Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ikiwa mtu anasumbuliwa na roho waovu, anaweza kufanya nini ili apate kitulizo?

Neno la Mungu linaonyesha kwamba wale wanaoteseka kwa sababu ya kushambuliwa na roho waovu wanaweza kuwekwa huru kutokana na usumbufu huo. Sala ni muhimu ili kuwekwa huru na uvutano huo wa roho waovu. (Marko 9:25-29) Hata hivyo, yule anayesumbuliwa na roho waovu huenda akahitaji kuchukua hatua za ziada. Matukio yanayowahusu Wakristo wa karne ya kwanza yanaonyesha mambo mengine ambayo huenda yakahitajiwa.

Watu fulani katika Efeso la kale walijihusisha katika kuwasiliana na roho waovu kabla ya kuwa wafuasi wa Kristo. Hata hivyo, baada ya kuamua kumtumikia Mungu, ‘wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi walileta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mtu.’ (Matendo 19:19) Kwa kuviharibu vitabu vyao vya uaguzi, waamini hao wapya huko Efeso waliweka kielelezo kizuri kwa wale wanaotaka kuwekwa huru kutokana na mashambulizi ya roho waovu leo. Ni muhimu sana kwa watu hao kuondolea mbali vitu vyote vinavyohusiana na kuwasiliana na pepo. Vitu hivyo vinatia ndani vitabu, magazeti, sinema, habari za Intaneti, muziki unaohusiana na mambo ya ushirikina, na pia hirizi au vitu vingine vinavyovaliwa ili ‘kujilinda’ au vinavyohusiana na zoea la kuwasiliana na pepo.—Kumbukumbu la Torati 7:25, 26; 1 Wakorintho 10:21.

Miaka michache baada ya Wakristo hao wa Efeso kuharibu vitabu vyao vya uchawi, mtume Paulo aliandika hivi: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12) Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.” (Waefeso 6:11) Shauri hilo bado linatumika. Lazima Wakristo wachukue hatua thabiti ili kuimarisha hali yao ya kiroho ambayo itawasaidia kujilinda dhidi ya roho waovu. Paulo alikazia hivi: “Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.” (Waefeso 6:16) Mtu huimarisha imani yake kupitia funzo la Biblia. (Waroma 10:17; Wakolosai 2:6, 7) Hivyo, funzo la Biblia la kawaida hutusaidia kusitawisha imani ambayo hutulinda dhidi ya uvutano wa roho waovu.—Zaburi 91:4; 1 Yohana 5:5.

Hata hivyo, Wakristo hao wa Efeso walihitaji kuchukua hatua nyingine muhimu. Paulo aliwaandikia hivi: “Kwa kila namna ya sala na dua mkiendeleza sala kila wakati katika roho.” (Waefeso 6:18) Naam, kusali kwa bidii ili Yehova atulinde ni muhimu kwa wale wanaotaka kuwekwa huru kutokana na mashambulizi ya roho waovu leo. (Methali 18:10; Mathayo 6:13; 1 Yohana 5:18, 19) Kwa kufaa, Biblia inasema hivi: “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yakobo 4:7.

Ingawa yule anayeshambuliwa na roho waovu anapaswa kusali kwa bidii ili apate kitulizo, Wakristo wengine wa kweli wanaweza pia kusali kwa ajili ya mtu anayetamani sana kumtumikia Yehova na ambaye anajitahidi sana kushinda roho waovu. Wanaweza kumwomba Mungu ili yule anayesumbuliwa na roho waovu apate kuimarishwa kiroho na kushinda mashambulizi ya roho waovu. Kwa kuwa Neno la Mungu linasema kwamba “dua ya mtu mwadilifu, inapofanya kazi, ina nguvu nyingi,” bila shaka, sala zinazotolewa na watumishi wa Mungu zitawafaidi wale wanaosumbuliwa na roho waovu na ambao wanajitahidi sana ‘kumpinga Ibilisi.’—Yakobo 5:16.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Waamini huko Efeso waliharibu vitabu vyao vya uchawi