Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Esta

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Esta

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Esta

BILA shaka, mpango huo utafaulu. Mpango wa kuwaangamiza Wayahudi utatekelezwa bila tatizo lolote. Kwa siku moja iliyokuwa imepangiwa kimbele, Wayahudi wote wanaoishi katika milki hiyo, inayoanzia India hadi Ethiopia, wataangamizwa. Hivyo ndivyo aliyepanga njama hiyo anavyofikiri. Hata hivyo, kuna jambo ambalo amesahau. Mungu wa mbinguni anaweza kuwakomboa watu wake aliowachagua kutoka katika hatari yoyote. Ukombozi huo umerekodiwa katika kitabu cha Biblia cha Esta.

Kitabu cha Esta kinazungumzia matukio ya miaka 18 hivi ya wakati wa utawala wa Mfalme wa Uajemi, Ahasuero au Shasta wa Kwanza, nacho kiliandikwa na mzee Myahudi aliyeitwa Mordekai. Masimulizi hayo yanaonyesha jinsi Yehova anavyowaokoa watu wake kutokana na njama za maadui wao, hata ingawa watumishi wake wametawanyika kotekote katika milki kubwa. Leo, habari hiyo inaimarisha imani ya watu wa Yehova wanaomtolea utumishi mtakatifu katika nchi 235. Isitoshe, watu wanaozungumziwa katika kitabu cha Esta wanatutolea mifano tunayoweza kuiga na ile ambayo tunapaswa kuepuka. Bila shaka, “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—Waebrania 4:12.

NI LAZIMA MALKIA AINGILIE KATI

(Esta 1:1–5:14)

Katika mwaka wake wa tatu wa utawala (493 K.W.K.), Mfalme Ahasuero anafanya karamu ya kifalme. Malkia Vashti anayejulikana kwa urembo wake, anamchukiza sana mfalme na anapoteza cheo chake. Hadasa, msichana Myahudi, anachaguliwa miongoni mwa mabikira wote warembo wa nchi ili achukue mahali pake. Akifuata maagizo ya Mordekai, binamu wake, msichana huyo hajitambulishi kama Myahudi bali anatumia jina la Kiajemi, yaani, Esta.

Punde si punde, mtu mmoja mwenye majivuno anayeitwa Hamani, anainuliwa na kupewa cheo cha waziri mkuu. Hamani anakasirika kwa sababu Mordekai anakataa ‘kuinama na kumsujudia,’ hivyo anapanga njama ya kuwaangamiza Wayahudi wote katika Milki ya Uajemi. (Esta 3:2) Hamani anamsihi Ahasuero akubaliane naye, na anafaulu kumfanya mfalme atoe amri ya mauaji hayo. Mordekai anavaa “nguo za magunia na majivu.” (Esta 4:1) Lazima Esta aingilie kati. Anamwalika mfalme na waziri wake mkuu kwenye karamu ya faragha. Wanafurahia kuhudhuria, naye Esta anawaomba warudi kwenye karamu nyingine siku inayofuata. Hamani anafurahi sana. Hata hivyo, anakasirika sana kwa sababu Mordekai amekataa kumpa heshima. Hamani anapanga njama ya kumuua Mordekai kabla ya karamu siku inayofuata.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:3-5—Je, karamu hiyo ilichukua siku 180? Andiko hilo halisemi kwamba karamu hiyo iliendelea kwa muda huo lakini kwamba mfalme aliwaonyesha wakuu utajiri na uzuri wa ufalme wake wenye utukufu kwa muda wa siku 180. Labda mfalme huyo alitumia tukio hilo la muda mrefu kuonyesha utukufu wake ili kuwapendeza wakuu na kuwasadikisha kwamba ana uwezo wa kutekeleza mipango yake. Hivyo, huenda mstari wa 3 na wa 5 unarejelea karamu ya siku saba iliyofanywa mwishoni mwa mkutano huo wa siku 180.

1:8—Ni katika njia gani ‘hakuna aliyekuwa akilazimishwa kuhusu wakati wa kunywa kulingana na sheria’? Pindi hii, Mfalme Ahasuero hakufuata desturi fulani inayodhaniwa kuwa ya Kiajemi ambapo watu waliambiana kiasi ambacho wanapaswa kunywa katika mikutano kama hiyo. Kitabu kimoja kinasema: “Wangekunywa kadiri walivyopenda.”

1:10-12—Kwa nini Malkia Vashti alizidi kukataa kuja kwa mfalme? Wasomi fulani hudokeza kwamba malkia huyo alikataa kutii kwa sababu hakutaka kujiaibisha mbele ya wageni wa mfalme waliokuwa wamelewa. Au huenda malkia huyo aliyekuwa mrembo kwa nje hakuwa mtiifu. Ingawa Biblia haitaji nia yake ya kutojitiisha, wanaume wenye hekima wa wakati huo waliona kwamba kutomtii mume wake kulikuwa jambo zito na mfano mbaya wa Vashti ungewaathiri wake wote katika mikoa ya Uajemi.

2:14-17—Je, Esta alifanya uasherati na mfalme? La hasha. Masimulizi yanasema kwamba asubuhi wale wanawake wengine walioletwa kwa mfalme walirudishwa katika nyumba ya pili wakiwa chini ya uangalizi wa towashi wa mfalme aliyekuwa “mlinzi wa masuria.” Hivyo, mwishowe wanawake waliokaa na mfalme wakati wa usiku wakawa masuria wake, au wake wa ziada. Hata hivyo, Esta hakupelekwa katika nyumba ya masuria baada ya kutoka kwa mfalme. Esta alipopelekwa mbele ya Ahasuero, ‘mfalme alimpenda Esta kuliko wale wanawake wengine wote, hata akapata kibali na fadhili zenye upendo kuliko wale mabikira wengine wote.’ (Esta 2:17) Esta alipataje “kibali na fadhili zenye upendo” za Ahasuero? Kwa njia ileile aliyopata kibali cha wengine. “Huyo mwanamke kijana akawa mwenye kupendeza machoni [pa Hegai], akapata fadhili zenye upendo mbele yake.” (Esta 2:8, 9) Esta alipata kibali mbele ya Hegai kwa sababu ya mambo ambayo Hegai alikuwa ameona, yaani, sura yake na sifa zake nzuri. Kwa kweli, “Esta alikuwa akizidi kupata kibali machoni pa kila mtu aliyemwona.” (Esta 2:15) Vivyo hivyo, mfalme alipendezwa na sifa za Esta na hivyo akampenda.

3:2; 5:9—Kwa nini Mordekai alikataa kumsujudia Hamani? Halikuwa kosa kwa Waisraeli kutambua cheo cha mtu mwenye mamlaka kwa kusujudu. Hata hivyo, katika kisa cha Hamani, mengi zaidi yalihusika. Hamani alikuwa Mwagagi, labda Mwamaleki, na Yehova alikuwa amewatia alama Waamaleki ili wakatiliwe mbali. (Kumbukumbu la Torati 25:19) Mordekai alijua kwamba kumsujudia Hamani kungemaanisha kukosa utimilifu kwa Yehova. Alikataa katakata na kusema kwamba alikuwa Myahudi.—Esta 3:3, 4.

Mambo Tunayojifunza:

2:10, 20; 4:12-16. Esta alikubali mwongozo na shauri kutoka kwa mwabudu mkomavu wa Yehova. Ni jambo la hekima ‘kuwatii wale wanaoongoza katikati yetu na kuwanyenyekea.’—Waebrania 13:17.

2:11; 4:5. Tunapaswa ‘kuendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yetu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’—Wafilipi 2:4.

2:15. Esta alionyesha kiasi na kujizuia. Hakuomba vito zaidi au mavazi bora zaidi kuliko yale aliyopewa na Hegai. Esta alipata kibali cha mfalme kwa sababu ya “yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole.”—1 Petro 3:4.

2:21-23. Esta na Mordekai waliweka mfano bora wa ‘kujitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa.’—Waroma 13:1.

3:4. Katika hali fulani, huenda likawa jambo la hekima kutojitambulisha, kama vile Esta alivyofanya. Hata hivyo, tunapolazimika kuchukua msimamo unaohusu masuala muhimu kama vile enzi kuu ya Yehova na utimilifu wetu, hatupaswi kuogopa kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova.

4:3. Tunapokabili majaribu, tunapaswa kumwomba Yehova atuimarishe na kutupa hekima.

4:6-8. Mordekai alitafuta suluhisho la kisheria kuhusiana na njama ya Hamani.—Wafilipi 1:7.

4:14. Mordekai aliweka mfano bora sana katika kumtumaini Yehova.

4:16. Akimtegemea Yehova kabisa, Esta alikabili kwa imani na ujasiri hali ambayo ingefanya auawe. Ni muhimu kujizoeza kumtegemea Yehova wala tusijitegemee.

5:6-8. Ili apate kibali cha Ahasuero, Esta alimwalika kwa karamu ya pili. Alitenda kwa busara, kama tunavyopaswa kutenda.—Methali 14:15.

MABADILIKO YAFUATANA

(Esta 6:1–10:3)

Muda si muda, hali inabadilika. Hamani anatundikwa juu ya mti aliokuwa ameutengeneza kwa ajili ya Mordekai, na hivyo aliyepaswa kuuawa anakuwa waziri mkuu! Namna gani ile njama ya kuwaua Wayahudi? Hiyo pia inakomeshwa.

Esta aliye mwaminifu anazungumza tena. Akihatarisha maisha yake, anaenda kwa mfalme na kumsihi azuie njama iliyokuwa imepangwa na Hamani. Ahasuero anajua kinachopaswa kufanywa. Kwa hiyo, siku ya kutekeleza njama hiyo inapofika, wale waliotaka kuwaua Wayahudi ndio wanaouawa bali si Wayahudi. Mordekai anaagiza Sherehe ya Purimu ifanywe kila mwaka ili kukumbuka ukombozi huo mkuu. Akiwa wa pili kwa Mfalme Ahasuero, Mordekai ‘anafanya kazi kwa ajili ya mema ya watu wake na kusema amani kwa uzao wao wote.’—Esta 10:3.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

7:4Kuangamizwa kwa Wayahudi kungemleteaje “mfalme hasara”? Kwa kutaja kwa busara uwezekano wa kuwauza Wayahudi kama watumwa, Esta alimwonyesha mfalme hasara ambayo ingesababishwa ikiwa Wayahudi wangeangamizwa. Vipande 10,000 vya fedha ambavyo Hamani alikuwa ameahidi havingeleta faida kubwa katika hazina ya mfalme kuliko utajiri ambao ungepatikana ikiwa Hamani angepanga njama ya kuwauza Wayahudi utumwani. Ikiwa njama hiyo ingetekelezwa, malkia pia angeangamizwa.

7:8—Kwa nini maofisa wa makao ya mfalme waliufunika uso wa Hamani? Huenda hiyo ilikuwa ishara ya aibu au mabaya ambayo yangempata. Kulingana na kitabu kimoja, “wakati mwingine watu wa kale walifunika vichwa vya watu ambao walikuwa karibu kuuawa.”

8:17—Ni kwa njia gani ‘watu wengi wa nchi walikuwa wakijitangaza wenyewe kuwa Wayahudi’? Yaelekea Waajemi wengi waligeuza imani na kuwa wafuasi wa dini ya Wayahudi wakifikiri kwamba kubatilishwa kwa ile amri iliyokuwa imetolewa kulithibitisha kwamba Wayahudi walikuwa na kibali cha Mungu. Kanuni hiyohiyo inatumika katika utimizo wa unabii fulani katika kitabu cha Zekaria. Unabii huo unasema hivi: “Watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’”—Zekaria 8:23.

9:10, 15, 16—Ingawa amri iliidhinisha kupora nyara, kwa nini Wayahudi hawakuzichukua? Kutochukua kulionyesha wazi kwamba kusudi lao hasa lilikuwa kuwaokoa watu wao wala si kujitajirisha.

Mambo Tunayojifunza:

6:6-10. “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.”—Methali 16:18.

7:3, 4Je, sisi hujitambulisha kwa ujasiri kuwa Mashahidi wa Yehova, hata ikiwa kufanya hivyo kunaweza kufanya tuteswe?

8:3-6. Tunaweza na tunapaswa kuomba mamlaka za kiserikali na za mahakama zitulinde kutokana na adui zetu.

8:5. Kwa busara Esta hakutaja daraka la mfalme katika amri hiyo ya kuwaangamiza Wayahudi. Vivyo hivyo, tunahitaji kuwa na busara tunapowahubiria wakuu wa serikali.

9:22. Hatupaswi kuwasahau walio maskini miongoni mwetu.—Wagalatia 2:10.

Yehova Atatoa “Msaada na Ukombozi”

Mordekai anadokeza kwamba Esta alipata utukufu wa kifalme ili kutimiza kusudi la Mungu. Wanapotishwa, Wayahudi wanafunga na kusali ili wapate msaada. Malkia anaenda mbele ya mfalme bila kualikwa na kila mara anapokewa vizuri. Mfalme hawezi kulala hasa katika usiku huo muhimu. Bila shaka, kitabu cha Esta kinazungumzia njia za Yehova za kuongoza mambo kwa faida ya watu wake.

Masimulizi hayo yenye kusisimua ya Esta yanatutia moyo hasa sisi tunaoishi “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) “Katika siku za mwisho,” au wakati wa mwisho unapokaribia kwisha, Gogu wa Magogu, Shetani Ibilisi, atawashambulia watu wa Yehova. Lengo lake hasa ni kuondolea mbali waabudu wa kweli. Lakini kama ilivyokuwa katika siku za Esta, Yehova atatoa “msaada na ukombozi” kwa ajili ya waabudu wake.—Ezekieli 38:16-23; Esta 4:14.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Esta na Mordekai mbele ya Ahasuero