Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uthibitisho wa Mapema wa Vitabu Vya Biblia Vinavyokubalika

Uthibitisho wa Mapema wa Vitabu Vya Biblia Vinavyokubalika

Uthibitisho wa Mapema wa Vitabu Vya Biblia Vinavyokubalika

“NI KANA kwamba kila mstari umeandikwa hasa ili kuamsha upendezi wa wale ambao wanapendezwa na historia ya mapema ya Ukristo.” Hivyo ndivyo hati moja ya kale ilivyofafanuliwa. Je, unaweza kuwazia hiyo ni hati gani?

Huenda umesikia au hujasikia kuhusu hati hiyo inayoitwa Hati ya Muratori. Kwa vyovyote, huenda ukajiuliza, ‘Ni nini kinachofanya Hati ya Muratori kuwa ya pekee sana?’ Hiyo ndiyo orodha ya kale zaidi ya vitabu vinavyokubalika vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Huenda ukakubali mara moja kwamba vitabu fulani ni sehemu ya Biblia. Lakini je, utashangaa kujua kwamba kuna wakati ambapo watu fulani walikuwa na shaka kuhusu vitabu ambavyo vinapaswa kukubaliwa kuwa sehemu ya Biblia? Hati ya Muratori ina orodha ya vitabu ambavyo inaaminika kwamba viliongozwa kwa roho ya Mungu. Utakubali kwamba orodha sahihi ya vitabu vya Biblia ni muhimu sana. Hivyo, hati hiyo ilionyesha nini kuhusu vitabu ambavyo sasa viko katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? Kwanza, acheni tuchunguze hati hiyo.

Kugunduliwa kwa Hati Hiyo

Hati ya Muratori ni sehemu ya kodeksi yenye kurasa 76, na kila moja ya kurasa hizo ina urefu wa sentimeta 27 na upana wa sentimeta 17. Ludovico Antonio Muratori (1672-1750), mwanahistoria Mwitaliano aliye maarufu sana, ndiye aliyegundua hati hiyo katika Maktaba ya Ambrosian, huko Milan, Italia. Muratori alichapisha hati hiyo mwaka wa 1740, nayo ikapewa jina lake, Hati ya Muratori. Yaelekea kodeksi hiyo ilitayarishwa katika karne ya nane katika nyumba ya watawa ya Bobbio, karibu na Piacenza, kaskazini mwa Italia. Ilihamishwa hadi kwenye Maktaba ya Ambrosian mwanzoni mwa karne ya 17.

Hati ya Muratori ina mistari 85 ya maandishi kwenye ukurasa wa 10 na 11 wa kodeksi hiyo. Maandishi ya hati hiyo ambayo yaelekea yalinakiliwa na mwandikaji ambaye hakuwa makini sana, yameandikwa katika Kilatini. Lakini baadhi ya makosa ya mwandikaji huyo yamegunduliwa kwa kuilinganisha hati hiyo na maandishi hayohayo ya hati nne za karne ya 11, na karne ya 12.

Iliandikwa Wakati Gani?

Huenda ukajiuliza ni wakati gani habari zilizomo katika Hati ya Muratori ziliandikwa kwa mara ya kwanza. Yaelekea hati ya awali iliandikwa katika Kigiriki karne nyingi kabla ya maandishi ya Hati hiyo, ambayo ni tafsiri ya Kilatini kutoka katika Kigiriki. Ufuatao ni uthibitisho unaotusaidia kujua tarehe ambayo hati ya awali iliandikwa. Hati hiyo inataja kitabu kisicho cha Biblia, yaani, Shepherd, na inasema kwamba mwanamume aliyeitwa Hermas ndiye aliyekiandika “hivi majuzi, katika nyakati zetu, katika jiji la Roma.” Wasomi wanasema kwamba maandishi ya Hermas yanayoitwa Shepherd yaliandikwa kati ya mwaka wa 140 W.K. na mwaka wa 155 W.K. Hivyo, unaweza kuelewa sababu iliyofanya maandishi ya awali ya Kigiriki ya Hati ya Muratori ya Kilatini yasemekane kuwa yaliandikwa kati ya mwaka wa 170 W.K. na mwaka wa 200 W.K.

Kwa kuwa Roma imetajwa moja kwa moja na pia kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika hati hiyo, huenda hati hiyo iliandikwa katika jiji hilo. Lakini, bado kuna ubishi kuhusu ni nani aliyeandika hati hiyo. Clement wa Aleksandria, Melito wa Sardi, na Polycrates wa Efeso wamefikiriwa kuwa ndio walioiandika. Hata hivyo, wasomi wengi, wanamtaja Hippolytus, mwandikaji mwenye ujuzi aliyeandika katika Kigiriki na aliyeishi huko Roma katika kipindi ambacho huenda mambo yaliyomo katika Hati ya Muratori yaliandikwa. Ingawa huenda usipendezwe sana na habari hiyo, labda ungependa kujua zaidi kuhusu mambo yaliyomo ambayo yanaifanya kuwa yenye thamani.

Habari Zilizomo

Hati hiyo si orodha tu ya vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Lakini pia inatoa maelezo juu ya vitabu hivyo na wale walioviandika. Ukisoma hati hiyo, utaona kwamba haina sentensi za kwanza, na yaelekea pia sentensi zinamalizika ghafula. Inaanza kwa kutaja Injili ya Luka, na inasema kwamba mwandikaji wa kitabu hicho cha Biblia alikuwa tabibu. (Wakolosai 4:14) Hati hiyo inasema kwamba kitabu cha Luka ni cha tatu katika vitabu vya Injili. Hivyo, unaweza kuona kwamba sehemu ya kwanza inayokosekana yaelekea inahusu vitabu vya Injili vya Mathayo na Marko. Ikiwa umefikia mkataa huo, jua kwamba maoni yako yanapatana na Hati ya Muratori, kwa kuwa inasema kwamba kitabu cha nne cha Injili ni Yohana.

Hati hiyo inathibitisha kwamba kitabu cha Matendo ya Mitume kiliandikwa na Luka kwa “mtukufu Theofilo.” (Luka 1:3; Matendo 1:1) Kisha, inaorodhesha barua za mtume Paulo kwa Wakorintho (mbili), kwa Waefeso, kwa Wafilipi, kwa Wakolosai, kwa Wagalatia, kwa Wathesalonike (mbili), kwa Waroma, kwa Filemoni, kwa Tito, na kwa Timotheo (mbili). Barua ya Yuda na barua mbili za Yohana zinatajwa pia kuwa vitabu vilivyoongozwa kwa roho ya Mungu. Barua ya kwanza ya mtume Yohana ilikuwa tayari imetajwa pamoja na kitabu chake cha Injili. Kitabu cha Ufunuo kinamalizia orodha ya vitabu vinavyoonwa kuwa viliongozwa kwa roho ya Mungu.

Ni muhimu kwamba Hati hiyo inataja kitabu cha Ufunuo wa Petro, lakini inasema kuwa wengine walihisi kwamba kitabu hicho hakipaswi kusomwa na Wakristo. Mwandikaji anaonya kwamba katika siku zake, tayari maandishi bandia yalikuwa yakisambazwa. Hati ya Muratori inaeleza kwamba maandishi hayo bandia hayapaswi kukubaliwa, “kwa kuwa haifai kuchanganya kitu kichungu na asali.” Pia, hati hiyo inataja maandishi mengine ambayo hayakupaswa kutiwa ndani ya maandishi matakatifu. Ilikuwa hivyo kwa sababu huenda maandishi hayo yaliandikwa baada ya kipindi cha mitume, kama ilivyokuwa kuhusiana na maandishi ya Hermas yanayoitwa Shepherd, au kwa sababu yaliandikwa ili kuunga mkono uasi-imani.

Huenda umetambua kutokana na yale ambayo yametajwa hapo juu kwamba barua kwa Waebrania, barua mbili za Petro, na barua ya Yakobo hazikutajwa katika orodha ya vitabu vya Biblia vinavyokubalika. Hata hivyo, baada ya kurejelea kazi ya mwandikaji aliyenakili kwa mkono maandishi hayo, Dakt. Geoffrey Mark Hahneman alisema kwamba “ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba huenda Hati hiyo ilikuwa na marejeo mengine ambayo kwa sasa yamepotea, na kwamba huenda vitabu vya Yakobo na Waebrania (na 1 Petro) vilikuwa miongoni mwa marejeo hayo.”—The Muratorian Fragment and the Development of the Canon.

Kwa hiyo, Hati ya Muratori inathibitisha kwamba karibu vitabu vyote vilivyomo sasa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vilikuwa tayari vimekubaliwa katika karne ya pili W.K. Bila shaka, orodha inayokubalika ya vitabu vya Biblia, yaani, haki ya vitabu hivyo kukubaliwa kuwa sehemu ya Biblia, haitegemei ikiwa vimetajwa katika orodha fulani ya kale. Kinachothibitisha kwamba vitabu vya Biblia viliandikwa chini ya mwongozo wa roho takatifu ni mambo yaliyomo. Vitabu vyote vya Biblia vinathibitisha kwamba Yehova Mungu ndiye mtungaji wa vitabu hivyo, navyo vinapatana kabisa. Upatano na usawaziko uliopo kati ya vitabu 66 vya Biblia unathibitisha umoja wa vitabu hivyo na kwamba vimekamilika kabisa. Hivyo, utafaidika ukivikubali kuwa Neno la Yehova lililoandikwa kwa mwongozo wa roho yake na kuhifadhiwa hadi leo.—1 Wathesalonike 2:13; 2 Timotheo 3:16, 17.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ludovico Antonio Muratori

[Picha katika ukurasa wa 14]

Maktaba ya Ambrosian

[Picha katika ukurasa wa 15]

Hati ya Muratori

[Hisani]

Diritti Biblioteca Ambrosiana. Vietata la riproduzione. Aut. No. F 157/05

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Fragments: Diritti Biblioteca Ambrosiana. Vietata la riproduzione. Aut. No. F 157 / 05; Muratori, based on line art: © 2005 Brown Brothers