Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kitakachokusaidia Kuielewa Biblia?

Ni Nini Kitakachokusaidia Kuielewa Biblia?

Ni Nini Kitakachokusaidia Kuielewa Biblia?

“UMEWAFICHA kwa uangalifu wenye hekima na walio na akili mambo hayo, nawe umeyafunua kwa watoto.” (Luka 10:21) Maneno hayo ambayo Yesu alimwambia Baba yake wa mbinguni yanaonyesha kwamba ili kuielewa Biblia, tunahitaji kuwa na mtazamo unaofaa. Hekima ya Yehova imeonekana wazi katika maana ya kwamba ametokeza kitabu ambacho ni wanyenyekevu tu, watu wanaokubali kufundishwa ndio wanaoweza kukielewa vizuri.

Wengi wetu huona ni vigumu kuwa wanyenyekevu. Sote tumerithi mwelekeo wa kuwa wenye kiburi. Isitoshe, tunaishi katika “siku za mwisho,” miongoni mwa watu “wenye kujipenda wenyewe, . . . wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:1-4) Hiyo ni mitazamo inayotuzuia tusilielewe Neno la Mungu. Inasikitisha kwamba, kwa kiasi fulani sote tunaathiriwa na watu tunaoshughulika nao. Hivyo basi, unawezaje kuwa na mtazamo unaohitajiwa ili kuielewa Biblia?

Kutayarisha Moyo na Akili

Ezra, kiongozi wa kale wa watu wa Mungu, “alikuwa ameutayarisha moyo wake kutafuta shauri katika sheria ya Yehova.” (Ezra 7:10) Je, kuna namna tunavyoweza kuutayarisha moyo wetu? Ndiyo. Tunaweza kuanza kwa kudumisha mtazamo unaofaa kuhusu Maandiko. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Ingawa watu walitumiwa kuiandika Biblia, mambo waliyoandika yalitoka kwa Yehova. Kutambua ukweli huo muhimu kutatusaidia kukubali mambo tunayosoma.—2 Timotheo 3:16.

Njia nyingine ya kutayarisha moyo wetu ni kupitia sala. Kwa kuwa Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu, roho hiyohiyo inaweza kutusaidia kuelewa ujumbe wake. Hivyo, tunapaswa kusali ili tupate msaada huo. Ona jinsi mtunga-zaburi alivyoandika kuhusiana na hilo: “Unifanye nielewe, ili nipate kuishika sheria yako nami nipate kuishika kwa moyo wote.” (Zaburi 119:34) Tunahitaji kusali si ili tupate uwezo wa akili wa kuelewa mambo yaliyoandikwa tu, bali pia tunahitaji kusali ili tuwe na mwelekeo wa moyo ambao utatuwezesha kukubali yale ambayo Biblia inasema. Ili kuielewa Biblia, tunahitaji kuwa tayari kukubali ukweli.

Unapotafakari ili kuwa na mtazamo unaofaa, fikiria jinsi kujifunza Biblia kunavyoweza kukusaidia. Tuna sababu nyingi nzuri za kulisoma Neno la Mungu, lakini sababu muhimu hata zaidi ni kwamba Biblia inatusaidia kumkaribia Mungu. (Yakobo 4:8) Tunaposoma jinsi Yehova anavyotenda katika hali mbalimbali, jinsi anavyowathamini wale wanaompenda, na jinsi anavyowatendea wale wanaomwacha, tunatambua yeye ni mtu wa aina gani. Sikuzote kusudi letu kuu la kusoma Biblia linapaswa kuwa kumjua Mungu vizuri zaidi na hivyo kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye.

Vizuizi vya Kuwa na Mtazamo Unaofaa

Ni nini kinachoweza kutuzuia tusilielewe Neno la Mungu? Kizuizi kimoja ni kushikilia maoni ya watu ambao tunahisi kwamba tunapaswa kuwa waaminifu kwao. Kwa mfano, huenda ukashikilia imani na maoni ya watu wenye kuheshimika. Hata hivyo, ungefanyaje ikiwa watu hao hawathamini kweli ya Neno la Mungu? Chini ya hali kama hizo, huenda ikawa vigumu kuelewa yale ambayo Biblia hufundisha hasa. Hivyo, Biblia inatutia moyo kuchunguza kwa uangalifu mambo ambayo tumefundishwa.—1 Wathesalonike 5:21.

Maria, mama ya Yesu, alikabili tatizo hilo. Alilelewa kulingana na mapokeo ya Wayahudi. Alifuata kwa uangalifu Sheria ya Musa na bila shaka alienda kwenye sinagogi. Baadaye, alitambua kwamba namna ya ibada ambayo alifundishwa na wazazi wake haikuwa yenye kukubaliwa tena na Mungu. Hivyo, Maria akakubali mafundisho ya Yesu naye akawa kati ya washiriki wa kwanza wa kutaniko la Kikristo. (Matendo 1:13, 14) Kwa kufanya hivyo hakuwadharau wazazi wake wala desturi zao; badala yake, alionyesha upendo wake kwa Mungu. Ili tufaidike kutokana na Biblia, kama vile Maria, tunapaswa kwanza kuwa waaminifu kwa Mungu kuliko kuwa waaminifu kwa mtu mwingine yeyote.

Kwa kusikitisha, watu wengi hawaithamini kweli ya Biblia. Baadhi yao wanafurahia kufuata mapokeo ya kidini yanayotegemea uwongo. Wengine wanaidharau kweli kwa maneno na kwa mtindo wao wa maisha. Hivyo, kuikubali kweli ya Biblia kunahitaji kujidhabihu kwa kadiri fulani: Kunaweza kukufanya usielewane na marafiki, majirani, wafanyakazi wenzako, na hata watu wa familia yako. (Yohana 17:14) Hata hivyo, mwanamume mwenye hekima Sulemani aliandika hivi: “Nunua kweli wala usiiuze.” (Methali 23:23) Ukiithamini sana kweli, Yehova atakusaidia uielewe Biblia.

Hata hivyo, kizuizi kingine cha kuuelewa ujumbe wa Biblia ni kukataa kutumia mambo inayosema. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu za ufalme wa mbinguni, lakini wao hawakupewa. Kwa maana moyo wa watu hawa umekuwa mgumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia.” (Mathayo 13:11, 15) Wengi wa wale ambao Yesu alihubiria hawakutaka kubadilika. Lo! Jinsi walivyokuwa tofauti sana na mwanabiashara msafiri ambaye Yesu alitaja katika mfano wake! Baada ya kupata lulu yenye thamani kubwa, mwanabiashara huyo aliuza haraka vitu vyote alivyokuwa navyo ili kuinunua. Vivyo hivyo, kuielewa kweli ya Biblia kunapaswa kuwa muhimu kwetu.—Mathayo 13:45, 46.

Ugumu wa Kukubali Kufundishwa

Tatizo kubwa ambalo huwazuia watu wasiielewe Biblia ni kutotaka kufundishwa. Huenda mtu akaona ni vigumu kukubali mawazo mapya kutoka kwa mtu anayeonekana kuwa wa hali ya chini. Hata hivyo, mitume wa Yesu Kristo walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:13) Akifafanua kwa nini mitume hao walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu,” Paulo aliandika hivi: “Mnaona mwito wake kwenu, akina ndugu, kwamba si wengi wenye hekima katika njia ya kimwili walioitwa, si wengi wenye nguvu, si wengi wa uzawa wa cheo; bali Mungu alivichagua vitu vipumbavu vya ulimwengu, ili awaaibishe watu wenye hekima.” (1 Wakorintho 1:26, 27) Ikiwa unaona kwamba ni vigumu kwako kunyenyekea unapofundishwa na mtu wa hali ya chini, kumbuka kwamba mtu huyo anatumiwa tu na Mungu ili kukufundisha. Je, kuna pendeleo kubwa zaidi kuliko lile la kufundishwa na Yehova, ‘Mfundishaji wetu Mkuu’?—Isaya 30:20; 54:13.

Naamani, kiongozi wa jeshi la Siria, aliona ni vigumu kukubali maagizo kutoka kwa mtu wa hali ya chini. Alimwendea Elisha nabii wa Yehova ili amponye ukoma. Hata hivyo, Naamani alipewa maagizo ya Mungu kuhusu uponyaji kupitia mtumishi fulani. Ujumbe huo na jinsi ulivyotolewa ulifanya iwe vigumu kwa Naamani kukubali maagizo hayo kwa unyenyekevu, hivi kwamba mwanzoni alikataa kutii neno la nabii wa Mungu. Baadaye, Naamani alibadili mtazamo wake naye akaponywa. (2 Wafalme 5:9-14) Tunakabili tatizo hilohilo tunapojifunza Biblia. Huenda tukajua kwamba ili kuponywa kiroho na kiadili, tunahitaji kufuata njia mpya ya maisha. Je, tutanyenyekea ili kuruhusu mtu fulani atufundishe mambo tunayopaswa kufanya? Ni wale tu walio tayari kufundishwa ndio wanaoweza kuielewa Biblia.

Mtu mmoja aliyekuwa na mamlaka chini ya Kandake, malkia wa Waethiopia, alionyesha mtazamo unaofaa. Alikuwa akirudi Afrika akiwa ndani ya gari lake la kukokotwa wakati mwanafunzi Filipo alipokimbia kandokando yake na kumkaribia. Filipo alimwuliza mwanamume huyo ikiwa alielewa mambo aliyokuwa akisoma. Ofisa huyo mnyenyekevu alijibu hivi: “Ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Baada ya kulielewa Neno la Mungu, mtu huyo alibatizwa. Baada ya hapo, “aliendelea kwenda zake akishangilia.”—Matendo 8:27-39.

Kwa ujumla, Mashahidi wa Yehova ni watu wa kawaida tu. Kila juma wanaongoza mafunzo ya Biblia katika nyumba za watu zaidi ya milioni sita. Kwa kuwa Biblia inafundisha njia bora zaidi ya maisha, inaeleza kuhusu tumaini hakika la pekee kwa wanadamu, na inatuwezesha kumjua Mungu, mamilioni ya watu wametambua kwamba kujifunza Biblia na kuelewa mambo inayosema huleta furaha kubwa. Wewe pia unaweza kupata furaha hiyo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Naamani aliona ni vigumu kukubali maagizo kutoka kwa mtumishi fulani wa hali ya chini

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuielewa Biblia huchangamsha mioyo yetu