Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujua Yaliyo Sawa na Kuyatenda

Kujua Yaliyo Sawa na Kuyatenda

Simulizi la Maisha

Kujua Yaliyo Sawa na Kuyatenda

LIMESIMULIWA NA HADYN SANDERSON

Pindi moja, Yesu aliwaambia mitume wake hivi: “Ikiwa mnajua mambo haya, wenye furaha ni ninyi ikiwa mnayatenda.” (Yohana 13:17) Naam, huenda tukajua yaliyo sawa, lakini nyakati nyingine tatizo ni kuyatenda! Hata hivyo, baada ya kuishi zaidi ya miaka 80, na kutumia miaka 40 katika utumishi wa umishonari, ninasadiki kwamba maneno hayo ya Yesu ni ya kweli. Kutenda yale ambayo Mungu husema kwa kweli huleta furaha. Acheni nieleze.

KATIKA mwaka wa 1925, nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, wazazi wangu walienda kusikiliza hotuba ya Biblia katika mji wa nyumbani kwetu, Newcastle, Australia. Hotuba yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” ilimsadikisha mama yangu kwamba alikuwa amepata kweli, naye akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Hata hivyo, kupendezwa kwa baba yangu kulipoa haraka. Alipinga imani mpya ya Mama na kutishia kuondoka nyumbani ikiwa mama hangeacha imani yake. Mama alimpenda Baba na alitaka sana familia yetu iwe na umoja. Hata hivyo, Mama alijua kwamba utii kwa Mungu ulikuwa muhimu sana, naye akaazimia kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Mungu. (Mathayo 10:34-39) Baba aliondoka nyumbani, na baadaye nilimwona mara mojamoja.

Ninapokumbuka miaka ya nyuma, ninavutiwa na ushikamanifu wa mama yangu kwa Mungu. Uamuzi wake ulinisaidia mimi na dada yangu mkubwa Beulah kupata baraka za Yehova. Pia, uamuzi wake ulitufunza jambo muhimu, yaani, tunapojua yaliyo sawa, tunapaswa kujitahidi kuyatenda.

Imani Yajaribiwa

Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walijitahidi kuisaidia familia yetu. Nyanya yangu alikuja kuishi nasi, naye pia akakubali kweli ya Biblia. Nyanya yangu na mama yangu walihubiri pamoja kwa ukawaida na waliheshimiwa na watu wengine kwa sababu walikuwa wenye urafiki na sifa nzuri.

Wakati huohuo, ndugu Wakristo wenye umri mkubwa walipendezwa nami kibinafsi, nao wakanipa mazoezi mazuri. Punde si punde, nilijifunza kutumia kadi ya kutoa ushuhuda ili kuwahubiria watu kwa urahisi nyumbani mwao. Pia, nilichezesha rekodi za hotuba za Biblia kwenye gramafoni ndogo na nikashiriki kubeba mabango katika barabara kuu ya mji. Haikuwa rahisi, kwa kuwa nilijitahidi kushinda woga wa mwanadamu. Hata hivyo, nilijua yaliyokuwa sawa na niliazimia kuyatenda.

Baada ya kumaliza shule, nilianza kufanya kazi katika benki moja. Kazi hiyo ilitia ndani kutembelea matawi mbalimbali ya benki katika jimbo lote la New South Wales. Ingawa kulikuwa na Mashahidi wachache katika sehemu hiyo ya nchi, mazoezi niliyopata yalinisaidia kuimarisha imani yangu. Mama aliniandikia barua zenye kutia moyo ambazo ziliniimarisha kiroho.

Barua hizo zilifika kwa wakati unaofaa. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimeanza, nami nikaamrishwa nijiandikishe jeshini. Msimamizi wa benki alikuwa mshiriki wa kanisa mwenye bidii na kamanda wa jeshi wa eneo hilo. Nilipoeleza msimamo wangu wa kutokuwamo kwa Kikristo, aliniwekea masharti, yaani, niache dini yangu au kazi! Mambo yalipamba moto nilipofika kwenye kituo cha kuwaandikisha wanajeshi. Msimamizi huyo alikuwapo na aliniangalia kwa makini sana nilipokaribia mahali pa kujiandikisha. Nilipokataa kutia sahihi karatasi za kujiandikisha jeshini, maofisa wakawa wenye uhasama. Ulikuwa wakati mgumu, lakini niliazimia kutenda yaliyo sawa. Yehova alinisaidia kuwa mtulivu na imara. Baadaye, nilipojua kwamba watu fulani wakatili walikuwa wakinitafuta, nilikusanya vitu vyangu na kupanda gari-moshi bila kukawia!

Baada ya kurudi Newcastle, nilipelekwa mbele ya mahakama ili kuhojiwa nikiwa pamoja na ndugu wengine saba waliokataa kufanya utumishi wa kijeshi. Hakimu alituhukumu miezi mitatu ya kazi ya kulazimishwa gerezani. Ingawa halikuwa jambo la kupendeza kuwa gerezani, nilipata baraka kwa kutenda yaliyo sawa. Baada ya kufunguliwa kwetu, mmoja wa wafungwa aliyeitwa Hilton Wilkinson, aliyekuwa Shahidi mwenzangu, alinipa kazi katika studio yake ya kupiga picha. Hapo ndipo nilikutana na yule ambaye angekuwa mke wangu, Melody, aliyefanya kazi ya kuwapokea wageni kwenye studio hiyo. Punde baada ya kufunguliwa, nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova.

Kujiwekea Mradi wa Utumishi wa Wakati Wote

Baada ya kufunga ndoa, mimi na Melody tulifungua studio yetu ya kupiga picha huko Newcastle. Punde si punde, tulikuwa na kazi nyingi sana hivi kwamba afya na hali yetu ya kiroho ilianza kuzorota. Wakati huo, Ted Jaracz, ambaye alikuwa akitumika kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Australia na ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alizungumza nasi kuhusu miradi yetu ya kiroho. Baada ya mazungumzo hayo, tuliamua kuuza studio yetu na kurahisisha maisha yetu. Mnamo mwaka wa 1954, tulinunua trela ndogo, nasi tukahamia jiji la Ballarat katika jimbo la Victoria, tukaanza kutumika tukiwa mapainia, au waeneza-injili wa wakati wote.

Tulipokuwa tukitumika pamoja na kutaniko dogo la Ballarat, Yehova alibariki jitihada zetu. Kwa muda wa miezi 18, idadi ya watu waliohudhuria mikutano ilipanda toka 17 hadi 70. Kisha, tukapokea mwaliko wa kuanza huduma ya kusafiri, au kazi ya mzunguko, katika jimbo la Australia Kusini. Kwa miaka mitatu iliyofuata, tulifurahia kutembelea makutaniko katika jiji la Adelaide na maeneo ya Mto Murray yenye kutokeza matunda na divai. Maisha yetu yalikuwa yamebadilika kabisa! Tulifurahi kutumika pamoja na ndugu na dada zetu wapendwa. Hiyo kwa kweli ilikuwa thawabu ya kutenda yale tuliyojua ni sawa!

Kazi ya Umishonari

Katika mwaka wa 1958, tulijulisha ofisi ya tawi ya Australia nia yetu ya kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Mapenzi ya Kimungu” huko New York City baadaye mwaka huo. Walitujibu kwa kututumia fomu kwa ajili ya shule ya umishonari ya Gileadi huko Marekani. Kwa kuwa tulikuwa na zaidi ya miaka 30, tulifikiri kwamba tulikuwa tumepitisha umri wa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Hata hivyo, tulituma fomu zetu nasi tukaalikwa kuhudhuria darasa la 32. Kabla ya kumaliza masomo, tulipata mgawo wetu wa umishonari wa kwenda India! Licha ya kuwa na wasiwasi mwanzoni, tulitaka kutenda yaliyo sawa na hivyo tukakubali kwa furaha mgawo wetu.

Tulisafiri kwa meli na kufika Bombay (ambayo sasa ni Mumbai) mapema asubuhi moja mnamo 1959. Mamia ya wafanyakazi walikuwa wamelala nje mahali pa kushukia. Harufu mbaya ilijaa hewani. Jua lilipochomoza, tulianza kufahamiana na mazingira yetu mapya. Hatukuwahi kuhisi joto kama hilo kabla ya wakati huo! Wenzi wa ndoa wamishonari, Lynton na Jenny Dower, ambao tulifanya nao kazi ya upainia huko Ballarat, walitukaribisha. Walitupeleka kwenye ofisi ya tawi ya India, nyumba ndogo iliyokuwa karibu na katikati ya jiji. Kulikuwa na Wanabetheli sita tu walioishi katika nyumba hiyo. Ndugu Edwin Skinner, ambaye alitumika akiwa mmishonari nchini India tangu mwaka wa 1926, alitushauri tununue mifuko miwili kwa ajili ya safari kabla ya kwenda katika mgawo wetu. Ilikuwa kawaida kusafiri na mifuko hiyo kwenye magari-moshi ya India.

Baada ya kusafiri kwa gari-moshi muda wa siku mbili, tulifika katika mgawo wetu huko Tiruchchirappalli, jiji lililo katika jimbo la kusini la Madras (sasa linaitwa Tamil Nadu). Huko, tulijiunga na mapainia wa pekee watatu wa India waliokuwa wakihubiri katika eneo lenye idadi ya watu 250,000. Hali ya maisha ilikuwa ya chini. Wakati mmoja, tulibaki tu na dola 4 za Marekani. Hata hivyo, pesa hizo zilipokwisha Yehova hakutuacha. Mtu mmoja aliyekuwa akijifunza Biblia alitukopesha pesa ili tukodishe nyumba ya kufanyia mikutano. Pindi moja, wakati ambapo hatukuwa na chakula, jirani mmoja mwenye fadhili alituletea mchuzi uliotiwa viungo vingi. Niliupenda mchuzi huo, lakini ulikuwa umetiwa viungo vingi sana hivi kwamba nikashikwa na kwikwi!

Katika Huduma

Ingawa baadhi ya watu huko Tiruchchirappalli walizungumza Kiingereza, wengi wao walizungumza Kitamil. Hivyo, tulifanya bidii kujifunza utangulizi rahisi katika lugha hiyo ili tuutumie katika utumishi wa shambani. Hilo lilifanya watu wengi wa eneo hilo watuheshimu.

Tulifurahia sana mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Kwa kawaida, Wahindi ni wakarimu, na wengi wao walitualika nyumbani mwao kwa ajili ya viburudisho. Kwa kuwa mara nyingi kulikuwa na joto la digrii 40 Selsiasi, tulifurahia sana ukarimu wao. Kabla ya kutoa ujumbe wetu, tulionyesha fadhili kwa kuzungumzia mambo ya kibinafsi. Mara nyingi wenye nyumba walituuliza hivi mimi na mke wangu: “Mnatoka wapi? Je, mna watoto? Kwa nini hamna watoto?” Walipojua kwamba hatukuwa na watoto, mara nyingi walituambia kwamba wangetuonyesha daktari fulani mwenye ujuzi! Hata hivyo, mazungumzo hayo yalituwezesha kujitambulisha na kueleza umuhimu wa kazi yetu ya kufundisha watu Biblia.

Watu wengi tuliohubiria walikuwa wa dini ya Kihindu, dini ambayo ina mafundisho yanayotofautiana sana na ya Ukristo. Badala ya kubishana na watu kuhusu falsafa ngumu za dini ya Kihindu, tulihubiri tu habari njema ya Ufalme wa Mungu, nasi tukapata matokeo mazuri. Baada ya miezi sita, karibu watu 20 walianza kuhudhuria mikutano kwenye makao yetu ya wamishonari. Mmoja kati ya watu hao aliyeitwa Nallathambi alikuwa injinia. Yeye na kijana wake, Vijayalayan, baadaye waliwasaidia watu 50 hivi kuwa watumishi wa Yehova. Pia, Vijayalayan alitumika kwa muda kwenye ofisi ya tawi ya India.

Kusafiri

Tulikuwa tumekaa India kwa muda usiozidi miezi sita hivi nilipoalikwa kutumika nikiwa mwangalizi wa kwanza wa wilaya nchini. Hilo lilitia ndani kusafiri India yote, kutayarisha makusanyiko na kufanya kazi pamoja na vikundi tisa vya lugha mbalimbali. Ilikuwa kazi ngumu. Kwa kuwa hatungerudi nyumbani kwa miezi sita, tuliingiza mavazi yetu na vifaa vyetu katika masanduku ya mabati na katika ile mifuko tuliyokuwa tukisafiri nayo kwa ukawaida, kisha tukaanza safari kutoka jiji la Madras (sasa Chennai) kwa gari-moshi. Kwa kuwa ukubwa wa eneo la wilaya ulikuwa kilometa 6,500 hivi za mraba, tulisafiri kila wakati. Pindi moja, tulimaliza kusanyiko Jumapili, kusini mwa jiji la Bangalore. Kisha, tukasafiri kaskazini hadi Darjeeling chini ya Milima ya Himalaya ili kusimamia kusanyiko lingine juma lililofuata. Safari hiyo ya kwenda Darjeeling ilikuwa ya kilometa 2,700 hivi, na tulitumia magari-moshi matano.

Katika safari zetu za kwanza, tulifurahia kuonyesha sinema The New World Society in Action (La Société du Monde Nouveau en Action). Sinema hiyo iliwasaidia watu kujua vizuri kazi inayofanywa na watumishi wa Yehova ulimwenguni pote. Mara nyingi, mamia ya watu walihudhuria maonyesho hayo ya sinema. Pindi moja, tulionyesha sinema hiyo kwa kikundi kimoja kilichokusanyika kando ya barabara. Sinema ilipokuwa ikiendelea, mawingu ya dhoruba yalitanda angani. Kwa kuwa wakati mmoja umati ulikuwa umefanya ghasia sinema ilipokatizwa, niliamua kuendelea kuonyesha sinema hiyo lakini kwa kasi. Tulishukuru kwamba sinema ilimalizika bila tatizo wakati matone ya kwanza ya mvua yalipoanza kuanguka.

Miaka iliyofuata, mimi na Melody tulisafiri karibu sehemu zote za India. Kwa kuwa kila eneo lilikuwa na chakula, mavazi, lugha, na mandhari tofauti, ilikuwa kana kwamba unasafiri kutoka nchi moja hadi nyingine. Bila shaka, Yehova ameumba viumbe wa ajabu wa aina mbalimbali! Hiyo ni kweli pia kuhusu wanyama wa India. Pindi moja, tulipokuwa tumepiga kambi katika msitu huko Nepal, tulimwona chui mkubwa mwenye milia. Alikuwa mnyama maridadi. Kumwona mnyama huyo kuliimarisha tamaa yetu ya kuwa katika Paradiso, ambako mwishowe kutakuwa amani kati ya wanadamu na wanyama.

Mabadiliko ya Kitengenezo

Katika siku hizo za mapema, akina ndugu huko India walihitaji kujipatanisha na utaratibu wa tengenezo la Yehova. Katika makutaniko fulani, wanaume walikaa upande mmoja wa jumba la mikutano na wanawake upande ule mwingine. Mara nyingi mikutano haikuanza kwa wakati. Mahali fulani, kengele ilipigwa kwa sauti ili kuwaita wahubiri kwa ajili ya mikutano. Katika maeneo mengine, wahubiri waliangalia jua ili kufahamu wakati wa kwenda mikutanoni. Makusanyiko na ziara za waangalizi wanaosafiri hazikufanywa kwa ukawaida. Akina ndugu walikuwa tayari kufanya yaliyokuwa sawa, lakini walihitaji kuzoezwa.

Katika mwaka wa 1959, tengenezo la Yehova lilianzisha Shule ya Huduma ya Ufalme. Programu hiyo ya mazoezi ya ulimwenguni pote iliwasaidia waangalizi wa mizunguko, mapainia wa pekee, wamishonari, na wazee wa makutaniko kutimiza vizuri zaidi madaraka yao ya Kimaandiko. Shule hiyo ilipoanza huko India mnamo Desemba 1961, nilipata pendeleo la kufundisha. Hatua kwa hatua, matokeo ya mazoezi hayo yalifaidi makutaniko yote nchini, nayo yakafanya maendeleo ya haraka. Ndugu walipojua yaliyokuwa sawa, roho ya Mungu iliwachochea kuyatenda.

Pia, makusanyiko makubwa yaliwatia moyo na kuwaunganisha akina ndugu. Moja kati ya hayo ni Kusanyiko la Kimataifa la “Habari Njema za Milele” lililofanywa huko New Delhi mwaka wa 1963. Mashahidi kutoka sehemu mbalimbali za India walisafiri maelfu ya kilometa ili kuhudhuria kusanyiko hilo. Wengi walitumia pesa zao zote ili kusafiri. Kwa kuwa wajumbe 583 kutoka nchi nyingine 27 walikuwapo pia, ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Mashahidi wenyeji kukutana na kushirikiana na ndugu wengi wageni.

Katika mwaka wa 1961, mimi na Melody tulialikwa kutumika Betheli huko Bombay, ambako baadaye nilitumika nikiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Mapendeleo mengine yalifuata. Kwa miaka mingi, nilitumika nikiwa mwangalizi wa eneo la dunia katika Asia na Mashariki ya Kati. Kwa kuwa kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku katika nchi nyingi za maeneo hayo, wahubiri wa nchi hizo walihitaji kuwa “wenye kujihadhari kama nyoka na hata hivyo wasio na hatia kama njiwa.”—Mathayo 10:16.

Ongezeko na Mabadiliko

Tulipofika mara ya kwanza nchini India mwaka wa 1959, kulikuwa na wahubiri wenye kutenda 1,514. Leo, idadi hiyo imeongezeka kufikia zaidi ya 24,000. Ili kukabiliana na ukuzi huo, tulihamia makao mapya ya Betheli mara mbili, huko Bombay na karibu na Bombay. Kisha, mnamo Machi 2002, familia ya Betheli ilihama tena, mara hii katika majengo mapya yaliyojengwa karibu na Bangalore, kusini mwa India. Kwa sasa, majengo hayo mapya yana Wanabetheli 240 na baadhi yao wanatafsiri vichapo vya Biblia katika lugha 20.

Ingawa mimi na Melody tulitazamia kwa hamu kuhamia Bangalore, matatizo ya afya yalitulazimu kurudi Australia mnamo 1999. Kwa sasa, tunatumika katika Betheli ya Sydney. Hata ingawa tulitoka India, bado upendo kwa ndugu zetu wapendwa na watoto wetu wa kiroho wa nchi hiyo ni wenye nguvu sikuzote. Sisi hufurahi sana kupokea barua kutoka kwao!

Tunapokumbuka miaka zaidi ya 50 ya utumishi wa wakati wote, mimi na Melody tunahisi tumebarikiwa sana. Zamani tulifanya kazi ya kuwapiga watu picha, lakini tulifanya uamuzi bora kwa kufanya kazi ya kuwasaidia watu wabaki katika kumbukumbu ya Mungu. Tumejionea mambo mengi yenye kupendeza sana kwa sababu ya uamuzi wetu wa kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani! Naam, kutenda yale ambayo Mungu husema ni sawa huleta furaha kwelikweli.

[Ramani katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

INDIA

New Delhi

Darjeeling

Bombay (Mumbai)

Bangalore

Madras (Chennai)

Tiruchchirappalli

[Picha katika ukurasa wa 13]

Hadyn na Melody, mwaka wa 1942

[Picha katika ukurasa wa 16]

Familia ya Betheli ya India, mwaka wa 1975