Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’

‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’

‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’

“Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—MATHAYO 28:19, 20.

1. Taifa la Israeli lilifanya uamuzi gani chini ya Mlima Sinai?

YAPATA miaka 3,500 iliyopita, taifa zima liliweka nadhiri kwa Mungu. Wakiwa wamekusanyika chini ya Mlima Sinai, Waisraeli walitangaza hivi waziwazi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” Kuanzia wakati huo, Waisraeli wakawa watu waliowekwa wakfu kwa Mungu, “mali [yake] ya pekee.” (Kutoka 19:5, 8; 24:3) Walitazamia kupata ulinzi wake, na vizazi vyao vyote vingeishi katika nchi “inayotiririka maziwa na asali.”—Mambo ya Walawi 20:24.

2. Watu wanaweza kuwa na uhusiano gani pamoja na Mungu leo?

2 Hata hivyo, kama mtunga-zaburi Asafu alivyotaja, Waisraeli ‘hawakulishika agano la Mungu, nao walikataa kutembea katika sheria yake.’ (Zaburi 78:10) Hawakutimiza nadhiri ambayo mababu zao waliweka kwa Yehova. Mwishowe, taifa hilo lilipoteza uhusiano wa pekee ambao mababu zao walikuwa nao pamoja na Mungu. (Mhubiri 5:4; Mathayo 23:37, 38) Hivyo, Mungu ‘alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14) Na katika siku hizi za mwisho, Mungu anakusanya “umati mkubwa, ambao hakuna mtu [anayeweza] kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” na umati huo unasema hivi kwa shangwe: “Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi juu ya kiti cha ufalme, na Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 7:9, 10.

3. Ni hatua gani ambazo mtu anahitaji kuchukua ili awe na uhusiano pamoja na Mungu?

3 Ili kuwa miongoni mwa wale walio na uhusiano huo wenye thamani pamoja na Mungu, ni lazima mtu ajiweke wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo hadharani kwa kubatizwa ndani ya maji. Kufanya hivyo ni kutii amri hii ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Waisraeli walisikiliza wakati “kitabu cha agano” kiliposomwa. (Kutoka 24:3, 7, 8) Hivyo, walielewa yale ambayo Yehova alitaka wafanye. Vivyo hivyo leo, kabla mtu hajachukua hatua ya kubatizwa, anahitaji kupata ujuzi sahihi kuhusu mapenzi ya Mungu ambao unapatikana katika Neno lake, Biblia.

4. Ni lazima mtu afanye nini ili astahili kubatizwa? (Tia ndani sanduku lililo hapa juu.)

4 Ni wazi kwamba Yesu alitaka wanafunzi wake wawe na msingi thabiti wa imani kabla ya kubatizwa. Aliwaagiza wafuasi wake waende na kufanya wanafunzi na vilevile kuwafundisha ‘kushika mambo yote ambayo aliamuru.’ (Mathayo 7:24, 25; Waefeso 3:17-19) Hivyo, kwa kawaida wale wanaostahili kubatizwa huwa wamejifunza Biblia kwa miezi kadhaa au hata kwa mwaka mmoja au miwili ili wasifanye uamuzi haraka au bila kufikiri. Wakati wa ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa huulizwa maswali mawili ya msingi, nao hujibu kwa kusema ndiyo. Kwa kuwa Yesu alikazia kwamba ‘neno letu Ndiyo linapaswa kumaanisha Ndiyo, na Siyo yetu, Siyo,’ inafaa sote tuchunguze kwa makini maana ya maswali hayo mawili ya ubatizo.—Mathayo 5:37.

Toba na Wakfu

5. Swali la kwanza la ubatizo linakazia hatua gani mbili muhimu?

5 Katika swali la kwanza la ubatizo, yule anayetaka kubatizwa huulizwa ikiwa ametubu kuhusiana na mambo aliyofanya zamani na ikiwa amejiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake. Swali hilo linakazia hatua mbili muhimu ambazo mtu anahitaji kuchukua kabla ya kubatizwa, yaani, toba na wakfu.

6, 7. (a) Kwa nini ni lazima wote wanaotaka kubatizwa watubu? (b) Ni lazima mtu afanye mabadiliko gani baada ya kutubu?

6 Kwa nini ni lazima mtu atubu kabla ya kubatizwa? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Wakati fulani sisi sote tulijiendesha . . . kupatana na tamaa za mwili wetu.” (Waefeso 2:3) Kabla ya kupata ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu, tuliishi kupatana na ulimwengu, kulingana na maadili yake na viwango vyake. Maisha yetu yaliongozwa na mungu wa mfumo huu, Shetani. (2 Wakorintho 4:4) Hata hivyo, baada ya kujua mapenzi ya Mungu, tunaazimia kuishi “si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.”—1 Petro 4:2.

7 Maisha hayo mapya huleta faida nyingi. Kwanza kabisa, yanatuwezesha kuwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Yehova, ambao Daudi aliulinganisha na mwaliko wa kuingia katika “hema” la Mungu na “mlima [wake] mtakatifu.” Hilo ni pendeleo kubwa ajabu! (Zaburi 15:1) Yehova hamkaribishi mtu yeyote bali anawakaribisha wale tu ‘wanaotembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wao.’ (Zaburi 15:2) Kwa kuwa tulikuwa katika hali mbalimbali kabla ya kujifunza kweli, ili tutimize matakwa hayo huenda tukalazimika kufanya mabadiliko fulani katika mwenendo na utu wetu. (1 Wakorintho 6:9-11; Wakolosai 3:5-10) Kile kinachomchochea mtu afanye mabadiliko hayo ni toba, yaani, kujutia kabisa maisha yetu ya zamani na kuazimia kwa bidii kumpendeza Yehova. Toba humwongoza mtu ageuke kabisa, yaani, aache maisha ya kilimwengu ya ubinafsi na kufuata njia inayompendeza Mungu.—Matendo 3:19.

8. Sisi hujiwekaje wakfu, na kujiweka wakfu kunahusianaje na ubatizo?

8 Katika sehemu ya pili ya swali la kwanza la ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa huulizwa ikiwa wamejiweka wakfu kwa Yehova ili wafanye mapenzi yake. Wakfu ni hatua muhimu ambayo inapaswa kutangulia ubatizo. Hatua hiyo hufanywa kupitia sala, na katika sala hiyo tunaeleza tamaa yetu ya kutoa maisha yetu kwa Yehova kupitia Kristo. (Waroma 14:7, 8; 2 Wakorintho 5:15) Kisha, Yehova anakuwa Bwana wetu na Mmiliki wetu, nasi tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu kama Yesu. (Zaburi 40:8; Waefeso 6:6) Ahadi hiyo nzito inayotolewa kwa Yehova hufanywa mara moja tu. Hata hivyo, kwa kuwa tunajiweka wakfu faraghani, siku ya ubatizo tunafanya tangazo la hadharani ili kuwaonyesha watu wote kwamba tumechukua hatua hiyo nzito ya kujiweka wakfu kwa Baba yetu wa mbinguni.—Waroma 10:10.

9, 10. (a) Mapenzi ya Mungu yanahusisha nini? (b) Maofisa wa Nazi walitambuaje kwamba tumejiweka wakfu?

9 Kuiga kielelezo cha Yesu cha kufanya mapenzi ya Mungu kunahusisha nini? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24) Hapa Yesu alitaja mambo matatu ambayo ni lazima tuyafanye. Kwanza, ‘tunajikana’ wenyewe, yaani, tunaacha mielekeo yetu ya ubinafsi ya kutokamilika, na badala yake tunakubali shauri na mwongozo wa Mungu. Pili, ‘tunauchukua mti wetu wa mateso.’ Katika siku za Yesu, mti wa mateso uliwakilisha aibu na kuteseka. Kwa kuwa sisi ni Wakristo, tunakubali kuteseka kwa ajili ya habari njema. (2 Timotheo 1:8) Ingawa watu katika ulimwengu wanaweza kutudhihaki au kutushutumu, sisi ‘hudharau aibu’ kama Kristo, nasi tunapata furaha kwa kujua kwamba tunampendeza Mungu. (Waebrania 12:2) Mwishowe, tunamfuata Yesu “sikuzote.”—Zaburi 73:26; 119:44; 145:2.

10 Inapendeza kwamba hata wapinzani fulani hutambua kuwa Mashahidi wa Yehova wamejiweka wakfu kwa Mungu ili wamtumikie kwa moyo wote. Kwa mfano, katika kambi ya mateso ya Buchenwald wakati wa utawala wa Nazi huko Ujerumani, Mashahidi waliokataa kukana imani yao walipaswa kutia sahihi taarifa hii iliyochapishwa: “Bado mimi ni Mwanafunzi wa Biblia mwaminifu, nami sitavunja kamwe kiapo changu mbele za Yehova.” Bila shaka, maneno hayo yanaonyesha wazi mtazamo wa watumishi wote waaminifu wa Mungu waliojiweka wakfu!—Matendo 5:32.

Kutambulishwa Kuwa Mmoja wa Mashahidi wa Yehova

11. Mtu anayebatizwa anapata pendeleo gani?

11 Katika sehemu ya kwanza ya swali la pili, yule anayetaka kubatizwa huulizwa ikiwa anaelewa kwamba ubatizo wake unamtambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kubatizwa, anakuwa mhudumu aliyewekwa rasmi ambaye anatambulishwa kwa jina la Yehova. Hilo ni pendeleo kubwa na daraka zito. Isitoshe, linamwezesha yule anayebatizwa awe na tazamio la kupata wokovu wa milele, maadamu anabaki mwaminifu kwa Yehova.—Mathayo 24:13.

12. Heshima ya kutambulishwa kwa jina la Yehova huleta daraka gani?

12 Bila shaka, ni heshima kubwa sana kutambulishwa kwa jina la Mungu mweza-yote, Yehova. Nabii Mika alisema hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Hata hivyo, heshima hiyo huleta daraka fulani. Tunahitaji kuishi kwa njia inayoleta heshima kwa Yehova, yule ambaye tunatambulishwa kwa jina lake. Paulo aliwakumbusha Wakristo huko Roma kwamba ikiwa mtu hatendi yale anayohubiri, jina la Mungu “linafanyiwa makufuru,” au kuchafuliwa.—Waroma 2:21-24.

13. Kwa nini watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wana daraka la kutoa ushahidi kuhusu Mungu wao?

13 Mtu anapokuwa Shahidi wa Yehova, anakubali pia daraka la kutoa ushahidi kuhusu Mungu wake. Yehova aliwaalika watu wa taifa la Israeli waliojiweka wakfu wawe mashahidi wake, ili watoe ushahidi kuhusu Uungu wake wa milele. (Isaya 43:10-12, 21) Lakini taifa hilo lilishindwa kutimiza daraka hilo, na mwishowe likapoteza kabisa kibali cha Yehova. Leo, Wakristo wa kweli wanajivunia pendeleo la kutoa ushahidi kumhusu Yehova. Tunafanya hivyo kwa sababu tunampenda na tunatamani jina lake litakaswe. Je, kweli tunaweza kunyamaza huku tukijua ukweli kuhusu Baba yetu wa mbinguni na kusudi lake? Tunahisi kama mtume Paulo, wakati aliposema: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!”—1 Wakorintho 9:16.

14, 15. (a) Tengenezo la Yehova hutusaidiaje kufanya maendeleo ya kiroho? (b) Ni maandalizi gani yanayotusaidia kiroho?

14 Katika swali la pili, yule anayetaka kubatizwa anakumbushwa pia kuhusu daraka lake la kushirikiana na tengenezo la Yehova linaloongozwa kwa roho. Hatuwezi kujitenga na wengine tunapomtumikia Mungu, nasi tunahitaji kusaidiwa, kutegemezwa, na kutiwa moyo na “ushirika mzima wa akina ndugu.” (1 Petro 2:17; 1 Wakorintho 12:12, 13) Tengenezo la Mungu linatimiza daraka muhimu katika maendeleo yetu ya kiroho. Linaandaa habari nyingi za Biblia zilizochapishwa ambazo zinatusaidia kuongeza ujuzi sahihi, kutenda kwa hekima tunapokabili matatizo, na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Kama mama anayehakikisha kwamba mtoto wake amelishwa vizuri na kutunzwa, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huandaa chakula tele cha kiroho kwa wakati unaofaa ili tufanye maendeleo ya kiroho.—Mathayo 24:45-47; 1 Wathesalonike 2:7, 8.

15 Kwenye mikutano ya kila juma, watu wa Yehova huzoezwa na kutiwa moyo wawe Mashahidi wa Yehova waaminifu. (Waebrania 10:24, 25) Shule ya Huduma ya Kitheokrasi hutufundisha kuzungumza mbele ya watu, na Mkutano wa Utumishi hutuzoeza kutangaza ujumbe wetu kwa njia yenye matokeo. Tunapohudhuria mikutano yetu na kujifunza kibinafsi habari za Biblia zilizochapishwa, tunaona roho ya Yehova ikifanya kazi ili kuongoza tengenezo lake. Kupitia maandalizi hayo yanayotolewa kwa ukawaida, Mungu hutuonyesha hatari, hutuzoeza kuwa wahudumu stadi, na kutusaidia tuendelee kukesha kiroho.—Zaburi 19:7, 8, 11; 1 Wathesalonike 5:6, 11; 1 Timotheo 4:13.

Nia ya Kufanya Uamuzi wa Kubatizwa

16. Ni nini kinachotuchochea kujiweka wakfu kwa Yehova?

16 Kwa hiyo, yale maswali mawili ya ubatizo yanawakumbusha wale wanaotaka kubatizwa maana ya ubatizo wa maji na madaraka yanayotokana na hatua hiyo. Basi, wanapaswa kuwa na nia gani wanapofanya uamuzi wa kubatizwa? Tunakuwa wanafunzi waliobatizwa, si kwa sababu mtu ametulazimisha, bali kwa sababu Yehova ‘anatuvuta.’ (Yohana 6:44) Kwa kuwa “Mungu ni upendo,” anatawala kwa upendo, wala si kwa mabavu. (1 Yohana 4:8) Sisi huvutwa kwa Yehova kwa sababu ya sifa zake nzuri na jinsi anavyotutendea. Yehova alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee kwa ajili yetu, naye anatuahidi maisha bora wakati ujao. (Yohana 3:16) Hivyo, tunachochewa kumpa maisha yetu, naam, kuyaweka wakfu kwake.—Methali 3:9; 2 Wakorintho 5:14, 15.

17. Hatukujiweka wakfu kwa mambo gani?

17 Sisi hujiweka wakfu, si kwa lengo fulani wala kwa kazi fulani, bali kwa Yehova mwenyewe. Kazi ambayo Mungu amewapa watu wake itabadilika, lakini wakfu wao kwake hauwezi kubadilika. Kwa mfano, mgawo ambao Yehova alimpa Abrahamu ni tofauti sana na ule aliompa Yeremia. (Mwanzo 13:17, 18; Yeremia 1:6, 7) Lakini, watu hao wawili walitimiza kazi hususa ambayo Mungu aliwapa kwa sababu walimpenda Yehova na walitaka kufanya mapenzi yake kwa uaminifu. Katika wakati huu wa mwisho, wafuasi wote wa Kristo waliobatizwa hujitahidi kutimiza amri ya Kristo ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kufanya kazi hiyo kwa moyo wote ni njia nzuri ya kuonyesha kwamba tunampenda Baba yetu wa mbinguni na kwamba tumejiweka wakfu kwake.—1 Yohana 5:3.

18, 19. (a) Tunapobatizwa, sisi hutoa taarifa gani hadharani? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

18 Bila shaka, ubatizo humwezesha mtu kupata baraka nyingi, lakini hiyo ni hatua inayopaswa kufikiriwa kwa uzito. (Luka 14:26-33) Inaonyesha azimio ambalo linapaswa kutangulizwa kabla ya madaraka mengine yote. (Luka 9:62) Tunapobatizwa, tunatoa taarifa hii hadharani: “Mungu huyu ni Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele. Yeye mwenyewe atatuongoza mpaka tufe.”—Zaburi 48:14.

19 Makala inayofuata itazungumzia maswali mengine yanayoweza kutokea kuhusiana na ubatizo wa maji. Je, mtu anaweza kuwa na sababu nzuri za kuepuka kubatizwa? Je, umri unapaswa kufikiriwa? Sote tunaweza kufanya nini ili kufanya pindi ya ubatizo iwe yenye kuheshimika?

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini kila Mkristo anahitaji kutubu kabla ya kubatizwa?

• Kujiweka wakfu kwa Mungu kunahusisha nini?

• Ni madaraka gani yanayotokana na heshima ya kutambulishwa kwa jina la Yehova?

• Ni nini kinachopaswa kutuchochea kuamua kubatizwa?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

Yale Maswali Mawili ya Ubatizo

Kwa msingi wa dhabihu ya Yesu Kristo, je, umetubu dhambi zako na kujiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake?

Je, unaelewa kwamba wakfu na ubatizo wako unakutambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayeshirikiana na tengenezo la Mungu linaloongozwa na roho?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wakfu ni ahadi nzito inayotolewa kwa Yehova kupitia sala

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kazi yetu ya kuhubiri huonyesha wakfu wetu kwa Mungu