Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafrija Zinazofaa na Zinazoburudisha

Tafrija Zinazofaa na Zinazoburudisha

Tafrija Zinazofaa na Zinazoburudisha

“Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 WAKORINTHO 10:31.

1, 2. Kwa nini pindi zenye kufurahisha zinaweza kuonwa kuwa “zawadi ya Mungu,” lakini Biblia inatoa onyo gani waziwazi?

NI JAMBO la kawaida kutaka kufanya mambo yanayotufurahisha. Mungu wetu mwenye furaha, Yehova, anataka tufurahie maisha, naye hutupa vitu vingi sana vya kutufurahisha. (1 Timotheo 1:11; 6:17) Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora . . . kuliko . . . kufurahi . . . na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.”—Mhubiri 3:12, 13.

2 Bila shaka, inaburudisha wakati mtu anapotenga wakati kufurahia na kufikiria kazi nzuri ambayo ametimiza, hasa anapofanya hivyo pamoja na watu wa familia au marafiki. Pindi kama hiyo inaweza kuonwa kuwa “zawadi ya Mungu.” Lakini, hatupaswi kuponda raha kupita kiasi eti kwa sababu Muumba ameandaa vitu vingi sana. Biblia inashutumu ulevi, ulafi, na ukosefu wa adili, na inaonya kwamba wale wanaozoea kufanya mambo hayo “hawataurithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10; Methali 23:20, 21; 1 Petro 4:1-4.

3. Ni nini kitakachotusaidia kukesha kiroho na kuitarajia siku kuu ya Yehova?

3 Katika siku hizi za mwisho zilizo hatari, Wakristo wanakabili ugumu wa kuishi kwa utimamu wa akili katika ulimwengu mbovu na kuepuka mazoea yake. (Yohana 17:15, 16) Kama ilivyotabiriwa, watu wa kizazi cha leo wamekuwa “wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu” hivi kwamba ‘hawajali’ uthibitisho unaoonyesha kwamba “dhiki kuu” inakaribia. (2 Timotheo 3:4, 5; Mathayo 24:21, 37-39) Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.” (Luka 21:34, 35) Tukiwa watumishi wa Mungu, tumeazimia kutii onyo hilo la Yesu. Tofauti na watu wa ulimwengu wasiomwogopa Mungu, sisi hujitahidi kukesha kiroho na kuitarajia siku kuu ya Yehova.—Sefania 3:8; Luka 21:36.

4. (a) Kwa nini ni vigumu kupata burudani zinazofaa? (b) Tunataka kutii shauri gani lililo kwenye Waefeso 5:15, 16?

4 Si rahisi kuepuka mazoea mabaya ya ulimwengu kwa kuwa Ibilisi ameyafanya yawe yenye kutamanika sana na yapatikane kwa urahisi. Inakuwa vigumu hasa tunapotaka kujiburudisha. Vitu vingi ambavyo ulimwengu huandaa vimekusudiwa kutosheleza “tamaa za kimwili.” (1 Petro 2:11) Burudani zisizofaa zinapatikana katika maeneo ya umma, lakini zinaweza kuingia pia nyumbani kwetu kupitia vichapo, televisheni, Intaneti, na video. Hivyo, Neno la Mungu linawashauri Wakristo hivi kwa hekima: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Waefeso 5:15, 16) Tukitii shauri hilo, hatutaruhusu burudani hatari zitushawishi, zitupotezee wakati, na hata kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova, na mwishowe tuangamizwe!—Yakobo 1:14, 15.

5. Furaha nyingi inatokana na nini?

5 Kwa kuwa Wakristo wana shughuli nyingi, mara kwa mara wanahitaji kufurahia tafrija fulani. Andiko la Mhubiri 3:4 linasema kwamba kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kurukaruka.” Hivyo, Biblia haisemi kwamba kuwa na tafrija ni kupoteza wakati. Lakini tafrija inapaswa kutuburudisha, bali si kuhatarisha hali yetu ya kiroho au kuingilia mambo ya kiroho. Wakristo wakomavu wamejionea kwamba furaha nyingi inatokana na kutoa. Wao hutanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwao na kupata ‘burudisho la kweli kwa ajili ya nafsi zao’ kwa sababu ya kukubali nira laini ya Yesu.—Mathayo 11:29, 30; Matendo 20:35.

Kuchagua Tafrija Zinazofaa

6, 7. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuamua ikiwa tafrija inafaa au haifai?

6 Tunaweza kuhakikishaje kwamba tafrija fulani inamfaa Mkristo? Wazazi huwaongoza watoto wao, na wazee husaidia pia. Hata hivyo, si lazima wengine watuambie kwamba kitabu fulani, sinema fulani, mchezo fulani, dansi fulani, au wimbo fulani haufai. Paulo alisema kwamba “nguvu . . . za ufahamu [za watu wakomavu] zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14; 1 Wakorintho 14:20) Biblia ina kanuni za kutuongoza. Dhamiri yako iliyozoezwa na Neno la Mungu itakusaidia ukiisikiliza.—1 Timotheo 1:19.

7 Yesu alisema kwamba “kwa matunda yake mti hujulikana.” (Mathayo 12:33) Ikiwa tafrija fulani inatokeza matunda yaliyooza kama vile kupenda jeuri, ukosefu wa adili, au kuwasiliana na pepo, basi inapaswa kuepukwa. Pia, ikiwa tafrija fulani inahatarisha uhai au afya, inasababisha hasara za kifedha au kumfanya mtu avunjike moyo, au ikiwa inawakwaza wengine, basi haifai. Mtume Paulo alituonya kwamba tukiumiza dhamiri za ndugu yetu tunatenda dhambi. Paulo aliandika hivi: “Ninyi mnapotenda dhambi hivyo juu ya ndugu zenu na kuiumiza dhamiri yao iliyo dhaifu, mnamtendea dhambi Kristo. Kwa hiyo, ikiwa chakula kinamkwaza ndugu yangu, mimi sitakula nyama tena kamwe, ili nisije nikamkwaza ndugu yangu.”—1 Wakorintho 8:12, 13.

8. Michezo ya kompyuta na video ina hatari gani?

8 Michezo mingi ya kompyuta na video inapatikana madukani. Baadhi ya michezo hiyo inaweza kufurahisha na kuburudisha bila kusababisha hatari yoyote, lakini michezo mingi ya aina hiyo inazidi kuonyesha mambo yanayoshutumiwa na Biblia. Ikiwa mchezo fulani unawalazimu wachezaji kulemaza au kuua au kutenda kwa njia iliyopotoka kabisa, hatupaswi kufikiri kwamba mchezo huo si hatari! Yehova anawachukia wale ‘wanaopenda jeuri.’ (Zaburi 11:5; Methali 3:31; Wakolosai 3:5, 6) Ikiwa mchezo fulani unakuchochea uwe na pupa au jeuri, unaathiri hisia zako, au kupoteza wakati wako muhimu, basi tambua kwamba mchezo huo unaweza kuhatarisha hali yako ya kiroho, na ufanye marekebisho haraka.—Mathayo 18:8, 9.

Jinsi ya Kuwa na Tafrija Zinazofaa

9, 10. Watu wenye ufahamu wanaweza kufanya nini ili kutosheleza mahitaji yao ya tafrija?

9 Nyakati nyingine Wakristo huuliza hivi: “Ni tafrija gani zinazofaa? Burudani nyingi ambazo ulimwengu huandaa hazipatani na viwango vya Biblia.” Uwe na hakika kwamba tafrija zinazofaa zinaweza kupatikana, lakini jitihada zinahitajiwa. Ili kuwa na tafrija zinazofaa, mipango mizuri inahitajiwa, hasa kwa upande wa wazazi. Wengi hufurahia tafrija katika familia na katika kutaniko. Kufurahia mlo wenye kuburudisha huku mkizungumzia matukio ya siku au habari fulani katika Biblia hufurahisha na kujenga. Mnaweza kupanga kwenda matembezi, kucheza michezo inayofaa, au kutembelea mbuga za wanyama. Tafrija hizo zinazofaa zinaweza kufurahisha na kuburudisha.

10 Mzee mmoja Mkristo na mke wake ambao wamelea watoto watatu wanasema hivi: “Tangu watoto wetu walipokuwa wachanga, tuliwauliza wachague mahali ambapo wangependa twende likizo. Nyakati nyingine, tulimwomba kila mtoto aalike rafiki yake wa karibu, na jambo hilo lilifanya likizo ifurahishe. Watoto wetu walipofanya maendeleo fulani, tulipanga tafrija. Nyakati nyingine tulialika watu wa familia na marafiki wetu katika kutaniko waje nyumbani kwetu. Nyakati nyingine, tulienda kwenye bustani fulani kula mlo na kucheza. Katika pindi nyingine, tulienda kutembea milimani, na tukatumia pindi hizo kujifunza kuhusu uumbaji wa Yehova.”

11, 12. (a) Unaweza kufanya nini kuwatia ndani wengine unapopanga tafrija mara kwa mara? (b) Wengi hukumbuka tafrija za aina gani?

11 Unapofanya mipango ya kibinafsi au ya familia ya kuwa na tafrija, je, unaweza kuwaalika wengine? Huenda wengine wanahitaji kutiwa moyo, kama vile mjane fulani, mseja fulani, au familia yenye mzazi mmoja. (Luka 14:12-14) Pia, unaweza kuwaalika wapya wachache, huku ukiwa mwangalifu wengine wasiathiriwe na uvutano wowote mbaya. (2 Timotheo 2:20, 21) Ikiwa wale ambao ni wagonjwa hawawezi kwenda matembezi, mipango inaweza kufanywa kupeleka mlo nyumbani kwao na kushiriki mlo huo pamoja nao.—Waebrania 13:1, 2.

12 Wengi hukumbuka pindi ambazo walialikwa kwenye tafrija kufurahia mlo usiogharimu pesa nyingi, kusikia jinsi wengine walivyopata kuwa Wakristo, na kusikia yale ambayo yamewasaidia kuwa waaminifu kwa Mungu. Habari za Biblia zinaweza kuzungumziwa, na wote wanaweza kuhusishwa, kutia ndani watoto. Mazungumzo hayo yanaweza kufaidi na kutia moyo bila kumfanya yeyote ahisi kwamba ameaibishwa au hafai.

13. Yesu na Paulo waliweka mfano gani katika kuonyesha na kukubali ukarimu?

13 Yesu aliweka mfano unaofaa katika kuonyesha na kukubali ukarimu. Nyakati zote alitumia pindi hizo kuwafaidi wengine kiroho. (Luka 5:27-39; 10:42; 19:1-10; 24:28-32) Wanafunzi wake wa mapema waliiga mfano wake. (Matendo 2:46, 47) Mtume Paulo aliandika hivi: “Ninatamani kuwaona ninyi, ili niwape sehemu ya zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; au, badala ya hivyo, kwamba kuwe na ubadilishanaji wa kitia-moyo kati yenu, kila mmoja kupitia imani ya mwingine, yenu na yangu pia.” (Waroma 1:11, 12) Vivyo hivyo, tafrija tunazopanga zinapaswa kuwawezesha watu kutiana moyo.—Waroma 12:13; 15:1, 2.

Vikumbusho na Tahadhari

14. Kwa nini si vizuri kuwa na tafrija zenye watu wengi sana?

14 Si jambo la hekima kuwaalika watu wengi sana kwenye tafrija kwa sababu mara nyingi inakuwa vigumu kusimamia mambo vizuri watu wanapokuwa wengi. Bila kutumia wakati wa shughuli za kiroho, familia kadhaa zinaweza kupanga kwenda matembezi au kucheza mchezo usiokazia sana mashindano. Wazee kadhaa, watumishi wa huduma, au wengine waliokomaa wanapohudhuria tafrija, wao huchangia hali nzuri na wanaweza kuifanya iwe yenye kuburudisha zaidi.

15. Kwa nini wale wanaopanga tafrija wanapaswa kuhakikisha kwamba imesimamiwa vizuri?

15 Wale wanaofanya mipango ya kuwa na tafrija wanapaswa kuhakikisha kwamba imesimamiwa vizuri. Ijapokuwa wewe hufurahia kuonyesha ukarimu, je, hutahisi vibaya ukisikia kwamba mgeni fulani alikwazwa na jambo fulani lililotukia nyumbani kwako kwa sababu ulilipuuza? Fikiria kanuni inayotajwa kwenye Kumbukumbu la Torati 22:8. Mwisraeli aliyejenga nyumba mpya alipaswa kujenga ukuta wa ukingoni kuzunguka dari lililokuwa tambarare ambalo lilitumiwa kwa ajili ya wageni. Kwa nini? “Ili usiletee nyumba yako hatia ya damu kwa sababu mtu anaweza kuanguka kutoka hapo.” Vivyo hivyo, yale unayofanya ili kuwalinda wageni wako kwenye tafrija yanapaswa kuonyesha kwamba unajali hali yao ya kimwili na ya kiroho, na unaweza kufanya hivyo bila kuweka masharti makali.

16. Ni mambo gani ya busara yanayohitaji kufikiriwa ikiwa kileo kitaandaliwa kwenye tafrija?

16 Ikiwa kileo kinaandaliwa kwenye tafrija, busara nyingi inahitajiwa. Wakristo wengi wanaopanga karamu huamua kuandaa kileo ikiwa tu wao binafsi wanaweza kusimamia vinywaji ambavyo wageni wao watatumia. Chochote kinachoweza kuwakwaza wengine au kumshawishi yeyote kunywa kupita kiasi hakipaswi kuruhusiwa. (Waefeso 5:18, 19) Huenda wageni fulani wakaamua kutokunywa kileo kwa sababu mbalimbali. Katika maeneo mengi, kuna sheria zinazoonyesha umri wa kuanza kunywa kileo, na Wakristo wanapaswa kutii sheria za Kaisari hata zikionekana kuwa ngumu kupita kiasi.—Waroma 13:5.

17. (a) Kwa nini ni muhimu mkaribishaji atumie busara anapochagua muziki utakaochezeshwa kwenye tafrija? (b) Ikiwa watu watacheza dansi kwenye tafrija, kiasi kinapaswa kuonyeshwaje?

17 Mkaribishaji wa wageni anapaswa kuhakikisha kwamba muziki, dansi, au burudani nyingine zinapatana na kanuni za Kikristo. Watu wana mapendezi mbalimbali ya muziki, na kuna muziki wa aina nyingi. Hata hivyo, miziki mingi leo hukazia roho ya uasi, ukosefu wa adili, na jeuri. Ni muhimu kuchagua muziki unaofaa. Si lazima muziki unaofaa uwe muziki taratibu, lakini kwa upande mwingine haupaswi kuwa na matusi au ukosefu wa adili wala haupaswi kuchezeshwa kwa sauti ya juu au kwa mdundo mzito. Usiache mtu ambaye haelewi umuhimu wa kudumisha kiasi kinachofaa cha sauti achague muziki utakaochezwa. Mkristo hapaswi kucheza dansi zinazopita kiasi, ambazo zinahusisha kuzungusha viuno na kutikisa matiti kwa njia inayoamsha hamu ya ngono.—1 Timotheo 2:8-10.

18. Wazazi wanaweza kuwalindaje watoto wao kwa kusimamia shughuli zao za kirafiki?

18 Wazazi Wakristo wanapaswa kuchunguza mipango ambayo imefanywa kwa ajili ya tafrija ambazo watoto wao wanaalikwa kuhudhuria, na ni jambo la hekima kuandamana na watoto wao mara nyingi. Inasikitisha kwamba wazazi fulani wamewaruhusu watoto wao kuhudhuria karamu zisizosimamiwa ambako wengine wameshawishiwa kujihusisha na ukosefu wa adili au matendo mengine mabaya. (Waefeso 6:1-4) Hata ikiwa vijana wanakaribia miaka 20 na wameonyesha kwamba wanategemeka, bado kuna uhitaji wa kuwasaidia ‘kukimbia tamaa zinazotukia ujanani.’—2 Timotheo 2:22.

19. Tunatambua jambo gani ambalo litatusaidia kukazia fikira yale tunayopaswa ‘kutafuta kwanza’?

19 Kuwa na tafrija na burudani zinazofaa na zinazoburudisha mara kwa mara kunaweza kufanya maisha yafurahishe zaidi. Yehova hatunyimi furaha hiyo, lakini tunatambua kwamba shughuli hizo za kujifurahisha hazitusaidii kujiwekea hazina zozote za kiroho mbinguni. (Mathayo 6:19-21) Yesu aliwasaidia wanafunzi wake kujua kwamba “kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu]” ndilo jambo muhimu maishani, bali si kile tunachokula wala tunachokunywa wala tunachovaa, “vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa.”—Mathayo 6:31-34.

20. Watumishi waaminifu wa Yehova wanaweza kutazamia vitu gani vyema kutoka kwa Mpaji Mkuu?

20 Naam, iwe ‘tunakula au kunywa au kufanya jambo lingine lolote,’ tunaweza kufanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu” na kumshukuru Mpaji Mkuu kwa kutupa vitu vyema ambavyo tunaweza kuvifurahia kwa kiasi. (1 Wakorintho 10:31) Katika dunia yake Paradiso inayokaribia, kutakuwa na pindi nyingi sana za kufurahia ukarimu wa Yehova, na vilevile ushirika unaofaa wa wale wote wanaofuata matakwa yake ya uadilifu.—Zaburi 145:16; Isaya 25:6; 2 Wakorintho 7:1.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini ni vigumu kwa Wakristo leo kupata burudani zinazofaa?

• Ni tafrija za aina gani ambazo zimeburudisha familia za Kikristo?

• Mtu anapaswa kutilia maanani vikumbusho gani na tahadhari gani anapofurahia tafrija zinazofaa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Chagua tafrija inayotokeza matunda yanayofaa

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wakristo hukataa tafrija za aina gani?