Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Melito wa Sardi Je, Alikuwa Mteteaji wa Kweli za Biblia?

Melito wa Sardi Je, Alikuwa Mteteaji wa Kweli za Biblia?

Melito wa Sardi Je, Alikuwa Mteteaji wa Kweli za Biblia?

KILA mwaka Wakristo wa kweli huadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana tarehe inayolingana na Nisani 14 ya kalenda ya Waebrania. Wakristo wa kweli wanatii amri hii ya Yesu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” Baada ya kuadhimisha Pasaka mnamo Nisani 14 mwaka wa 33 W.K., Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake cha kidhabihu. Alikufa kabla ya siku hiyo kwisha.—Luka 22:19, 20; 1 Wakorintho 11:23-28.

Katika karne ya pili W.K., watu wengine walianza kubadili wakati wa kuadhimisha ukumbusho na namna ya kufanya hivyo. Tarehe ya kifo cha Yesu iliendelea kutumiwa huko Asia Ndogo. Hata hivyo, kama vile kichapo kimoja cha kitaalamu kinavyosema, ‘huko Roma na Aleksandria watu walikuwa na desturi ya kuadhimisha si kifo cha Yesu, bali ufufuo wake mnamo Jumapili baada ya tarehe ya kifo chake,’ nao wakauita mwadhimisho huo Pasaka ya Ufufuo. Kikundi fulani cha watu kiliunga mkono Nisani 14 kuwa tarehe ya kuadhimishwa kwa kifo cha Yesu Kristo. Melito wa Sardi alikuwa na maoni kama hayo. Melito alikuwa nani? Ni katika njia gani alitetea kweli hiyo na kweli nyingine za Biblia?

‘Mtu Mashuhuri’

Katika kitabu chake (Ecclesiastical History), Eusebio wa Kaisaria anasema kwamba mwishoni mwa karne ya pili, Polycrates wa Efeso alituma barua Roma iliyotetea kuadhimisha “siku ya 14 ya Pasaka kulingana na vitabu vya Injili, kutoiacha kamwe, na kuendelea kuifuata kulingana na kanuni ya imani.” Kulingana na barua hiyo, Melito, Askofu wa Sardi, huko Lidia, alikuwa mmoja wa wale waliotetea Nisani 14 kuwa tarehe ya kuadhimishwa. Barua hiyo ilisema kwamba watu wa siku zake walimwona kuwa mmoja wa ‘watu mashuhuri ambao wamekufa.’ Polycrates alisema kwamba Melito hakuoa na kwamba “alijihusisha kabisa na mambo ya Roho Takatifu na alizikwa huko Sardi akingoja mwito kutoka mbinguni wakati atakapofufuliwa.” Huenda hilo linamaanisha kwamba Melito alikuwa kati ya wale walioamini kwamba ufufuo haungeanza hadi Kristo arudi.—Ufunuo 20:1-6.

Hivyo, inaonekana kwamba Melito alikuwa mtu jasiri na mwenye kuazimia. Aliandika kitabu (Apology) kwa ajili ya Wakristo ambacho kilikuwa cha kwanza kuandikiwa Marcus Aurelius, Maliki Mroma, aliyetawala kuanzia mwaka wa 161 hadi 180 W.K. Melito hakuogopa kutetea Ukristo na kuwashutumu watu waovu na wenye pupa. Watu hao walitafuta amri mbalimbali kutoka kwa Maliki kuwa visingizio ili kuwatesa Wakristo na kupora mali zao.

Kwa ujasiri, Melito alimwandikia hivi maliki: “Tunakuomba jambo moja tu, kwamba wewe mwenyewe uwachunguze wale wanaosababisha fujo [Wakristo], na uhukumu kwa haki ikiwa wanastahili kifo na adhabu au ikiwa wanastahili kulindwa na kutoadhibiwa. Lakini ikiwa si wewe uliyetunga shauri hili na amri hiyo mpya ambayo haifai hata dhidi ya maadui wakatili, tunakusihi usitupuuze, sisi tunaoumia kutokana na wale wanaotutesa.”

Kutumia Maandiko ili Kutetea Ukristo

Melito alipenda sana kujifunza Maandiko Matakatifu. Hatuna orodha kamili ya maandishi yake, lakini majina ya baadhi ya maandishi yake yanafunua jinsi alivyopendezwa na habari za Biblia. Yafuatayo ni baadhi ya maandishi yake: Maisha ya Ukristo na Manabii, Imani ya Mwanadamu, Uumbaji, Ubatizo na Kweli na Imani na Kuzaliwa kwa Kristo, Kukaribisha Wageni, Ufunguo, na Ibilisi na Ufunuo wa Yohana (On Christian Life and the Prophets, On the Faith of Man, On Creation, On Baptism and Truth and Faith and Christ’s Birth, On Hospitality, The Key, and On the Devil and the Apocalypse of John).

Melito alisafiri kwenda katika nchi za Biblia ili kufanya utafiti kuhusu hesabu kamili ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania. Kuhusu utafiti huo Melito aliandika hivi: “Kwa hiyo, nilipokwenda Mashariki na kufika mahali ambapo mambo hayo yalihubiriwa na kutendeka, na baada ya kujifunza kuhusu vitabu vya Agano la Kale kwa usahihi na kuandika mambo hayo, niliyatuma kwako.” Orodha ya Melito ya vitabu vinavyokubalika vya Maandiko ya Kiebrania haitaji vitabu vya Nehemia na Esta, lakini ndiyo ya kale zaidi kati ya maandishi ya wale wanaodai kuwa Wakristo.

Wakati wa utafiti huo, Melito alitayarisha orodha ya mistari ya Maandiko ya Kiebrania ambayo ina unabii mbalimbali kumhusu Yesu. Orodha hiyo ya Melito (Extracts) inaonyesha kwamba Yesu ndiye Masihi aliyetarajiwa kwa muda mrefu na kwamba alikuwa amerejelewa katika Sheria ya Musa na Manabii.

Kutetea Thamani ya Fidia

Kulikuwa na Wayahudi wengi katika majiji makubwa ya Asia Ndogo. Wayahudi wa Sardi, ambapo Melito aliishi, walikuwa wakiadhimisha Pasaka ya Kiyahudi mnamo Nisani 14. Melito aliandika hotuba yenye kichwa Pasaka (The Passover) ambayo ilithibitisha uhalali wa Pasaka chini ya Sheria na kutetea mwadhimisho wa Kikristo wa Mlo wa Jioni wa Bwana mnamo Nisani 14.

Baada ya kutoa maelezo kuhusu kitabu cha Kutoka sura ya 12 na kuonyesha kwamba Pasaka iliwakilisha dhabihu ya Kristo, Melito alieleza kwa nini Wakristo hawakuhitaji kuiadhimisha. Ilikuwa hivyo kwa sababu Mungu alikuwa amekomesha Sheria ya Musa. Kisha, akaonyesha kwa nini dhabihu ya Kristo ilikuwa muhimu: Mungu alimweka Adamu katika paradiso ili aishi maisha yenye furaha. Lakini yule mtu wa kwanza hakutii amri ya kutokula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Kwa sababu hiyo, fidia ilihitajiwa.

Melito alieleza kwamba Yesu alitumwa duniani na kufa mtini ili kuwakomboa wanadamu waaminifu kutokana na dhambi na kifo. Inapendeza kuona kwamba Melito alitumia neno la Kigiriki xylon, linalomaanisha “mbao,” alipoandika kuhusu mti ambao Yesu alikufa juu yake.—Matendo 5:30; 10:39; 13:29.

Melito alijulikana hata nje ya Asia Ndogo. Tertullian, Clement wa Aleksandria, na Origen walifahamu vizuri maandishi yake. Hata hivyo, mwanahistoria Raniero Cantalamessa anasema hivi: “Kupungua kwa umaarufu wa Melito, kulianza hatua kwa hatua maandishi yake yalipoanza kutoweka—baada ya desturi ya Pasaka ya Jumapili kutia mizizi, yaani, wakati waadhimishaji wa Nisani 14 walipoanza kuonwa kuwa waasi-imani.” Mwishowe, maandishi mengi ya Melito yalipotea kabisa.

Je, Melito Aliathiriwa na Uasi-Imani?

Baada ya kifo cha mitume, uasi-imani uliotabiriwa ulijipenyeza katika Ukristo wa kweli. (Matendo 20:29, 30) Ni wazi kwamba uasi-imani huo ulimwathiri Melito. Maandishi yake magumu yanafanana na falsafa ya Kigiriki na hali za Roma. Labda ndiyo sababu Melito alitaja Ukristo kuwa “falsafa yetu.” Pia, alisema kwamba uhusiano kati ya watu waliodai kuwa Wakristo na Milki ya Roma ndilo “jambo kuu zaidi linaloonyesha mafanikio.”

Bila shaka, Melito hakutii shauri lifuatalo la mtume Paulo: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” Hivyo, ingawa Melito alitetea kweli za Biblia kwa kadiri fulani, katika mambo mengi hakuzifuata.—Wakolosai 2:8.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana mnamo Nisani 14