Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Haki ya Kuwa na Jina

Haki ya Kuwa na Jina

Haki ya Kuwa na Jina

KILA mtu ana haki ya kuwa na jina. Huko Tahiti, hata mtoto mchanga aliyezaliwa na kutupwa ambaye baba na mama yake hawajulikani, hupewa jina. Ofisi ya uandikishaji humpa mtoto aliyetupwa jina la kwanza na la pili.

Hata hivyo, kuna mtu ambaye kwa njia fulani amenyimwa haki hiyo ya msingi, yaani, haki ambayo wanadamu wote wamepewa. Jambo la kushangaza ni kwamba yeye ndiye “Baba . . . ambaye kila familia mbinguni na duniani hupata jina kutokana naye”! (Waefeso 3:14, 15) Hata hivyo, watu wengi hukataa kutumia jina la Muumba kama linavyoonyeshwa katika Biblia. Badala yake, wanapendelea kutumia majina yake ya cheo kama vile “Mungu,” “Bwana,” au “Aliye wa Milele.” Hivyo basi, jina lake ni nani? Mtunga-zaburi anajibu swali hilo: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—Zaburi 83:18.

Mapema katika miaka ya 1800 wakati wamishonari wa Shirika la Wamishonari la London walipofika huko Tahiti, Wapolinesia walikuwa wakiabudu miungu mbalimbali. Kila mungu alikuwa na jina lake la pekee, na Oro na Taaroa ndio waliokuwa miungu muhimu. Ili kumtofautisha Mungu wa Biblia na miungu hiyo mingine, wamishonari hao hawakusita kulitumia sana jina la Mungu, ambalo lilitafsiriwa kuwa Iehova katika Kitahiti.

Hivyo, jina hilo likajulikana sana na kutumiwa katika mazungumzo ya kila siku na katika barua. Mfalme Pomare wa Pili wa Tahiti, ambaye alitawala mapema katika miaka ya 1800, alilitumia mara kwa mara katika barua zake. Hilo linathibitishwa na barua inayoonyeshwa katika picha hii. Barua hiyo iliyoandikwa katika Kiingereza inapatikana katika Jumba la Makumbusho la Tahiti na Visiwa Vyake. Barua hiyo inathibitisha kwamba, wakati huo, watu walikubali kulitumia jina la Mungu. Zaidi ya hilo, jina la kibinafsi la Mungu hupatikana mara nyingi katika tafsiri ya kwanza ya Biblia ya Kitahiti, ambayo ilikamilishwa mwaka wa 1835.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Mfalme Pomare wa Pili

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]

King and letter: Collection du Musée de Tahiti et de ses Îles, Punaauia, Tahiti