Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Washiriki Wapya wa Baraza Linaloongoza

Washiriki Wapya wa Baraza Linaloongoza

Washiriki Wapya wa Baraza Linaloongoza

MNAMO Jumatano asubuhi, Agosti 24, 2005, Wanabetheli wa Marekani na wa Kanada, walisikia tangazo lenye kusisimua walipokuwa wakifuata pamoja programu ya asubuhi kwenye video. Kuanzia Septemba 1, 2005, washiriki wawili wapya, Geoffrey W. Jackson na Anthony Morris wa Tatu, wangeongezwa kwenye Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

Ndugu Jackson alianza upainia mnamo Februari 1971 huko Tasmania, kisiwa cha Australia. Mnamo Juni 1974, alimwoa Jeanette (Jenny). Muda mfupi baadaye, waliwekwa rasmi kutumika wakiwa mapainia wa pekee. Tangu mwaka wa 1979 hadi 2003, walitumika wakiwa wamishonari huko Tuvalu, Samoa, na Fiji, mataifa ya visiwa vya Pasifiki huko Pasifiki Kusini. Wakiwa huko visiwani, Ndugu na Dada Jackson walisaidia sana katika kazi ya kutafsiri vichapo vya Biblia. Kuanzia mwaka wa 1992, Ndugu Jackson alitumika akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Samoa, na tangu mwaka wa 1996, akawa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Fiji. Mnamo Aprili 2003, yeye na Jenny wakawa washiriki wa familia ya Betheli ya Marekani na wakaanza kufanya kazi katika Idara ya Utumishi wa Tafsiri. Muda mfupi baadaye, Ndugu Jackson aliwekwa rasmi kuwa msaidizi wa Halmashauri ya Kufundisha ya Baraza Linaloongoza.

Ndugu Morris alianza utumishi wa painia mwaka wa 1971 nchini Marekani. Mnamo Desemba mwaka huohuo, akamwoa Susan, nao wakaendelea na upainia karibu miaka minne hadi mwana wao wa kwanza, Jesse, alipozaliwa. Baada ya muda, walizaa mwana mwingine, Paul. Ndugu Morris alirudia utumishi wa wakati wote mwaka wa 1979 akiwa painia wa kawaida. Mke wake alijiunga naye katika utumishi wa wakati wote wavulana hao walipoanza shule. Familia hiyo ilihubiri mahali ambapo uhitaji ulikuwa mkubwa katika Kisiwa cha Rhode na North Carolina nchini Marekani. Huko North Carolina, Ndugu Morris alitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala, na wavulana wake wakawa mapainia wa kawaida. Jesse na Paul walialikwa kutumika kwenye ofisi ya tawi ya Marekani walipokuwa na umri wa miaka 19. Wakati huohuo, Ndugu Morris alianza kazi ya mzunguko. Kisha, mwaka wa 2002 yeye na Susan waliitwa kutumika Betheli. Walianza mgawo wao mpya Betheli Agosti 1. Ndugu Morris alitumika katika Idara ya Utumishi huko Patterson na baadaye akawa msaidizi katika Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza.

Zaidi ya washiriki hao wapya wawili, washiriki wengine wa Baraza Linaloongoza ni C. W. Barber; J. E. Barr; S. F. Herd; M. S. Lett; G. Lösch; T. Jaracz; G. H. Pierce; A. D. Schroeder; D. H. Splane; na D. Sydlik. Washiriki wote wa Baraza Linaloongoza ni Wakristo watiwa-mafuta.