Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Suluhisho Pekee la Kifo!

Suluhisho Pekee la Kifo!

Suluhisho Pekee la Kifo!

MWANAMUME aliyeitwa Lazaro na dada zake, Martha na Maria, waliishi Bethania, mji uliokuwa kilometa 3 hivi kutoka Yerusalemu. Siku moja wakati Yesu rafiki yao hakuwapo, Lazaro akawa mgonjwa sana. Dada zake wakawa na wasiwasi. Wakamtumia Yesu ujumbe. Muda mfupi baada ya kupata habari hizo, Yesu alienda kumwona Lazaro. Akiwa njiani, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba alikuwa anasafiri kwenda kumwamsha Lazaro kutoka usingizini. Mwanzoni wanafunzi wake hawakumwelewa, lakini Yesu aliwaeleza waziwazi hivi: “Lazaro amekufa.”—Yohana 11:1-14.

Yesu alipofika kwenye kaburi la Lazaro, aliagiza jiwe lililokuwa kwenye mwingilio liondolewe. Baada ya kusali kwa sauti, aliamuru hivi: “Lazaro, njoo huku nje!” Kisha Lazaro akatoka nje. Mtu huyo aliyekuwa mfu kwa siku nne akafufuliwa.—Yohana 11:38-44.

Masimulizi hayo kuhusu Lazaro yanaonyesha kwamba suluhisho la kifo ni ufufuo. Lakini je, muujiza huo wa kumrudisha Lazaro kwenye uhai ulitukia kweli? Biblia inaonyesha kwamba ulitukia. Soma masimulizi kwenye Yohana 11:1-44, nawe utaona jinsi yalivyo wazi. Je, unaweza kupinga kwamba muujiza huo ulitukia? Kuupinga kunaweza kukufanya utilie shaka miujiza mingine yote ambayo imerekodiwa katika Biblia, kutia ndani kufufuliwa kwa Yesu Kristo mwenyewe. Biblia inasema: “Ikiwa Kristo hakufufuliwa, imani yenu ni bure.” (1 Wakorintho 15:17) Ufufuo ni fundisho la msingi la Maandiko. (Waebrania 6:1, 2) Lakini, neno “ufufuo” linamaanisha nini?

“Ufufuo” Unamaanisha Nini?

Neno “ufufuo” linapatikana zaidi ya mara 40 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kusimama tena.” Neno la Kiebrania linalolingana nalo linamaanisha “kuwarudisha wafu kwenye uhai.” Hata hivyo, ni nini kinachofufuliwa baada ya mtu kufa? Kile kinachofufuliwa si mwili kwa sababu unaoza na kurudi mavumbini. Si mwili uleule unaofufuliwa bali ni mtu yuleyule aliyekufa. Hivyo, ufufuo unatia ndani kurudisha maisha ya mtu, yaani, utu wake, mambo aliyofanya alipokuwa hai, na mambo yote yanayomtambulisha.

Yehova Mungu aliye na kumbukumbu kamilifu anakumbuka maisha ya watu ambao wamekufa. (Isaya 40:26) Kwa kuwa yeye ndiye Mwanzilishi wa uhai, Yehova anaweza kumfufua mtu na kumpa mwili mwingine mpya. (Zaburi 36:9) Isitoshe, Biblia inasema kwamba Yehova Mungu ‘anatamani,’ yaani, anataka sana kuwafufua wafu. (Ayubu 14:14, 15) Tunafurahi sana kujua kwamba mbali na kwamba Yehova anaweza kumfufua mtu, anatamani pia kufanya hivyo!

Yesu Kristo pia anatimiza sehemu kubwa katika kuwafufua wafu. Zaidi ya mwaka mmoja hivi baada ya kuanza huduma yake, Yesu alisema: “Kama vile Baba anavyowafufua wafu na kuwafanya hai, ndivyo Mwana pia anavyowafanya hai wale anaotaka kuwafanya hai.” (Yohana 5:21) Je, mfano wa Lazaro hauonyeshi kwamba Yesu Kristo ana nguvu na vilevile anatamani kuwafufua wafu?

Namna gani lile wazo la kwamba kuna kitu ndani ya mwanadamu kinachoendelea kuishi baada ya yeye kufa? Fundisho la ufufuo linapingana na wazo la kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu au roho. Ikiwa kuna kitu ndani yetu kinachoendelea kuishi baada ya kifo, basi kuna haja gani ya ufufuo? Martha, dada ya Lazaro, hakuamini kwamba ndugu yake alipokufa, aliendelea kuishi katika makao ya roho. Aliamini ufufuo. Yesu alipomhakikishia hivi: “Ndugu yako atafufuka,” Martha akamwambia: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:23, 24) Baada ya kurudishwa kwenye uhai, Lazaro hakueleza mambo yoyote aliyoona katika makao ya roho. Alikuwa amekufa. Biblia inasema: “Wafu, hawajui lolote kamwe. . . . Hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.”—Mhubiri 9:5, 10.

Basi, kulingana na Biblia, ufufuo ndilo suluhisho pekee la kifo. Lakini kati ya watu wote ambao wamekufa, ni nani watakaofufuliwa na wataenda wapi?

Ni Nani Watakaofufuliwa?

Yesu alisema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Kulingana na ahadi hiyo, wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho, yaani, wale walio katika kumbukumbu ya Yehova, watafufuliwa. Basi swali ni, Kati ya watu wote ambao wamekufa, ni nani walio katika kumbukumbu ya Mungu wakingojea kufufuliwa?

Kitabu cha Biblia cha Waebrania sura ya 11 kinaorodhesha majina ya wanaume na wanawake ambao walimtumikia Mungu kwa uaminifu. Wao pamoja na watumishi washikamanifu wa Mungu ambao wamekufa katika miaka ya karibuni, watafufuliwa. Namna gani watu ambao hawakuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, labda kwa sababu ya kutokuwa na ujuzi? Je, wao pia wamo katika kumbukumbu ya Mungu? Ndiyo, wengi wamo, kwa kuwa Biblia inaahidi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

Hata hivyo, kuna watu ambao hawatafufuliwa. Biblia inasema hivi: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi, lakini kuna tarajio hakika lenye kuogopesha la hukumu.” (Waebrania 10:26, 27) Watu fulani walifanya dhambi ambazo haziwezi kusamehewa. Hawamo Hadesi (kaburini), wamo Gehena, mahali pa mfano pa uharibifu wa milele. (Mathayo 23:33) Hata hivyo, tunapaswa kujihadhari tusikate kauli kwamba watu fulani watafufuliwa au hawatafufuliwa. Mungu ndiye anayeamua. Anajua ni nani walio katika Hadesi na ni nani walio katika Gehena. Kwa upande wetu, inafaa tuishi kulingana na mapenzi ya Mungu.

Ni Nani Wanaofufuliwa Kwenda Mbinguni?

Ufufuo wa Yesu Kristo ulikuwa wa pekee sana. “Aliuawa katika mwili, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.” (1 Petro 3:18) Kabla ya wakati huo, hakuna mwanadamu aliyekuwa amepata ufufuo wa namna hiyo. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni ila yule aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu.” (Yohana 3:13) Mwana wa binadamu ndiye aliyekuwa wa kwanza kufufuliwa akiwa mtu wa roho. (Matendo 26:23) Na kungekuwa na wengine baada yake. Maandiko yanasema hivi: “Kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.”—1 Wakorintho 15:23.

Kikundi kidogo cha watu, yaani, “wale walio wa Kristo,” watafufuliwa ili waishi mbinguni kwa kusudi la pekee. (Waroma 6:5) Watatawala pamoja na Kristo wakiwa “wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10) Isitoshe, watakuwa makuhani katika maana ya kwamba watashiriki kuondoa madhara ya dhambi ambayo wanadamu walirithi kutoka kwa yule mtu wa kwanza, Adamu. (Waroma 5:12) Hesabu ya wale watakaotawala na Kristo wakiwa wafalme na makuhani ni 144,000. (Ufunuo 14:1, 3) Wanapokea mwili wa aina gani wanapofufuliwa? Biblia inasema wanapokea “mwili wa roho.” Mwili huo utawawezesha kuishi mbinguni.—1 Wakorintho 15:35, 38, 42-45.

Wale walio na tumaini la kwenda mbinguni hufufuliwa wakati gani? Andiko la 1 Wakorintho 15:23 linajibu hivi: “Wakati wa kuwapo” kwa Kristo. Matukio ya ulimwengu tangu mwaka wa 1914 yanaonyesha wazi kwamba kuwapo kwa Kristo na “umalizio wa mfumo wa mambo” ulianza mwaka huo. (Mathayo 24:3-7) Hivyo, tuna sababu ya kukata kauli kwamba ufufuo wa Wakristo waaminifu walio na tumaini la kwenda mbinguni umeanza, ingawa wanadamu hawawezi kuuona. Hiyo inamaanisha kwamba mitume na Wakristo wa mapema wamefufuliwa kwenda mbinguni. Namna gani Wakristo wanaoishi sasa ambao wana tumaini hakika kutoka kwa Mungu la kutawala pamoja na Kristo mbinguni? Wanafufuliwa kana kwamba ni kwa “kufumba na kufumbua jicho,” yaani, mara tu baada ya kufa. (1 Wakorintho 15:52) Kwa kuwa ufufuo wa kikundi hicho kidogo cha wale 144,000 unatangulia ule wa watu wengi watakaofufuliwa kuishi duniani, unaitwa “ule ufufuo wa mapema” na “ufufuo wa kwanza.”—Wafilipi 3:11; Ufunuo 20:6.

Ni Nani Watakaofufuliwa Ili Waishi Duniani?

Kulingana na Maandiko, watu wengi waliokufa watarudishwa kwenye uhai duniani. (Zaburi 37:29; Mathayo 6:10) Akieleza maono yake yenye kustaajabisha ya wale watakaofufuliwa, mtume Yohana aliandika hivi: “Bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi [“Hadesi,” maelezo ya chini] vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, nao walihukumiwa kila mmoja kulingana na matendo yake. Na kifo na Kaburi vikatupwa ndani ya lile ziwa la moto. Hili linamaanisha kifo cha pili, lile ziwa la moto.” (Ufunuo 20:11-14) Wale walio katika Hadesi au Sheoli, yaani, kaburini, wamo katika kumbukumbu ya Mungu. Kila mmoja wao atafufuliwa. (Zaburi 16:10; Matendo 2:31) Kila mmoja wao atahukumiwa kulingana na mambo atakayofanya baada ya kufufuliwa. Kisha itakuwaje kwa kifo na Kaburi? Vitatupwa katika “ziwa la moto.” Hiyo inamaanisha kwamba wanadamu hawataathiriwa tena na kifo ambacho walirithi kutoka kwa Adamu.

Hebu wazia jinsi ufufuo unavyotoa tumaini zuri kwa wale ambao wamefiwa na wapendwa wao! Yesu alipomfufua mwana wa pekee wa mjane wa Naini, mjane huyo alifurahi sana! (Luka 7:11-17) Biblia inasema hivi kuhusu wazazi wa msichana mwenye umri wa miaka 12 aliyefufuliwa na Yesu: “Mara moja wakawa na shangwe kubwa.” (Marko 5:21-24, 35-42; Luka 8:40-42, 49-56) Katika ulimwengu mpya wa Mungu tutafurahi kuwapokea wapendwa wetu.

Kujua ukweli kuhusu ufufuo kunaweza kuwa na matokeo gani kwetu leo? Kitabu kimoja (The World Book Encyclopedia) kinasema: “Watu wengi wanaogopa kifo na hujaribu kuepuka kukifikiria.” Kwa nini? Kwa sababu wengi huona kifo kuwa jambo lisiloeleweka, lisilojulikana, na lenye kutisha. Kujua ukweli kuhusu hali ya wafu na kuwa na tumaini la ufufuo kunaweza kutupa nguvu ikiwa tutakabili ‘adui wa mwisho, kifo.’ (1 Wakorintho 15:26) Ujuzi huo hutusaidia pia kuvumilia wakati rafiki wa karibu au mtu wa ukoo anapokufa.

Ufufuo utaanza wakati gani duniani? Leo, dunia imejaa jeuri, mizozo, umwagaji wa damu, na uchafuzi wa mazingira. Kwa kweli ikiwa wafu wangefufuliwa waishi katika dunia iliyojaa mambo hayo, basi hakuwezi kuwa na furaha ya kudumu. Hata hivyo, Muumba ameahidi kwamba karibuni ataleta mwisho wa ulimwengu wa sasa unaoongozwa na Shetani. (Methali 2:21, 22; Danieli 2:44; 1 Yohana 5:19) Kusudi la Mungu kwa dunia litatimizwa karibuni. Kisha, katika ulimwengu mpya wenye amani wa Mungu, mabilioni ambao wamelala katika kifo, wataishi tena.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watu wengi waliokufa watafufuliwa waishi duniani