Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mtume Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba wanawake wanapaswa ‘kukaa kimya katika makutaniko’?

Paulo aliwaandikia Wakristo wa kutaniko la Korintho hivi: “Kama ilivyo katika makutaniko yote ya watakatifu, wanawake na wakae kimya katika makutaniko, kwa maana hairuhusiwi kwao kusema.” (1 Wakorintho 14:33, 34) Ili tuelewe vizuri maneno hayo, ni muhimu tuchunguze muktadha wa shauri hilo la Paulo.

Kwenye 1 Wakorintho sura ya 14, Paulo alizungumzia mambo yanayohusiana na mikutano ya kutaniko la Kikristo. Alieleza kuhusu mambo yaliyopaswa kuzungumziwa kwenye mikutano hiyo na akapendekeza jinsi ilivyopaswa kuendeshwa. (1 Wakorintho 14:1-6, 26-34) Zaidi ya hayo, alikazia kusudi la mikutano ya Kikristo, yaani, “ili kutaniko lijengwe.”—1 Wakorintho 14:4, 5, 12, 26.

Agizo la Paulo kuhusu “kukaa kimya” linarudiwa mara tatu kwenye 1 Wakorintho sura ya 14. Kila mara, linatolewa kwa kikundi tofauti kutanikoni, lakini katika pindi zote hizo, linatolewa kwa sababu ileile, yaani, ili ‘mambo yote yatendeke kwa adabu na kwa mpango.’—1 Wakorintho 14:40.

Kwanza, Paulo alisema: “Mtu akisema kwa lugha, na wawe wawili au, ikiwa ni zaidi, watatu, wasipite hapo, na kwa zamu; na mtu fulani atafsiri. Lakini ikiwa hakuna mtafsiri, na akae kimya katika kutaniko na aseme moyoni mwake mwenyewe na kwa Mungu.” (1 Wakorintho 14:27, 28) Hilo halikumaanisha kwamba mtu huyo hakupaswa kamwe kusema kwenye mikutano, lakini lilimaanisha kwamba kulikuwa na nyakati ambapo alipaswa kukaa kimya. Ni wazi kwamba kusudi la mikutano, ambalo ni kujengana, lisingetimizwa ikiwa mtu huyo angezungumza katika lugha isiyoeleweka.

Pili, Paulo alisema: “Manabii wawili au watatu na waseme, na wale wengine waitambue maana. Lakini ikiwa kuna ufunuo kwa mwingine wakati ameketi hapo, yule wa kwanza na akae kimya.” Hilo halikumaanisha kwamba yule nabii wa kwanza hakupaswa kusema kwenye mikutano, lakini linamaanisha tu kwamba nyakati nyingine alihitaji kukaa kimya. Kisha, yule aliyepata ufunuo kwa njia ya kimuujiza angehutubia kutaniko, na kusudi la mkutano lingetimizwa, yaani, “wote watiwe moyo.”—1 Wakorintho 14:26, 29-31.

Tatu, Paulo alisema hivi kuhusu wanawake Wakristo peke yao: “Wanawake na wakae kimya katika makutaniko, kwa maana hairuhusiwi kwao kusema, bali na wajitiishe.” (1 Wakorintho 14:34) Kwa nini Paulo alitoa amri hiyo kwa akina dada? Aliitoa ili kuwe na utaratibu kutanikoni. Alisema hivi: “Basi, ikiwa wanataka kujifunza jambo fulani, acheni wawaulize waume zao wenyewe nyumbani, kwa maana inafedhehesha kwa mwanamke kusema katika kutaniko.”—1 Wakorintho 14:35.

Labda dada wengine walikuwa wakipinga yale yaliyosemwa kutanikoni. Shauri la Paulo liliwasaidia akina dada kuepuka roho hiyo inayosababisha mvurugo na kukubali kwa unyenyekevu mahali pao katika mpango wa Yehova wa ukichwa, hasa kuhusiana na waume zao. (1 Wakorintho 11:3) Isitoshe, kwa kukaa kimya, akina dada wangeonyesha kwamba hawakutamani daraka la kuwa walimu kutanikoni. Alipomwandikia Timotheo, Paulo alionyesha kwamba haingefaa kwa mwanamke kuwa mwalimu kutanikoni: “Simruhusu mwanamke kufundisha, wala kuwa na mamlaka juu ya mwanamume, bali kuwa kimya.”—1 Timotheo 2:12.

Je, hilo linamaanisha kwamba mwanamke Mkristo hapaswi kamwe kusema wakati wa mkutano wa kutaniko? Hapana. Wakati wa Paulo kulikuwa na pindi ambazo wanawake Wakristo, labda wakiwa wamechochewa na roho takatifu, walisali au walitoa unabii kutanikoni. Katika pindi kama hizo, walitambua mahali pao kwa kufunika vichwa vyao. * (1 Wakorintho 11:5) Isitoshe, wakati wa Paulo na pia leo, akina dada na ndugu wanahimizwa kutoa tangazo la hadharani la tumaini lao. (Waebrania 10:23-25) Zaidi ya kufanya hivyo katika mahubiri, akina dada hutangaza tumaini lao na kuwatia wengine moyo wakati wa mikutano ya kutaniko wanapoombwa kutoa maelezo yaliyotayarishwa vizuri na pia kwa kukubali migawo ya kufanya maonyesho au kutoa hotuba za wanafunzi.

Hivyo, wanawake Wakristo ‘hukaa kimya’ kwa kutojaribu kuchukua daraka la mwanamume na kufundisha kutaniko. Hawatokezi maswali yanayosababisha ubishi ambayo yanaweza kupinga mamlaka ya wale wanaofundisha kutanikoni. Kwa kutimiza daraka lao kutanikoni, dada Wakristo husaidia sana kutokeza hali ya amani ambayo hufanya “mambo yote [kwenye mikutano ya kutaniko] yatendeke kwa ajili ya kujengana.”—1 Wakorintho 14:26, 33.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Siku hizi, dada wakomavu wanafuata kielelezo hicho wakati hali zinapowalazimu kufanya mambo ambayo kwa kawaida hufanywa na mwanamume aliyebatizwa kutanikoni.—Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2002, ukurasa wa 26.