Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tueleze Zaidi!”

“Tueleze Zaidi!”

“Tueleze Zaidi!”

HUKO Nezlobnaya, Urusi, wanafunzi wa fasihi katika shule moja ya sekondari walikuwa wakisoma vitabu vya mwandikaji Mrusi, Mikhail Bulgakov. Kati ya vitabu hivyo kulikuwa na kimoja kinachozungumza kumhusu Yesu Kristo kwa njia inayomvunjia heshima, huku kikimtaja Shetani kuwa shujaa. Baada ya mazungumzo darasani, mwalimu aliwapa wanafunzi mtihani unaotegemea kitabu hicho. Hata hivyo, mwanafunzi mmoja anayeitwa Andrey, ambaye ni Shahidi wa Yehova mwenye umri wa miaka 16, aliomba asifanye mtihani huo kwa sababu dhamiri yake haimruhusu kusoma kitabu kama hicho. Badala yake, aliomba aandike maoni yake kumhusu Yesu Kristo. Mwalimu akakubali.

Katika maandishi yake, Andrey alieleza kwamba ingawa anaheshimu maoni ya wengine, ametambua kwamba njia bora ya kumjua Yesu ni kusoma mojawapo ya yale masimulizi manne ya Injili. Kwa kufanya hivyo, “utajifunza kuhusu maisha na mafundisho ya Yesu kama yanavyosimuliwa na watu waliomwona.” Andrey aliongeza hivi: “Tatizo lingine linahusu jinsi Shetani anavyofafanuliwa. Huenda wengine wakaliona kuwa jambo lenye kuchekesha kusoma kitabu kinachomfafanua Shetani kuwa shujaa, lakini mimi sifurahishwi na kitabu kama hicho.” Alieleza kwamba Shetani ni kiumbe mwovu wa roho mwenye nguvu ambaye alimwasi Mungu, na kutokeza uovu, huzuni, na mateso kwa wanadamu. Andrey alimalizia maandishi yake hivi: “Siamini kwamba kusoma kitabu hiki kutanifaidi. Bila shaka, simchukii Bulgakov. Lakini mimi binafsi ninapendelea kusoma Biblia ili kujifunza ukweli kumhusu Yesu Kristo.”

Mwalimu wa Andrey alifurahia sana habari hiyo hivi kwamba akamwomba atayarishe simulizi kumhusu Yesu Kristo. Andrey alikubali. Katika somo la fasihi lililofuata, Andrey alisoma simulizi hilo mbele ya wanafunzi wenzake. Alieleza kwa nini alihisi kwamba Yesu ndiye mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Kisha, akasoma sura moja kuhusu kifo cha Yesu katika kitabu cha Biblia cha Mathayo. Kwa kuwa wakati aliopewa wa kutoa simulizi lake ulielekea kwisha, Andrey alitaka kumaliza, lakini wanafunzi wenzake walimhimiza hivi: “Tueleze zaidi! Ni nini kilichotukia baadaye?” Hivyo, akaendelea kusoma simulizi la Mathayo kuhusu ufufuo wa Yesu.

Andrey alipomaliza, wanafunzi wenzake walimwuliza maswali mengi kuhusu Yesu na Yehova. Andrey anasema hivi: “Nilimwomba Yehova anipe hekima, naye akajibu sala yangu. Niliweza kujibu maswali yao yote!” Baada ya masomo, Andrey alimpa mwalimu wake nakala moja ya kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, * ambacho alikubali kwa furaha. Andrey alieleza hivi: “Alinipa maksi za juu sana kwa sababu ya simulizi langu, naye akanisifu kwa kuwa na imani yangu mwenyewe na kwa kutoona aibu kuieleza. Pia, alisema kwamba anaamini baadhi ya mafundisho yetu.”

Andrey anafurahi kwamba aliamua kufuata dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kwa kukataa kusoma habari ambazo zinamvunjia heshima Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Msimamo huo haukumlinda tu asiathiriwe na maoni yasiyopatana na maandiko, bali pia ulimpa nafasi nzuri ya kuwaeleza wengine kweli muhimu za Biblia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.