Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Wanaofuata Mafundisho ya Kristo Leo?

Ni Nani Wanaofuata Mafundisho ya Kristo Leo?

Ni Nani Wanaofuata Mafundisho ya Kristo Leo?

KATIKA sehemu nyingi watu humwona Yesu Kristo kuwa mmoja wa watu wakuu zaidi waliopata kuishi. Wengi humwona kuwa ndiye mtu mkuu zaidi. Kwa miaka 2,000 hivi, mafundisho yake yamekuwa na uvutano mkubwa katika maisha ya watu. Yamegusa “maisha ya watu wa kawaida na wenye fadhili, na kuwasukuma wengine kutoa misaada kwa wingi,” aandika Melvyn Bragg, mwandikaji Mwingereza.

Watu Wanauonaje Ukristo?

Watu wanauonaje Ukristo? Ukristo umefafanuliwa kuwa “mojawapo ya maendeleo makubwa zaidi ya kiroho ya wanadamu.” David Kelso wa Chuo Kikuu cha Glasgow Caledonian huko Scotland, alitoa maoni yake kuhusu Ukristo. Aliandika hivi: “Kwa miaka 2,000 hivi, Ukristo umepiga hatua kubwa sana katika sanaa, usanifu, falsafa, muziki, na mambo ya kijamii.”

Hata hivyo, wengine wengi wana maoni tofauti. Hawapingi maana ya Ukristo kama unavyofafanuliwa katika kamusi moja: “Dini inayoamini kuwa Mungu ni mmoja, inayofuata mafundisho ya Yesu Kristo.” (Kamusi ya Kiswahili Sanifu—Toleo la Pili) Badala yake, kinachowachukiza ni mwenendo wa mashirika ya kidini yanayodai kuwakilisha Ukristo.

Kwa mfano, mwanafalsafa Mjerumani wa karne ya 19, Friedrich Nietzsche, alisema kwamba Ukristo ndilo “kosa la mwanadamu linalodumu.” Aliandika hivi: “Ukristo ni mojawapo ya laana kubwa, upotovu mkubwa zaidi, . . . unaotumia njia yoyote mbovu, isiyo halali, na ya kichinichini ili kutosheleza malengo yake.” Yaelekea, maoni ya Nietzsche yalikuwa yamepita kiasi, lakini watu wengine wenye kufikiri wamefikia mkataa kama huo. Kwa nini? Kwa sababu, kwa karne nyingi, wale wanaodai kuwa Wakristo wametambuliwa kwa “mwenendo wao mpotovu, matendo ya ukatili na yenye kukufuru,” wala si kwa kuonyesha sifa za Yesu Kristo.

Je, Mafundisho ya Kristo Yanafuatwa Katika Ukristo?

Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kuuliza hivi: “Je, mafundisho ya Kristo bado yanafuatwa katika Ukristo?” Huenda wengine wakasema, “Bila shaka yanafuatwa. Je, Kristo hakuwaahidi wafuasi wake kwamba angekuwa pamoja nao ‘hadi mwisho wa dunia’?” (Mathayo 28:20, Neno Agano Jipya) Naam, Kristo alisema hivyo. Lakini je, alisema kwamba angekuwa pamoja na kila mtu anayedai kuwa Mkristo haidhuru mwenendo wa mtu huyo?

Kumbuka kwamba baadhi ya viongozi wa kidini wa siku za Yesu walifikiri kwamba Mungu alikuwa pamoja nao haidhuru mwenendo wao. Kwa kuwa Mungu alikuwa amewachagua Waisraeli kwa kusudi la pekee, baadhi ya viongozi wa kidini walifikiri kwamba Mungu hatawaacha hata kama wangemkosea. (Mika 3:11) Hata hivyo, mwishowe walikataa kabisa sheria na kanuni za Mungu. Kwa hiyo, Yesu Kristo aliwaambia hivi waziwazi: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:38) Mfumo wote wa kidini ulikataliwa na Mungu. Aliukataa na kuyaruhusu majeshi ya Roma yaharibu Yerusalemu, jiji lao kuu, na hekalu lake mwaka wa 70 W.K.

Je, jambo kama hilo linaweza kuupata Ukristo? Acheni tuone ni matakwa gani ambayo Yesu alihusianisha na ile ahadi yake ya kuwa pamoja na wafuasi wake hadi “mwisho wa dunia.”

[Picha katika ukurasa wa 2, 3]

Mafundisho ya Yesu Kristo yamekuwa na uvutano mkubwa kwa mamilioni ya watu ulimwenguni pote