Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kufurahia Kuielewa Biblia

Unaweza Kufurahia Kuielewa Biblia

Unaweza Kufurahia Kuielewa Biblia

BIBLIA ina kweli zenye thamani kutoka kwa Mungu. Inatueleza kuhusu kusudi la maisha, kile kinachosababisha mateso ya wanadamu, na wakati ujao wa wanadamu. Inatufundisha jinsi ya kupata furaha, jinsi ya kupata marafiki, na jinsi ya kusuluhisha matatizo. Zaidi ya hayo, tunajifunza kuhusu Muumba wetu ambaye ni Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Ujuzi huo hutuletea furaha na hutupa kusudi maishani.

Biblia inalinganisha kupata ujuzi kumhusu Mungu na kula. Yesu alisema hivi: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4; Waebrania 5:12-14) Kama vile ni muhimu kwetu kula chakula kinachojenga mwili kila siku ili tuendelee kuishi, ndivyo ilivyo muhimu kulisoma Neno la Mungu kwa ukawaida ili tufaidike na ahadi ya Mungu ya uzima wa milele.

Tunafurahia kula kwa sababu ya jinsi tulivyoumbwa na kwa sababu kula hutosheleza uhitaji wa msingi. Hata hivyo, tuna uhitaji mwingine wa msingi ambao tunapaswa kuutosheleza pia ikiwa tunataka kuwa wenye furaha. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Inawezekana kupata furaha kwa sababu uhitaji wetu wa kiroho unaweza kutoshelezwa kwa kulielewa Neno la Mungu.

Ni kweli kwamba watu wengine huona ni vigumu kuielewa Biblia. Kwa mfano, huenda ukahitaji msaada kuyaelewa maandiko yanayorejelea desturi usizozijua au yale yanayotumia lugha ya mfano. Pia, kuna unabii mbalimbali ulioandikwa kwa lugha ya mfano ambao unaeleweka tu kwa kuyachunguza maandiko mengine ya Biblia yanayozungumzia habari hiyo. (Danieli 7:1-7; Ufunuo 13:1, 2) Hata hivyo, unaweza kuielewa Biblia. Ni nini kinachoonyesha kwamba inawezekana uielewe?

Wote Wanaweza Kufurahia

Biblia ni Neno la Mungu. Ndani yake Mungu anatueleza yale anayotaka tufanye. Je, Mungu angeandaa kitabu ambacho ingekuwa vigumu kukielewa au ambacho kingeeleweka tu na watu wenye elimu ya juu? Hapana, Yehova hangetenda hivyo. Kristo Yesu alisema hivi: “Ni baba gani kati yenu ambaye, ikiwa mwana wake anaomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? Au ikiwa pia anaomba yai, atampa nge? Kwa hiyo, ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:11-13) Hivyo, uwe na hakika kwamba unaweza kuielewa Biblia na kwamba ukimwomba Mungu kwa unyoofu, atakupa msaada ambao unahitaji ili ulielewe Neno lake. Ni wazi kwamba hata watoto wanaweza kuyaelewa na kuyathamini mafundisho ya msingi ya Biblia.—2 Timotheo 3:15.

Ingawa jitihada zinahitajiwa ili kuielewa Biblia, kufanya hivyo kunaweza kutuimarisha na kutuchochea sana. Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake wawili na kuzungumza nao kuhusu unabii mbalimbali wa Biblia. Simulizi la Luka linasema hivi: “Akaanzia Musa na Manabii wote, akawafasiria mambo yanayomhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.” Matokeo yakawaje? Jioni hiyo, walipokuwa wakifikiria mambo waliyojifunza, wanafunzi hao waliambiana hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?” (Luka 24:13-32) Walifurahia kulielewa Neno la Mungu kwa sababu liliimarisha imani yao katika ahadi za Mungu nalo likawasaidia kuwa na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao.

Badala ya kuwa mzigo, ni jambo lenye kufurahisha na lenye manufaa kulielewa Neno la Mungu, kama vile inavyofurahisha kula chakula kinachojenga mwili. Unahitaji kufanya nini ili upate uelewaji huo? Makala inayofuata inaonyesha jinsi unavyoweza kufurahia “kumjua Mungu.”—Methali 2:1-5.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kama baba mwenye upendo, Yehova anatupa roho takatifu ili itusaidie kuielewa Biblia