari 1, 1989, ukurasa wa 10-15.

Kwa Kupitia

• Kwa nini Yehova aliumba dunia na kumweka mwanadamu ndani yake?

• Kwa nini ilibidi Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova ajaribiwe duniani?

• Kwa nini Yehova aliwachagua wale watakaotawala pamoja na Kristo kutoka kati ya wanadamu?

[Maswali ya Funzo]