Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kila Mmoja Ataubeba Mzigo Wake Mwenyewe”

“Kila Mmoja Ataubeba Mzigo Wake Mwenyewe”

“Kila Mmoja Ataubeba Mzigo Wake Mwenyewe”

“Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—WAROMA 14:12.

1. Vijana watatu Waebrania walitimiza wajibu gani?

VIJANA watatu Waebrania wanaoishi Babiloni wanahitaji kufanya uamuzi unaohusu maisha yao. Je, waifuate sheria ya nchi hiyo kwa kuisujudia sanamu kubwa? Au je, wakatae kuabudu sanamu hiyo na kutupwa ndani ya tanuru inayowaka moto? Shadraki, Meshaki, na Abednego hawana wakati wa kushauriana na mtu mwingine, wala hawahitaji kufanya hivyo. Bila kusitasita, wanatangaza hivi: “Ujue hivi, Ee mfalme, kwamba sisi hatuitumikii miungu yako, na sanamu ambayo umeisimamisha hatutaiabudu.” (Danieli 3:1-18) Waebrania hao watatu walitimiza wajibu wao kwa kukubali kubeba mzigo wao.

2. Ni nani waliomchochea Pilato kufanya uamuzi uliomhusu Yesu Kristo, na je, hilo lilimwondolea hatia gavana huyo Mroma?

2 Karne sita baadaye, gavana anamaliza kusikiliza mashtaka ambayo yametolewa dhidi ya mtu fulani. Baada ya kuchunguza kesi hiyo, anasadiki kwamba mshtakiwa hana hatia. Hata hivyo, umati unasisitiza kwamba ni lazima mtu huyo auawe. Gavana anajaribu kukataa jambo hilo, lakini mwishowe anachochewa na umati kufanya uamuzi, na hivyo anashindwa kutimiza wajibu wa kubeba mzigo wake. Ananawa mikono na kusema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu huyu.” Kisha anatoa ruhusa mtu huyo atundikwe mtini. Naam, badala ya kutimiza wajibu wake wa kufanya uamuzi kumhusu Yesu Kristo, Pontio Pilato anawaacha wengine wamfanyie uamuzi. Hata Pilato akinawa mikono yake namna gani, hawezi kujiondolea hatia ya kumhukumu Yesu isivyo haki.—Mathayo 27:11-26; Luka 23:13-25.

3. Kwa nini hatupaswi kuacha wengine watufanyie maamuzi?

3 Namna gani wewe? Unapohitaji kufanya maamuzi, je, wewe ni kama wale Waebrania watatu, au je, unaacha wengine wakufanyie maamuzi? Si rahisi kufanya maamuzi. Ukomavu unahitajiwa ili kufanya maamuzi yanayofaa. Kwa mfano, wazazi wanahitaji kufanya maamuzi yanayofaa kwa ajili ya watoto wao wadogo. Bila shaka, si rahisi kufanya uamuzi wakati hali unayokabili ni ngumu sana na ikiwa mambo mbalimbali yanahitaji kufikiriwa kwa uangalifu. Hata hivyo, wajibu wa kufanya maamuzi si mzito kupita kiasi, na hivyo hauwezi kuhusianishwa na “mizigo mizito” au matatizo ambayo wale walio na “sifa za kustahili kiroho” wanaweza kutubebea. (Wagalatia 6:1, 2) Badala yake, kufanya maamuzi ni mzigo ambao “kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:12) Biblia inasema: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5) Basi, tunaweza kufanyaje maamuzi kwa hekima maishani? Kwanza, tunapaswa kutambua mipaka yetu tukiwa wanadamu na kujua yale yanayohitajiwa ili kutenda kwa njia inayofaa.

Takwa Muhimu

4. Tendo la Adamu na Hawa la kutotii linapaswa kutufunza jambo gani muhimu kuhusu kufanya maamuzi?

4 Mapema katika historia ya wanadamu, wenzi wa kwanza wa ndoa walifanya uamuzi uliosababisha msiba. Waliamua kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwanzo 2:16, 17) Uamuzi wao ulitegemea nini? Biblia inasema hivi: “Mwanamke akaona kwamba mti huo ulikuwa mzuri kwa chakula na kwamba ulikuwa kitu cha kutamanika kwa macho, ndiyo, mti huo ulikuwa wenye kupendeza kuutazama. Kwa hiyo akaanza kuchukua kati ya matunda yake akala. Baadaye akampa mume wake pia alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.” (Mwanzo 3:6) Uamuzi wa Hawa ulitegemea tamaa yake ya ubinafsi. Matendo yake yalimfanya Adamu amuunge mkono. Hivyo, dhambi na kifo ‘vikaenea kwa watu wote.’ (Waroma 5:12) Kutotii kwa Adamu na Hawa kunapaswa kutufundisha jambo hili muhimu kuhusu mipaka ya wanadamu: Wanadamu wasipofuata mwongozo wa Mungu, wanaweza kufanya maamuzi mabaya.

5. Yehova ametupa mwongozo gani, nasi tunapaswa kufanya nini ili tufaidike kutokana nao?

5 Lo! Tunashukuru kwamba Yehova Mungu ametupa mwongozo! Maandiko yanatuambia hivi: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake,’ iwe mtakwenda upande wa kuume au iwe mtakwenda upande wa kushoto.” (Isaya 30:21) Yehova huzungumza nasi kupitia Neno lake Biblia, ambalo liliandikwa kwa mwongozo wa roho yake. Ni lazima tujifunze Maandiko na kupata ujuzi sahihi kuyahusu. Ili tufanye maamuzi yanayofaa, tunapaswa kula “chakula kigumu [ambacho] ni cha watu wakomavu.” Pia, ‘tunapozitumia, nguvu zetu za ufahamu huzoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Tunaweza kuzoeza nguvu zetu za ufahamu kwa kutumia mambo tunayojifunza katika Neno la Mungu.

6. Ni nini kinachohitajiwa ili dhamiri yetu ifanye kazi vizuri?

6 Dhamiri tuliyorithi ni muhimu katika kufanya maamuzi. Dhamiri inaweza kutoa hukumu, na tunaweza ‘kushtakiwa au hata kutetewa’ nayo. (Waroma 2:14, 15) Hata hivyo, ili dhamiri yetu ifanye kazi vizuri tunahitaji ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kuizoeza kwa kutenda kupatana na Neno hilo. Dhamiri ambayo haijazoezwa huathiriwa kwa urahisi na mila na desturi. Mazingira yetu na maoni ya watu wengine yanaweza pia kutupotosha. Dhamiri yetu hupatwa na nini tunapoendelea kupuuza mwongozo wake na kuvunja kanuni za Mungu? Mwishowe, inaweza kutiwa alama “kama kwa chuma cha kutilia alama” na kuwa kama nyama yenye makovu, yaani, inaweza kufa ganzi. (1 Timotheo 4:2) Kwa upande mwingine, dhamiri iliyozoezwa na Neno la Mungu inaweza kutuongoza vizuri.

7. Ili tufanye maamuzi kwa hekima tunahitaji nini hasa?

7 Basi, ili tutimize wajibu wetu wa kufanya maamuzi kwa hekima tunahitaji hasa kuwa na ujuzi sahihi wa Maandiko na kufahamu jinsi tunavyoweza kuutumia. Badala ya kufanya maamuzi haraka-haraka, tunahitaji kutumia muda wa kutosha kuchunguza kanuni za Biblia na kutumia uwezo wetu wa kufikiri tunapofuata kanuni hizo. Ikiwa tuna ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na dhamiri yetu imezoezwa na Neno hilo, tutakuwa tayari kufanya maamuzi, hata tunapoombwa kufanya hivyo papo hapo kama vile Shadraki, Meshaki, na Abednego. Ili tuone jinsi uwezo wetu wa kufanya maamuzi unavyoweza kuboreshwa kwa kusonga mbele kufikia ukomavu, acheni tuchunguze mambo mawili maishani.

Tunapaswa Kushirikiana na Nani?

8, 9. (a) Ni kanuni gani zinazoonyesha umuhimu wa kuepuka mashirika mabaya? (b) Je, kuwa na mashirika mabaya humaanisha tu kushirikiana na watu wasio na maadili? Eleza.

8 Mtume Paulo aliandika hivi: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Yesu Kristo aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Baada ya kujifunza kanuni hizo, tunatambua mara moja kwamba tunahitaji kuepuka kushirikiana na waasherati, wazinzi, wezi, walevi, na watu wengine kama hao. (1 Wakorintho 6:9, 10) Isitoshe, tunapoongeza ujuzi wa kweli ya Biblia, tunatambua kwamba ni hatari kushirikiana na watu kama hao kwa kuwatazama kwenye sinema, televisheni, kompyuta, au kwa kusoma juu yao katika vitabu. Pia, ni hatari kushirikiana na “wale wanaoficha jinsi walivyo” kwenye Intaneti.—Zaburi 26:4.

9 Namna gani kuhusu kushirikiana kwa ukaribu pamoja na wale ambao huonekana kuwa safi kiadili lakini hawamwamini Mungu wa kweli? Maandiko yanatuambia hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Tunatambua kwamba mashirika mabaya hayahusishi tu watu wasio na maadili. Hivyo, ni jambo la hekima tuwe na urafiki wa karibu pamoja na wale tu wanaompenda Yehova.

10. Ni nini kitakachotusaidia kuonyesha ukomavu tunapofanya maamuzi kuhusu kushirikiana na ulimwengu?

10 Haiwezekani wala hatupaswi kuwaepuka kabisa wale walio katika ulimwengu. (Yohana 17:15) Sisi hukutana na watu ambao si waabudu wa Yehova katika huduma ya Kikristo, shuleni, na kazini. Huenda Mkristo aliyefunga ndoa pamoja na mtu ambaye si Shahidi wa Yehova akalazimika kushirikiana na ulimwengu kuliko wengine. Hata hivyo, ikiwa nguvu zetu za ufahamu zimezoezwa, tutatambua kwamba kushirikiana na ulimwengu kwa muda mfupi kwa sababu za lazima ni tofauti na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na ulimwengu. (Yakobo 4:4) Hivyo, tunaweza kuamua kwa ukomavu ikiwa tutashiriki katika shughuli za baada ya shule, kama vile michezo na dansi, na ikiwa tutahudhuria karamu na tafrija zinazopangwa kazini kwa ajili ya wafanyakazi.

Kufanya Uamuzi Kuhusu Kazi

11. Tunapaswa kufikiria nini kwanza tunapohitaji kufanya maamuzi kuhusu kazi?

11 Kutumia kanuni za Biblia kwa ukomavu hutusaidia kufanya maamuzi yanayohusu daraka letu la ‘kuwaandalia washiriki wa nyumba zetu.’ (1 Timotheo 5:8) Jambo la kwanza la kufikiria ni kazi yenyewe, yaani, mambo ambayo tutafanya katika kazi hiyo. Bila shaka, ni kosa kuchagua kazi ambayo inaunga mkono mambo yanayokatazwa waziwazi katika Biblia. Ndiyo sababu Wakristo wa kweli hawakubali kazi zinazohusisha ibada ya sanamu, wizi, kutumia damu vibaya, au mazoea mengine yasiyopatana na Maandiko. Pia, hatupaswi kusema uwongo wala kudanganya, hata mkubwa wetu kazini anapotuamuru tufanye hivyo.—Matendo 15:29; Ufunuo 21:8.

12, 13. Zaidi ya kufikiria kazi yenyewe, ni mambo gani mengine ambayo ni muhimu kufikiria tunapofanya maamuzi kuhusu kazi?

12 Namna gani ikiwa kazi yenyewe haivunji kanuni yoyote ya Biblia waziwazi? Tunapopata ujuzi zaidi kuhusu kweli na kuendelea kuzoeza nguvu zetu za ufahamu, tunatambua mambo mengine ambayo tunahitaji kufikiria. Namna gani ikiwa kazi hiyo itatuhusisha katika mazoea yasiyopatana na Maandiko, kama vile kufanya kazi ya kupokea simu katika kampuni ya mchezo wa kamari? Tunahitaji pia kufikiria chanzo cha pesa tunazolipwa na mahali ambapo tunafanya kazi hiyo. Kwa mfano, je, inafaa Mkristo ambaye ana kampuni ya ujenzi atafute kazi ya kupaka rangi kanisa la Jumuiya ya Wakristo na hivyo kuunga mkono dini ya uwongo?—2 Wakorintho 6:14-16.

13 Namna gani ikiwa mkubwa wetu kazini anataka wafanyakazi wake wafanye kazi ya kupaka rangi mahali panapotumiwa kwa ajili ya ibada ya uwongo? Katika kisa hiki, tunahitaji kufikiria mamlaka tuliyo nayo katika kazi hiyo na vilevile tutahusika kwa kadiri gani. Namna gani kuhusu kufanya kazi ambayo haivunji kanuni za Biblia, kama vile kupeleka barua kila mahali katika jamii, kutia ndani sehemu zinazoendeleza mazoea mabaya? Je, hatuwezi kutumia kanuni inayotajwa katika Mathayo 5:45 tunapofanya uamuzi kuhusu jambo hilo? Pia, tunapaswa kufikiria jinsi dhamiri yetu inavyoweza kuathiriwa tunapofanya kazi hiyo siku baada ya siku. (Waebrania 13:18) Naam, tunahitaji kuboresha nguvu zetu za ufahamu na kuzoeza dhamiri yetu tuliyopewa na Mungu ili tuweze kubeba mzigo wetu na kuonyesha kwamba tumekomaa tunapofanya maamuzi kuhusu kazi.

“Mtambue Yeye Katika Njia Zako Zote”

14. Tunapohitaji kufanya maamuzi, tunapaswa kufanya nini sikuzote?

14 Namna gani maamuzi tunayofanya kuhusu mambo mengine, kama vile kuongeza elimu ya kilimwengu au kukubali au kukataa matibabu fulani? Tunapohitaji kufanya uamuzi wowote, ni lazima tuchunguze kanuni za Biblia zinazohusika kisha tutumie uwezo wetu wa kufikiri tunapofuata kanuni hizo. Mfalme Sulemani wa Israeli la kale mwenye hekima alisema hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

15. Tunajifunza nini kuhusu kufanya maamuzi kutokana na Wakristo wa karne ya kwanza?

15 Mara nyingi, maamuzi tunayofanya huwaathiri wengine, na tunahitaji kufikiria jambo hilo pia. Kwa mfano, Wakristo wa karne ya kwanza hawakuwa chini ya wajibu wa kutokula vitu fulani vilivyokatazwa katika Sheria ya Musa. Wangeweza kuamua kula vyakula fulani ambavyo vilionwa kuwa si safi chini ya Sheria na ambavyo havikuwa na ubaya wowote. Hata hivyo, mtume Paulo aliandika hivi kuhusu nyama ambayo ilikuwa na uhusiano fulani na hekalu la sanamu: “Ikiwa chakula kinamkwaza ndugu yangu, mimi sitakula nyama tena kamwe, ili nisije nikamkwaza ndugu yangu.” (1 Wakorintho 8:11-13) Wakristo wa mapema walihimizwa wafikirie dhamiri za wengine ili wasiwakwaze. Maamuzi yetu hayapaswi kutufanya tuwe “vikwazo.”—1 Wakorintho 10:29, 32.

Tafuta Hekima Kutoka kwa Mungu

16. Sala inatusaidiaje tunapofanya maamuzi?

16 Sala ni muhimu sana tunapofanya maamuzi. Mwanafunzi Yakobo anasema hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Kwa imani, tunaweza kusali kwa Yehova na kumwomba hekima ili tufanye maamuzi yanayofaa. Tunapomweleza Mungu wa kweli mahangaiko yetu na kutafuta mwongozo wake, roho takatifu inaweza kutusaidia kuelewa vizuri zaidi maandiko tunayochunguza na kutukumbusha yale ambayo huenda tumesahau.

17. Wengine wanaweza kutusaidiaje tunapohitaji kufanya maamuzi?

17 Je, wengine wanaweza kutusaidia tunapohitaji kufanya maamuzi? Naam, Yehova ameandaa watu wakomavu kutanikoni. (Waefeso 4:11, 12) Wanaweza kuombwa mashauri, hasa ikiwa tunahitaji kufanya uamuzi mzito. Wale walio na ufahamu mwingi wa kiroho na walio na uzoefu maishani wanaweza kutuonyesha kanuni zaidi za Biblia ambazo zinahusiana na uamuzi ambao tunataka kufanya, na wanaweza kutusaidia ‘kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:9, 10) Hata hivyo, tunahitaji kukumbuka jambo hili: Hatupaswi kuacha wengine watufanyie maamuzi. Sisi ndio wenye wajibu wa kubeba mzigo.

Je, Matokeo Yatakuwa Mazuri Nyakati Zote?

18. Tunaweza kusema nini kuhusu matokeo ya uamuzi unaofaa?

18 Je, maamuzi yanayotegemea kabisa kanuni za Biblia na yanayofanywa kwa busara huwa na matokeo mazuri nyakati zote? Naam, hatimaye matokeo huwa mazuri. Hata hivyo, nyakati nyingine maamuzi yanayofaa huwa na matokeo mabaya mwanzoni. Shadraki, Meshaki, na Abednego walijua kwamba huenda wangeuawa kwa sababu ya uamuzi wao wa kutoabudu ile sanamu kubwa. (Danieli 3:16-19) Vivyo hivyo, baada ya mitume kuiambia Sanhedrini ya Wayahudi kwamba ni lazima wamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu, walipigwa viboko kabla ya kuachiliwa huru. (Matendo 5:27-29, 40) Isitoshe, matokeo ya maamuzi yoyote yanaweza kuathiriwa sana na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Tukiteseka kwa njia fulani baada ya kufanya uamuzi unaofaa, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia kuvumilia na atatubariki mwishowe.—2 Wakorintho 4:7.

19. Tunaweza kutimizaje kwa ujasiri wajibu wa kubeba mzigo wetu wenyewe tunapofanya maamuzi?

19 Hivyo basi, tunapofanya maamuzi, tunapaswa kuchunguza kanuni za Maandiko na kutumia uwezo wetu wa kufikiri tunapofuata kanuni hizo. Tunashukuru kwamba Yehova ameandaa msaada kupitia roho yake takatifu na wale waliokomaa kutanikoni! Kwa kuwa tuna mwongozo huo na maandalizi hayo, acheni tutimize kwa ujasiri wajibu wa kubeba mzigo wetu wenyewe na kufanya maamuzi kwa hekima.

Umejifunza Nini?

• Ili tufanye maamuzi yanayofaa tunahitaji nini?

• Kusonga mbele kufikia ukomavu hutusaidiaje tunapochagua watu wa kushirikiana nao?

• Tunahitaji kufikiria mambo gani muhimu tunapofanya maamuzi kuhusu kazi?

• Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia tunapofanya maamuzi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Tunajifunza jambo muhimu kutokana na kutotii kwa Adamu na Hawa

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kabla ya kufanya uamuzi muhimu, chunguza kanuni za Biblia